jueves, 17 de diciembre de 2015

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 3 YA MAJILIO MWAKA-C

IJUMAA WIKI YA 3 YA MAJILIO-C
18/12/2015
Somo: Yer 23:5-8
Zab: 72:1-2, 12-13, 18-19
Injili: Mt 1: 18-25
Nukuu:
Tazama siku zinakuja, asema Bwana, nitakapomchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu na haki katika nchi,” Yer 23:5 
Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu,” Yer 23:6 

Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu,” Mt 1:18
Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri,” Mt 1:19

Basi alipokuwa akifikiri hayo, tazama, malaika wa Bwana alimtokea katika ndoto, akisema, Yusufu, mwana wa Daudi, usihofu kumchukua Mariamu mkeo, maana mimba yake ni kwa uweza wa Roho Mtakatifu,” Mt 1:20

asimjue kamwe hata alipomzaa mwanawe; akamwita jina lake YESU,” Mt 1:25

TAFAKARI: “Yusufu, Mumewe Bikira Maria, Mtu wa haki.”

Wapendwa wana wa Mungu, sehemu hii ya Injili tuliyoisoma leo, na hasa, Mt 1:18-19, inatufanya tujiulize swali hili. Kwa nini Yusufu alikusudia kumwacha Mariamu ikiwa walikuwa bado kuoana? Ukweli ni kwamba, mila na desturi za Kiyahudi zilikuwa tofauti na zetu. Mwanaume na mwanamke waliunganishwa pamoja wakati wanapopeana miadi ya kuoana (uchumba), ingawa hawakuruhusiwa kuhusiana kimwlili hadi baada ya harusi. Yusufu alikuwa anapanga kuuvunja uchunba wao rasmi baada ya kugundua kuwa Mariamu ana mimba ili hali hakuwahi kukutana naye kimwili.

Yusufu anataka kulifanya jambo hili kuwa siri ili kumnusuru Mariamu kifo cha aibu ambacho kingempata kama jambo lile lingegundulika katika jamii. Kama Yusufu angetaka kutafuta haki yake, sheria ilisema hivi kuhusu ubikira;  Mtu akitwaa mke, akamwingilia na kumchukia, kisha akamshitaki mambo ya aibu kumzushia jina baya, akasema, Nimemtwaa mwanamke huyu, nami nilipomkaribia sikuona kwake alama za ubikira; Lakini likiwa ni kweli neno hili, la kutoonekana kwake yule kijana alama za ubikira; na wamtoe nje yule kijana (kike) mlangoni pa nyumba ya baba yake, na waume wa mji wake wampige kwa mawe hata afe; kwa vile alivyofanya upumbavu katika Israeli, kwa kufanya ukahaba katika nyumba ya baba yake; ndivyo utakavyoondoa uovu katikati yako,” Kumb 22:13-14, 20-21. Kwa hali aliyokuwa nayo Mariamu si tu tatizo la ubikira, ila alionekana ana mimba.Kuzaliwa kwake Yesu Kristo kulikuwa hivi. Mariamu mama yake alipokuwa ameposwa na Yusufu, kabla hawajakaribiana, alionekana ana mimba kwa uweza wa Roho Mtakatifu,” Mt 1:18

Kwa vile Yusufu alimpenda sana Mariamu aliona ni vyema kumwondoa katika aibu ile, ili asife kwa kupigwa mawe. Naye Yusufu, mumewe, kwa vile alivyokuwa mtu wa haki, asitake kumwaibisha, aliazimu kumwacha kwa siri,” Mt 1:19. Hapa ndipo tunapoona utu wa Yusufu. Utu huu ndio unaomfanya kuhesabiwa haki na Mungu kama mtu wa haki. Yusufu hakupenda kulihukumu jambo lile asilolijua. Yusufu alimjua vizuri Mariamu ikiwa ni pamoja na malezi aliyopata kutoka kwa wazazi wake. Hata hivyo tukio hili la mimba lilibaki kitendawili kikubwa kwa Yusufu. Kwa upande mwingine hapa tunafundishwa kwamba ukiwa na mashaka na kitu fulani usitende chochote. Jambo au kitu kile kipe kwanza Muda. Kitendo cha Yusufu kutaka kumwacha kwa siri Mariamu ilikuwa kulipa jambo lile muda. Je, ingetokea kwako au kwangu kwa namna yoyote ile ungelipa jambo hili muda?

Swali lingine ambalo linatujia katika habari hii, Mt 1:18 ni hili; Je Mariamu alikuwa na mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, au Yesu alikuwa uzao wa viuno vya Daudi kwa mujibu wa Mdo 2:30?-(“Basi kwa kuwa ni nabii, akijua ya kuwa Mungu amemwapia kwa kiapo, ya kwamba katika uzao wa viuno vyake atamketisha mmoja katika kiti chake cha enzi”). Mariamu alikuwa bikira; Biblia inasema Roho Mtakatifu "alimfunika" Mariamu, si kwa jinsi ya kuhusiana kimwili. Yusufu alikuwa baba pekee wa kisheria aliyemuasili Yesu, hakuwa baba halisi. Lakini Yesu alikuwa mzao halisi wa ukoo wa Daudi kupitia Mariamu, kama orodha ya vizazi yenye kupitia kwa Mariamu ya Lk 3:23-37 inavyoonyesha. Aya nyingine zenye kusema kuwa Yesu ni mtoto (mzao wa ukoo) wa Daudi ni Mt 12:23; 15:22; 20:30; 21:9,15; Mk 10:47-48; 12:35; Lk 10:41; 18:38-39; Yoh 7:42; 2 Tim 2:8; Ufu 5:5; 22:16. Je, Mat 1:23 (Tazama, bikira atachukua mimba, Naye atazaa mwana; Nao watamwita jina lake Imanueli; Yaani, Mungu pamoja nasi)  inatafsiri Isa 7:14 (Kwa hiyo Bwana mwenyewe atawapa ishara. Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye atamwita jina lake Imanueli) kimakosa kwa kutumia jina "bikira?"

