JUMATATU WIKI YA 1 YA MWAKA-C
11/1/2016
Somo: 1Sam 1:1-8
Zab: 116: 12-13, 14-19
Injili: Mk 1:14-20
Nukuu:
“Elkana mumewe akamwambia, Hana, unalilia nini? Kwani huli
chakula? Kwa nini moyo wako una huzuni? Je! Mimi si bora kwako kuliko watoto
kumi?”
Isam 1:8
“akisema, Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni,
na kuiamini Injili,” Mk 1:15
“Yesu akawaambia, Njoni mnifuate, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa
watu,” Mk 1:17
“Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata,” Mk 1:18
TAFAKARI: “Wakati umetimia, na ufalme
wa Mungu umekaribia; tubuni, na kuiamini Injili.”
Wapendwa wana wa Mungu, maisha yanayoongozwa na malengo
lazima yasukumwe na kauli mbiu yenye mwelekeo wa umilele. Ufupisho wa kile
ambacho Kristo anakifanya ndani ya maisha yetu kimejumuishwa katika kauli mbiu
hii: “Wakati umetimia, na ufalme wa Mungu umekaribia; tubuni, na
kuiamini Injili,” Mk 1:15. Kauli mbiu hii ya Yesu imeweka wazi muda maalum wa
kuanza mradi huu wa umilele, kudumu kwa mradi huu kabla ya kufikia umilele,
mapaswa ya mradi huu, na kielelezo
kinacho sadifu mradi huu.
Kwa
ujumla maisha ya hapa duniani ni ya muda mfupi ukilinganisha na umilele. Hivyo
kauli mbiu hii ya Yesu inatutaka kutambue ukweli huu wa uchache wa muda tungali
hapa duniani. Ninapopata nafasi ya kuishi hata kwa dakika moja nielewa muda huo
haujirudii tena na nishapunguza muda wa maandalizi kuelekea umilele. Kwa maana
nyingine yanipasa kuishi nikijua nina muda na wakati huu tu katika maisha
yangu.
Wakati
kwa Mkristo umetimilizwa na Kristo mwenyewe kwa tendo la Neno kufanyika mwili
na kukaa kwetu, Yoh 1.14. “Mungu, ambaye alisema zamani na baba zetu katika manabii kwa
sehemu nyingi na kwa njia nyingi, mwisho wa siku hizi amesema na sisi katika
Mwana, aliyemweka kuwa mrithi wa yote, tena kwa yeye aliufanya ulimwengu,” Ebr
1:1-2. Hivyo Kristo ndiye dira ya maisha yako na yaliyo mafupi hapa duniani
katika dhana nzima ya kujiandaa na umilele. Ufalme wa Mungu umekaribia kwa
sababu Neno huyu, yaani, Emmanueli, ni Mungu pamoja nasi, Mt 1:23. Mungu ambaye
hapo mwanzo alioneka yupo mbali sana na watu sasa kamwilishwa na kuwa sawa na
sisi isipokuwa hakutenda dhambi, 1Pet 2:22.
Pamoja na
ukweli kwamba sasa tupo karibu sana na Mungu kupitia mwanaye Yesu Kristo, hiyo
haimaanishi wakovu ni bwerere! La hasha! Yatupasa kutubu na kuamini habari
njema, yaani Injili. Toba yetu ni kuanza upya na Mungu kupitia mwanaye Mpenzi
Yesu Kristo. Ni kuuvua utu wetu wa zamani na kuuvaa utu mpya kama asemavyo
Paulo Mtume. “Ikiwa mlimsikia mkafundishwa katika yeye, kama kweli ilivyo
katika Yesu, mvue kwa habari ya
mwenendo wa kwanza utu wa zamani, unaoharibika kwa kuzifuata tamaa zenye
kudanganya; na mfanywe wapya
katika roho ya nia zenu; mkavae
utu mpya, ulioumbwa kwa namna ya Mungu katika haki na utakatifu wa kweli,” Efe
4:22-24. Habari njema iwe kweli habari njema kwako na wote wale waliokata tamaa
katika maisha yao, wewe ukiwa mjumbe wa habari hiyo yenye matumaini. Kristo
ndiye tumaini jipya kwetu sote katika safari yetu hii kuelekea maisha ya
umilele.
