domingo, 2 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 5 YA KWARESMA


JUMATATU WIKI YA 5 YA KWARESMA

Somo: Dan 13:1-9, 15-17, 19-30, 33-62,

Somo fupi: Dan 13:41c-62

Zab: 23:1-3a, 3b-4, 5, 6

Injili: Yoh 8:1-11, Au Yoh 8:12-20

Nukuu:

“Ewe mzao wa Kaanani, wala si wa Yuda, uzuri umekudanganya, na tamaa imeupotosha moyo wako. Hivyo ndivyo ulivyowafanyia binti za Israeli, na kwa hofu walitembea nawe; bali huyu binti Yuda hakuweza kuustahimili uovu wako,” Dan 13:56-57

“Mara hiyo makusanyiko yote wakapaza sauti kwa nguvu, wakamhimidi Mungu awaokoaye wamtumainio,” Dan 13:60

“Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe.” Yoh 8:7

“Wala mimi sikukuhumu. Enenda zako; wala usitende dhambi tena.” Yoh 8: 11b

“Basi Yesu akawaambia tena akasema, Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima,” Yoh 8:12

“Ninyi mwahukumu kwa kufuata mambo ya mwili; mimi simhukumu mtu,” Yoh 8:15

“Nami nijapohukumu, hukumu yangu ni kweli; kwa kuwa mimi si peke yangu, bali ni mimi na yeye aliyenipeleka,” Yoh 8:16

TAFAKARI: “Mungu mtetezi wa wanyonge, haki na hukumu vina Bwana Mungu wetu.”

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, leo tutafakari neno hili, “Mungu mtetezi wa wanyonge, haki na hukumu vina Bwana Mungu wetu.” Wanyonge mara zote huishi kwa kudra za Mwenyezi Mungu. Kujisalimisha kwao katika unyonge wao ndiyo njia pekee iliyobaki. Haki na mastahili ya mtu ni moja ya asili wake. Binadamu kwa hulka yake (hali ya kutokuwa na utoshelevu na u mimi) na nafasi yake kijamii huvuka mipaka na kuvitwalia haki na mastahili ya wengine (hasa wanyonge) kwa mabavu (ikiwa ni pamoja na kuzipindisha sheria). Kunapokuwa na hali hii, mtetezi wa huyu mnyonge ni Mungu tu, ambaye kwa asili ndiye aliyevifanya hivyo vyote ndani ya mwanadamu.

Somo letu la leo pamoja na Injili, yanatufikirisha ni nini hasili ya haki na hukumu kwa lililo haki na kweli. Binadamu kwa hulka yake ya kujipendelea yeye zaidi, hupora haki ya binadamu mwenzake kwa tamaa zake. Mtume Yakobo anasema, “Lakini kila mmoja hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe huku akivutwa na kudanganywa. Halafu ile tamaa ikiisha kuchukua mimba huzaa dhambi, na ile dhambi ikiisha kukomaa huzaa mauti,” Yak 1:14-15. Wazee ambao kutokana na mang’amuzi yao kimaisha walitegemewa sana kuwa watu wenye hekina, na hivyo kusimamia kweli na haki. Lakini kwa bahati mbaya wanaheshimu tamaa zao za mwili na kudondoka katika uovu.

Kutokana na tatizo hilo katika jamii, Susana anakuwa mmoja ya wale ambao hukandamizwa na kuporwa haki zao. Susana katika hali hii, kimbilio lake na usalama wake unabaki kuwa ni Mungu anayeona yote kwa hali na nyakati zote. Susana anajisalimisha kwa Mungu katika unyonge wake kwa kusema, “Ee Mungu wa milele, Wewe wajua yaliyositirika, wajua mambo yote yasijekuwako, Wewe wajua ya kwamba wananishuhudia uongo, na, tazama, imenipasa kufa; walakini sikufanya kamwe mambo kama hayo, ambayo watu hawa wameyabuni juu yangu kwa ukorofi.” Dan 13:42-43. Ni katika kujiachia huku kwa Mungu aliye hai, Mungu anasikia kilio cha Susana na kutoa utetezi wake na kumsimamisha kijana Danieli ambaye anatenda kweli na haki ya Mungu.

