miércoles, 2 de diciembre de 2015

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 1 YA MAJILIO MWAKA-C

ALHAMISI WIKI YA 1 YA MAJILIO
3/12/2015
Somo: Isa 26:1-6
Zab: 118:1, 8-9, 19-21, 25-27a
Injili: Mt 7:21, 24-27
Nukuu:
 “Utamlinda yeye ambaye moyo wake umekutegemea Katika amani kamilifu, kwa kuwa anakutumaini,” Isa 26:3 

Mtumainini Bwana siku zote Maana Bwana YEHOVA ni mwamba wa milele,” Isa 26:4

Kwa kuwa amewashusha wakaao juu, Mji ule ulioinuka, aushusha, Aushusha hata nchi, auleta hata mavumbini,” Isa 26:5 

Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 7:21 

Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba,” Mt 7:24-25

Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa,” Mt 7:26-27

TAFAKARI: “Afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni ndiye atakayeingia katika ufalme wa mbinguni.”

Wapendwa wana wa Mungu, kila kitu chenye uhai kwacho chenyewe au kundi huongozwa na mamlaka fulani. Ni kweli pia hata kwa upande wa mwanadamu katika ishi yake ikiwa ni pamoja na fikiri yake, tenda yake, amini yake, husukumwa na kitu fulani. Ukweli huu ni pamoja na kundi la watu ambao pia kwa kukaa pamoja husukumwa na nguvu ya mfumo fulani. Nguvu hizi au misukumo hii tunapoitimiza kama ilivyo ndiyo kwa namna hiyo tunalandana nayo na kujishikamanisha nayo. Huku ndiko kuwa na utii wa kweli katika mamlaka hizo kwani kwa kupitia utii huu tumeshikamanishwa na kile kinachotusukuma (mamlaka) kufanya hivyo.

Ndugu zangu katika Kristo, Injili ya leo inatuweka wazi kwa kutufunulia ni kipi kipasacho kusukuma maisha yetu. Kitu hicho ndicho kinachotakiwa kuwa na mamlaka juu ya maisha yako. Yesu anatupa angalizo na kusema, Si kila mtu aniambiaye, Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni,” Mt 7:21. Kwa maana nyingine unaweza kuwa Mbwekaji mzuri sana kwa kuwapendezesha watu wanaokuzunguka kwa kuwaaminisha pasipo kumaanisha, ukawa kama Mbwa anayebweka usiku kucha kumwaminisha tajiri yake kwamba ulinzi upo kumbe ni woga wa miluzi ya upepo. Kumbe ukweli ni kwamba, ni yule tu “afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni (Mungu) ndiye atakayeingia katika ufalme wa mbinguni.” Je, kufanya mapenzi ya Mungu kunamaanisha nini?

Wapendwa wana wa Mungu, kufanya mapenzi ya Mungu ni “kukaa katika pendo” la Mungu. Nasi tumelifahamu pendo alilo nalo Mungu kwetu sisi, na kuliamini. Mungu ni upendo, naye akaaye katika pendo, hukaa ndani ya Mungu, na Mungu hukaa ndani yake,” 1Yoh 4:16. Ni kuwa tayari kuongozwa na mamlaka ya Mungu katika mfumo wa Upendo. Tunakaa katika upendo wa Mungu kwa kuyatimiza mapenzi yake pale tu tunapolipokea neno lake, tunapolisoma neno lake, tunapolifanyia tafiti neno lake, tunapolikumbuka neno lake, na tunapolitafakari neno lake. Haya mambo matano ni muhimu sana kama tunataka kweli kukaa naye na kuyafanya mapenzi yake. Basi kila asikiaye hayo maneno yangu, na kuyafanya, atafananishwa na mtu mwenye akili, aliyejenga nyumba yake juu ya mwamba; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, isianguke; kwa maana misingi yake imewekwa juu ya mwamba,” Mt 7:24-25. Hakuna awezaye kutung’oa kwenye mwamba huu wa imani hata kikija kimbunga cha tsunami. 

 Tusipo lishika neno lake la Mungu vizuri tutakuwa tayari kuongozwa na mamlaka hizi; mila zetu (kwa kufanya yale yanayotutia hofu bila kuhoji sababu yake), desturi zetu (kwa kufanya kadiri ya mapokea ya wazee wetu katika hali ya upofu), hisia zetu (kwa kufanya kadiri ya miyeuko yetu na siyo utashi wetu). Na kila asikiaye hayo maneno yangu asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumba yake juu ya mchanga; mvua ikanyesha, mafuriko yakaja, pepo zikavuma, zikaipiga nyumba ile, ikaanguka; nalo anguko lake likawa kubwa,” Mt 7:26-27. Hakika kwa hali hii tunabaki kuwa kama bendera fuata upepo. Na kwa sababu hiyo, kila ajitokezaye na kutushawishi hatutakuwa na nguvu ya kuimili vishindo vya imani kwani tu wepesi kama pamba.

Hivyo ndugu zangu katika kipindi hiki cha majilio tunapomsubiri Masiha wetu tukae katika neno la uzima. Ni katika hali hii kwamba Mungu atamlinda yeye ambaye moyo wake umekutegemea Katika amani kamilifu, kwa kuwa anakutumaini,” Isa 26:3. Mungu wetu ndiye mwamba wetu wa milele. Tumia muda wako vizuri kulitafakari neno lake la uzima. Kama unaweza kutumia masaa mawili au matatu kwenye runinga, tenga basi hata robo saa kulisoma neno la Mungu na ubaki nalo kwani ndilo lenye uzima. Mtumainini Bwana siku zote Maana Bwana YEHOVA ni mwamba wa milele, kwa kuwa amewashusha wakaao juu, Mji ule ulioinuka, aushusha, Aushusha hata nchi, auleta hata mavumbini,” Isa 26:4-5. Yote yanayotupa matumaini leo na sasa bila Mungu hufifia kama mkaa wa mabua ya mahindi.

Tumsifu Yesu Kristo!


Kila akaaye ndani yake hatendi dhambi; kila atendaye dhambi hakumwona yeye, wala hakumtambua,” 1Yoh 3:6

No hay comentarios:

Publicar un comentario