sábado, 12 de diciembre de 2015

TAFAKARI: JUMAPILI YA 3 YA MAJILIO YA MWAKA-C

JUMAPILI YA 3 YA MAJILIO YA MWAKA C
13/12/2015
Somo I: Sef 3:14-18a
Zab: 12:2-6
Somo II: Flp 4:4-7
Injili: Lk 3:10-18
Nukuu:
Imba, Ee binti Sayuni; piga kelele, Ee Israeli; Furahi na kushangilia kwa moyo wako wote, Ee binti Yerusalemu,” Sef 3:14

Bwana ameziondoa hukumu zako, Amemtupa nje adui yako; Mfalme wa Israeli, naam, yeye Bwana, yu katikati yako; Hutaogopa uovu tena,” Sef 3:15 

Katika siku ile Yerusalemu utaambiwa, Usiogope, Ee Sayuni; mikono yako isilegee,” Sef 3:16 

Bwana, Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa; Atakushangilia kwa furaha kuu, Atakutuliza katika upendo wake, Atakufurahia kwa kuimba,” Sef 3;17

Furahini katika Bwana sikuzote; tena nasema, Furahini,” Flp 4:4 

Upole wenu na ujulikane na watu wote. Bwana yu karibu,” Flp 4:5 

Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu,” Flp 4:6 

Na amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu,” Flp 4:7

Akawajibu akiwaambia, Mwenye kanzu mbili na ampe asiye na kanzu; na mwenye vyakula na afanye vivyo hivyo,” Lk 3:11 

Akawaambia, Msitoze kitu zaidi kuliko mlivyoamriwa,” Lk 3:13 

Akawaambia, Msidhulumu mtu, wala msishitaki kwa uongo; tena mtoshewe na mshahara wenu,” Lk 3:14b 

Yohana alijibu akawaambia wote, Kweli mimi nawabatiza kwa maji; lakini yuaja mtu mwenye nguvu kuliko mimi, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto,” Lk 3:16

ambaye pepeo lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake, na kuikusanya ngano ghalani mwake, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika,” Lk 3:17

TAFAKARI: “Tufanye nini basi?”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya tatu ya majilio ya mwaka “C” wa Kanisa. Dominika hii hujulikana kama dominika ya furaha. Masomo yetu yote hasa somo la kwanza na la pili yanafunua furaha na ujumbe wa Mungu kwetu kuhusu yule tunayemtarajia kuja, yaani mwokozi wetu. Pamoja na hayo yote, leo Mama Kanisa anatualika kuwa tayari kila mmoja wetu kujua ni nini cha kufanya ili ajapo Masiha wetu atukute tupo tayari. Moja ya hatua muhimu za kuchukua ni kuachana na mazoea yetu. Nabii Isaya anatuwasa tuachane na ibada zisizomfuraisha Mungu. Yeye, yaani Mungu, ni maminifu tunapokuwa tayari kutembea naye katika kweli na haki. Kila mmoja wetu yampasa kujitakasa na kuacha kutenda mabaya, Isa 1:16. Mungu aliye upendo na huruma yupo tayari kuanza upya nasi na kusahau yote yaliyopita, ila kwa sharti ya kuongoka kweli. Jifunzeni kutenda mema; takeni hukumu na haki; wasaidieni walioonewa; mpatieni yatima haki yake; mteteeni mjane. “Haya, njoni, tusemezane, asema Bwana. Dhambi zenu zijapokuwa nyekundu sana, zitakuwa nyeupe kama theluji; zijapokuwa nyekundu kama bendera, zitakuwa kama sufu,” Isa 1:17-18

Bila shaka kila mmoja wetu anajua yaliyoko ndani ya moyo wake, na wapi anatakiwa kufanya mabadiliko. Ni vizuri ukatumia muda huu kujitazama kile ulicho ndani ya moyo wako. Kile ambacho hatupo tayari kukisema au kukisimulia ndicho kile tulicho. Mahubiri ya Yohani Mbatizaji wanaibua hisia za ndani za wale waliomsikiliza. Wote kwa pamoja wanamuuliza wafanye nini? Naye anawajibu kwa kusema, “Mwenye kanzu mbili na ampe asiye na kanzu; na mwenye vyakula na afanye vivyo hivyo,” Lk 3:11. Kumbe wajibu wa kwanza katika safari hii ya utakaso ni kutambua mahitaji ya wengine. Matendo yetu kama kielelezo cha wongofu wetu yalenge katika upendo kwa jirani. Mkristo asiyeona uchungu na mateso ya mkristo mwenzake huyu bado hajamjua Kristo anayemwamini na Mungu anayemwabudu na kumtumikia. Kati yetu wapo wanaokula na kusaza na kesho yake kumwaga vyakula hivyo kwenye majalala wakati jirani yake anayesali naye jumuiya moja hana chakula.

