JUMAPILI WIKI YA 2 YA MWAKA-C
17/1/2016
Somo I: Isa 62:1-5
Zab: 96: 1-3, 7-8, 9-10
Somo II: 1Kor 12:4-11
Injili: Yoh 2:1-12
Nukuu:
“Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili ya Yerusalemu
sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu wake kama taa
iwakayo,” Isa 62:1
“Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule,” 1Kor 12:4
“Lakini kila mmoja
hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana,” 1Kor 12:7
“lakini kazi hizi zote
huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule, akimgawia kila mtu peke yake kama
apendavyo yeye,” 1Kor 12:11
“Yesu naye alikuwa
amealikwa arusini pamoja na wanafunzi wake,” Yoh 2:2
“Hata divai ilipowatindikia, mamaye Yesu akamwambia, Hawana divai,” Yoh 2:3
“Yesu akamwambia,
Mama, tuna nini mimi nawe? Saa yangu haijawadia,” Yoh 2:4
“Mamaye akawaambia
watumishi, Lo lote atakalowaambia, fanyeni,” Yoh 2:5
“Basi kulikuwako huko
mabalasi sita ya mawe, nayo yamewekwa huko kwa desturi ya Wayahudi ya
kutawadha, kila moja lapata kadiri ya nzio mbili tatu,” Yoh 2:6
“Yesu akawaambia,
Jalizeni mabalasi maji. Nao wakayajaliza hata juu,” Yoh 2:7
“Naye mkuu wa meza
alipoyaonja yale maji yaliyopata kuwa divai, (wala asijue ilikotoka, lakini
watumishi walijua, wale walioyateka yale maji), yule mkuu wa meza alimwita
bwana arusi, akamwambia,
Kila mtu kwanza huandaa divai iliyo njema; hata watu wakiisha kunywa sana ndipo
huleta iliyo dhaifu; wewe umeiweka divai iliyo njema hata sasa,” Yoh 2:9
TAFAKARI: “Mama, tuna nini mimi nawe?
Saa yangu haijawadia.”
Wapendwa
wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 2 ya mwaka ‘C’
wa Kanisa. Leo kwa namna ya pekee Mama Kanisa anatualika kutafakari kwa undani
Upendo na Huruma ya Mungu kupitia Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo. Pia ni kwa Upendo
na Huruma hii ya Mungu inaakisi kilele chake, yaani, sadaka ya Kristo pale
Msalabani. Kuuthamini na kuuishi upendo na huruma hii ya Mungu, yanipasa mimi
na wewe kuijua “SHAPE” au “KAMOUHUMA” yako. SHAPE ni ufupisho wa maneno haya:-
S, ‘Spiritual gifts’-Karama za kiroho ulizo nazo, H, ‘Heart-Moyo,
ujue moyo wako, A, ‘Abilities’-Uwezo, jua uwezo wako, P, ‘Personality’-Hulka,
jua nafsi na mapungufu yako, E, ‘Experience’-Mang’amuzi, yatumie vyema
mang’amuzi yako uliyoyapata katika maisha. Kama ilivyo ‘mwana wa Adamu asivyokuja
kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi, Mt 20:28,
nasi kwa kujua ‘SHAPE au KOMOUHUMA’ yetu tutumika kama yeye alivyotumika kwa
ajili yetu.
Kwa kujua
SHAPE au KAMOUHUMA yako, Mungu huzimimina baraka zake zisizo na kipimo kwako
kwa sababu Mungu kamwe habariki pasipo na kitu wala pasipo na juhudi njema za
Mtu husika. Leo Mama yake Yesu, Yesu mwenyewe, na wanafunzi wake wanaalikwa
kwenye Harusi huko Kana. Wakiwa katikati ya shamrashamra za Harusi ile divai
inawaishia. Mama Bikira Maria anakwenda moja kwa moja kwa Yesu na kumwambia
hawana divai, Yoh 2:3. Kwa nini Bikira
Maria anakwenda kwa Yesu? Mama Bikira Maria anakwenda kwa mwanaye kwa sababu ya
‘mang’amuzi’ aliyonayo juu ya mtoto wake. Bikira Maria anajua ‘uwezo’ wa mtoto
wake. Pamoja na ukweli huu, “Yesu akamwambia,
Mama, tuna nini mimi nawe? Saa yangu haijawadia,” Yoh 2:4. Maneno haya “Mama,
tuna nini mimi na nawe,” ni maneno mazito sana na yenye kubeba ujumbe mzito.
Yesu
anataka Mama yake na wanafunzi wake waelewe kwamba kwa tukio lile wao ni
waalikwa tu kwanye harusi au karamu ile. Tendo hili linawakumbusha Mama Bikira
Maria na wanafunzi wake “uwezo” na hali waliyonayo kutokana na ubinadamu wao.
Kwa uwezo wao kama wanadamu wanaweza kufanya tu yaliyo ndani ya uwezo huo wa kibinadamu.
Nasi kwa namna ya pekee, Yesu anatukumbusha uwezo na ubinadamu wetu. Tuwapo
hapa duniani sote ni waalikwa na kwa zawadi ya uhai ni kama harusi au karamu
ambayo kwa namna ya kuishi lolote laweza kutokea katika safari yetu hii. Pamoja
na ukweli huu ambao mimi na wewe yatupasa kuufahamu, Yesu anaenda mbele zaidi
na kusema, “Saa yangu haijawadia.” Maneno haya yanaakisi utimilifu wa kile
alichokijia hapa duniani. Ukweli huu utatupeleka kwenye utimifu wa upendo na
huruma ya Mungu pale Msalabani ambapo kwenye mti ule wa msalaba ndipo
utakapotundikwa wokovu wetu.
Baada ya
maneno hayo machache na mazito ya Yesu, Mama Bikira Maria hajibizani na Yesu
kwa sababu ndani ya “Moyo” wake Mama Bikira anayajua mang’amuzi juu ya mtoto
wake, na uwezo wake. Bikira Maria akijua ujumbe ushafika kwa mwanaye-“Message
send and delivered,” na akijua hawezi kumwangusha, Maria Bikira anakwenda moja
kwa moja kwa watumishi wa ile harusi na kuwaambia, “Lo lote atakalowaambia,
fanyeni,” Yoh 2:5. Mama Bikira Maria hapa anatukumbusha uwezo wa Mwanaye na hakika hatupaswi
kuwa na shaka. Yeye kama Mama anamfahamu vizuri mtoto wake kwani ameshiriki kwa
namna ya pekee kabisa katika makuzi yake. Tunapotindikiwa katika maisha yetu,
tukumbuke ujumbe huu wa Bikira Maria kwa wale watumishi wa Kana, “lo lote
atakalowaambia, fanyeni.” Yesu anatuambia mambo sita ya muhimu:-
- “Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa
kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe,” Yoh 6:35
- “Aniaminiye mimi, kama vile maandiko
yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake,” Yoh 7:38
-“Mimi ndimi huo ufufuo, na
uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je!
Unayasadiki hayo?” Yoh 11:25-26
- “Naye Yesu akapaza sauti, akasema, Yeye
aniaminiye mimi, haniamini mimi bali yeye aliyenipeleka,” Yoh 12:44
- “Mimi nimekuja ili niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu
aniaminiye mimi asikae gizani,” Yoh 12:46
- “Amin, amin, nawaambieni, Yeye aniaminiye mimi, kazi
nizifanyazo mimi, yeye naye atazifanya; naam, na kubwa kuliko hizo atafanya,
kwa kuwa mimi naenda kwa Baba,” Yoh 14:12
Wapendwa wana wa Mungu, haya aliyoyasema Yesu ndiyo
anayotukumbusha Mama Bikira Maria tuyafanye, katika maana ya kumwamini pasipo
shaka mwanaye Mpendwa Yesu Kristo. Kabla ya kufanya kile Yesu atakachokisema,
tunapewa hali halisi ya mazingira yale ya harusi ya Kana ikiwa ni pamoja na
mila na desturi zao. “Basi kulikuwako huko mabalasi sita ya mawe, nayo yamewekwa huko
kwa desturi ya Wayahudi ya kutawadha, kila moja lapata kadiri ya nzio mbili
tatu,” Yoh 2:6. Mungu kupitia Mwanaye
Mpenzi Yesu Kristo hutenda kadiri ya hali na mazingira yetu. Mtakatifu Thomas
wa Aquina anasema hivi, “neema hufanya kazi katika uhalisi wa kitu.”
