sábado, 15 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMATATU YA OKTAVA YA PASAKA


JUMATATU YA OKTAVA YA PASAKA

Somo: Mdo 2:14, 22-32

Zab: 16:1-2a, 5, 7-8, 9-10, 11

Injili: Mt 28:8-15

Nukuu:

“Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake,” Mdo 2:32

“Kisha Yesu akawaambia, Msiogope; enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona,” Mt 28:10

“Wakakusanyika pamoja na wazee, wakafanya shauri, wakawapa askari fedha nyingi, wakisema, Semeni, ya kwamba wanafunzi wake walikuja usiku, wakamwiba, sisi tulipokuwa tumelala,” Mt 28:12-13 

TAFAKARI: “Kuishi imani ya kweli”

Wapendwa wana wa Mungu, tukiwa katika oktava ya pasaka, yaani siku nane za Pasaka, kwa leo tutafakari neno hili, “kuishi imani ya kweli.” Moja ya kweli kwamba Kristo amefufuka na yu hai, ni ujasiri wa jumuiya ya kwanza ya Wakristo kuishi kwa matendo na kumuhubiri Kristo mfufuka bila shaka na wasiwasi wowote. Jumuiya hii ya kwanza wapo tayari kwa lolote limuhusuyo Kristo Mfufuka. “Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake,” Mdo 2:32. Ushupavu huu ni kutokana na kuguswa na kuishi uhasilia wa Ufufuko wa Kristo. Hapana shaka kwamba Kristo amefufuka na yu hai katika maisha yetu na hali zetu kila siku.

Uthibitisho huu wa imani huondoa hofu yote kwani tegemeo kubwa lishajionyesha katika maisha ya kila siku. Kufufuka kwa Bwana wetu Yesu Kristo, Yesu analiweka jambo hili wazi kwa wale waliomfia na kumtumainia, “Kisha Yesu akawaambia, Msiogope; enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona,” Mt 28:10.

Ndugu yangu, galilaya yako ni pale unapoishi maisha ya kila siku. Kama mtu wa ndoa, uaminifu wako katika Sakramenti hiyo ni makutano ya Kristo mfufuka na ndiyo Galilaya yako. Kama wewe ni mtawa kama mimi, maisha haya ndiyo ninapokutana na Kristo mfufuka pale ninapoisha nadhiri zangu kwa uaminifu kadiri ya mwongozo wa mwanzilishi wetu na mtazamo wa Kanisa. Nje ya hapo ni kupoteza muda tu. Ni katika hali hii naweza kukutana na Yesu Mfufuka. Hakuna mbadala wake. Ndugu yangu tuheshimu na kuzijali ndoa na maagano yetu na nadhiri zetu katika maisha. Mateso na mahangaiko katika wito wako ni ishara ya wazi kwamba unachokitaka na kukitafuta kina gharama, thamani, na baraka mbele ya uso  wa Mungu. Kifo na ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo kinatufundisha kwamba hakuna UTUKUFU PASIPO MSALABA.

Ukweli huu kuhusu ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo walijaribu kuupotosha lakini hawakuweza. “Wakakusanyika pamoja na wazee, wakafanya shauri, wakawapa askari fedha nyingi, wakisema, Semeni, ya kwamba wanafunzi wake walikuja usiku, wakamwiba, sisi tulipokuwa tumelala,” Mt 28:12-13. Ndugu yangu, huwezi kuzuiya upepe kwa mikono yako. Nguvu na kweli ya Mungu hii juu ya maarifa yetu yote. Hivyo usipo jikabidhi kwa Kristo utajikabidhi kwa shetani. Uchaguzi huu upo chini ya uwezo wako. Njia sahihi na ya kweli ni kujisalimisha mikoni mwa Kristo ambaye ameyashinda yote.

Ndugu yangu, hakuna maisha ya usalama kama hujikabidhi kila siku mikoni mwa KRISTO. Huyu ndiye ajuaye yaliyo kabla na mwisho wa nyakati zetu. Kujikabidhi mikoni mwake kunaitaji utayari wetu tu. Utayari huu ni kufanya mapenzi yake kila siku ya maisha yetu. Ukaribu wetu na Kristo ni kuyafanya mapenzi ya Baba yake aliye Mbinguni. Kwa maana ye yote atakayeyafanya mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni, huyu ndiye ndugu yangu, na umbu langu, na mama yangu,” Mt 12:50.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake,” Mdo 2:32

Tusali:-Ee Yesu Mwema, niongoze katika kuyafanya mapenzi yako na Baba aliye Mbinguni. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario