sábado, 29 de abril de 2017

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 3 YA PASAKA


IJUMAA WIKI YA 3 YA PASAKA

Somo: Mdo 9:1-20

Zab: 117:1ab, 2

Injili: Yoh 6:53-58

Nukuu:

Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe,” Mdo 9:5

“Lakini Anania akajibu, Bwana, nimesikia habari za mtu huyu kwa watu wengi, mabaya mengi aliyowatenda watakatifu wako Yerusalemu; hata hapa ana amri itokayo kwa wakuu wa makuhani awafunge wote wakuitiao Jina lako,” Mdo 9:13-14

“Lakini Bwana akamwambia, Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli,” Mdo 9:15

“Mara akamhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba yeye ni Mwana wa Mungu,” Mdo 9:20

Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu,” Yoh 6:53

“Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi,” Yoh 6:57

TAFAKARI: “Hakuna lisilowezekana kwa Mungu; Sauli afanywa chombo kiteule cha Kristo,”

Wapendwa wana wa Mungu, tukiwa tunazidi kutafakari hujuma dhidi ya jumuiya ya kwanza ya Wakristo huko Yerusalemu, na baada ya kuuwawa Shahidi Stefano, Sauli anaomba barua ili awakamate watu wa njia hii na kuwafunga gerezani. Ni katika mateso haya Kristo mwenyewe analisimamia jambo hili, na kumwongoa mtesaji mkuu wa kundi lake. Tendo hili la Yesu Kristo Mfufuka kulisimamia Kanisa lake na hasa wongofu wa Sauli, linathibitisha kweli ya sala la Yesu kabla ya mateso na kifo chake cha Msalaba. Yesu anasali, “Nilipokuwapo pamoja nao, mimi naliwalinda kwa jina lako ulilonipa, nikawatunza; wala hapana mmojawapo wao aliyepotea, ila yule mwana wa upotevu, ili andiko litimie,” Yoh 17:12. Sauli anapigwa upofu na kuanguka chini. Katika hali hii ya giza na ukimya, Sauli anasema, “U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe,” Mdo 9:5.

Kwa matendo haya ya Sauli, Kanisa la mwanzo halikuwa na amani hata kidogo. Pamoja na hofu hii ya Kanisa la Mwanzo juu ya Sauli na genge lake katika hujuma, anatukumbusha siku ile ya kukamatwa kwake alipowauliza wale Maaskari, ‘Mnamtafuta nani?’ Yoh 18:7. “Yesu akajibu, Nimekwisha kuwaambieni ya kwamba ni mimi; basi ikiwa mnanitafuta mimi, waacheni hawa waende zao. Ili litimizwe lile neno alilolisema, Wale ulionipa sikumpoteza hata mmoja wao,” Yoh 18:8-9. ‘Ili litimizwe lile neno alilolisema-wale ulionipa sikumpoteza hata mmoja wao,’ Mwinjili Yohane anatukumbusha ile sala ya Yesu kabla ya mateso yake, Yoh 17:12, na Yesu Kristo ni nani katika safari hii ya ukombozi wa Mwanadamu, Yoh 1:1-3, 14, 17 (Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. Huyo mwanzo alikuwako kwa Mungu. Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika. Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli. Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo)

Kwa nyakati zetu za leo na hasa Kanisa letu la Tanzania kuna kila aina za dalili kuibuka taswira ya Sauli mwingine wa nyakati zetu. Sauli huyu amefanikiwa kwa kiasi kikubwa kujenga hofu ndani ya waamini leo. Imani yetu leo inawindwa sana. Tumeanza kusongwa na hofu na mashaka hasa tunapokusanyika kwa wingi kumsifu na kumwabudu Mungu. Leo tunaye Sauli mwingine, ambaye huwalipua wakristo na kuwachinja kama kuku. Je, ni mungu gani anayekubali, kubariki na kutetewa na binadamu anayemtoa binadamu mwenzake sadaka tena kwa ukatili kama huu?

