IJUMAA WIKI YA 1 YA MAJILIO
4/12/2015
Somo: Isa 29:17-24
Zab: 27:1, 4, 13-14
Injili: Mt 9:27-31
Nukuu:
“Na katika siku hiyo viziwi watasikia maneno ya hicho chuo, na
macho ya vipofu yataona katika upofu na katika giza,” Isa 29:18
“Wanyenyekevu nao wataongeza furaha yao katika Bwana, na
maskini katika wanadamu watafurahi katika Mtakatifu wa Israeli,” Isa 29:19
“Kwa maana mwenye kutisha ameangamizwa, naye mwenye dharau
amekoma, nao wote watazamiao uovu wamekatiliwa mbali; hao wamfanyao mtu kuwa amekosa katika
neno, na kumtegea mtego yeye aonyaye langoni, na kumgeuza mwenye haki kwa kitu
kisichofaa,” Isa 29:20-21
“Basi, Bwana aliyemkomboa Ibrahimu asema hivi, katika habari
za nyumba ya Yakobo; Yakobo hatatahayarika sasa, wala uso wake hautabadilika
rangi yake,” Isa 29:22
“vipofu wawili
wakamfuata wakipaza sauti, wakisema, Uturehemu, Mwana wa Daudi,” Mt 9:27
“Naye alipofika
nyumbani, wale vipofu walimwendea; Yesu akawaambia, Mnaamini kwamba naweza
kufanya hili? Wakamwambia, Naam, Bwana,” Mt 9:28
“Ndipo alipowagusa
macho, akasema, Kwa kadiri ya imani yenu mpate,” Mt 9:29
“Macho yao
yakafumbuka. Naye Yesu akawaagiza kwa nguvu, akisema, Angalieni hata mtu mmoja
asijue,” Mt 9:30
TAFAKARI: “Mnaamini kwamba naweza kufanya hili? Kwa kadiri ya imani
yenu mpate.”
Wapendwa wana wa Mungu, tukiachana
na yote yale mazuri yaletwayo na Masiha wetu katika tuonavyo katika somo letu
la kwanza kutoka kitabu cha Nabii Isaya, ni vyema tukajikita katika kuviondoa
vilema vyetu na mapungufu yetu ili tuufaidi ujio wa Masiha. Huu ndio wito wa
kipindi hiki cha Majilio. Hivyo leo tuangalie kwa undani juu ya mahangaiko yetu
na mateso ambayo kwa kiasi kikubwa yanatutoa katika mwelekeo mzima wa Imani ya
kweli. Ni kwa kadiri ya Imani yetu tutapata yale tuyaombayo.
Bila shaka wewe ni mmoja wa wale ambao kwa namna mmoja au
nyingine umekuwa ukizunguka kila kona ukitafuta suluhu la tatizo lako bila
mafanikio. Hakuna shaka pia kwa tatizo hilo au matatizo hayo umeshasali kila
aina ya sala na novena bila mafanikio. Kwa mtiririko huu naona pia
unavyoangaika kutafuta majibu ya matatizo yako kutoka kanisa moja kwenda
lingine, toka mchungaji mmoja kwenda mwingine bila mafanikio yenye utulivu wa
kutosha. Naona unavyoshawishika kufanya ibada za giza kwa maagizo ya waganga wa
kienyeji kupitia marafiki zako unaowaamini.
Wapendwa katika Kristo, leo Yesu anakuambia wewe na mimi
maneno haya ya uzima kama alivyowaambia wale vipofu waliotaka kuona tena;
“Mnaamini kwamba naweza kufanya hili? Kwa kadiri ya imani yenu mpate.” Swali
hili analotuuliza leo Yesu ni swali la msingi sana. Wengi wetu ni wakristo wa
majina na zaidi sana ni wakrito wa jumapili. Dini na Imani ya wengi imekuwa
kama kautaratibu fulani kitumikacho kama utambulisho wa kawaidi katika mtukio
fulani ya maisha, na kisicho sema chochote kuhusu undani wa maisha wa mtu huyo.