Wapendwa katika Kristo, kila mmoja wetu yampasa kuwajibika vyema pale alipo. Tumeumbwa ili tuwajibike kila mmoja kadiri ya wito na nafasi ya kile alicho mbele ya jamii inayomzunguka. Wajibu huu unatuwajibisa kutenda mema na kuchukia mabaya kama anavyotuasa Nabii Amosi na kusema, “Tafuteni mema, wala si mabaya, mpate kuishi; hivyo Bwana, Mungu wa majeshi, atakuwa pamoja nanyi, kama msemavyo. Yachukieni mabaya; yapendeni mema; mkaithibitishe haki langoni; yamkini kwamba Bwana, Mungu wa majeshi, atawafanyia fadhili mabaki ya Yusufu,” Amo 5:14-15. Mfano halisi wa nini cha kufanya tunao katika Injili ya leo ambapo watoza ushuru wanataka kujua mapaswa yao ili wawe mkono salama wa Mungu. Naye Yohane Mbatizaji anawajibu kwa kusema, “Msitoze kitu zaidi kuliko mlivyoamriwa,” Lk 3:13. Hapa tunaonywa kuhusu tamaa ya kujilimbikizia mali kusiko halali na kutowajali masikini. Leo tunapolitazama Taifa letu la Tanzania, wapo baadhi yetu wanaishi maisha ya anasa kupindukia, ilhali wapo wengi ambao maisha yao niyadhiki sana. Ukweli ni kwamba, ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu,” Rum 14:17

Wapendwa katika Kristo, si jambo la kushangaza leo tunapoona wengi wetu waliopewa dhamani na umma wamekuwa mstari wa mbele kufinyanga haki za wanyonge. Ndugu yangu, nafasi uliyo nayo siyo nafasi ya kujijenga nafsi yako na kusahau wale waliokupa dhamana. Yakupasa “kutumika” kwanza na siyo kutumikiwa. Pili, yakupasa “kujitoa” kwa ajili ya wengine. Yeyote yule anaye wajibika na kujito kwa wengine yupo mikono salama ya Kristo, na kwake itathibitika kama vile Mwana wa Adamu asivyokuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mt 20:28 

Kama ilivyokuwa kwa watoza ushuru ndivyo ilivyokuwa kwa maaskari. Nao wanamuuliza Yohane Mbatiza nini cha kufanya ili wawe mkono salama. Yohana  Mbatizaji anawajibu, “Msidhulumu mtu, wala msishitaki kwa uongo; tena mtoshewe na mshahara wenu,” Lk 3:14b. Je, hali lep ipo vipi kwa baadhi ya Maaskari wetu? Wanatenda haki kweli kwa mujibu wa sheria? Licha ya kwamba hatuwezi kuwajumuisha wote katika ubaya, ila kwa kiasi kikubwa askari wetu hawatendi haki kwa raia wao. Wakati mwingine askari wetu wanalazimika kufanya hivyo si kwa matakwa na utashi wao, bali kwa matakwa ya wakubwa wao. Bado tunaishi katika siasa za kiimla na kibwana. Baadhi ya wale walio madarakani wanafanya mahali hapo kama umilele wao. Baadhi ya watawala wetu leo hawapo tayari kuachia nafasi zao hata pale wanapotakiwa kufanya hivyo wa utaratibu ulio wazi na wakikatiba. Viongozi hawa wapo tayari kupindisha Katiba kama mwongozo mama, na kuwatumia askari wetu na vyombo vya usalama kama kukidhi malengo yao. Ila tujue kwamba mwisho wa siku, Kadiri ya matendo yao, kwa kadiri iyo hiyo atawalipa, ukali kwao wampingao, malipo kwa adui zake,” Isa 59:18a