Hivyo
ishi yetu leo siyo tena ishi ile inayosukumwa na mitazamo ya watu, ikiwa ni
pamoja na mila na desturi zetu zilizopotofu. Kuishi kwetu leo ndani na katika
Kristo siyo kuwapendezesha wanadamu, bali Mungu mwenyewe, Gal 1:10. Tatizo hili
tunaliona katika somo letu la kwanza Hana mke wa Halkana anakosa furaha na
kuhuzunika kwa vile hakuwa na mtoto. Ni kweli kabisa kama mama ilimpasa kuwa na
mtoto kadiri mitizamo, mila na desturi. Hata leo zipo ndoa nyingi hazina amani
kwa vile tu hawakubahatika kupata watoto. Ndoa Takatifu haikamilishwi kwa kuwa
na watoto. Watoto ni matunda ya Ndoa Takatifu, na hata bila watoto ndoa hiyo
hubaki kuwa Takatifu. Kitu cha muhimu katika ndoa ni upendo wa dhati kati ya
mume na mke na kusindikizana katika Utakatifu. Halkana anamkumbusha mkewe Hana
msingi huu wa ndoa ambao wengi uingiwa upofu na kutokuuona. “Elkana mumewe akamwambia,
Hana, unalilia nini? Kwani huli chakula? Kwa nini moyo wako una huzuni? Je!
Mimi si bora kwako kuliko watoto kumi?” Isam 1:8.
Vile vile
ishi letu leo siyo tena ile kwamba ulimwengu huu ndiyo kikomo cha kila kitu na
kutufanya kuwekeza hapa duniani. Yote tuyafanyayo, tena kwa ukamilifu wake,
yawe ni moja ya njia ya kutufikisha katika umilele ambao ndio kikomo cha kila
kitu. Tumeumbwa na Mungu tuishi milele kama Yeye alivyo wa milele. Ukitizama
kwa makini chagua ya Yesu kwa wale Mitume wake utaona ukweli huu. Ni kama vile
Yesu anataka kusema hivi, “najua kazi yako ndiyo kila kitu kwako, ila hili
nikuambialo ni muhimu na lina umilele ndani yako.” Yesu hakudharau waliyokuwa
wanayafanya kabla wale aliowachagua, bali aliwaonyesha lililomuhimu na lakudumu
katika kufanya. “Yesu akawaambia, Njoni mnifuate, nami nitawafanya kuwa wavuvi wa
watu,” Mk 1:17. Pamoja na sintofahamu hii, Mitume na wanafunzi hawa wa Yesu
wanaacha kazi zao na kumfuata Yesu. “Mara wakaziacha nyavu zao, wakamfuata,” Mk 1:18. Nani kati yetu
leo atakuwa tayari kuacha mkate wake, kazi yake nzuri na yenye mshahara ulio
nona na kumfuata mtu tu asiyemjua vizuri?
Ni changamoto kubwa sana!
Ila ndugu
yangu tuliyesafiri wote katika tafakari hii, kama unataka kuishi katika
umilele, yakupasa kuiisikia sauti ya Mungu. Yote tuliyonayo hapa duniani licha
ya umuhimu wake, hayana umilele. Tunaangaika sana kuvipata vitu hivyo tena kwa
jasho na gharama kubwa, ila ukweli ni kwamba ipo siku tutaviacha na kwenda bila
kitu. Kumbe tumia muda wako vizuri katika utume wako kwa sababu hilo litadumu
milele hata baada ya maisha yako hapa duniani.
Tumsifu
Yesu Kristo!
Msijiwekee
hazina duniani, nondo na kutu viharibupo, na wevi huvunja na kuiba; bali jiwekeeni hazina
mbinguni, kusikoharibika kitu kwa nondo wala kutu, wala wevi hawavunji wala
hawaibi; kwa kuwa hazina yako
ilipo, ndipo utakapokuwapo na moyo wako,” Mt 6:19-21
No hay comentarios:
Publicar un comentario