Jibu ni hapana. Si tu kwamba neno la Kiebrania lililotumiwa hapa linamaanisha amaa "Bikira" ama "msichana," lakini pia fafsri ya Kigiriki ya Agano la Kale (Septuagint) imelitafsiri neno hili kuwa "parthenos," yaani bikira. Swali lingine ambalo tunaweza kujiuliza ni hili: Kwenye Mt 1:23 na Lk 1:26-35, inawezekanaje  Yesu aliyezaliwa na bikra awe mzao wa ukoo wa Daudi? Hapa kuna mambo matatu ya kuzingatia;

1. Yesu hakuwa mtoto halisi wa Yusufu. Kama angekuwa. Yer 29:32 ingekuwa ni unabii wa uongo.
2. Yesu alikuwa mtoto wa Yusufu kisheria. Leo hii, mwanaume anayemuoa mwanamke aliye na mtoto anakuwa baba wa mtoto huyo kisheria, ingawa si baba halisi.
3. Yesu alikuwa mtoto halisi wa Mariamu. Yesu alikuwa wa ukoo wa Daudi kisheria kupitia Yusufu, na Yesu alikuwa wa ukoo wa Daudi kiuhalisi kupitia Mariamu. Kadiri ya Mt 1:25, "asimjue kamwe hata alipomzaa mwanawe: akamwita jina lake YESU." Mt 1:25. Je Mariamu alikuwa na watoto wengine wowote? Mstari huu hautakuwa na maana yoyote na mwenye kupotosha kama Yusufu na Mariamu hawakuwa wamewahi kuwa na uhusiano wa kimwili.

Zaidi ya hapo, Mt 13:55-56; Mk 6:4; Gal 1:19; na Yuda 1, pia zimerekodi kuwa Yesu alikuwa na wadogo wake wa kiume (ndugu). Eusebius, katika kitabu chake kiitwacho Ecclesiastical History (karibu mwaka 360) 2:20 na d 3:20 pia anasema kuwa wadogo wanne wa kiume wa Yesu walikuwa Yakobo aliyeitwa mwenye haki), Yose (au Yusufu), Yuda na Simoni.


Moja ya majibu yatolewayo na Kanisa Katoliki ni kuwa Yusufu alikuwa na watoto kupitia ndoa yake ya awali, lakini si kupitia kwa Mariamu. Hata hivyo, hakuna ushahidi toka kwenye historia ya Kanisa kuwa Yusufu aliwahi kuwa na ndoa nyingine kabla ya ile na Mariamu, au mdogo wake yoyote wa kiume hakutokana na Yusufu na Mariamu.


Jibu lingine la Kanisa Katoliki ni kuwa kwenye jamii za Kimediteranian neno "ndugu" linaweza kuamaanisha binamu na ndugu/jamaa wa karibu wenye umri unaofanana, na si tu kaka au wadogo wa mtu. Hata hivyo, Ambrose wa Milani alikuwa wazi kuwa Yesu hakuhitaji msaada wowote ili aweze kuwaunganisha watu na Mungu, na Mariamu hakupaswa kusujudiwa (On the Holy Spirit kitabu cha 3 sura ya 11 na.80 mwaka 381 BK). Alisema, " Na mtu yeyote asihamishie jambo hili kwa Bikira Maruamu; Mariamu alikuwa hekalu la Mungu. Na kwa hiyo Yeye (Mungu) pekee ndiye aliyepaswa kuabudiwa Yeye afanyaye kazi katika hekalu lake (mwenyewe)"


Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na kuona ukweli huo hatuwezi kupinga kwamba yote hayo yalifanyika chini ya mpango mzima wa Mungu. Mungu hawezi kujikanganya mwenyewe. Hivyo Nabii Yeremia anasema, Tazama siku zinakuja, asema Bwana, nitakapomchipushia Daudi Chipukizi la haki; naye atamiliki mfalme, atatenda kwa hekima, naye atafanya hukumu na haki katika nchi,” Yer 23:5. Huyu ndiye Bwana wa haki na utawala wake ni utawala wa hekima na hukumu zake ni za haki. Ujio wa Masiha ni habari ya wokovu na kuwekwa huru mwili na roho. Katika siku zake Yuda ataokolewa, na Israeli atakaa salama, na jina lake atakaloitwa ni hili, Bwana ni haki yetu,” Yer 23:6. Basi na tuwe watu wa haki, tukitenda yaliyo kweli na haki, na kuhukumu kwa haki.

Tumsifu Yesu Kristo!


Kicho cha Bwana ni kitakatifu, Kinadumu milele. Hukumu za Bwana ni kweli, Zina haki kabisa,” Zab 19:9

No hay comentarios:

Publicar un comentario