SIKUKUU YA BIKIRA MARIA MKINGIWA DHAMBI YA
ASILI
8/12/2015
Somo I: Mwa 3:9-15, 20
Zab: 98:1, 2-3abcd-4
Somo II: Efe 1:3-6, 11-12
Injili: Lk 1:26-38
Nukuu:
“Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye
aliyenipa matunda ya mti huo, nikala,” Mwa 3:12
“Bwana Mungu akamwambia nyoka, Kwa sababu umeyafanya hayo,
umelaaniwa wewe kuliko wanyama wote, na kuliko hayawani wote walioko mwituni;
kwa tumbo utakwenda, na mavumbi utakula siku zote za maisha yako,” Mwa 3:14
“Adamu akamwita mkewe jina lake Hawa; kwa kuwa yeye ndiye
aliye mama yao wote walio hai,” Mwa 3:20
“kama vile alivyotuchagua katika yeye kabla ya kuwekwa misingi ya
ulimwengu, ili tuwe watakatifu, watu wasio na hatia mbele zake katika pendo,”
Efe 1:4
“Kwa kuwa alitangulia kutuchagua, ili tufanywe wanawe kwa njia ya
Yesu Kristo, sawasawa na uradhi wa mapenzi yake,” Efe 1:5
“na ndani yake sisi nasi tulifanywa urithi, huku tukichaguliwa
tangu awali sawasawa na kusudi lake yeye, ambaye hufanya mambo yote kwa shauri
la mapenzi yake,” Efe 1:11
“Malaika akamwambia, Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema
kwa Mungu,” Lk 1:30
“Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake
utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu
atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake,” Lk 1:31-32
“Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako,
na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho
kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu,” Lk 1:35
“Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto
mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna neno
lisilowezekana kwa Mungu,” Lk 1:36-37
“Mariamu akasema, Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu
kama ulivyosema,” Lk 1:38a
TAFAKARI:
“Mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama ulivyosema.”
Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa
anaadhimisha Sikukuu ya Bikira Maria Mkingiwa dhambi ya Asili. Basi katika
tafakari hii leo ili tuelewe fumbo hili ni vyema kujiuliza maswali yafuatayo.
Ni kwa nini Bikira Maria akingiwe dhambi ya Asili? Kabla ya kujibu swali hili,
ni vyema kujua dhambi ya Asili ni nini? Kadiri ya Maandiko Matakatifu hasa
tuliyoyasoma kutoka somo la kwanza, na mafundisho ya Kanisa, dhambi hii ya
asili ni mwelekeo wa kutenda dhambi ambao chanzo chake kilitokana na anguko la
wazazi wetu wa kwanza, yaani Adamu na Hawa. Je, pamoja na anguko hili
hatukuweza kurudi na kuuchuchumilia Utakatifu? Jibu ni kwamba tunaweza. Ukweli
ni kwamba licha la anguko hili la wazazi wetu wa kwanza, Mungu hakutuondolea
ili hali ya uhuru ndani mwetu. Hivyo basi, ni kwa kupitia uhuru huu twaweza
kumrudia Mungu kwa njia ya toba na majuto, na vile vile kwa uhuru huu pia
twaweza kuasi kabisa. Ni nini basi kilitokea kule Bustanini Edeni kati ya Adamu
na Hawa?
Wapendwa wana wa Mungu, ni kweli kwamba mahali popote
anapoishi zaidi ya mtu mmoja kuna kuwa na kautaratibu kake ili mawasiliano
yaende vizuri. Utaratibu huu unaweza kuwa kimaandishi, au kimapokea katika hali
ya kuaminiania na kujenga mazoea ya kuishi katika misingi hiyo. Hivyo Mungu
alivyomuumba Adamu na kumpatia msaidizi wake, yaani Hawa. “Bwana Mungu akasema, Si vema huyo mtu awe peke
yake, nitamfanyia msaidizi wa kufanana naye. Bwana
Mungu akamletea Adamu usingizi mzito, naye akalala; kisha akatwaa ubavu wake
mmoja, akafunika nyama mahali pake, na
ule ubavu alioutwaa katika Adamu Bwana Mungu akaufanya mwanamke, akamleta kwa
Adamu,” Mwa 2:18,21-22. Mungu aliwapa mahali pa kuishi na mahali
hapo palijulikana kama bustani ya Edeni. Mungu aliwapa utaratibu wa kuishi
mahali hapo kadiri ya mpango wake mwenyewe ili uzima uwepo ndani yao milele na
kuepuka kifo. “Bwana Mungu akamwagiza huyo mtu, akisema, Matunda ya kila mti
wa bustani waweza kula, walakini
matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula
matunda ya mti huo utakufa hakika,” Mwa 2:16-17
Makatazo haya yanajenga udadisi na ushawishi wa yule mwovu
shetani. Hii ndiyo dhambi ile ya tamaa, ambayo hutujengea hali ya kutojipokea
na kutoridhika kwa kile tulicho. Shetani kwa umbo la nyoka anatumia mwanya huu
kumshawishi Eva. Dhambi hii inashirikishwa kwa wote wawili, yaani Hawa an
Adamu. Matokeo yake ni anguko kubwa la wazazi wetu wa kwanza. Mungu anapotaka
kujua kilichojiri kila mmoja anamtupia lawama mwenzake. Mwanamke anamlaumu
nyoka, na Adamu anamlaumu mkewe. “Adamu akasema, Huyo mwanamke uliyenipa awe pamoja nami ndiye
aliyenipa matunda ya mti huo, nikala,” Mwa 3:12. Tukio hili linamfanya Mungu
kutoa adhabu kwa yule mwovu-nyoka na kuvunja agano kati yake na Adamu na Hawa. “Bwana Mungu akamwambia nyoka, Kwa sababu
umeyafanya hayo, umelaaniwa wewe kuliko wanyama wote, na kuliko hayawani wote
walioko mwituni; kwa tumbo utakwenda, na mavumbi utakula siku zote za maisha
yako,” Mwa 3:14. Tangu hapa Hawa anakuwa Mama wa wote walio hai. “Adamu akamwita mkewe jina lake Hawa; kwa kuwa
yeye ndiye aliye mama yao wote walio hai,” Mwa 3:20. Na tangu nyakati hizo la
anguko hili la wazee wetu wa kwanza, kifo hakikuepukika tena hadi leo.
Kwa vile Mungu ni Huruma na Upendo, alipenda kuurejesha
uhusiano wake na wale aliowaumba kwa sura na mfano wake. Mpango huu ni tendo
zima la kumwilishwa kwake, yaani Neno kufanyika mwili. Bikira Maria kwa
upendeleo Mkubwa anachukua nafasi ya Hawa aliye dondoka. Bikira Maria katika
mpango huu anakuwa sababu ya kuinuliwa mzazi wetu wa kwanza yaani Hawa. Hivyo
kukingiwa kwa dhambi ya asili Bikira Maria kunaendana na kile kitarajiwacho
kuzaliwa, “Neno kufanyika mwili.” Mama Bikira Maria anapatwa na mshtuko kwa
jambo hili Mungu analotaka litokee kwake. Malaika Gabrieli anamwambia, “Usiogope, Mariamu, kwa maana umepata neema kwa Mungu,” Lk 1:30.
Kukingiwa dhambi hii ya Asili Bikira Maria, yaani ule mwelekeo wa kutenda
dhambi, kuliwezekana pia kwa sababu “alipata neema kwa Mungu.” Akijua ubinadamu wake, Bikira Maria anauliza
jambo hili litawezekanaje? “Malaika akajibu akamwambia, Roho Mtakatifu atakujilia juu yako,
na nguvu zake Aliye juu zitakufunika kama kivuli; kwa sababu hiyo hicho
kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu,” Lk 1:35. Kwa hiyo neema
ile kutoka kwa Mungu inajidhihirisha kwa nguvu na uwepo wa Roho Mtakatifu na
kufanya kile kitakachozaliwa kuitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu.
Habari
njema hii kwa Bikira Maria haikuishia hapo tu. Kuthibitisha jambo hilo linawezekana
mbele ya Mungu kwake yeye Bikira Maria kukingiwa dhambi ya Asili na kumzaa
Mwana wa Mungu kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, Malaika anampa yaliyojiri kwa
Elizabeti. “Tena, tazama, jamaa yako Elisabeti naye amechukua mimba ya mtoto
mwanamume katika uzee wake; na mwezi huu ni wa sita kwake yeye aliyeitwa tasa; kwa kuwa hakuna neno
lisilowezekana kwa Mungu,” Lk 1:36-37. Mungu wetu aliye hai siyo Mungu wa
kushindwa. Kwa unyenyekevu mkubwa Mama Bikira Maria anaupokea mpango mzima wa
Mungu na kusema, “Tazama, mimi ni mjakazi wa Bwana; na iwe kwangu kama
ulivyosema,” Lk 1:38a
Na kwa vile kile kitakachozaliwa kitakuwa kitakatifu, Mwana
wa Mungu, “ndani yake sisi nasi tulifanywa urithi, huku tukichaguliwa tangu
awali sawasawa na kusudi lake yeye, ambaye hufanya mambo yote kwa shauri la
mapenzi yake,” Efe 1:11. Mungu alichagua kutuumba kama tulivyo kwa sura na
mfano wake “kama vile alivyotuchagua katika yeye kabla ya kuwekwa misingi ya
ulimwengu, ili tuwe watakatifu, watu wasio na hatia mbele zake katika pendo,”
Efe 1:4. Tunaupata ukweli huu kutoka Mwinjili Yohane juu ya huyu atakaye
mwilishwa, yaani Mwana wa Mungu. “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho
chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Hivyo kila alifanyalo Mungu linamakusudi yake
katika umilele. Hakuna yeyote katika yetu yupo katika ulimwengu huu kwa bahati
mbaya. Hivyo vyote vinamuunganiko na Kristo Yesu. “Kwa kuwa alitangulia
kutuchagua, ili tufanywe wanawe kwa njia ya Yesu Kristo, sawasawa na uradhi wa
mapenzi yake,” Efe 1:5.
Wapendwa
katika Kristo, tumshangilie Mama Bikira Maria leo tunapo fanya sikukuu hii ya
kukingiwa dhambi ya Asili. Tunamshangilia kwanza kabisa kwa utayari wake wa
kuupokea mpango mzima wa Mungu kuelekea ukamilisho wa historia ya wokovu wetu.
Pili, kwa utayari wake nasi tunahesabiwa haki na kufanywa wanawe Mungu kwa njia
ya Yesu Kristo, sawasawa na uradhi wa mapenzi yake Mungu.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Kwa kuwa Mwenye nguvu amenitendea makuu, Na jina lake ni
takatifu,” Lk 1:49
No hay comentarios:
Publicar un comentario