jueves, 14 de enero de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 1 YA MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 1 YA MWAKA-C
14/1/2016
Somo: 1Sam 4:1-11
Zab: 44:10-11, 14-15, 24-25
Injili: Mk 1:40-45
Nukuu:
Nao Wafilisti wakajipanga juu ya Israeli; na walipopigana, Israeli wakapigwa mbele ya Wafilisti; wakauawa watu wa jeshi lao lililokuwa uwandani wapata watu elfu nne,” ISam 4:2

Hata watu walipofika kambini, wazee wa Israeli wakasema, Mbona Bwana ametupiga leo mbele ya Wafilisti? Twende tukalilete sanduku la agano la Bwana toka Shilo hata huku, lije kati yetu, na kutuokoa katika mikono ya adui zetu,” 1 Sam 4:3 

Basi wakatuma watu kwenda Shilo, nao wakalileta toka huko sanduku la agano la Bwana wa majeshi, akaaye juu ya makerubi; na Hofni na Finehasi, wana wawili wa Eli, walikuwako huko pamoja na sanduku la agano la Mungu,” 1Sam 4:4

Na sanduku la agano la Bwana lilipoingia kambini, Israeli wote wakapiga kelele kwa sauti kuu, hata nchi ikavuma,” 1Sam 4:5

 “Ole wetu! Ni nani atakayetuokoa na mkono wa miungu hawa walio hodari? Hawa ndio miungu waliowapiga Wamisri kwa mapigo ya kila namna jangwani,” 1Sam 4:8 

Iweni hodari, na kufanya kiume enyi Wafilisti, msije mkawa watumwa wa Waebrania, kama wao walivyokuwa watumwa wenu; fanyeni kiume, mkapigane nao,” 1Sam 4:9 

Wafilisti wakapigana nao, Israeli wakapigwa, wakakimbia kila mtu hemani kwake; wakauawa watu wengi sana; maana katika Israeli walianguka watu thelathini elfu wenye kwenda vitani kwa miguu,” 1Sam 4:10 

Akaja kwake mtu mwenye ukoma, akamsihi na kumpigia magoti, na kumwambia, Ukitaka, waweza kunitakasa,” Mk 1:40

Naye akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika. Na mara ukoma wake ukamtoka, akatakasika,” Mk 1:41-42

Akamkataza kwa nguvu, akamwondoa mara, akamwambia, Angalia, usimwambie mtu neno lolote, ila enenda zako ukajionyeshe kwa kuhani, ukatoe alivyoamuru Musa kwa kutakasika kwako, iwe ushuhuda kwao,” Mk 1:43-44

TAFAKARI: “Mungu wetu si wakuchezewa na wala si wamajaribio. Mungu hutenda kadiri unavyojiachia kwake bila kujibakiza.”

Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na uovu tulionao, hali hiyo isiwe kibali cha kuendelea kufanya uovu tukijidanganya kuwa Mungu hayaoni matendo yetu. Mungu wetu ni Huruma, Upendo, Msahama, Haki na Kweli. Kukaa kwake kimya pale tunapomkosea kunathibitisha mambo makuu mawili: kwanza, kunathibisha ukweli wa sifa hizo nilizozitaja kuhusu Mungu. Pili, Mungu hataki tuangamie bali tuongoke na kumrudia. Mungu hutupa muda wa kutosha kwa ajili ya wongofu wetu. Bwana wa Majeshi asema hivi, Tena, mtu mwovu atakapoghairi, na kuuacha uovu wake alioutenda, na kutenda yaliyo halali na haki, ataponya roho yake, nayo itakuwa hai. Kwa sababu atafakari, na kughairi, na kuyaacha makosa yake yote aliyoyatenda, hakika ataishi, hatakufa,” Eze 18:27-28. Hivyo Mungu hafurahii hata kidogo kuangamia kwa mtu kutokana na dhambi zake. Tatizo ni pale tunapocheza na Mungu.