Wapendwa
katika Kristo, “Mabalasi sita ya mawe,” yanatukumbusha umuhimu na tafsiri ya
namba kadiri ya mila na desturi ya Wayahudi. Namba sita inawakilisha udhaifu,
isiyo kamili au kutokukamilika, na isiyotosha. Kwa upande mwingine, namba kama
7, 14, na 40, huwakilisha ukamilifu, utoshelevu, na yakutosha.
Fundisho
la kwanza hapa ni kwamba licha la udhaifu ule na kutokutosheleka kule kutokana
na hali na ubinadamu wetu, kwa Upendo na Huruma aliokuwa nao Mungu, Yesu anafanya kitu licha ya kwamba saa yake
bado, yaani ukamilifu wa sadaka yake pale msalabani. Naye “Yesu
akawaambia, Jalizeni mabalasi maji. Nao wakayajaliza hata juu,” Yoh 2:7.
Tunapomwelekea Mungu kwa unyenyekevu licha ya mapungufu yetu kibinadamu, hawezi
kukaa kimya. “Kwa ajili ya Sayuni sitanyamaza, na kwa ajili
ya Yerusalemu sitatulia, hata haki yake itakapotokea kama mwangaza, na wokovu
wake kama taa iwakayo,” Isa 62:1.
Fundisho la pili katika tendo hili tunafundishwa ukweli huu kama
asemavyo Mt. Augustino, “Aliyekuumba wewe, pasipo wewe, hatokusaidia wewe,
pasipo wewe.” Mungu anahitaji ushirikiano wako kukamilisha uwezo wake juu yako.
Mungu ulifanya hilo endapo utagundua “SHAPE au KAMOUHUMA” yako. Mungu kamwe
habariki kisichokuwepo. Siyo kwamba Mungu hawezi kufanya hivyo, ila anapenda
ushiriki wako katika jambo hilo kama kiumbe shirikishwa katika uumbaji na
Mungu. Uumbaji wa kwanza Mungu aliumba vyote kutoka kisichokuwepo. Uumbaji huu
wa pili Mungu anapenda kutushirikisha kama viumbe vyake shirikishwa katika
uumbaji naye. Muujiza huu wa maji kujeuka kuwa divai, binadamu anashiriki kwa
tendo la kuyajaliza yale mabalazi maji hadi juu. Hivyo haitoshi kuuomba tu ili
ufanikishwe na Mungu, bali yakupasa pia kufanya kitu kadiri ya “SHAPE au
KAMOUHUMA yako.
Moja ya “SHAPE au KAMOUHUMA yako ni karama zako za kiroho
ulizojaliwa na Mungu. Mtume Paulo amezichambua vizuri karama hizi katika somo
letu la pili. Sisi tunapobatizwa
tunampokea roho huyu wa Mungu, Roho Mtakatifu. Anatufanya kuwa wana wa Mungu na
wana wa Kanisa. Kwa sakramenti ya Kipaimara, Roho Mtakatifu anatufanya kuwa
askari hodari wa Yesu Kristo kwa njia ya mapaji yake saba tunayopokea. Kuwa
tayari kutoa ushuhuda juu ya Yesu.
Ni katika Kanisa tunapewa
karama ya Roho Mtakatifu. “Na Mungu ameweka wengine katika Kanisa, wa
kwanza mitume, wa pili manabii, wa tatu waalimu, kisha miujiza, kisha karama za
kuponya wagonjwa, na masaidiano, na maongozi, na aina za lugha,” 1Kor 12:28. Anatoa
karama mbalimbali kwa wafuasi wa Kristo. Karama hizi ni kwa ajili ya manufaa ya
Kanisa lote, ingawa zinaweza kuwa na msaada kwa aliyepewa. “Lakini kila
mmoja hupewa ufunuo wa Roho kwa kufaidiana. Maana mtu mmoja kwa Roho apewa
neno la hekima; na mwingine neno la maarifa, apendavyo Roho yeye
yule; mwingine imani katika Roho yeye yule; na mwingine karama za kuponya
katika Roho yule mmoja; na mwingine matendo ya miujiza; na mwingine
unabii; na mwingine kupambanua roho; mwingine aina za lugha; na mwingine tafsiri
za lugha; lakini kazi hizi zote huzitenda Roho huyo mmoja, yeye yule,
akimgawia kila mtu peke yake kama apendavyo yeye,” 1Kor 12:7-11. Kanisa
lina wajibu wa kupima kwamba karama inapojitokeza kama kweli ni kutoka kwa Roho
Mtakatifu. Kama si kutoka kwa Roho Mtakatifu, hii si karama bali ni kitu
kingine. “Basi pana tofauti za karama; bali Roho ni yeye yule,” 1Kor 12:4
Kama wafuasi wa Yesu,
tunapojaliwa karama na Roho Mtakatifu, tunavutwa daima kumtazama yule
waliyemchoma, Yoh 19:28-37. Yohani Mtakatifu anaunganisha tukio la kifo cha
Yesu na kutukuzwa kwake. Yesu anaonyeshwa akiwa anaiendea saa yake, ndio saa ya
kutukuzwa kwake, kwa kifo, ufufuko na kupaa kwake Mbinguni. Anamwonyesha Yesu
anatoka kwa Baba na anarudi kwa Baba.
Yesu anapokufa msalabani anatoa
roho yake, anatupa roho huyu aliyempokea wakati anaanza kazi yake, aliposema,
“Roho wa Bwana yu juu yangu, Kwa maana amenitia mafuta kuwahubiri maskini
habari njema. Amenituma kuwatangazia wafungwa kufunguliwa kwao, Na vipofu
kupata kuona tena, Kuwaacha huru waliosetwa, Na kutangaza mwaka wa Bwana
uliokubaliwa,” Lk 4:18-19. Yohani anaunganisha tukio la kifo cha Yesu, tukio la
msalaba na Pentekoste. Pale msalabani Yesu anatoa roho wake, nasi tunampokea
kutoka ubavuni mwake tunapopokea sakramenti zake, “damu na maji”, katika Kanisa
lake. “Lakini askari mmojawapo alimchoma ubavu kwa mkuki; na mara ikatoka
damu na maji,” Yoh 19:34
Hivyo, tunapojaliwa karama
na Roho Mtakatifu, tunavutwa daima kumtazama yule waliyemchoma. Tukifanya hivyo
karama na vipaji vyetu havitakosa kuwa vya manufaa kwa Kanisa zima.
Tunapomtazama tunatambua kweli tuna karama. Je, tutamtazama namna gani? Katika
Kanisa lake hasa anapotufundisha kwa njia ya neno lake alilowakabidhi mitume,
viongozi wa Kanisa ambao ndio wenye madaraka ya kututafsiria neno la Mungu na
karama mbalimbali katika Kanisa na kuona kama kweli ni karama au ni hisia au
maigizo au mahangaiko ya kisaikolojia n.k.
Wapendwa wana wa Mungu,
Karismatiki katoliki ni karama ya Roho Mtakatifu katika Kanisa. Ni tofauti
na karismati za kilokole na madhehebu mengine au dini nyingine. Ipo hatari ya
kuchanganya Karismatiki katoliki na hasa karismatiki ya kilokole. Siku hizi
katika Karismatiki Katoliki wengi wanaiga mambo mengi ya kilokole
kama nyimbo, namna ya kucheza, namna ya kuongea na kuhubiri, namna ya
kusalimiana na kufurahi, namna ya uponyaji na kukemea uovu n.k. Je, haya hapa
kwetu hayapo? Si tu Karismatiki Katoliki wamekumbwa na tamaa hii ya kuiga na
kutumia mambo ya wengine, bali hata wakatoliki wengi hutumia nyimbo, muziki, na
hisia za kilokole katika tafrija, sherehe, mikutano na semina zao. Kweli sisi
wakatoliki tumechuja kiasi hicho kwamba tulivyo navyo, mathalani nyimbo zetu
hazigusi nafsi na hisia zetu? Kuna kila dalili ya kuweka vya kwetu chini, au
kuvichimbia na kukumbatia vya wengine na kuwasaidia kuvieneza hata ndani ya
Kanisa Katoliki.