Danieli anakuwa mfano bora na wakuigwa katika jamii kwa kuona uovu ule na kusimama kutetea kweli. Danieli anawaonya hata wale waliokuwa na kauli nzito katika jamii, yaani wazee ambao kwa kuwashwa na tamaa zao wanashindwa kutenda haki na kusimamia kweli. Danieli katika jamii yetu leo anasimama badala ya wasomi hasa waliobobea katika fani ya sheria, ila kwa kuwaka tamaa zao na uroho wa mali wanashindwa kusimamia haki na kweli kwa wote na hasa wanyonge. Danieli anasimama katika nuru ya kweli, na ndani yake umo uzima. Yesu anasema, Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe, bali atakuwa na nuru ya uzima,” Yoh 8:12

Ni katika nuru na uzima huu Danieli anayasema maneno mazito kwa watesi wa Susana bila kupepesa macho, “Ewe mzao wa Kaanani, wala si wa Yuda, uzuri umekudanganya, na tamaa imeupotosha moyo wako. Hivyo ndivyo ulivyowafanyia binti za Israeli, na kwa hofu walitembea nawe; bali huyu binti Yuda hakuweza kuustahimili uovu wako,” Dan 13:56-57. Mmoja kati yetu anaposimama katika kweli, na kutenda haki, Mungu huonekana katika tendo hilo kupitia mtu huyo. “Mara hiyo makusanyiko yote wakapaza sauti kwa nguvu, wakamhimidi Mungu awaokoaye wamtumainio,” Dan 13:60. Ndugu yangu, usiache kutenda mema na kusimama katika kweli. Kutokufanya hivyo ni kumsaliti Mungu aliye kweli, haki, huruma, upendo na hukumu zake zina Yeye daima.

Tukio la Susana linatuonyesha ni kwa namna gani watu wengi na hasa wafungwa wanavyoweza jikuta katika hali ya ufungwa pasipo haki na ukweli, na wakati mwingine hata kupoteza maisha na mali zao. Na si jambo la kushangaza, wezi wakubwa na wahujumu wa kubwa wa uchumi wa nchi hii kuwaona mitaani wakifurahia maisha. Jambo hili si kwamba Mungu haoni, ila lina muda na wakati wake. Mungu kwa kutumia watu wake ipo siku atamsimamisha mmoja kati yetu kama Danieli na yote yatakuwa sawa.

Injili yetu ya leo inasema jambo hilo hilo juu ya kutokuwa na haki sawa kwa wote, ambapo mizani ya hukumu huegemea upande mmoja. Injili inatupa angalizo pia pale tunapotaka kupingana na Mungu na hata kumjaribu. Yesu anapoletewa mbele yake Mwanamke mzinifu, watu hawa, ambao wakiwemo na Wazee, wanataka kumtia hatiani. Yesu Kristo anatambua uovu wao na kuzikumbusha dhamiri zako zilizokufa. Yesu anafufua ndani ya waovu hawa neema na uelewa wa amri ya mapendo. Upendo ambao wameufifisha kwa kutenda uovu, Yesu Kristo anaufufua dhamiri hiyo iliyokufa na kuwafanya watende mema. Kipimo cha kutenda mema ni wao wenyewe kwa kujiweka katika hali ya wanyonge na wale ambao haki zao zinafinyangwa. Zoezi hili la dhamiri Yesu analifanya baada ya kutafakari na kujua uovu wao, na kusema “Yeye asiye na dhambi miongoni mwenu na awe wa kwanza wa kumtupia jiwe.” Yoh 8:7. Kwa maneno haya siyo kwamba Yesu anatutaka tusitoe haki kwa njia ya sheria na hukumu iliyo kweli. La hasha! bali tunapolifanya jambo hili, tujipime kwanza kama na sisi tunayo mastahili hayo mbele ya Mungu. Vile vile, Yesu anatukumbusha kwamba, uhai ni zawadi ya Mungu kwetu, na ni mali yake Mungu. Hukumu yoyote ile kabla na baada  itanguliwe na huruma na upendo wa kweli.

Ndugu yangu, huruma na msamaha wa kweli, ni dawa na njia mwafaka wa kumrekebisha aliyetenda kosa. Mara nyingi watu wengi hawabadiliki tabia zao kwa sababu hawajawahi samehewa wala kuonewa huruma. Unapomsamehe mtu kwa kosa ambalo anajua wazi si rahisi kusamehewa, msamaha huo huwa dawa ya ugonjwa wake wa muda mrefu. Yesu Kristo anatumia njia hii kwa mwanamke huyu mzinifu, na kusema, “Wala mimi sikukuhumu. Enenda zako; wala usitende dhambi tena.” Yoh 8: 11b. Furaha aliyoipata mwanamke huyu ni kubwa sana. Inawezekana katika maisha yake, hakuwahi kupata msamaha kama huu. Hapa pia tunajifunza kwamba, “Mungu mtetezi wa wanyonge, haki na hukumu vina Bwana Mungu wetu.” Ndugu yangu, kwa nini unakosa huruma na msamaha wa kweli hasa katika hali kama ya huyu mwanamke aliyokuwa nayo? Je, wasubiri kupigiwa chetezo na matari?

Tumsifu Yesu Kristo.

“Nami nijapohukumu, hukumu yangu ni kweli; kwa kuwa mimi si peke yangu, bali ni mimi na yeye aliyenipeleka,” Yoh 8:16

Tusali:-Ee Bwana, unifanye chombo cha amani yake. (Mt. Franscisco wa Assis).

No hay comentarios:

Publicar un comentario