JUMATATU WIKI YA 2 YA MWAKA-C
Somo: 1Sam 15:16-23
Zab: 50:8-9, 16bc-17, 21, 23
Injili: Mk 2:18-22
Nukuu:
“Basi Samweli akasema, Ingawa ulikuwa mdogo machoni pako
mwenyewe, je! Hukufanywa kuwa kichwa cha kabila za Israeli? Naye Bwana akakutia
mafuta uwe mfalme wa Israeli,” 1Sam 15:17
“Mbona, basi, hukuitii sauti ya Bwana, bali ukazirukia nyara
ukafanya yaliyo maovu machoni pa Bwana?” 1Sam
15:19
“Sauli akamwambia Samweli, Hakika mimi nimeitii sauti ya
Bwana, nami nimemleta Agagi, mfalme wa Waamaleki, tena nimewaangamiza Waamaleki
kabisa,” 1Sam 15:20
“Naye Samweli akasema, je! Bwana huzipenda sadaka za
kuteketezwa na dhabihu Sawasawa na kuitii sauti ya Bwana? Angalia, kutii ni bora
kuliko dhabihu, Na kusikia kuliko mafuta ya beberu,” 1 Sam 15:22
“Kwani kuasi ni kama dhambi ya uchawi, Na ukaidi ni kama
ukafiri na vinyago; Kwa kuwa umelikataa neno la Bwana, Yeye naye amekukataa
wewe usiwe mfalme,” 1Sam 15:23
“Nao wanafunzi wake
Yohana na Mafarisayo walikuwa wakifunga; basi walikuja, wakamwambia, Kwani
wanafunzi wa Yohana na wanafunzi wa Mafarisayo hufunga, bali wanafunzi wako
hawafungi?” Mk 2:18
“Yesu akawaambia,
Walioalikwa arusini wawezaje kufunga maadamu bwana-arusi yupo pamoja nao? Muda
wote walipo na bwana-arusi pamoja nao hawawezi kufunga,” Mk 2:19
“Hakuna mtu ashonaye
kiraka cha nguo mpya katika vazi kuukuu; ikiwa ashona, kile kipya kilichotiwa
huliharibu lile vazi kuukuu, na pale palipotatuka huzidi,” Mk 2:21
“Wala hakuna mtu
atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; ikiwa atia, ile divai mpya itavipasua
viriba vile, divai ikamwagika, vile viriba vikaharibika. Bali hutia divai mpya
katika viriba vipya,” Mk 2:22
TAFAKARI: “Kutii ni
bora kuliko dhabihu.”
Wapendwa wana wa Mungu, kutii ni kutambua kuwa kuna kitu
zaidi ya kile ulicho ambacho kwa namna moja au nyingine kinaathiri uwepo wako
hasi au chanya. Kutii hakuna gharama yoyote kama utatambua kile ulicho na kile
kilicho zaidi ambacho kina uhusiano nawe katika kuwa, kutenda, kufikiri na
kuamua. Kati ya mambo magumu kufanya binadamu ni kutii. Kutii kunamlazimu mtu
wakati mwingine kwenda kinyumbe na ufahamu wake kiakili na kimantiki. Kutii
wakati mwingine kutakulazimu kuachilia yake uyafahamuyo kiufasaha. Kutii ni
kujisalimisha kuliko kwa hiari kwa kile ukifahamucho kwa undani. Kutii ni
kuruhusu jambo lingine lifanyike hata kama lile ulifanyalo una uhakika nalo.
Mfalme Sauli anakosa utii mbele za Mungu kwanza kabisa kwa
kutokutambua yeye kama Mfalme yupo pale si kwa sababu yake binafsi bali kwa
kuchakuliwa na Mungu na kufanya kazi ya Mungu. “Basi Samweli akasema, Ingawa ulikuwa mdogo machoni pako
mwenyewe, je! Hukufanywa kuwa kichwa cha kabila za Israeli? Naye Bwana akakutia
mafuta uwe mfalme wa Israeli,” 1Sam 15:17.
Sauli ni Mfalme wa Israeli kwa mkono wa Mungu mwenyewe.
Ndani
yetu Mungu katuwekea kwa namna ya pekee dhamiri yenye kutuongoza katika
kuchagua lililo jema. Kwa nafasi uliyonayo katika jamii inakuruhusu na kukuzuia
baadhi ya mambo kuyafanya na kutokuyafanya. Utii huja pale unapoweza kuizuia
nafsi yako kufanya kile ambacho kwa nafasi na uwezo wako unaweza kukifanya.
Kosa la Sauli ni kuruhusu kwa nafasi yake na cheo chake watu wafanye yale
yaliyokatazwa kufanyika hata kama uhalalishwaji wake unawezwa kufanywa kutokana
na mamlaka ya mtu aliyo nayo. Angalia utetezi wa Sauli katika hili: “Ila watu waliteka nyara, kondoo na ng'ombe
walio wazuri, katika vitu vilivyowekwa wakfu, kusudi wavitoe dhabihu kwa Bwana,
Mungu wako, huko Gilgali,” 1Sam 15:21.
Yapo mambo mengi ambayo tunaondolewa uhalali wake wa kuwa
kile tulicho kwa sababu ya kutokutii. Mfano: Katiba ya nchi ni matokeo ya
mapendekezo ya watu ya namna watakavyo kuongozwa, na kujiwajibishwa wenyewe
pale wanaposhindwa kufanya yale waliyokubaliana. Tunapowachagua viongozi wetu,
mfano Rais, tunategemea ailinde Katiba na awe mfano wa utii katiba hiyo na awe
mfano wa kuigwa. Lakini kitu tunachokiona hadi sana na hasa katika Taifa letu
la Tanzania, hawa tuliowapa dhamana ya kuilinda na kuitetea katiba ndio
wanakuwa wa kwanza kuibadili na kuitafsiri ili kukidhi matakwa yao binafsi au
vyama wanavyoviwakilisha. Kwa kufanya hivyo hata kama utaendelea kuwa mtawala
kwa nguvu ya mtutu wa bunduki kuwaogopesha watu, hautakuwa halali kwa kile
unachokiwakilisha mbele ya umma uliokuweka. “Bwana huzipenda sadaka za
kuteketezwa na dhabihu Sawasawa na kuitii sauti ya Bwana? Angalia, kutii ni
bora kuliko dhabihu, Na kusikia kuliko mafuta ya beberu,” 1 Sam 15:22. Mtakatifu Agustino aliwahi kusema hivi,
“Vox populi, vox Dei,” akimaanisha “Sauti ya watu ni Sauti ya Mungu. Kuendelea
kujinasibu kuwa kiongozi katika mazingira kama haya ya ujanja ujanja ni
kukataliwa na watu na Mungu pia. Adhabu yake ni Kubwa.
Sauli anakutwa na tatizo hilo nililolisema hapo juu. Hivyo
Mungu anamkataa licha ya kwamba anajinasibu kama Kiongozi. “Kwani kuasi ni kama dhambi ya uchawi, Na ukaidi
ni kama ukafiri na vinyago; Kwa kuwa umelikataa neno la Bwana, Yeye naye
amekukataa wewe usiwe mfalme,” 1Sam 15:23. Je, hali ya kisiasa Zanzibar ya leo
inatofauti na ule ufalme wa Sauli?
Tutafakari!
Injili ya leo tunaona wanafunzi wa Yesu wanashitumiwa kwa
kutokufunga kadiri ya mila na desturi za kiyahudu. Yesu anawakumbusa wasome
alama za nyakati. Wazo kuu hapa ni hili: nini hatma ya kile unachokifanya? Kama Yesu ndiye kila
kitu, je wale walio karibu naye wafuate lipi? Ni kwa mtazamo huo Yesu anawajibu, “Walioalikwa arusini wawezaje kufunga
maadamu bwana-arusi yupo pamoja nao? Muda wote walipo na bwana-arusi pamoja nao
hawawezi kufunga,” Mk 2:19. Hivyo kile wasichokijua jibu lake ni Kristo. Wakati
wa kuyafanya hayo utakuja kadiri na mila na desturi zetu utakuja. “Lakini siku
zitakuja watakapoondolewa bwana-arusi, ndipo watakapofunga siku ile,” Mt 2:20.
Kristo
ndiyo kila kitu kwetu. Yesu anataka tuanze yote naye. Yesu hataki habari za
historia zetu, bali utayari wetu wa kuanza naye katika kweli na haki. “Wala hakuna mtu atiaye divai mpya katika viriba vikuukuu; ikiwa
atia, ile divai mpya itavipasua viriba vile, divai ikamwagika, vile viriba
vikaharibika. Bali hutia divai mpya katika viriba vipya,” Mk 2:22. Je, upo
tayari kuanza yote na Kristo? Basi kuwa wazi kuhusu wewe mwenyewe na jiachie
mikoni mwa Kristo.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Nayaweza mambo yote
katika yeye anitiaye nguvu,” Flp 4:13
No hay comentarios:
Publicar un comentario