sábado, 12 de diciembre de 2015

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 2 YA MAJILIO MWAKA-C

JUMAMOSI WIKI YA 2 YA MAJILIO-C
11/12/2015
Somo: YbS 48:1-4, 9-11
Zab: 79, 2ac, 3b, 15-16, 18-19
Injili: Mt 17:10-13
Nukuu:
Bila shaka wamebarikiwa wale waliokuona kwa macho, wakafa; lakini wewe umezidi kubarikiwa, kwa maana unaishi,” YbS 48:11

Naye akajibu, akawaambia, Kweli Eliya yuaja kwanza, naye atatengeneza yote,” Mt 17:11

ila nawaambia, ya kwamba Eliya amekwisha kuja, wasimtambue, lakini wakamtenda yote waliyotaka. Vivyo hivyo Mwana wa Adamu naye yuaenda kuteswa kwao,” Mt 17:12 

TAFAKARI: “Wewe umezidi kubarikiwa, kwa maana unaishi.”

Wapendwa wana wa Mungu, kuuishi ushuhuda katika maisha si kitu cha ajabu. Kuishi ushuhuda ni kuguswa na habari fulani katika maisha, na habari hiyo ikawa kielelezo na dira ya maisha ya mtu. Ushuhuda huu waweza kuwa mvuto wa maisha ya mtu yaliyojaa maadili mazuri na roho ya upendo wa ajabu. Mvuto huu ukawa kioo cha kujitazama na kuwa kielelezo cha maisha. Ushuhuda waweza kuwa wosia anaotoa mtu uliojaa hekima na busara kwa wale anaowaacha. Hivyo watu wakavutwa na kuishi wosia huo kama kielelezo cha maisha.

Mungu katika safari ya wokovu wa mwanadamu alitumia watu mbalimbali kujifunua kwake na kuacha jumbe mbalimbali kama kielelezo katika maisha. Watu hawa walikuwa: Waamuzi, Manabii, Wafalme, na Mwishoni kabisa Neno aliyemwilishwa na kukaa kwetu. Kumbe baraka na neema ziliwafikia waja wa Mungu kwa kupitia watu mbalimbali. Lakini pamoja na neema na baraka hizo, kinachokaziwa hapa ni mwendelezo wa ile roho iliyoachwa na wale wapeleka ujumbe. Kuishi kwa ile roho katika mioyo ya watu ni kuzuri zaidi kwa sababu ni kuishi katika uzima wa Mungu. Hivyo, “Bila shaka wamebarikiwa wale waliokuona kwa macho, wakafa; lakini wewe umezidi kubarikiwa, kwa maana unaishi,” YbS 48:11

Wanafunzi wa Yesu wanamuuliza Yesu katika Injili ya leo, “kwa nini waandishi hunena ya kwamba imempasa Eliya kuja kwanza?” Msingi wa swali hili unajijenga katika mwono wa Yesu ulivyo kwa jamii ile iliyomzunguka. Bila shaka kulikuwa na mfanano mkubwa sana kati ya Yesu na Manabii waliomtangulia ikiwa ni pamoja na Nabii Isaya. Naye Yesu anawajibu wanafunzi wake, “Kweli Eliya yuaja kwanza, naye atatengeneza yote,” Mt 17:11. Bila shaka hapa Yesu anamzungumzia Yohane Mbatizaji kwani ndiye aliyeitoboa siri ya Masiha, yaani, Yesu Kristo kadiri ya utabiri wa Nabii Isaya. Kwa sababu huyo ndiye aliyenenwa na nabii Isaya, akisema, Sauti ya mtu aliaye nyikani, Itengenezeni njia ya Bwana, Yanyosheni mapito yake,” Mt 3:3. Watu waliishi roho hii na matumaini haya ingawa hawakujua ni lini itakuwa kweli.

Kwa kuufafanua ukweli huu, Yesu anaenda mbali zaidi na kusema, ila nawaambia, ya kwamba Eliya amekwisha kuja, wasimtambue, lakini wakamtenda yote waliyotaka. Vivyo hivyo Mwana wa Adamu naye yuaenda kuteswa kwao,” Mt 17:12. Huyu waliyemtenda kama walivyotaka ni Yohani Mbatizaji ambaye alikatwa kichwa siku ya sherehe ya ukumbusho wa kuzaliwa Herode. Mauti yanamfika Yohane Mbatizaji kwa kusimamia kweli na haki. Yohane Mbatizaji alimkemea Mfalme Herode kwa tendo baya la kumchukua mke wa ndugu yake Filipo. Kwa maana Herode mwenyewe alikuwa ametuma watu, akamkamata Yohana, akamfunga gerezani, kwa ajili ya Herodia, mkewe Filipo ndugu yake, kwa kuwa amemwoa; kwa sababu Yohana alimwambia Herode, Si halali kwako kuwa na mke wa nduguyo,” Mk 6:17-18.  

Kifo cha Yohane Mbatizaji kinaashiria pia kifo cha Yesu Kristo. Yesu analiona hilo katika maisha yake. Kwetu ni ushuhuda wa maisha kwamba tunaposimama katika kweli na haki, maisha hayo yatatugharimu. Hata kama tutakufa kwa kuishi ushuhuda huu, tutaishi na Kristo milele kwa sababu Yeye ndiyo kielelezo halisi cha maisha yetu. Huyu ndiye Masiha tunayemsubiri. Tunapomsubiri Masiha wetu kwa hamasa hii kumbwa na matumaini, yatupasa pia kutambua mapaswa yetu katika ufuasi wake.

Tumsifu Yesu Kristo!

Na kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu,” 1Yoh 3:3


No hay comentarios:

Publicar un comentario