3/1/2016
Somo
I: Isa 60:1-6
Zab:
71: 2, 7-8, 10-11, 12-13
Somo
II: Efe 3:2-3a, 5-6
Injili:
Mt 2:1-12
Nukuu:
“Ondoka, uangaze; kwa kuwa nuru yako imekuja, Na utukufu wa
Bwana umekuzukia,” Isa 60:1
“Na mataifa wataijilia nuru yako, Na wafalme kuujia mwanga wa
kuzuka kwako,” Isa 60:3
"Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, Na moyo wako
utatetemeka na kukunjuka; Kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia, Utajiri
wa mataifa utakuwasilia,” Isa 60:5
“ikiwa mmesikia habari
ya uwakili wa neema ya Mungu niliyopewa kwa ajili yenu; ya kwamba kwa kufunuliwa nalijulishwa
siri,” Efe 3:2-3a
“Siri hiyo
hawakujulishwa wanadamu katika vizazi vingine; kama walivyofunuliwa mitume wake
watakatifu na manabii zamani hizi katika Roho; ya kwamba Mataifa ni warithi pamoja
nasi wa urithi mmoja, na wa mwili mmoja, na washiriki pamoja nasi wa ahadi yake
iliyo katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili,” Efe 3:5-6
“Yesu alipozaliwa
katika Bethlehemu ya Uyahudi zamani za mfalme Herode, tazama, mamajusi wa mashariki
walifika Yerusalemu, wakisema, Yuko
wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi? Kwa maana tuliiona nyota yake
mashariki, nasi tumekuja kumsujudia,” Mt 2:1-2
“Basi mfalme Herode
aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye,” Mt 2:3
“Akawapeleka
Bethlehemu, akasema, Shikeni njia, mkaulize sana mambo ya mtoto; na mkiisha
kumwona, nileteeni habari, ili mimi nami niende nimsujudie,” Mt 2:8
“Wakaingia nyumbani,
wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye, wakaanguka wakamsujudia; nao
walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu; dhahabu na uvumba na
manemane,” Mt 2:11
“Nao wakiisha kuonywa
na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode, wakaenda zao kwao kwa njia nyingine,”
Mt 2:12
TAFAKARI:
“Mataifa wataijilia nuru yako, Na
wafalme kuujia mwanga wa kuzuka kwako.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya Epifania, yaani, Toleo la Bwana. Leo
Mama Kanisa anatukumbusha mambo makuu matatu muhimu. Kwanza, ni ufunuo na
udhihirisho wa Kristo katika ulimwengu. Ni ufunuo wa Kristo kwa Mataifa yote ya
ulimwengu ambapo kunajidhihirisha kwa wataalamu wa nyota-Mamajusi wakiongozwa
na nyota ile ya ajabu. “Na mataifa wataijilia nuru yako, Na wafalme kuujia mwanga wa kuzuka
kwako,” Isa 60:3. Wokovu wa Yesu Kristo unajionyesha kama nuru au
mwanga wa alfajiri unaoliondoa jiza na
uvuli wa mauti ambao unautawala ulimwengu. Mungu mwenyewe ndiye pambazuko. Siku ya leo inadhihirika wazi
machoni mwa wanadamu kwamba Kristo ndiye Mfalme wa ulimwengu wote, kwa ajili ya
watu wote, na mmiliki wa utajiri wote. "Ndipo utakapoona na kutiwa nuru, Na moyo
wako utatetemeka na kukunjuka; Kwa kuwa wingi wa bahari utageuzwa kukujia,
Utajiri wa mataifa utakuwasilia,” Isa 60:5. Ukweli
huu unajifunua kwa tunu zile alizopewa mtoto Yesu. “Wakaingia
nyumbani, wakamwona mtoto pamoja na Mariamu mamaye, wakaanguka wakamsujudia;
nao walipokwisha kufungua hazina zao, wakamtolea tunu; dhahabu na uvumba na
manemane,” Mt 2:11.
Toleo hili la Bwana la
dhihirisha ukuhani wa Kristo kwa tunu ile ya uvumba. Huyu ndiye kwa huduma yake
atavitakatifuza vyote katika ulimwengu huu na kuvikomboa. Tendo hili linakwenda
sambamba na sadaka ile atakayo itoa pale Msalabani. Tendo hili la upendo mkubwa
wa Mungu kwa wanadamu leo linajifunua kwa tunu hii ya manemane. Manemane
yanatabiri kifo chake kama ilivyo taratibu za Wayahudi kuhifadhi Maiti na
kuzika. “Akaenda Nikodemo naye, (yule
aliyemwendea usiku hapo kwanza), akaleta machanganyiko ya manemane na uudi,
yapata ratli mia. Basi
wakautwaa mwili wake Yesu, wakaufunga sanda ya kitani pamoja na yale manukato,
kama ilivyo desturi ya Wayahudi katika kuzika,” Yoh 19:39-40. Mambo haya makuu
matatu yanajifunua kwetu leo.
Pili, toleo hili la Bwana, Epifania, linatupa namna ya
kuishi kama Wakristo-wafuasi wa Kristo. Tendo hili ya kufunuliwa na kudhihishwa
kwa Kristo ulimwenguni pote kunatuondoa katika hali ile ya kuwa wakristo wa
kidunia na kutufanya Wakristo wa ulimwengu-wamishionari. Leo tunafanywa
Wakristo wa tabaka la ulimwengu wote na siyo Mkristo wa kidunia. Wakristo wa
kidunia kadiri ya Rich Warren, humtazama Mungu kwanza kwa ajili ya kukidhi haja
zao binafsi. Wanapenda kuhudhuria mikutano na semina za kujenga, lakini
hutawakuta katika mkutano wa umisheni kwa sababu hawaupendelei. Maombi yao
yanajali mahitaji yao binafsi, baraka, na furaha yao. Ni ile imani ya ‘mimi
kwanza.’ Husukumwa mara zote na swali hili: Je, Mungu anawezaje kufanya maisha
yangu kuwa na furaha? Wanapenda kumtumia Mungu kwa malengo yao badala ya wao
kutumiwa kwa malengo yake.
Wapendwa wana wa Mungu, kinyume cha hapo, Wakristo wa
tabaka la ulimwengu mzima wanajua waliokolewa ili watumike na kutayarishwa kwa
ajili ya utume. Wako tayari kupokea jukumu la mtu binafsi na wanafurahia
upendeleo huo wa kutumiwa na Mungu. Wakristo wa tabaka la ulimwengu wote ndio
watu pekee walio hai kikamilifu katika sayari hii. Furaha yao, uhakika na
hamasa yao vinaambukiza kwa sababu wanajua wanafanya tofauti. Wanaamka asubuhi
wakitazamia Mungu kufanya kazi kuwapita katika njia mpya. Je, unataka kuwa
Mkristo wa aina gani? Leo katika toleo la Bwana, Mungu anakualika kushiriki
katika tendo kubwa kuliko yote, la aina yake na la muhimu sana katika
historia-ufalme wake. Hivi ndivyo Yesu alivyowaambia wanafunzi wake kabla ya
kapaa, “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani. Basi, enendeni, mkawafanye mataifa yote
kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba, na Mwana, na Roho Mtakatifu; na kuwafundisha
kuyashika yote niliyowaamuru ninyi; na tazama, mimi nipo pamoja nanyi siku
zote, hata ukamilifu wa dahari,” Mt 28:18-20. Tendo hili linamfanya Kristo
kuendelea kudhihika ulimwenguni kote.
Tatu,
toleo hili la Bwana leo linatukumbusha kwamba Uinjilishaji hapa duniani ni
jambo la pekee. Yapo malengo matano ya Mungu kwa maisha yako hapa duniani.
Mungu alikuumba ili uwe mshiriki katika jamii yake, kielelezo cha tabia yake,
mtu anayetukuza utukufu wake, mtumishi wa neema yake, na mjumbe wa Habari zake
Njema. Katika malengo haya matano, hii la tano linaweza tu kutendwa hapa
duniani. Yale mengine manne utaendelea kuyafanya milele kwa namna fulani. Hivyo
kutangaza Habari Njema ni muhimu sana; una muda mfupi tu wa kushirikisha
wengine ujumbe wa maisha yako na kutimiza utume wako.
Ujumbe wa Mtume Paulo kwa watu wa mataifa anaonyesha mpango
wa wokovu wa Mungu umejifunua wazi kwa Watakatifu, Mitume wake na Manabii. Hata
hivyo watu hawa wa mataifa wameupokea wokovu wa Mungu kwa ufunuo wa Roho. Watu
hawa wa Mataifa ni warithi pia wa ahadi hizi za Mungu. Katika mpango huu wa
wokovu hakuna tena matabaka. Hii ndiyo siri kubwa inayoibuliwa leo kwa tendo
hili la toleo la Bwana. “Siri hiyo hawakujulishwa wanadamu katika vizazi vingine; kama
walivyofunuliwa mitume wake watakatifu na manabii zamani hizi katika Roho; ya kwamba Mataifa ni warithi pamoja
nasi wa urithi mmoja, na wa mwili mmoja, na washiriki pamoja nasi wa ahadi yake
iliyo katika Kristo Yesu kwa njia ya Injili,” Efe 3:5-6. Sote tu huru ndani na katika Kristo. Hivyo tuna
mwili mmoja tu wa Kristo, nalo ndilo Kanisa. Sote tu viungo vya mwili huo mmoja
na Kanisa hilo moja yaani Kanisa la Kristo. Kwa utarajibu na mwono huu, sote
tunashiriki fumbo la Kristo kwa Sakramenti ya Ubatizo. Kristo katika mtazamo
huu ndiye mrithi wa kweli wa ahadi zile za Mungu. “Basi ahadi zilinenwa kwa Ibrahimu na kwa mzao wake. Hasemi, Kwa
wazao, kana kwamba ni wengi, bali kana kwamba ni mmoja, Kwa mzao wako, yaani,
Kristo,” Gal 3:16
Yesu
Kristo Mfalme na Masiha kwa mara ya kwanza anakutana na wana wa ulimwengu wote.
Injili ya Matayo inatajirisha simulizi la toleo la Bwana kwa vielelezo vya
Kibiblia-Maandiko Matakatifu. Unabii ule wa Nabii Mika unatimia, yaani; (nyota
Yakobo, zawadi za dhahabu na uvumba). Kristo ndiye Mfalme Mpya wa Wayahudi, na
Musa mpya, mwakilishi wa ulimwengu mzima. Tendo hili la toleo la Bwana ni
tishio kwa falme nyingine la ulimwengu huu. “Basi mfalme Herode
aliposikia hayo, alifadhaika, na Yerusalemu pia pamoja naye,” Mt 2:3. Habari za
ufalme huu mpya ni habari njema wa masikini na wenye hofu ya Mungu. Wale wote
wasio na hofu ya Mungu huongozwa na mipango miovu ya shetani. Mungu hata hivyo
uiweka mipango yao miovu wazi kwa ajili ya kuwanusuru wanyonge na waadilifu
wake. “Nao wakiisha kuonywa na Mungu katika ndoto wasimrudie Herode,
wakaenda zao kwao kwa njia nyingine,” Mt 2:12. Huyu ndiye Mungu asiyeshindwa
katika mipango yake kwa wapendwa wake. Na huyu ndiye tunayesujudia leo siku ya
Epifania, toleo la Bwana.
Je,
ungepata leo nafasi ya kumtolea Yesu tunu ungempa kitu gani? Mathias Makyadi
kutoka Kongo alikuwa ni mmoja wa wanavisi kati ya wanovisi kumi wa shirika
fulani la kimisionari. Kila wiki mmoja wa wanovisi hupewa muda wa saa moja
kutafakari mbele ya Ekaristi Takatifu. Waweza kutumia muziki wa ala ukuongoze
katika tafakuri yako au ukimya tulivu.
Tendo la
kufanya tafakuri lilikuwa gumu sana kwa Mathias Makyadi. Hivyo ilipofika zamu
yake ulikuwa mtihani mkubwa sana. Hata hivyo Mathias alimwambia Yesu wa
Ekaristi hivi, “kutafakari kwa ukimya kadiri ya utaratibu uliozoeleka mimi
siwezi. Hivyo naomba nikupe kile nilichonacho kama shukrani na upendo wangu
kwako.” Mathias aliondoka na kwenda chumbani mwake akachukua redio kaseti yake
na kuweka mziki wa kwao “ndombolo” na kucheza kwa nguvu zake sote, kwa kutumia
akili yake yote, na moyo wake wote.
Mara
aliingia Mlezi wake kwenye kile kikanisa
kwani kelele zele zilisikika kila mahali katika nyumba ile ya Unovisi.
“Kwa nini unafanya kelele mahali hapa na kucheza mbele ya Yesu wa Ekaristi?”
Mlezi wa wanavisi alisema kwa jazba na hasira. “Baba, hiki ndicho ninachoweza
kumpa Yesu wa Ekaristi kilicho cha thamani kubwa na ninachoweza kumpa kwa moyo
wangu wote,” Mathias amjibu Mlezi wake kwa upole. Baada ya kuyatafakari maneno
yale ya Mathias, Mlezi wake aliondoka bila ya kusema neno.
Wapendwa
wana wa Mungu, kila mmoja wetu anacho cha kumpa Yesu leo kama walivyofanya
Mamajusi na alivyofanya Mathias. Lakini zaidi ya yote, mimi na wewe tunaweza
kumpa dhambi zetu kwani ndiyo mali yetu halali. Tunapoutazama mwaka huu wa
huruma ya Mungu, tutazame mali hii halali tuliyonayo. Kristo Mfalme, ni Huruma,
Upendo, Msamaha, Haki, na Kweli. Zawadi hii ataibadilisha na kuwa nyeupe kama
sufu. “Haya,
njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa
nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu,” Isa
1:18
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Na majeshi yaliyo
mbinguni wakamfuata, wamepanda farasi weupe na kuvikwa kitani nzuri, nyeupe,
safi,” Ufu 19:14
No hay comentarios:
Publicar un comentario