JUMAMOSI WIKI YA 1 YA MAJILIO
5/12/2015
Somo: Isa 30:19-21, 23-26
Zab: 147:1-6
Injili: Mt 9:35-10:1, 6-8
Nukuu:
“Na ingawa Bwana atawapeni chakula cha shida na maji ya msiba,
lakini waalimu wako hawatafichwa tena, ila macho yako yatawaona waalimu wako,” Isa
30:20
“Na tena nuru ya mwezi itakuwa kama nuru ya jua, na nuru ya
jua itaongezeka mara saba, kama nuru ya siku saba, katika siku ile Bwana
atakapofunga mapigo ya watu wake, na kuliponya pigo la jeraha yao,” Isa 30:26
Ndipo
alipowaambia wanafunzi wake, Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache. Basi mwombeni Bwana wa mavuno,
apeleke watenda kazi katika mavuno yake,” Mt 9:37-38
“Akawaita wanafunzi wake kumi na wawili, akawapa amri juu ya
pepo wachafu, wawatoe, na kupoza magonjwa yote na udhaifu wa kila aina,” Mt 9:1
“Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema, Ufalme wa
mbinguni umekaribia,” Mt 9:7
“Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye ukoma, toeni
pepo; mmepata bure, toeni bure,” Mt 9:8
TAFAKARI: “Ufalme wa mbinguni umekaribia.”
Wapendwa wana wa Mungu, kauli mbiu hii “Ufalme wa mbinguni
umekaribia,” inatualika kujiandaa kimwili na kiroho. Maandalizi haya yatuguse
na kuona umuhimu wa kufanya hivyo. Wakati mwingine tunajisahau sana na kuishi
bila mwelekeo wowote hasa kiroho. Ufalme wa mbinguni kwanza ni mwito binafsi
kwa sababu hatujui siku wala saa. Hivyo ni mwaliko kwa kila mmoja binafsi, na
pili wote kwa ujumla. Hiki ndicho Yesu anachowataka wafuasi wake wakifanye. “Na katika kuenenda kwenu, hubirini, mkisema,
Ufalme wa mbinguni umekaribia,” Mt 9:7. Ufalme huu wa mbinguni uliokaribu
unajidhihirisha kwa matendo makuu ya Mungu ya upendo na huruma yake. “Pozeni wagonjwa, fufueni wafu, takaseni wenye
ukoma, toeni pepo; mmepata bure, toeni bure,” Mt 9:8.
Matendo haya ya huruma na upendo yaanze hapo ulipo kwa kila kadiri ya nafasi
yako na wito wako.
Ufalme
wa mbinguni ambao tunausubiria ni hali ile ya kuanza upya vyote na Mungu.
Kuanza huku upya na Mungu tunatudai kujiandaa vyema mwili na roho. Huku ndiko
kutakakotupelekea kuponywa majeraha yetu. “Na tena nuru ya mwezi itakuwa kama nuru ya jua,
na nuru ya jua itaongezeka mara saba, kama nuru ya siku saba, katika siku ile
Bwana atakapofunga mapigo ya watu wake, na kuliponya pigo la jeraha yao,” Isa
30:26.
Wapendwa wana wa Mungu, tutumie vizuri muda huu
kujiweka vyema mwili na roho ili ufalme huo utakapofika tuwe tayari kuupokea.
Chambua mahusiano yako na Mungu, jirani, na mazingira yako ya kila siku. Je,
katika mahusiano hayo ni wapi palipokosa afya? Nenda kwa tabibu ili upate tiba
stahiki. Sakramenti ya upatanisho inatuwezesha kuyarejesha mahusiano yetu na
Mungu, Jirani, na mazingira yetu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Basi
zaeni matunda yapasayo toba,” Mt 3:8
No hay comentarios:
Publicar un comentario