Vyombo hivi badala ya kuwa usalama wa watu na mali zao, vimekuwa vyombo vya dhuluma na uvunjifu wa haki za raia zao kwa kutimiza matakwa maovu ya wakubwa wao. Hakika Mungu atasimama katika kweli na haki, na hata vumilia milele uovu huu. Kwa kila mwenye hofu ya Mungu, wongofu siyo tu kuacha dhambi kwa kuzitubu, ila kuwa tayari kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu na kuongozwa naye.  Petro akawaambia, Tubuni mkabatizwe kila mmoja kwa jina lake Yesu Kristo, mpate ondoleo la dhambi zenu, nanyi mtapokea kipawa cha Roho Mtakatifu,” Mdo 2:38. Tendo hili la kutubu kwa mwono huu linaturejesha kwenye asili ya kuumbwa kwetu, yaani, kwa sura na mfano wa Mungu, Mwa 1:27, kuliko fifishwa na dhambi zetu. Tendo hili pia lina tupatia nyakati za kuburudishwa kwa uwepo wa Kristo tunaye mtumainia. Hivyo wapendwa katika Kristo,  Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana,” Mdo 3:19. 

Wapendwa wana wa Mungu, Masiha huyu tunayemsubiri siye Yohane Mbatizaji, ambaye kazi yake ilikuwa kuandaa njia tu. Yohane Mbatizaji anaweka kweli hii juu ya Masiha wetu na kusema, “mimi nawabatiza kwa maji; lakini yuaja mtu mwenye nguvu kuliko mimi, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto,” Lk 3:16. Huyu ndiye Masiha tunaye mngoja. Basi hii furaha yangu imetimia. Yeye hana budi kuzidi, bali mimi kupungua,” Yoh 3:30. Yatupasa kupungu katika majivuno yetu, dharau zetu, kujigamba kwetu, kujua kwetu, umaarufu wetu, ili yeye aongezeke. Masiha wetu ndiye kila kitu kwetu, yaani ndiye njia, kweli, na uzima, Yoh 14:6.

Tunapojitafiti ni nini cha kufanya ili kuwa mikono salama ya Masiha wetu, yatupasa kuufahamu ukweli huu kwamba huyu tunayemngoja ni hukumu katika utimilifu wake. Ni hukumu katika maana ya kwamba ni ambaye pepeo lake li mkononi mwake, naye atausafisha sana uwanda wake, na kuikusanya ngano ghalani mwake, bali makapi atayateketeza kwa moto usiozimika,” Lk 3:17. Kwake hakuna rushwa wala ufisadi na wala haongeki. Kila mtu atalipwa kadiri ya matendo yake. Hivyo ni vyema kuishi na tenda mema ili kuepuka karaha zisizo na tija siku ya kuja kwake.

Pamoja na mapaswa hayo ikiwa ni pamoja na maandalizi ya ujio wake, tendo la ujio wake ni furaha kubwa sana kwetu. Ni furaha kwa sababu Mungu amekisikia kilio chetu na kuthibitisha kwamba, Yeye ndiye Mungu na wala hakuna kama yeye. Nabii Sefania nauthibitisha ukuu huu wa Mungu kwa kusema, Bwana ameziondoa hukumu zako, Amemtupa nje adui yako; Mfalme wa Israeli, naam, yeye Bwana, yu katikati yako; Hutaogopa uovu tena,” Sef 3:15. Hii ndiyo furaha ambayo kila kwenye kuishi kwa hofu ya Mungu na kutenda haki yampasa kuifurahia. Hivyo, Imba, Ee binti Sayuni; piga kelele, Ee Israeli; Furahi na kushangilia kwa moyo wako wote, Ee binti Yerusalemu,” Sef 3:14. Furaha hizi zitakuwa na maana kwetu kama tunatambua vyema wajibu wetu kwa Mungu, jirani, na mazingira yanayotuzunguka. Mambo haya yakiwa sawa bila ukinzani, hofu juu ya kuja kwake Masiha hutoweka na kubaki na furaha. Hatuna sababu ya kuogopa ujio wake kwetu. Katika siku ile Yerusalemu utaambiwa, Usiogope, Ee Sayuni; mikono yako isilegee,” Sef 3:16. Je, ni nini kinachokutia hofu kwa ujio wa Masiha? Kama kipo basi ni wakati wa kukitafutia tiba. Wakati ndio sasa!