Licha ya kwamba mtu akiwa amebanwa na tatizo kubwa huweza kutekeleza ushauri
wowote apewao, ni vyema kusimama katika Imani dhabiti bila kuterereka. “Naye alipofika nyumbani, wale vipofu walimwendea; Yesu
akawaambia, Mnaamini kwamba naweza kufanya hili? Wakamwambia, Naam, Bwana,” Mt
9:28. Yote hutendwa ndani yetu kwa uzito ule ule tulionao kuhusu kile tuaminicho. “Ndipo alipowagusa macho, akasema, Kwa kadiri ya imani yenu
mpate,” Mt 9:29.
Mungu ana
lengo kwa kila tatizo. Yeye hutumia mazingira kukuza tabia yetu kwa kweli. Yeye
hutegemeza zaidi mazingira katika kutufanya tufanane na Kristo. Ukweli ni
kwamba unakabiliwa na mazingira masaa ishirini na nne kila siku. Yesu alituonya
kwamba tutakuwa na matatizo ulimwenguni. “Hayo nimewaambieni
mpate kuwa na amani ndani yangu. Ulimwenguni mnayo dhiki; lakini jipeni moyo;
mimi nimeushinda ulimwengu,” Yoh 16:33. Hakuna aliye sugu kwa matatizo au
amefunikwa asipatwe na mateso, wala hakuna aliye huru mbali na matatizo katika
maisha. Maisha ni mfululizo wa matatizo. Kila unapotatua moja, jingine
linasubiri kutokea. Si yote makubwa, lakini yote yana maana kwa Mungu katika
kukuza tabia yako. Petro anatuhakikishia kwamba mtatizo ni ya kawadia, “Wapenzi, msione kuwa ni ajabu ule msiba ulio kati yenu,
unaowapata kama moto ili kuwajaribu, kana kwamba ni kitu kigeni kiwapatacho,”
1Pet 4:12.
Mungu
anatumia matatizo kukusogeza karibu yake. “Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, Na waliopondeka roho
huwaokoa,” Zab 34:18. Ndugu yangu, wakati wako mzuri wa kuwa na ibada ya karibu
na Mungu unaweza kuwa siku zile za giza sana-moyo wako unapokuwa umepondeka,
unapohisi kuachwa, unapokuwa huna uchaguzi, maumivu yanapokuwa makubwa-na
unamgeukia Mungu peke yake. Ni wakati wa taabu
ndipo tunajifunza kusali sala za kweli na uaminifu kutoka moyoni. Tunapokuwa
katika maumivu, hatuna nguvu za sala za juu juu. Maisha yakiwa ya raha,
tunaweza kumfahamu Yesu juu juu tu, tukimwiga na kumnukuu na kusema juu yake.
Lakini ni katika taabu ndipo tutamjua Yesu. Tunajifunza mambo katika mateso,
mambo ambayo hatuwezi kujifunza kwa njia nyingine yeyote.
Mungu
angeweza kuzuia Yusufu asitiwe gerezani, Mwa 39:20-22. Mungu angezuia Danieli
asitupwe kwenye shimo la simba, Dan 6:16-23. Mungu angezuia Yeremia asitupwe
katika shimo la matope, Yer 38:6. Mungu angezui Paulo asivunjikiwe na jahazi
mara tatu, 2Kor 11:25. Na Mungu angewazuia vijana watatu Waebrania wasitupwe
katika tanuru la moto, Dan 3:1-26. Pamoja ha hali hiyo Mungu hakufanya hivyo.
Aliruhusu matatizo hayo kutokea, na matokeo yake kila mmoja wao alimsogelea
Mungu karibu zaidi.
Matatizo
hutulazimisha kumtazama Mungu na kumtegemea badala ya nafsi zetu wenyewe. Mtume
Paulo anashuhudia faida hii. “Naam, sisi wenyewe tulikuwa na hukumu ya mauti
katika nafsi zetu ili tusijitumainie nafsi zetu, bali tumtumaini Mungu,
awafufuaye wafu,” 2Kor 1:9. Kamwe hutajua kwamba unachohitaji ni Mungu tu mpaka
pale utakapojikuta umebaki na Mungu tu. Bila kujua chanzo, hakuna tatizo lolote
linaloweza kukupata bila ruhusa ya Mungu. Kila kinachotokea kwa mtoto wa Mungu
kinachujwa na Baba, na amekusudia kukitumia kuleta mema ingawa Shetani na watu
wengine wanakusudia mabaya.
Kwa kuwa
Mungu anatawala yote, ajali ni matukio tu katika mpango mzuri wa Mungu kwa
ajili yako. Kwa sababu kila siku ya maisha yako iliandikwa kwenye kalenda ya
Mungu kabla hujazaliwa. “Macho yako yaliniona kabla sijakamilika; Chuoni mwako
ziliandikwa zote pia, Siku zilizoamriwa kabla hazijawa bado,” Zab 139:16. Hivyo
kila kinachotoka kwako kina umuhimu wa kiroho. Kila kitu! “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu hufanya kazi pamoja
na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale walioitwa kwa kusudi lake. Maana wale aliowajua
tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili
yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi,” Rum 8:28-29
Wengi wetu hiki kifungu
(Rum 8:28-29) hukinukuu na kukieleza vibaya. Hakisema, “Mungu husababisha kila
kitu kufanya kazi kama ninavyopenda mimi.” Wala hakisemi, “Mungu husababisha
kila kitu kufanya kazi ili kuleta maisha ya furaha duniani.” Hiii si kweli pia
kuna miisho ya huzuni duniani. Tunaishi katika ulimwengu ulioanguka. Ni mbinguni
tu ndiko mambo yanatendeka kikamilifu kama Mungu alivyokusudia. Ndiyo maana
katika sala ya Baba Yetu tumeelezwa kusali, “Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni,”
Mt 6:10. Ili kuelewa vyema kifungu hicho kutoka Barua ya Mtume Paulo kwa Warumi
ni vyema tuangalie kwa makini kila fungu la maneno.
“Twajua:” Tumaini letu wakti wa magumu hutegemea kufikiri
chanya, kufikiri kwa kutarajia, au kule kutegemea mazuri kwa kawaida. Huu ni
uhakika uliojengwa kwenye kweli ya kwamba Mungu anatawala kikamilifu ulimwengu
na kwamba anatupenda.
“Katika mambo yote:” Mpango
wa Mungu kwa maisha yako unahusisha ote yanaokutokea-pamoja na makosa yako,
dhambi zako, na maumivu yako. Pia ni pamoja na magonjwa, madeni, majanga,
talaka, kifo cha uwapendao. Mungu anaweza kuleta mema kutokana na jambo ovu
sana. Alifanya hivyo pale Kalvari.
“Mungu hufanya:” Kuna
mbunifu nyuma ya kila kitu. Maisha yako siyo matokeo ya bahati mbaya, ajali, au
bahati nzuri. Kuna msanifu nyuma. Historia ni hadithi yake. Mungu anavuta nyuzi.
Tunafanya makosa, lakini Mungu hakosei kamwe. Mungu hawezi kufanya kosa-kwa
sababu yeye ni Mungu.
“Hufanya
kazi pamoja:” Siyo kwa kipekee au kwa kujitegemea. Matukio katika maisha yako
hufanya kazi pamoja katika mpango wa Mungu. Siyo matukio yaliyojitenga, lakini
matukio yanayotegemeana katika machakato mzima wa kukufanya ufanane na Kristo.
Ili kutengeneza keki lazima utumie unga wa ngano, chumvi, yai bichi, sukari, na
mafuta. Kama kila kimoja kikiliwa peke yake hakina ladha nzuri au hata ni
kichungu. Lakini ukivioka pamoja vinakuwa chakula kitamu. Na hiyo ndiyo keki.
Kama ukimpa Mungu maono yako yote mabaya, matukio yasiyopendeza, atayaunganisha
pamoja kuwa kitu chema.
“Wale
wampendao katika kuwapatia mema:” Hii si kwamba kila kitu maishani ni chema.
