ALHAMISI
YA OKTAVA YA PASAKA
Somo: Mdo 3:11-26
Zab: 8: 2ab, 5, 6-7, 8-9
Injili: Lk 24:35-48
Nukuu:
“Tubuni basi,
mrejee, ili dhambi zenu zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako
kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu
mliyewekewa tangu zamani; ambaye
ilimpasa kupokewa mbinguni hata zije zamani za kufanywa upya vitu vyote,
zilizonenwa na Mungu kwa kinywa cha manabii wake watakatifu tokea mwanzo wa
ulimwengu,” Mdo 3:19-21.
“Mungu wa Ibrahimu na
wa Isaka na wa Yakobo, Mungu wa baba zetu, amemtukuza mtumishi wake Yesu,
ambaye ninyi mlimsaliti na kumkana mbele ya Pilato, alipokuwa ametoa hukumu
yake afunguliwe. Bali ninyi
mlimkana yule Mtakatifu, yule Mwenye haki, mkataka mpewe mwuaji; mkamwua yule Mkuu wa uzima, ambaye Mungu
amemfufua katika wafu; na sisi tu mashahidi,” Mdo 3:13-15.
“Na walipokuwa katika kusema habari hiyo, yeye mwenyewe
alisimama katikati yao, akawaambia, Amani iwe kwenu,” Lk 24:36.
“Tazameni mikono yangu na miguu yangu, ya kuwa ni mimi mwenyewe.
Nishikenishikeni, mwone; kwa kuwa roho haina mwili na mifupa kama mnavyoniona
mimi kuwa nayo,” Lk 24:39.
“Akawaambia,
Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba
na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya,” Lk
24:46-48.
TAFAKARI: “Amani iwe kwenu; ni Salamu, Zawadi na
Mtazamo mapya wa maisha ya Ufufuo na Uzima.”
Wapendwa
wana wa Taifa la Mungu, maisha ya ufufuko ni maisha ya amani ya kweli ndani ya
kila mmoja wetu anayeamini ufufuko wa Kristo. Ni kwa maana hii leo tunaalikwa
kutafakari neno hili, “amani iwe kwenu; ni Salamu, Zawadi, na Mtazamo mpya wa
maisha ya Ufufuo na Uzima. Amani kama maisha ya ufufuo na uzima yanajionyesha
na kutendeka wazi katika jumuiya ya kwanza ya Wakristo. Mtume Petro haogopi
kulisema hili mbele ya Wayahudi wenye itikadi kali za kidini na hasa juu ya
Yesu Kristo waliyeutoa uhai wake bila huruma. “Mungu
wa Ibrahimu na wa Isaka na wa Yakobo, Mungu wa baba zetu, amemtukuza mtumishi
wake Yesu, ambaye ninyi mlimsaliti na kumkana mbele ya Pilato, alipokuwa ametoa
hukumu yake afunguliwe. Bali ninyi
mlimkana yule Mtakatifu, yule Mwenye haki, mkataka mpewe mwuaji; mkamwua yule Mkuu wa uzima, ambaye Mungu
amemfufua katika wafu; na sisi tu mashahidi,” Mdo 3:13-15.
Wapendwa
kwa kosa hili la kumwua aliye uzima, yaani, Bwana wetu Yesu Kristo, kurejesha
huruma na msamaha wa Mungu, yatupasa kufanya toba ya kweli. Neema na baraka
huja kwa kukiri pale tulipojikwaa kwa kujua na hata kwa kutokujua, kunakotokana
hasa na kutotimiza wajibu wetu wa kila siku. Toba ya kweli ndicho kielelezo cha
kujenga tena urafiki na uhusiano na Mungu ambao ulibomolewa kwa dhambi zetu, na
tunazidi kuubomoa kwa dhambi zetu hata sasa. Daraja la kuelekea upatanisho huo
na Mungu, limekwisha jengwa tayari kwa sadaka ya Kristo pale msalabani. Naye
Petro anasema, “Tubuni basi, mrejee, ili dhambi zenu
zifutwe, zipate kuja nyakati za kuburudishwa kwa kuwako kwake Bwana; apate kumtuma Kristo Yesu mliyewekewa tangu
zamani; ambaye ilimpasa kupokewa
mbinguni hata zije zamani za kufanywa upya vitu vyote, zilizonenwa na Mungu kwa
kinywa cha manabii wake watakatifu tokea mwanzo wa ulimwengu,” Mdo 3:19-21
Wapendwa
wana wa Mungu, kwa sasa twaweza kuuona uso wa Mungu kwa kupitia kwanaye Yesu
Kristo. Hivyo kupatanishwa na Mungu kunawezekana tu kwa kupitia mwanaye Yesu
Kristo ambaye hata sasa Kanisa linamshuhudia. Kanisa kama chombo katika safari
ya kuelekea uzima wa milele, na Sakramenti ya Wokovu, kinatuwezesha kwa kupitia
maadhimisho ya Sakramenti zake kuuona uso wa Mungu baada ya kushiriki
Sakramenti hizi kwa uaminifu wa kweli. Ndugu yangu, leo tunapatanishwa na Mungu
kupitia mwanaye Yesu Kristo, kwa Sakramenti ya kitubio. Na hapa kwa namna ya
pekee tunaonja upya huruma na neema ya Mungu. Je, lini ilikuwa mara yako ya
mwisho kupokea sakramenti hii?
