jueves, 14 de enero de 2016

TAFAKARI: JUMATANO WIKI YA 1 YA MWAKA-C

JUMATANO WIKI YA 1 YA MWAKA-C
13/1/2016
Somo: 1Sam 3:1-10, 19-20
Zab: 40:2, 5, 7-8a, 8b-9, 10
Injili: Mk 1:29-39
Nukuu:
Basi Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake,” 1Sam 3:7 

Bwana akamwita Samweli mara ya tatu. Naye akaondoka akamwendea Eli, akasema, Mimi hapa; kwa maana uliniita. Ndipo Eli akatambua ya kuwa Bwana ndiye aliyemwita yule mtoto,” 1Sam 3:8

Kwa hivyo Eli akamwambia Samweli, Enenda, kalale; itakuwa, akikuita, utasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia. Basi Samweli akaenda akalala mahali pake,” 1Sam 3:9

Bwana akaja, akasimama, akaita vile vile kama kwanza, Samweli! Samweli! Ndipo Samweli akasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia,” 1Sam 3:10 

Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia habari zake,” Mk 1:30

Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia,” Mk 1:31

Akawaambia, Twendeni mahali pengine, mpaka vijiji vilivyo karibu, nipate kuhubiri huko nako; maana kwa hiyo nalitokea,” Mk 1:38

TAFAKARI:Samweli alikuwa hamjui Bwana bado, na neno la Bwana lilikuwa bado halijafunuliwa kwake.”

Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na kwamba kumjua Mungu ni hatua kama tulivyoona kwa Samweli, zipo njia mbili zinazoweza kutupeleka katika uwepo wa Mungu na ufahamu wake. Njia ya kwanza ni ‘kukisia.’ Eli anakuwa msaada kwa Samweli katika kutafsiri tendo lile la kusikia sauti ikimwita mara tatu. Kwa hivyo Eli akamwambia Samweli, Enenda, kalale; itakuwa, akikuita, utasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia,” 1Sam 3:9a. Namna ya kuita kwake Mungu kulivyo kwa pekee, Eli moja kwa moja anakisia kwa namna hiyo huyo atakuwa Mungu.

Kwa kiasi kikubwa kila siku ya maisha yetu tunakumbana na matukia mbalimbali na mengine hatuelewi sawa sawa. Mungu anapenda tumtafute wenyewe hadi tumpate. Tukimpata Mungu kwa kumtafuta si rahisi kuachana naye. Na Mungu hupenda kukutana nasi katika matukio mbalimbali, na wakati mwingine matukio hayo huwa ya huzuni na kukata tamaa. Mungu kwa kufanya hivyo siyo kwamba haoni wala hatujui, la hasha! Mungu anatujua hata kabla ya kuzaliwa kwetu. Hivyo uwepo wako leo ni kusudi kubwa sana la Mungu. Mungu anataka katika mahangaiko hayo sasa umtafute ili ufanye kazi naye.

Kila tukio linalotokea katika maisha yako lichukulie kama somo la kumfahamu Mungu zaidi na vizuri. Usikubali kamwe lawama ikawa ndiyo salamu yako ya kwanza unapokabiliana na tatizo lolote lile. Salamu yako ya kwanza muulize Mungu hivi: katika tukio hili wataka kunifundisha nini Ee Mungu wangu? Kumbe jambo la kwanza yatupasa kupokea hali hiyo. Kwa msaada wa Eli, Samweli anapokea hali ile kwanza. Bwana akaja, akasimama, akaita vile vile kama kwanza, Samweli! Samweli! Ndipo Samweli akasema, Nena, Bwana; kwa kuwa mtumishi wako anasikia,” 1Sam 3:10.