Mengi yanayotokea katika ulimwengu ni maovu na mabaya, lakini Mungu ni mtaalam
wa kutoa mema kutokana na hayo. Katika ukoo wa Yesu Kristo, Mt 1:1-6, wanawake
wanne wameorodheshwa: Tamari, Ruthu, Rahabu, na Bethsheba. Tamari alimhadaa
baba mkwe wake. Rahabu alikuwa kahaba. Ruthu hakuwa Myahudi na alivunja sheria
kwa kuolewa na Myahudi. Bethsheba alitenda uzinzi na Daudi, jambo lililopelekea
mauaji ya mume wake. Hizi hazikuwa ni sifa nzuri, lakini Mungu alileta mema
kutokana na mabaya, na Yesu akaja kupitia ukoo wao. Kusudi la Mungu ni kubwa
kuliko mataatizo yetu, maumivu yetu na
hata dhambi yetu.
“Wale
walioitwa:” Ahadi ya Mungu ni kwa watoto wa Mungu tu. Si kwa kila mmoja. Kila
kitu hufanya kazi pamoja kwa ubaya kwa wale wanaoishi wakimpinga Mungu na
kukazia kufuata njia zao.
“Kwa
kusudi lake:” Kusudi hilo ni lipi? Ni kwamba sisi “tufananishwe na mfano wa
Mwana wake,” Kila kitu Mungu anachokiruhusu kutokea katika maisha yako
kinaruhusiwa kwa kusudi hilo.
Wapendwa
wana wa Mungu, sisi ni kama lulu, tumechongwa kwa nyundo n atezo ya taabu
nyingi. Kama nyundo ya sonara haina nguvu sana kuweza kuondoa mikwaruzo, Mungu
atatumia nyundo nzito zaidi. Kama sisi ni jeuri zaidi, anatumia nyundo nzito ya
kunyanyuliwa na chombo maalum. Atatumia chochote kile.
Hivyo,
kila tatizo ni nafasi ya kujenga tabia, na kadiri linavyokuwa gumu zaidi,
ndivyo kunakuwa na matokeo makubwa katika kujenga msuli wa kiroho na uadilifu. “Wala si hivyo tu, ila na mfurahi katika dhiki pia; mkijua ya
kuwa dhiki, kazi yake ni kuleta saburi; na
kazi ya saburi ni uthabiti wa moyo; na kazi ya uthabiti wa moyo ni tumaini,”
Rum 5:3-4. Kila kinachotokea kwa maisha yako ya nje si cha muhimu sana katika
kama kile kinachotokea ndani yako. Mazingira yako ni ya muda mfupi, lakini
tabia yako itadumu milele.
Maandiko
Matakatifu hufananisha majaribu na moto wa kusafisha madini ambao huchoma
takataka zote. Mtume Petro anasema, “ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu,
ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa
moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima,”
1Pet 1:7a-d. Mfua fedha aliulizwa, “Je, unafahamu vipi kwamba sana fedha ni
safi? Alijibu, “ninapoona sura yangu ndani yake.” Unapokuwa umesafishwa kwa
majaribu, watu wanaweza kuiona sura ya Kristo ndani yako. Yakobo anasema, “mkifahamu ya
kuwa kujaribiwa kwa imani yenu huleta saburi,” Yak 1:3.
Kwa kuwa
Mungu anakusudia ufanane na Kristo, atakupitisha katika yale Yesu aliyopitia.
Hii ni pamoja na upweke, majaribu, dhiki, kulaumiwa, kukataliwa, na matatizo
mengine mengi. Biblia inasema Yesu “Alijifunza kutii kwa njia ya mateso” na
alikamilishwa kwa njia ya mateso,” Ebr 5:8-9. Kwa nini Mungu atuepushe kutoka
yale aliyomruhusu Mwana wake kuyapata? Mtume Paulo anasema, “na kama tu watoto, basi, tu warithi; warithi wa Mungu, warithio
pamoja na Kristo; naam, tukiteswa pamoja naye ili tupate na kutukuzwa pamoja
naye,” Rum 8:17.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Mateso ya mwenye haki ni mengi, Lakini Bwana
humponya nayo yote,” Zab 34:19
No hay comentarios:
Publicar un comentario