domingo, 13 de diciembre de 2015

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 3 YA MAJILIO-C

JUMATATU WIKI YA 3 YA MAJILIO-C
14/12/2015
Somo: Hes 24:2-7, 15-17a
Zab: 25:4-5ab, 6-7bc, 8-9
Injili: Mt 21:23-27
Nukuu:
Namwona, lakini si sasa; Namtazama, lakini si karibu; Nyota itatokea katika Yakobo Na fimbo ya enzi itainuka katika Israeli; Nayo itazipiga-piga pembe za Moabu, Na kuwavunja-vunja wana wote wa ghasia,” Hes 24:17

“Ni kwa amri gani unatenda mambo haya? Naye ni nani aliyekupa amri hii?” Mt 21:23b

Yesu akajibu akawaambia, Na mimi nitawauliza neno moja; ambalo mkinijibu, nami nitawaambia ni kwa amri gani ninatenda haya,” Mt 21:24 

Ubatizo wa Yohana ulitoka wapi? Ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu?” Mt 21:25

Wakamjibu Yesu wakasema, Hatujui. Naye akawaambia, Wala mimi siwaambii ninyi ni kwa amri gani ninatenda haya,” Mt 21:27

TAFAKARI: “Ni kwa amri gani unatenda mambo haya?”

Wapendwa wana wa Mungu, Taifa la wana wa Israeli linaingiwa hofu juu ya Mfalme Balaki wa Moabu. Balaamu akiwa amejawa na roho wa Mungu aliyaandaa maombi kuhusu sintofahamu ile waliyokutana nayo jangwani. Mungu anampa maono naye anayatafsiri kama ifuatavyo; Namwona, lakini si sasa; Namtazama, lakini si karibu; Nyota itatokea katika Yakobo Na fimbo ya enzi itainuka katika Israeli; Nayo itazipiga-piga pembe za Moabu, Na kuwavunja-vunja wana wote wa ghasia,” Hes 24:17. Je, maono haya ni ashirio la kuja kwake Masiha, hasa Nyota hii kutoka katika Yakobo?

Hakika nyota hiyo na yote yanayoambatana nayo ni ashirio la kuja kwa Masiha, ambaye atawaweka huru wana wa Taifa hili teule la Mungu. Utabiri huu unathibitishwa na Malaika Gabrieli alipompasha habari  Bikira Maria na kusema, “Tazama, utachukua mimba na kuzaa mtoto mwanamume; na jina lake utamwita Yesu. Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Ataimiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho,” Lk 1:31-33. Injili kama ilivyoandikwa na Mathayo, tunaona  Malaika anazungumzia kazi ya yule atakaye zaliwa na Bikikira Maria na  kusema, Naye atazaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, maana, yeye ndiye atakayewaokoa watu wake na dhambi zao,” Mt 1:21. Hivyo tendo hili ni mpango mahususi wa wokovu wa mwanadamu.

Hata hivyo pamoja na tabiri zote hizi na uthibitisho wa kweli kwa neno kufanyika Mwili na kukaa kwetu, bado  Taifa hili Teule hawakutaka kuachana na mitazama yao ya kibinadamu, wakabaki kushikilia sheria za kibinadamu na tafsiri zao zilizokuwa na mwelekeo wa  ubinadamu. Kwa maana hiyo, waliingiwa upofu wa kiroho na kutokuona ishara zilizokuwa zinaufunua Umungu wa Yesu Kristo. Hivyo Wayahudi, na hasa Wakuu wa Makuhani na wazee wanahoji mamlaka ya Yesu na kumwambia, “Ni kwa amri gani unatenda mambo haya? Naye ni nani aliyekupa amri hii?” Mt 21:23b. Yesu hakuhitaji mamlama yoyote kutenda aliyoyatenda kwa sababu licha ya kuwa na hali ya ubinadamu, Yeye ni Mungu pasipo shaka, Yoh 1:1-3.