Wana wa Israeli wanashindwa katika vita dhidi ya Wafilisti kwa sababu wanacheza na Mungu. Wanatumia vibaya Upendo wa Mungu na Huruma yake. Watoto wa Eli ambao kwa kiasi kikubwa ndiyo walikuwa daraja kati ya watu na Mungu, hawakutenda sawa sawa na mapenzi ya Mungu. Walipatumia vibaya patakatifu pa Mungu kwa tamaa zao za mwili na ibada haikufanyika kadiri ya uchaji wa Mungu. Kushindwa kwa wana wa Israeli katika vita kunatokana na historia yao mbaya, tena ikiongozwa na makuhani wao, yaani watoto wa Eli, Hofni na Finehasi. Basi Eli alikuwa mzee sana; naye alisikia habari za mambo yote ambayo wanawe waliwatenda Waisraeli; na jinsi walivyolala na wanawake waliokuwa wakitumika mlangoni pa hema ya kukutania. Akawaambia, Mbona mnatenda mambo kama hayo? Maana nasikia habari za matendo yenu mabaya kwa watu hawa wote,” 1Sam 2:22-23. Kwa mtindo huu wa maisha, kifo cha watoto wa Eli kinatabiriwa. Mungu wetu si wakuchezewa hata kama yupo kimya pale tunapotenda maovu. Na hii ndiyo ishara itakayokuwa kwako, itakayowapata wana wako wawili, Hofni na Finehasi; watakufa wote wawili katika siku moja,” 1Sam 2:34

Mungu wetu siyo Edgar wala Athmani. Hasira ya Mungu ikiwaka hakuna wa kuizuia. Je, Mungu wakulaumiwa? La Hasha! Adhabu ya Mungu kwetu ni matokeo ya kukaidi kwetu. Uhusiano wetu na Mungu hupaswi kuwa ule wa matukio tu. Kama Mungu ni uhai kwetu ni kwa maana hiyo hiyo hatuwezi kuishi bila Mungu. Wana wa Israeli wanamkumbuka Mungu wakati wa shida ilhali hawakuwa waaminifu mbele zake. Mungu anaruhusu wapigwe na hata kupoteza maisha ili liwe somo na fundisho kwao na kwa wengine wenye hofu ya Mungu.Nao Wafilisti wakajipanga juu ya Israeli; na walipopigana, Israeli wakapigwa mbele ya Wafilisti; wakauawa watu wa jeshi lao lililokuwa uwandani wapata watu elfu nne,” ISam 4:2.  Wana wa Israeli wanachukua sanduku la Agano kama kinga yao juu ya adui zao. Hata watu walipofika kambini, wazee wa Israeli wakasema, Mbona Bwana ametupiga leo mbele ya Wafilisti? Twende tukalilete sanduku la agano la Bwana toka Shilo hata huku, lije kati yetu, na kutuokoa katika mikono ya adui zetu,” 1 Sam 4:3. Tendo hili ni sawa na kufanya USHIRIKINA. Ushirikina ni kutegemea nguvu fulani kutoka kitu fulani ambacho kwa kweli hakuna uhusiano nawe kati ya uaminifu wako kimaisha na kitu hicho. Basi wakatuma watu kwenda Shilo, nao wakalileta toka huko sanduku la agano la Bwana wa majeshi, akaaye juu ya makerubi; na Hofni na Finehasi, wana wawili wa Eli, walikuwako huko pamoja na sanduku la agano la Mungu,” 1Sam 4:4

Pamoja na ushirikina huu, wakujifanya wanautambua uwepo wa Mungu, wana wa Israeli walipigwa vibaya na kuuwawa. Wafilisti wakapigana nao, Israeli wakapigwa, wakakimbia kila mtu hemani kwake; wakauawa watu wengi sana; maana katika Israeli walianguka watu thelathini elfu wenye kwenda vitani kwa miguu,” 1Sam 4:10. Mungu wetu hachezewi rafu wala hapewi rushwa. Yanipasa kuishi kweli ndani yangu mwenyewe na kweli hiyo ijithihirishe kwa Mungu kwa matendo yangu mema na yanayompendeza Mungu. Yesu mwenyewe anatukumbusha kweli hii na kusema,Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 7:21. Hivyo tuonje moyoni tunayotamka mdomoni. Hakika tusipoyafanya mapenzi ya Mungu tujiandaye kwa kupigwa mshangao kama walivyopingwa na mshangao wana wa Israeli. Wafilisti wakapigana nao, Israeli wakapigwa, wakakimbia kila mtu hemani kwake; wakauawa watu wengi sana; maana katika Israeli walianguka watu thelathini elfu wenye kwenda vitani kwa miguu. Hilo sanduku la Mungu Likatwaliwa; na Hofni na Finehasi, wale wana wawili wa Eli, wakauawa,” 1Sam 4:10-11. Na hapa ndipo ule unabii ulipotimilika kwamba watoto wote wa Eli watakufa pamoja siku moja.

Wapendwa wana wa Mungu, tumeona kwa undani kwamba Mungu wetu si wakuchezewa na wala si wamajaribio. Sehemu yetu ya pili tumtazame Mungu wetu katika kutenda kwake. Mungu wetu hutenda kadiri unavyojiachia kwake bila kujibakiza. Hivyo Injili yetu ya leo inathibisha jambo hili. Akaja kwake mtu mwenye ukoma, akamsihi na kumpigia magoti, na kumwambia, Ukitaka, waweza kunitakasa,” Mk 1:40. ‘Ukitaka, waweza kunitakasa.’ Maneno haya yamebeba kauli ya kujiachia pasipo shaka. Ni kumruhusu Mungu atende kadiri aonavyo na kumpendeza. Nasi waja wake tunajua wazi kabisa hawezi kutupatia kile kisicho uzuri wake. “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa; kwa maana kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa. Au kuna mtu yupi kwenu, ambaye, mwanawe akimwomba mkate, atampa jiwe? Au akiomba samaki, atampa nyoka? Basi ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! Si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?Mt 7:7-11

Kwa kuona nia ya mtu yule na kujiachia kwake pasipo shaka, Yesu “akamhurumia, akanyosha mkono wake, akamgusa, akamwambia, Nataka, takasika. Na mara ukoma wake ukamtoka, akatakasika,” Mk 1:41-42. Ndugu yangu tuliyesafiri wote katika tafakari hii, wamwamini Yesu wana wa Mungu? Baada ya uponyaji huu, Yesu anamwamuru mtu huyu aende kwa makuhani kujitambulisha. Kujitambulisha kwa makuhani ilikuwa ni wajibu wa lazima ili kupata kibali cha kushiriki tena maisha katika jamii. Wale wote ambao walifikwa na ukoma walitengwa na jamii na kuishi sehemu yao wenyewe. Makuhani ndio waliokuwa na uwezo kisheria wa kuwatenga hawa wenye ukoma na kuwarudishia stahiki zao pale wanapopona ugongwa huu. Akamkataza kwa nguvu, akamwondoa mara, akamwambia, Angalia, usimwambie mtu neno lolote, ila enenda zako ukajionyeshe kwa kuhani, ukatoe alivyoamuru Musa kwa kutakasika kwako, iwe ushuhuda kwao,” Mk 1:43-44. Yesu anathibitisha kweli yeye ni Masiha na Mfalme wa Upendo na Amani, na Haki. Yesu anaturudishia heshima na kutambulika kwetu tena kati ya watu. Hakika wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu,” Rum 8:39. AMINA!

Tumsifu Yesu Kristo!


Kwa kuwa Bwana ndiye mwenye haki, Apenda matendo ya haki, Wanyofu wa moyo watamwona uso wake,” Zab 11:7

No hay comentarios:

Publicar un comentario