Injili
ya leo inatuelekeza kuyaona maisha ya Uzima na Ufufuo kupitia Amani ya kweli
ndani mwetu. Zawadi ya Yesu Mfufuka kwa wanafunzi wake na wale wote waliomridhia
ni Amani. “Na walipokuwa katika
kusema habari hiyo, yeye mwenyewe alisimama katikati yao, akawaambia, Amani iwe
kwenu,” Lk 24:36. Baada ya tukio hili, amani
inakuwa ndicho kielelezo cha maisha ya Uzima na Ufufuo. Hakika Mungu hapatikani
katika fujo na machafuko yanayosababishwa na tamaa na ubinafsi wetu. Uhakikisho
huu, yaani, Amani ndani ya mioyo ya Wakristo wa kwanza unaondoa woga na mashaka
yote. Kristo yu hai kweli kweli na siyo hadithi za kufikirika. Yesu Kristo
anawaambia wanafunzi wake waliokuwa wamejificha kwa hofu, “Tazameni
mikono yangu na miguu yangu, ya kuwa ni mimi mwenyewe. Nishikenishikeni, mwone;
kwa kuwa roho haina mwili na mifupa kama mnavyoniona mimi kuwa nayo,” Lk 24:39
Hili ni
hakikisho la wazi kwamba Yesu Kristo hakuwa mzimu fulani katika hali yake ya
kufufuka kwake. Hivyo kuthibitisha kwamba yeye si mzimu, alikula pia kipande
cha samaki wa kuoka kuwahakikishia alikuwa mtu kweli baada ya ufufuko wake.
Mtazamo huu, ndio mtazamo wa Kanisa leo, licha ya changamoto nyingi
tunazozipata nje ya Imani yetu ya Kikristo ambao kwao wanataka kutulazimisha na
kutufanya tuamini kwamba kilichotokea kwa mateso, kifo na ufufuko wa Kristo
kilikuwa ni mchezo wa kuingiza. Kwa mantiki hiii, Kristo Mfufuka anasisitiza
kwa kusema, “Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya
tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba
na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya,” Lk
24:46-48. Ndugu yangu uliyeimarishwa, wewe ni shahidi kweli wa Kristo?
Wapendwa
katika Kristo, hapana shaka kabisa kwa sasa wengi wetu tunaishi kwa hofu kubwa
sana tunapoona Wakristo wenzetu wanauwawa kwa ukatili uliokithiri kwa sababu tu
wao ni Wakristo. Hata hivyo tusisahau ukweli kwamba hata Kanisa hili tunaloishi
leo na kushuhudia imani, limekuwa Imara kama lilivyo kutokana na Damu za wafiadini waliotutangulia kwa
nyakati tofauti katika historia ya Kanisa letu. Bila shaka ni wakati wetu pia
kutoa ushuhuda huo kwa kufa kifo Dini na Imani ya kweli.
Tumsifu Yesu Kristo!
Yesu Akawaambia, “Ndivyo
ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba
na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya,” Lk 24:46-48
Tusali:-Ee Yesu Kristo, katika
hali hii ya sintofahamu juu ya Imani na Ukristo wetu leo, tujalie neema ya kufa
kifo dini katika Imani ya kweli. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario