martes, 18 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMAPILI YA 2 YA PASAKA-A


JUMAPILI YA 2 YA PASAKA-A

Somo I: Mdo 2:42-47

Zab: 118:2-4, 13-15, 22-24

Somo II: 1Pet 1:3-9

Injili: Yoh 20:19-31

Nukuu:

“Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali,” Mdo 2:42

“Kila mtu akaingiwa na hofu; ajabu nyingi na ishara zikafanywa na mitume,” Mdo 2:43

“Na wote walioamini walikuwa mahali pamoja, na kuwa na vitu vyote shirika, wakiuza mali zao, na vitu vyao walivyokuwa navyo, na kuwagawia watu wote kama kila mtu alivyokuwa na haja,” Mdo 2:44-45

“Na siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, wakimega mkate nyumba kwa nyumba, na kushiriki chakula chao kwa furaha na kwa moyo mweupe, wakimsifu Mungu, na kuwapendeza watu wote. Bwana akalizidisha kanisa kila siku kwa wale waliokuwa wakiokolewa,” Mdo 2:46-47.

“Akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia, Amani iwe kwenu,” Yoh 20:19b

“akawaonyesha mikono yake na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana,” Yoh 20:20

“Akawavuvia, akawaambia, Pokeeni Roho Mtakatifu. Wowote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa,” Yoh 20:22-23

“Mimi nisipoziona mikononi mwake kovu za misumari, na kutia kidole changu katika mahali pa misumari, na kutia mkono wangu katika ubavu wake, mimi sisadiki hata kidogo,” Yoh 20:25

“Lete hapa kidole chako; uitazame mikono yangu; ulete na mkono wako uutie ubavuni mwangu, wala usiwe asiyeamini, bali aaminiye,” Yoh 20:27.

“Tomaso akajibu, akamwambia, Bwana wangu na Mungu wangu!” Yoh 20:28

“Wewe, kwa kuwa umeniona, umesadiki; wa heri wale wasioona, wakasadiki,” Yoh 20:29

Lakini hizi zimeandikwa ili mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini mwe na uzima kwa jina lake,” Yoh 20:31

“Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu,” 1 Pet 1:3:4.

“ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo,” 1Pet 1:7

TAFAKARI: “Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali,” Mdo 2:42.

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya pili ya Pasaka ya mwaka “A” wa Kanisa. Na leo kwa namna ya pekee tutafakari neno hili: “Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate, na katika kusali,” Mdo 2:42. Mafanikio ikiwa ni pamoja na maendeleo makubwa ya Imani katika jumuiya ya kwanza ya Wakristo yalijengeka katika msingi wa UPENDO KWA KWELI, WALIPOISHI NDANI NA KATIKA KRISTO. Tendo hili la upendo, Kristo akiwa kielelezo cha yote, uliwafanya wanajumuiya hawa wa kwanza kujitoa bila kujibakiza. “Na siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu, wakimega mkate nyumba kwa nyumba, na kushiriki chakula chao kwa furaha na kwa moyo mweupe, wakimsifu Mungu, na kuwapendeza watu wote. Bwana akalizidisha kanisa kila siku kwa wale waliokuwa wakiokolewa,” Mdo 2:46-47.

Ndugu yangu, hutoweza kuwa shahidi wa Kristo na neno lake kama haupo tayari kushirikisha wengine kweli ya Kristo iliyopo ndani yako. Kuishirikisha kweli ya Kristo ndani yako kwa wengine ni tokeo la kulitafakari neno la uzima kwa kina kila siku ya maisha yako. Hutoweza kusimama katika neno la Mungu kama hujalielewa na kuwa sehemu ya maisha yako. Kama neno hili ni uzima basi yanipasa kulisoma kila siku na kulitafakari ili liwe uzima ndani yangu. Ni vigumu pia kulitafakari neno la Mungu na kuwa sehemu ya uzima wako kama huwezi kulisikia.