Ndugu yangu, usipolipokea NENO hutoweza kulitafakari, kulitafiti, kulikumbuka, na kulishirikisha kwa wengine kama moja ya utume wako. Ni muhimu kuelewa ni Mungu tu anayetuita kwa sababu ilimpendeza kutuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Kazi yangu na yako ni kuwasaidia wengine waelewe sauti ile ya Mungu anamwita au kuwaita. Tusiwe wepesi wa kukatisha safari za wito kwa wengine kwa vigezo ambavyo wakati mwingine ni ubinadamu wetu tena usio na chembe ya umungu ndani yake.

Njia ya pili ya kutupeleka katika uwepo wa Mungu na ufahamu wake ni ‘ufunuo.’ Kwa namna yoyote ile na kwa yeyote yule, Mungu huweza kujifunua kwake. Kwa vile kila mmoja wetu yupo duniani hapa kwa kusudi maalum kadiri ya mpango wa Mungu, ni Mungu huyo huyo ujifunua kwake kwa lengo la kumshirikisha makuu yake. Tendo hili la UFUNUO ndilo lililoibeba historia nzima ya wokovu wetu. 

Wapendwa wana wa Mungu, kuwepo pale Mungu alipo ni kuwa ndani na katika Kristo kwa sababu ya kile akisemacho Mungu kuhusu mwanaye, na kile mwana akisemacho kuhusu Mungu Baba. Siku ya Ubatizo wa Bwana tuliona kile Mungu alichokisema kuhusu mwana wake. Kisha likatokea wingu, likawatia uvuli; sauti ikatoka katika lile wingu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, msikieni yeye,” Mk 9:7. Je, ni nani unayemsikiliza? Kwa upande wa pili kile asemacho Mwana, yaani Yesu kuhusu Baba yake tunaweza kusoma, Yoh 8:12-59. Katika mahusiano ya Mwana na Baba, Yesu anasema nini kuhusu hukumu? “Nami nijapohukumu, hukumu yangu ni kweli; kwa kuwa mimi si peke yangu, bali ni mimi na yeye aliyenipeleka,” Yoh 8:16. Kumbe kujua pale Mungu alipo pamoja na ufahamu wake ni kuwa na Kristo Yesu.

Ufunuo huo wa Mungu wajionyesha moja kwa moja ndani na katika Kristo katika Injili ya leo. Tunaona uponyaji wa Mama Mkwe wa Simoni Petro ulivyokuwa. Naye mkwewe Simoni, mamaye mkewe, alikuwa kitandani, hawezi homa; na mara wakamwambia habari zake. Akamkaribia, akamwinua kwa kumshika mkono, homa ikamwacha, akawatumikia,” Mk 1:30-31. Je, ulipoguswa na Mungu na kuponywa, ulikuwa tayari kutumika kama shukrani kwa Mungu? Huyu ndiye Mungu aliye hai na atupaye uzima. Mungu huyu anayo mamlaka pia ya kuuchukua uzima huo. Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu,” 1Sam 2:6-7.

Pamoja na ufunuo huo wa wazi wa Neno kufanyika mwili na kukaa kwetu, lengo kubwa sasa ni sisi kumjua Mungu na kumwelekea yeye katika umilele. Pamoja na ishara zote alizozifanya kwa kuwaponya watu wenye shida mbalimbali, Mk 1:34, Yesu anawakumbusha wanafunzi wake, na kwa upande mwingine tukiwa wewe na mimi kile alichokijia hapa duniani. Naye Akawaambia, Twendeni mahali pengine, mpaka vijiji vilivyo karibu, nipate kuhubiri huko nako; maana kwa hiyo nalitokea,” Mk 1:38. Kwa ubatizo wako wewe ni mmisionari. Hivyo peleka habari njema ya wokovu ukianza hapo ulipo.

Tumsifu Yesu Kristo!

Kwa hiyo ndugu, jitahidini zaidi kufanya imara kuitwa kwenu na uteule wenu; maana mkitenda hayo hamtajikwaa kamwe,” 2Pet 1:10


No hay comentarios:

Publicar un comentario