Tunaposimama katika kweli na haki Mungu wetu husimama nasi hata pale panapoonekana hapawezekani. Kanisa la mwanzo lilitesaka katika kweli na haki, na wakati huo huo walionya furaha katika mateso. Nao wakatoka katika ile baraza, wakifurahi kwa sababu wamehesabiwa kuwa wamestahili kuaibishwa kwa ajili ya Jina hilo,” Mdo 5:41. Silaha kubwa ya kuushinda uovu ni kujenga tabia ya kutenda mema. Mungu hutuinua kwa kuushinda uovu kwa wema na si vinginevyo. Nabii Sefania anatuambia, Bwana, Mungu wako, yu katikati yako shujaa awezaye kuokoa; Atakushangilia kwa furaha kuu, Atakutuliza katika upendo wake, Atakufurahia kwa kuimba,” Sef 3;17. Kumbe kutambulika kwetu kuwe kwa matendo mema na wema kwa wote. Hii ndiyo nuru kwa kila mwenye hofu ya Mungu.

Nabii Isaya anaelezea nuru hii kwa kusema,  Na mataifa wataiona haki yako, na wafalme wote watauona utukufu wako; nawe utaitwa jina jipya, litakalotajwa na kinywa cha Bwana,” Isa 62:2.  Bwana uthibitisha ukaribu wake kwetu pale tunapoishi kwa amani na wengine. Mungu ndiye atakayeigeuza uzuni yetu kuwa furaha hata pale ulimwengu utakapo furahia mateso yetu yatokanayo na kutenda mema. Naye Yesu anasema,Amin, amin, nawaambia, Ninyi mtalia na kuomboleza, bali ulimwengu utafurahi; ninyi mtahuzunishwa, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha,” Yoh 20:20. Bwana ndiye mfalme wa Amani, Upendo, Haki, na Msamaha. Ni kwa maana hiyo kwamba, Upole wenu na ujulikane na watu wote. Bwana yu karibu,” Flp 4:5. Huku ndiko kuishi ndani na katika Kristo. Hata imekuwa, mtu akiwa ndani ya Kristo amekuwa kiumbe kipya; ya kale yamepita tazama! Yamekuwa mapya, 2Kor 5:17.  Zaidi ya hayo ni kudumu katika sala na kuomba. Maombi yetu yatakuwa na uzito kwa sababu tunajua ni nani tunayemtumikia na kumfuata. Hivyo, Msijisumbue kwa neno lo lote; bali katika kila neno kwa kusali na kuomba, pamoja na kushukuru, haja zenu na zijulikane na Mungu,” Flp 4:6. Je, ndugu yangu katika maisha yako nini kinachochukua muda wako mwingi?

Kudumu katika kweli kadiri ya maelekezo ya Mungu kutatupasa uvumilivu na sadaka kubwa. Mungu wetu hana haraka, ila anatutaka tudumu katika amani ya kweli na kukua kila siku katika kweli na haki. Utulivu wa kweli ndani na katika Kristo, ndicho kielelezo cha amani ya kweli katika utimilifu wa umilele wa Mungu. Maisha ya Kristo ndiyo kielelezo sahihi kwetu. Ni mfano ulio hai kwetu na ndiyo jibu sahihi kwa hiki ambacho bado hakijajifua kwetu katika ukamilifu wake. Pamoja na sintofahamu nyingi katika maisha yetu, Kristo bado ndio mlango sahihi wa pitia. Hivyo ndugu zangu katika Kristo, amani ya Mungu, ipitayo akili zote, itawahifadhi mioyo yenu na nia zenu katika Kristo Yesu,” Flp 4:7.  Kristo ndiye mlango sahihi wa kupita kwa sababu hata katika majaribu yetu hutupatia mlango wa kutokea. Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili,” 1Kor 10:13.  Je, wataka kujua zaidi kuhusu nini cha kufanya? Zama ndani ya nafsi yako na ongea juu ya yale ambayo umekuwa ukiyaficha maisha yako yote. Hapo ndipo penye uhai wako, na ndicho ulicho. Kupekua na kufika kwenye kilindi hiki cha nafsi kunahitaji ujarisi. Huu ndio ujasiri na furaha anaouzungumzia Mtume Paulo kwa Wakorintho na kusema, Ninao ujasiri mwingi kwenu; naona fahari kuu juu yenu. Nimejaa faraja, katika dhiki yetu yote nimejaa furaha ya kupita kiasi,” 2Kor 7:4. Ndugu yangu tuliyesafiri sote katika tafakari hii, usipopagusa pale usipotaka kupagusa kwa kuogopa, huwezi kuwa na furaha ya kweli, kwa sababu bado hujajitambua kile ulicho. Bado umejivika kinyago na kuukataa ukweli ambao ndio wewe mwenyewe.

Jumuiya ya Bikira Maria Mama wa Faraja ni moja ya Jumuiya katika Parokia ya Huruma ya Mungu. Jumuiya hii imebarikiwa kwa kuwa na familiya nyingi zenye uwezo, na mara kwa mara jumuiya hii huwa ya kwanza katika majitoleo yao kiparokia. Familia ya Mzee Misalaba ni moja ya familia kumi na mbili katika jumuiya hii ya Bikira Maria Mama wa Faraja.

Familia ya Mzee Misalaba ni familia yenye watoto nane. Ni familia iliyo masikini kuliko familia zote za jumuiya hii ya Bikira Maria Mama wa Faraja, na Parokia kwa ujumla wake. Watoto wawili wa mwisho wa  Mzee Misalaba, yaani Mateso na Fikiri mara kwa mara huonekana wakiwa nje ya nyumba yao mapema sana asubuhi kabla hata majirani zao kuamka.

Ukweli ni kwamba sio hupenda kudamka mapema hivyo, bali usiku kwao ni safari ndefu sana. Hulalia mikeka na kujifunika vipande vya kanga na maboksi. Hivyo mara waonapo mwanga kupitia matundi ya kuta za nyumba yao hujilazimu kutoka nje. Tatizo ni pale kunapokuwa na mbalamwezi nje. Huamka na kurudi tena ndani na kuendea na safari yao ndefu. Jambo la pili linalowafanya watoke nje mapema ni uwepo wa shimo la kutupia takataka na mabaki ya vyakula kuto mmoja ya nyumba ya jirani yao ambaye ni tajiri wa kupindukia.

Hivyo Mateso na Fikiri huwa hawachezi mbali na shimo hili kwani wakati mwingine mikate na vipande vya nyama na samaki hutupwa ndani mwa shimo hili vingali bado havijaharibika. Siku mmoja mapema asubuhi, mfanyakazi wa ndani wa nyumba ya huyu tajiri alimwaga vipande vya samaki kwenye shimo hili. Mara alitokea Mbwa ambaye alianza kuvishambulia huku mfanyakazi huyu wa ndani akiwa anamwangalia. Kitendo hiki kiliwahuzunisha sana Mateso na Fikiri kwa sababu walijua hawana chao kwa siku ile.

Mbwa yule akiwa amebakiza vipande vitatu kumaliza, mfanyakazi yule wa ndani aliondoka. Hapa ndipo hasira ya watoto wale ilipowaka juu ya mbwa yule. Mateso akiwa na fimbo kubwa baada ya kuuvunja mti uliokua jirani yake, na Fikiri akiwa na mawe, walimkimbiza mbwa yule na kumpiga bila huruma. Mbwa alizidiwa nguvu na kuanguka chini huku akitapika vipande vile vya samaki alivyokula. Na hapa ndipo ulipofika mwisho wa maisha ya yule Mbwa.

Wapendwa wana wa Mungu, kwa ujumla mbwa hakuwa na makosa hata kidogo. Kungalikuwa na upendo wa kweli wa kuwajibika na kuwa tayari kujitoa kwa ajili ya wengine, amani ingekuwa kwa wote, yaani familia ya Mzee Misalaba na majirani zake matajiri, na kwa viumbe kama mbwa yule. Tunapokosa kuishi upendo wa kweli hatuubomoi tu uhusiano kati yetu na jirani zena na Mungu, bali tunaubomoa uhusiano huo na viumbe vingine visivyo na utashi kama mbwa.

Kama hiyo haitoshi, tunaharibu pia mazingira yanayotuzunguka. Mfano, Mateso kuchukua fimbo kubwa ilimpasa kuuvunja mti ule ambao ulihitaji kukua kadiri ya makusudi yake na asili yake. Fikiri kuchukua mawe na kumponda Mbwa yule kulisababisha mtikisiko na mmomonyoko wa udongo pale jiwe lile lilipochukuliwa na lilipotua baada ya kurushwa.

Tumsifu Yesu Kristo!

 “Basi ninyi hivi sasa mna huzuni; lakini mimi nitawaona tena; na mioyo yenu itafurahi, na furaha yenu hakuna awaondoleaye,” Yoh 16:22


No hay comentarios:

Publicar un comentario