Tufanyeje basi? Tuanze
kumtazama yule waliyemtoboa, tuliyemtoboa, ndio kutumia vile ambavyo kweli ni
mapokeo sahihi ya Kanisa na kuacha kuwasaidia walokole kueneza ibada zao na
namna zao za kusali. Tutafanikiwa hili tukiwa na ushirikiano sisi wenye, na
viongozi halali wa Kanisa, tukiwatumia wataalamu wetu [kwaya zetu, waalimu wa
kwaya, makatekista wetu] na pia tukitumia vipawa tulivyopewa kama wakatoliki na
si kama walokole au wanakarismatiki wa dini nyingine. Yapo mengi tunaweza kuiga
toka kwa wenzetu yakatusaidia lakini hii inahitaji umakini wa hali ya juu na
ruhusa ya Kanisa. Si kila mtu anajiamulia kitu chake na kukileta katika Kanisa
Katoliki, kuna utaratibu tangu enzi za mitume ambao unaongozwa na Roho
Mtakatifu. Kila mtu akileta utaratibu wake au kitu chake itakuwa ni fujo na
hakutakuwa na umoja ambao unaletwa na Roho Mtakatifu. Penye migogoro, ubinafsi
na hali ya kupenda kuwa juu ya mamlaka ya Kanisa, ambapo hakuna utii, hakuna karama,
bali kiburi na majivuno ndio vinatawala.
Wapendwa wana wa Mungu,
Maria Kasumuni ni mwana Legio Maria aliye hai. Kipindi fulani miaka michache
iliyopita kulikuwa na shindano la “voda fasta jishindie milioni 100.” Kutokana
na uhitaji wa fedha hizi, Maria Kasumuni alifanya novena ya siku 90 kupitia
maombezi ya Bikira Maria aweze kushinda shindano hili.
Hivyo Maria Kasumuni
alifanya Novena hii kwa uaminifu Mkubwa kwa mambo makuu matatu aliyojiwekea:
kuhudhuria Misa Tatatifu kila siku, kuwatembelea wagonjwa, na kuijongea
Sakramenti ya kitubio kila wiki. Siku tisini ziliisha na Yasinta Masikio
alitangazwa kama mshindi. Maria Kasumuni alihuzunika sana na kwenda kwenye
Pango la Mama Bikira Maria na kumlilia.
Mara Maria Kasumuni
alichukuliwa katika njozi na alimwona Bikira Maria katika hali ya tabasamu na
alimwambia, “Maria Kasumuni usinilaumu kwa sababu mimi nilifanya kazi yangu
vyema na nilikuwakilisha vizuri kwa mwanangu Yesu Kristo. Tatizo lilikuwa kwako
kwa sababu hukufanya kadiri alivyokuambia.”
Maria Kasumuni alimjibu
Bikira Maria na kusema, “mbona nilifanya yote kwa uaminifu mkubwa Mama wa
Mungu?” Bikira Maria akamjibu kwa kumwelewesha na kusema, “Mwanangu Yesu Kristo
huongea nasi kadiri ya hali, mazingira, na desturi zetu. Ulikuwa mpango wake
pia kuamsha hari ya Kampuni hii ya VODA kuandaa shindano hilo ili nawe ushinde.
Ila wewe hukufanya kadiri ya vigezo na masharti ya kampuni hii ya voda. Je,
unatumia ‘line’ gani ya simu?”
Akiwa ameinamisha kichwa
chake, Maria Kasumuni akamjibu Mama Bikira Maria na kusema, “natumia ‘line’ ya
TIGO.” Bikira Maria akamwambia Maria
Kasumuni, “Ni kwa sababu hiyo hukuweza kushinda shindano la kampuni ya VODA.”
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lo lote atakalowaambia, fanyeni,” Yoh 2:5
No hay comentarios:
Publicar un comentario