Sauli wa nyakati za jumuiya ya kwanza ya Wakristo aliogopeka sana. Hata katika hatua za kumrudishia kuona kwake, haikuwa rahisi wakristo kusadiki kama mtu huyu amemjeukia Kristo. Anania anapoambiwa na Bwana katika maono kufanya kazi hii, anaingiwa na hofu kubwa na mashaka. Anania anajibu, “Bwana, nimesikia habari za mtu huyu kwa watu wengi, mabaya mengi aliyowatenda watakatifu wako Yerusalemu; hata hapa ana amri itokayo kwa wakuu wa makuhani awafunge wote wakuitiao Jina lako,” Mdo 9:13-14. Jambo hili si rahisi kulifanya. Sauli wa leo, siyo tu anamilipuko, bali amejikoka risasi, visu, mapanga, mashoka, na tindikali. Nani anaweza kumsogelea? Nani anaweza kupeleka ujumbe kwa Sauli wa leo kama Anania? Wapendwa wana wa Mungu, leo tunaishi nyakati tofauti kabisa. Mtume Paulo ambaye kabla ya wongofu wake alijulikana kama Sauli, anatupa njia ya kupambana na Sauli wa nyakati hizi kwa kusema, “Usishindwe na ubaya, bali uushinde ubaya kwa wema,” Rum 12:21.

Ndugu yangu, pasipo njia Bwana hufanya njia, I Kor 10:13. Ninayo imani kubwa sana juu ya vita hivi vya kidini. Ni Kristo mwenyewe atakayempiga upofu Sauli huyu wa sana, na kati yetu Kristo atawainua akina Anania na kufanya kazi yake. Yesu Kristo anaondoa hofu ya Anania kwa kumpa ujumbe huu, “Nenda tu; kwa maana huyu ni chombo kiteule kwangu, alichukue Jina langu mbele ya Mataifa, na wafalme, na wana wa Israeli,” Mdo 9:15. Ninaimani katika neno hili kwa Sauli wa leo. Kristo yupo tayari kumtumia Sauli wa leo alichukue Jina lake mbele ya Mataifa, na wakuu wote wa dunia hii. “Kwa kuwa torati ilitolewa kwa mkono wa Musa; neema na kweli zilikuja kwa mkono wa Yesu Kristo,” Yoh 1:17. Sauli wa leo ameibuka na ndoto kubwa na yupo mbioni kuunda dola ya Kisauli. Ni kwa neema na kweli ndani na katika Kristo, naamini kwa kupitia njia hii ya kuushinda ubaya kwa wema Kristo atalisimamia Kanisa lake pote duniani na kumshinda Sauli wa nyakati zetu leo. Kristo tunayemwamini na kumfuata ni Kristo hai na siyo wa historia.

Ni Kristo huyu ninayemwamini na kumhubiri atakaye mgeuza Sauli huyu wa sasa, na kwa kinywa chake atasema kama alivyosema mara ile ya kwanza baada ya kupigwa upofu, na “mara akamhubiri Yesu katika masinagogi, kwamba yeye ni Mwana wa Mungu,” Mdo 9:20. Naweza nisieleweke katika hili, ila hakuna lisilowezekana kwa Mungu. Siamini kabisa kwamba Kristo atavumilia mateso ya waja wake wanaochinjwa kama kuku huko Somalia, Ethiopia, Misri, na Irak. Siamini jambo hili hata kidogo. Ni swala la wakati tu.

Ndugu yangu, ni katika kuushiriki mwili na damu yake Kristo, hasa katika hali hii ya mateso tunapata uzima wa milele. Naye anasema, “Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu,” Yoh 6:53. Mwili huu na damu hii twaweza kuula na kunywa katika hali ya mateso kama sasa, na ndipo tunapofunuliwa na kuupata uzima huo wa milele ndani yetu. Uhai wetu u salama ukiwa ndani ya Kristo kama Yeye alivyo ndani ya Baba daima. “Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba; kadhalika naye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi,” Yoh 6:57. Je, waliamini neno hili?

Tumsifu Yesu Kristo!

Akasema, U nani wewe, Bwana? Naye akasema, Mimi ndimi Yesu unayeniudhi wewe,” Mdo 9:5

Tusali: -Ee Yesu nipe Neema ya kujua maana ya Mateso yangu katika wewe na ndani yako. Nifanye Chombo cha Amani yako, ili niushinde ubaya kwa wema kama ulivyo tupenda upeo na kujitoa sadaka pale Msalabani. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario