viernes, 4 de diciembre de 2015

TAFAKARI: JUMAPILI 2 YA MAJILIO YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 2 YA MAJILIO YA MWAKA C
6/12/2015
Somo I: Bar 5:1-9
Zab: 126:1-6
Somo II: Flp 1:3-6, 8-11
Injili: Lk 3:1-6
Nukuu:
“Ee Yerusalemu, vua nguo za matanga na huzuni, uvae uzuri wa utukufu utokao kwa Mungu milele,” Bar 5:1

“Jifungie nguo ya haki itokayo kwa Mungu, jipige kilemba kichwani cha utukufu wake Aliye wa Milele, maana Mungu ataidhhirisha nuru yako duniani mwote,” Bar 5: 2-3

Nami niliaminilo ndilo hili, ya kwamba yeye aliyeanza kazi njema mioyoni mwenu ataimaliza hata siku ya Kristo Yesu,” Flp 1:6

Na hii ndiyo dua yangu, kwamba pendo lenu lizidi kuwa jingi sana, katika hekima na ufahamu wote; mpate kuyakubali yaliyo mema; ili mpate kuwa na mioyo safi, bila kosa, mpaka siku ya Kristo,” Flp 1:9-10

hali mmejazwa matunda ya haki, kwa njia ya Yesu Kristo, kwa utukufu na sifa ya Mungu,” Flp 1:11

“neno la Mungu lilimfikia Yohana, mwana wa Zakaria, jangwani. Akafika nchi yote iliyo karibu na Yordani, akihubiri ubatizo wa toba liletalo ondoleo la dhambi,” Lk 3:2b-3 

“Sauti ya mtu aliaye nyikani, Itengenezeni njia ya Bwana, Yanyosheni mapito yake,” Lk 3:4b

Kila bonde litajazwa, Na kila mlima na kilima kitashushwa; Palipopotoka patakuwa pamenyoka, Na palipoparuza patalainishwa,” Lk 3:5

Na wote wenye mwili watauona wokovu wa Mungu,” Lk 3:6

TAFAKARI:Na wote wenye mwili watauona wokovu wa Mungu.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya pili ya Majilio ya Mwaka “C” wa Kanisa. Leo tuikite tafakari yetu kwenye maneno haya ya Yohani Mbatizaji, “Na wote wenye mwili watauona wokovu wa  Mungu.” Wapendwa katika Kristo, kwa vile kila mmoja wetu licha ya utofauti wake kimwonekano kauumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, Mwa 1:27, ni kwa maana hiyo kwamba wote tumealiwa katika ukamilifu wa Mungu ambao ndio Utakatifu wenyewe. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Wote wanaoitwa katika ukamilifu huu ni viumbe dhaifu ukiwemo wewe na mimi. Ni katika kuushinda udhaifu wetu kama wanadamu ndipo tutakapo ufikia ule ukamilifu. Ni kwa mantiki hii kwamba “wote wenye mwili watauona wokovu wa Mungu,” Lk 3:6

Tunapotambua udhaifu wetu utokanao na  ubinadamu wetu ndipo tunapozama ndani zaidi katika tafakari huku tukijitakasa katika kipindi hiki cha Majilio. Tafakari ya kina na kujitakasa huku kunaamsha matumaini mapya na yenye nguvu kumpokea Masiha wetu, na hakimu wetu wa haki. Noeli itakuwa na maana tu pale tunapotambua wajibu huu muhimu wa kujitakasa. Huu ndio ujumbe wa Yohani Mbatizaji kutoka jangwa, kwamba, “Itengenezeni njia ya Bwana, Yanyosheni mapito yake,” Lk 3:4b. Kuitengeneza njia kwa mtazamo wa kiroho ni kujitakasa, yaani kuyatoa yale yote yasiyoendana na ukamilifu wa Mungu tulioitiwa. Ni kuyanyoosha mahusiano yetu na Mungu, jirani, na mazingira yetu yaliyokunjamana kwa sababu ya dhambi. Ni kufanya toba ya kweli, Lk 3:2b-3. Yohane anaiita hali hii sawa na kujaza kila bonde, kushusha kila mlima wa dhambi; kunyoosha kila mahali palipopotoka, na kulainisha pale palipo paruzika, Lk 3:5. Kwa maneno mengine ni kuutengeneza uso wako ufanane na uso wa mfalme ajaye yaani mwokozi wetu Yesu Kristo.

Ili tufanane na ule uso wa Masiha na Mfalme watu wa haki na amani, yakupasa wewe na mimi kuvua nguo ya matanga na uzuni yetu, na kuvaa uzuri wa utukufu utokao kwa Mungu wetu kama asemavyo Nabii Baruku: “Ee Yerusalemu, vua nguo za matanga na huzuni, uvae uzuri wa utukufu utokao kwa Mungu milele,” Bar 5:1. Utayari huu wa kulivua vazi hili la matanga na uzuni ni tendo la toba ya kweli. Na baada ya toba ya kweli yanipasa kuishi na kudumu katika kweli na haki. Ni kuishihali mmejazwa matunda ya haki, kwa njia ya Yesu Kristo, kwa utukufu na sifa ya Mungu,” Flp 1:11. Kweli na haki hii idumu ndani yangu, ionekane kwa jirani zangu, na iwe dira ya kuniongoza katika kweli na haki ya milele ambayo nitahesabiwa haki na kweli hiyo na Mungu mwenyewe. Hivyo basi, “Jifungie nguo ya haki itokayo kwa Mungu, jipige kilemba kichwani cha utukufu wake Aliye wa Milele, maana Mungu ataidhhirisha nuru yako duniani mwote,” Bar 5: 2-3. Je, waipenda nuru?

Wapendwa wana wa Mungu, nuru hii tunayo ndani mwetu kwanza kabisa kwa kupitia Sakramenti ya ubatizo, na kwa kuendelea kuyapokea Masakramenti katika hali ya usafi. Hii nuru kwa maana nyingine ndiyo neema zile tuzipatazo kwa kupokea Sakramenti katika hali ya usafi. Nuru hii au neema hizi ufifishwa ndani kwetu kwa kuchafuliwa na hali ya dhambi. Tunatakaswa na kung’arishwa tena kwa kuweka makusudi ya kweli ya kutokutenda dhambi kwa kupitia tanuri lile la utakaso, yaani Sakramenti ya upatanisho. Sakramenti hizi katika Kanisa ni mbubujiko wa chemichemu za neema isiyo na kikomo. Ili neema hizi kupitia Sakramenti hizi zifanye kazi kadiri ya mastahili yake yatupasa kuwa katika hali ya usafi. Huku ndiko kuishi katika hali ya usafi kama dua la  Mtume Paulo kwa Mungu kwa ajili ya watu wake: Na hii ndiyo dua yangu, kwamba pendo lenu lizidi kuwa jingi sana, katika hekima na ufahamu wote; mpate kuyakubali yaliyo mema; ili mpate kuwa na mioyo safi, bila kosa, mpaka siku ya Kristo,” Flp 1:9-10.

Basi wapendwa katika Kristo tuelewe kwamba kipindi hiki cha Majilio tunajiandaa kwa hali ya kuwa safi mwili na roho tukilenga kufanana na usafi wa yule tunayamngoja kwa hamu, yaani, Bwana na Mwokozi wetu. Bila kusahau ukweli kwamba, wote wenye mwili watauona wokovu wa Mungu,” Lk 3:6

Mtawa Mark Mpole siku moja jioni akiwa kwenye tafakari katika pango la Mama Bikira Maria alichukuliwa katika njozi na mara akajikuta akiwa anaongozana na Mama Bikira Maria kuelekea sehemu moja iliyokuwa ikisikika kwa kelele za nyundo na vyuma. Wakiwa njiani Bikira Maria alimwambia Mark Mpole kuwa huru kuuliza chochote nami nitakujibu.

Baada ya mwendo wa dakika kumi hivi, Mark Mpole na Mama Bikira Maria walifika eneo lile lililokuwa likisikika kwa kelele za nyundo na vyuma. Mark Mpole aliwaona watu wangi wakiwa wanaponda vyuma kwa nyundo na wengine wakikata vyuma vile kwa misumeno ya chuma. Kwa upande wa pili Mark Mpole aliona rundo kubwa kama mlima la vipande vya vyuma vyenye maumbo tofauti tofauti vikiwa na kutu.

Ndipo Mark Mpole alipomuuliza Mama Bikira Maria, “kwa nini pamoja na kazi kubwa wanayofanya wafua vyuma hivi kuna rundo kubwa la vyuma vilivyo na kutu na vimekusanywa upande mmoja?” Mama Bikira Maria huku akitazama mlima ule alimjibu Mark Mpole, “Mlima wa vyuma hivyo vilivyo na kutu ni ‘vyuma chakavu.’ Vyuma hivyo havifai kwa matumizi yoyote yale na ndiyo maana vimekusanywa kwa ajili ya kutupwa. Katika maisha yako jitahidi usiwe kama vyuma hivyo. Vyuma hivyo mapoja na kufuliwa kwa muda mrefu vilikosa kuwa na umbo lile walilotaka wahunzi wale viwe.”

Mbele kidogo waliona mkusanyo mdogo wa vyuma, ndipo Bikira Maria akamuuliza Mark Mpole, “Je, hapa unaona nini?” “Hapa naona sura yangu na yako kwenye vyuma hivi,” Mark Mpole alimjibu Mama Bikira Maria kwa mshangao. Bikira Maria akamwambia, “Hivi ndivyo vyuma vinavyofaa na vilivyo imara kwa matumizi yoyote yale ya kudumu. Jitahidi kuwa kama vyuma hivi katika maisha yako. Tumeziona sura zetu kwenye vyuma hivi kwa sababu hakuna uchafu wowote uliobaki ndani yake. Hivyo haviwezi kupata kutu katika umilele wake. Visababishi vyote vya uwezekano wa kupata kutu umeondolewa kwa moto mkali, na kufanya upondaji wake kuwa mrahisi kwa kuliumba umbo hili kama tunavyoona.”

Wapendwa wana wa Mungu, hapana shaka kabisa kwamba tunapovumilia mateso yetu na kuvishinda vishawishi, ndiyo kwa namna hiyo tunatakaswa na kuifunua sura na mfano halisi wa Mungu ndani yetu uliofifishwa kwa dhambi zetu.

Tumsifu Yesu Kristo!


Na kama tulivyoichukua sura yake yule wa udongo, kadhalika tutaichukua sura yake yeye aliye wa mbinguni,” 1Kor 15:49

No hay comentarios:

Publicar un comentario