Hivyo kwa kutambua udhaifu wao, naye Yesu anawauliza swali, Ubatizo wa Yohana ulitoka wapi? Ulitoka mbinguni, au kwa wanadamu?” Mt 21:25. Jibu lao liliwaweka katika mtego mkubwa kwa sababu wakijibu ubatizo huo ulitoka mbinguni wataonekana hawana imani, hasa kile alichokitabiri Yohani kuhusu Yesu. Na wakisema ulikoka mwa mwanadamu waliogopa kwani watu wote waliujua utakatifu wa Yohani Mbatizaji. Kuepukana na hoja hii ya msingi waliamua kusema hatujui ingawa ukweli waliujua. Naye Yesu aliwaacha jinsi walivyo kwa sababu ujumbe ulifikia bara’bara. Pasipo shaka yoyote, Wakuu wa Makuhani na Wazee wanahoji mamlaka ya Yesu kwa sababu wanahofia nafasi zao na hasa maslahi yao kutokana sheria kandamizi walizojitungia wenyewe, kutoka amri kumi za Mungu hadi kufikia sheria 613. Uwepo wa Yesu na nguvu na mamlaka yake katika kufundisha na kutenda kuliwatia hofu kubwa sana. Kitumbua chao kilianza kuingia mchanga!

Hivyo ndugu zangu, katika Kristo tunawekwa huru, na yatupasa kutokunaswa katika kongwa la utumwa wa dhambi. “Katika ungwana huo Kristo alituandika huru; kwa hiyo simameni, wala msinaswe tena chini ya kongwa la utumwa,” Gal 5:1. Maisha mapya ndani ya Kristo na katika Kristo hayatulazimu tena kuhofia au kuwajibika kwa sheria za kibinadamu. Tunawajibika kufanya yote katika imani itendayo kazi kwa upendo. Maana katika Kristo Yesu kutahiriwa hakufai neno, wala kutokutahiriwa, bali imani itendayo kazi kwa upendo,” Gal 5:6. Kuyatumikia haya ni kujitia hofu pasipo sababu.

Yesu Kristo hakuacha kukemea mambo haya yasiyo ya msingi kuhusu imani ya kweli. Wayahudi nyakati za Yesu walionekana kufuata zaidi tafsiri ya torati kuliko torati yenyewe. Tafsiri hii, yaani, TALMUD, ulikuwa ukweli wa Mungu uliopotoshwa kwa maslahi ya kibinadamu. Mambo muhimu ya kuzingatia yalikuwa kuhusu adili, rehema, na imani ya kweli. Yesu anatoa karipio kwa Waandishi na Mafarisayo na kuwaambia, Ole wenu waandishi na Mafarisayo, wanafiki! Kwa kuwa mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani; hayo imewapasa kuyafanya, wala yale mengine msiyaache,” Mt 23:23. Sheria hizi ambazo kwa kiasi kikubwa zilikuwa kandamizi zikiendana na utoaji wa sadaka ulionyambuliwa kwa manufaa yao binafsi. Sheria hizi hazikuwa na mwelekeo wa uzima wa milele. Ukweli ni kwamba, kumpenda yeye (Mungu) kwa moyo wote, na kwa ufahamu wote, na kwa nguvu zote, na kumpenda jirani kama nafsi yako, kwafaa kuliko sadaka nzima za kuteketezwa na dhahibu zote pia,” Mk 12:33. Mtakatifu Agustino anasema, ‘kupenda kweli utafanya yote.’

Wapendwa katika Kristo, ni vyema tukatambua wajibu wetu na mapaswa yetu ili tuweze kutumika vyema kadiri ya mpango wa Mungu. Mungu anakila sababu na wewe ikiwa ni pamoja na maisha yako. Hivyo pigania cheo chako ambacho ni UTAKATIFU wako. Bila huo huwezi kumwona Mungu.

Tusifu Yesu Kristo!

Tafuteni kwa bidii kuwa na amani na watu wote, na huo utakatifu, ambao hapana mtu atakayemwona Bwana asipokuwa nao,” Ebr 12:14


No hay comentarios:

Publicar un comentario