Kulisikia neno la Mungu siyo tu kwa kupitia masikio yetu kama njia moja ya mlango wa fahamu, bali kulisikia kwa kila kiumbe alichokiumba Mungu, na zaidi kutoka mazingira yale unayoyaishi leo na sasa. “Ndipo akawafunulia akili zao wapate kuelewa na maandiko. Akawaambia, Ndivyo ilivyoandikwa, kwamba Kristo atateswa na kufufuka siku ya tatu; na kwamba mataifa yote watahubiriwa kwa jina lake habari ya toba na ondoleo la dhambi, kuanza tangu Yerusalemu. Nanyi ndinyi mashahidi wa mambo haya,” Lk 24:45-48. Neno “kuanza tangu Yerusalemu,” linaweza kutafsiriwa kuwa ni mazingira uliyopo na namna ile ulivyo kila mmoja kadiri ya wito wake. Kuwa shahidi wa neno hili la uzima yanipasa kuanzia pale nilipo. Neno hili lilete uzima ndani ya ndoa yako, maisha yako ya wakfu, na katika huduma unayoitoa kwa watu.

Ni vigumu vile vile kusikia neno hili la uzima kama haupo tayari kulipokea. Kulipokea Neno la Uzima kamwe lisiwe Neno kihistoria, yaani simulizi fulani kwangu na lenye kunipa taarifa ya mambo yaliyopita, bali Neno hilo lanihusu mimi leo na sasa na siyo mtu mwingine. Huku ndiko kulipokea Neno la Uzima kutakapo kupelekea kulisikia, kulitafakari, kulishirikisha, na mwisho kuwa shahidi na kufa shahidi. “Mimi Yohana, ndugu yenu na mwenye kushiriki pamoja nanyi katika mateso na ufalme na subira ya Yesu Kristo, nalikuwa katika kisiwa kiitwacho Patmo, kwa ajili ya Neno la Mungu, na ushuhuda wa Yesu,” Ufu 1:9.

Wapendwa katika Kristo, ushuhuda wa Neno la Uzima ulipelekea kujali na kutaabikiana kwa upendo wa kweli kwa jumuiya ya kwanza ya Wakristo, na kuliweza kutatua matatizo mengi makubwa. Hakuna miongoni mwao aliyeitaji akakosa mahitaji yake. Mt. Augustino ambaye alichukua kielelezo hiki cha maisha ya jumuiya ya kwanza ya Wakristo, na kufanya ndicho msingi wa jumuiya ya Kiagustino, anasema “UKIPENDA UTAFANYA YOTE.” Ni kwa msingi huu na upendo huu wa kweli kwamba, “…wote walioamini walikuwa mahali pamoja, na kuwa na vitu vyote shirika, wakiuza mali zao, na vitu vyao walivyokuwa navyo, na kuwagawia watu wote kama kila mtu alivyokuwa na haja,” Mdo 2:44-45. Jambo la kushangaza leo katika familia zetu, licha ya wanafamilia, yaani Baba na Mama kuunganishwa kwa Sakramenti ya ndoa, wamekuwa wabinafsi kiasi kwamba kila mmoja wao hujifanyia mambo yake bila kumshirikisha mwenzake.

Tatizo kubwa hapa lipo kwa akina Baba. Utaona kila mmoja wao anasema hiki ni changu. Wakati mwingine Baba huwa na viwanja na hata biashara kubwa ambazo mkewe hajui lolote. Mwisho wa siku kinapotokea kifo kwa upande wa Baba, mali yote hupotea na familia kubaki katika hali ya umasikini uliokithiri. Hivi nyie akina Baba, inawezekanaje kumwamini rafiki wako wa kufikia, kuliko kumwamini mkeo na wanafamilia yako? Marafiki hawa wa kufikia ndio wanaojua mikataba yote ya mali na biashara za Baba huyu wa familia. Tujirekebishe! Mkeo ni zaidi ya ndugu na marafiki. Huyu umeunganishwa naye na kuwa kitu kimoja. Unapoanza kumtenga unajipasua mwenyewe na mwisho wake hutobaki salama.

Ndugu zangu, tusipoishi kweli hii hasa katika ngazi ya familia, hakika bado hatujamjua Kristo. Katika kitabu cha ufunuo tunaona namna Yesu anavyojifunua kwa Mtume Yohane kwa njia ya maona na kusema, “Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, na aliye hai; nami nalikuwa nimekufa, na tazama, ni hai hata milele na milele. Nami ninazo funguo za mauti, na za kuzimu,” Ufu 1:17b-18. Mimi na wewe tusipo ijua kweli hii tu bado katika giza, na tunaishi maisha ya kuigiza kwa miaka yote, kila mmoja kadiri ya wito wake. “Kila mtu aaminiye kwamba Yesu ni Kristo amezaliwa na Mungu. Na kila mtu ampendaye mwenye kuzaa, ampenda hata yeye aliyezaliwa na yeye,” 1Yoh 5:1.

Upendo wa kweli ndiyo amri kuu kwa kila aliyebatizwa na kumwamini Kristo. Kwa yeyote anayejiita Mkristo na anayejitambua kuwa ni Mkristo, hakuna mbadala dhidi ya kupenda kuliko kwa kweli. “Kwa maana huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito,” 1Yoh 5:3. Ukipenda kweli, utafanya yote kama asemavyo Mt. Augustino. Wepesi wa amri yeyote ni upendo katika agizo hilo na kwa kutimiza matakwa ya hiyo amri. Jumuiya ya kwanza ya Wakristo inaishi pendo la kweli na kuwa kivutio cha kweli katika huduma na huruma ya Mungu. Na ndivyo ilivyokuwa kwamba, “Nayo makutano ya watu wa miji iliyoko kandokando ya Yerusalemu wakakutanika, wakileta wagonjwa, nao walioudhiwa na pepo wachafu; nao wote wakaponywa,” Mdo 5:16.

Kupenda kuliko kweli ndiko kuzaliwa na Mungu, na kuushinda ulimwengu dhidi ya uovu. Silaha kubwa ya kuushinda ulimwengu huu dhidi ya uovu, ni kupenda kuliko kwa kweli. Wengi wetu ujikuta kufanya maovu kwa vile tu hawakuwahi kupendwa na mara zote hujisikia kusalitiwa na kuhuzunishwa. “Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu,” 1Yoh 5:4.

Jambo hili la kutokupenda kutokana na majeraha na kuumizwa kwetu, linaonekana wazi katika Injili ya leo ambapo tunaona watu wawili (Yesu Kristo Mfufuka na Mtume Tomaso) waliojeruhiwa, ambao mwisho wa siku mmoja wao (Yesu Kristo Mfufuka) anamponya mjeruhiwa mwenzake (Tomaso).

Uponyaji wa kwanza anaoutoa Yesu Kristo kwa wanafunzi wake ni kuiondoa hofu kwa salamu yake ya upendo, “Akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia, Amani iwe kwenu,” Yoh 20:19b. Tendo hili la kuwa na Amani ya kweli ndiyo mwanzo wa kuanza kupenda kuliko kwa kweli na furaha ya kweli. Wanafunzi wa Yesu wanaonyesha furaha hii, na kuanza kupenda tena, ingawa Mtume Tomaso hakuwepo katika kundi. Naye Yesu baada ya salamu ya upendo iliyojaa matumaini mapya, “akawaonyesha mikono yake na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana,” Yoh 20:20.

Furaha hii inaendana na maagizo ya kufanya anayoyatoa Kristo kwa wanafunzi wake. Naye Kristo akawavuvia, akawaambia, “Pokeeni Roho Mtakatifu. Wowote mtakaowaondolea dhambi, wameondolewa; na wo wote mtakaowafungia dhambi, wamefungiwa,” Yoh 20:22-23. Kristo hapendi furaha ya kweli aliyotupatia tubaki nayo wenyewe. Hivyo furaha hii twapasa kuisambaza kwa wengine kila mmoja kadiri ya wito wake, vipaji vyake, dhamana na nafasi yake katika jamii anayoishi. Ndugu yangu ukiona hapo unapoishi hata mbwa wanakukimbia bila sababu, ujue wewe ni shiiiiida!

Tomaso aliporejea anakokujua mwenyewe kwa kupoteza imani yake juu ya Kristo, anapoambiwa jambo hili la kuonekana kwa Kristo, hakuamini hata kidogo. Naye kwa ufahamu wake anatoa vigezo vya kutambua ukweli aliousikia kutoka kwa wenzake. Naye anatoa vigezo na masharti ambavyo lazima vizingatiwe: -“Mimi nisipoziona mikononi mwake kovu za misumari, na kutia kidole changu katika mahali pa misumari, na kutia mkono wangu katika ubavu wake, mimi sisadiki hata kidogo,” Yoh 20:25. Kwa masharti haya na vigezo hivi tunaweza kuona ni kwa jinsi gani Tomaso alivyo jeruhiwa na kusononeshwa kwa tukio la kifo cha Bwana wetu Yesu Kristo.

Wapendwa, baada ya siku nane, tunaona tukio la kukutana kwa wajeruhiwa hawa wawili, yaani Yesu Kristo Mfufuka na Mtume Tomaso. Mjeruhiwa wa kwanza ni Yesu Kristo. Yesu anamkuta Tomaso na kumwonyesha majeraha yake, na kusema, “Lete hapa kidole chako; uitazame mikono yangu; ulete na mkono wako uutie ubavuni mwangu, wala usiwe asiyeamini, bali aaminiye,” Yoh 20:27. Tendo hili la Yesu kumwonyesha Tomaso majeraha yake na kuumizwa kwake kunatoa picha ya majivuno ya Yesu na wakati mwingine kama kujigamba vile. Jambo hili lina ukweli wake kwa mtazamo huu wa majeraha na makovu aliyokuwa nayo Yesu. Majereha ya Kristo na maumivu yake hayakuwa majeraha ya kushindwa, bali majeraha ya UPENDO WA KWELI. Majeraha ya Kristo yalikuwa majeraha ya USHINDI uliotukuka. Hayakuwa majeraha ya kuuma, bali majeraha ya UTUKUFU. Ni majeraha ya UPENDO. Upendo ambao upo tayari kujitoa sadaka bila kipimo na kutojibakiza. Kristo anaonyesha ubavu wake na mikono yake ilivyotobolewa si kwa kujionyesha, kujigamba wala kumuhukumu yeyote, bali kuonyesha uzito na undani wa upendo wake kwa Mitume na kwetu sote.

Japokuwa Tomaso hakuwa na majereha kwenye ngozi yake, na hakuwa na kuvuja damu kutoka mwilini mwake, majeraha yake yalikuwa ndani ya moyo wake. Haya ni maumivu ya ndani. Moyo wake ulijeruhiwa kwa kusikitishwa na kifo cha Bwana wake. Alijisikia kudanganywa na Bwana wake Yesu Kristo. Alijisikia kushindwa baada ya kuyaweka matumaini yote kwa Kristo kwa sababu alifikiri Yesu Kristo ni Masiha, Mfalme, na kuhoji kwa nini Yesu afe kifo katili kama kile cha msalaba? Alifikiri Yesu Kristo angeikomboa Israeli kutoka kwenye dola ya Kirumi. Anajiuliza hivi, kwa nini hata yeye mwenye-Yesu ameshindwa kujinasua kutoka watesi wake? Mtume Tomaso alisikitishwa na kusijikia kusalitiwa na Yesu. Tomaso alishawishika kabisa kwamba alifanya uchaguzi usio sahihi kumfuata mseremala huyu wa Galilaya. Kwa kweli Tomaso alikuwa na maumivu makubwa sana!

Wapendwa maumivu na majeraha ya Moyo huchukua muda mrefu kupona. Majeraha haya na maumivu ya Moyo yanachukua kuda mrefu kupona kwa sababu twaweza kuyaficha na kujifanya hayapo. Twaweza kuongea na kutenda mambo yetu kama vile hakuna jambo lolote baya au upungufu wowote kwetu. Wengi wetu twaweza kukaa katika hali hii kwa miaka mingi kwa kujivisha taswira nyingine na mwonekano mwingine ambao sio uhalisia wa kile kilicho ndani mwetu ingawa tunaendelea na mateso na maumivu hayo. Lakini ukweli ni kwamba hatuwezi kudumu katika hali hii kwa muda wote na nyakati zote. Mara tutaanza kujisikia vibaya na kujisikitikia na kufikiri marafiki zetu wametutenga na wapo mbali bila kutusikiliza maumivu yetu yanayotusonga moyoni. Mara tunajisikia kwamba hawajali na wanaubaridi kuhusu maumivu yetu, na hivyo kuwachukia pia.

Hivyo, katika kukutana kwa wawili hawa hasa kipindi hiki cha pasaka, mmoja wao yaani Yesu Kristo ana majeraha ya UTUKUFU, na mwingine yaani Tomaso ana majereha ya maumivu ya ndani. Yesu Kristo alikuwa tayari kujiponya kwa nguvu ya majeraha yake. Tomaso alihitaji kuponywa majeraha yake lakini hapakuwa na mtu wa kumponya. Hapa ndipo wanapokutana wajeruhiwa hawa wawili. Mjeruhiwa wa kwanza anamponya wa pili. Uponyaji huu unajionyesha kwa maneno ya Tomaso mwenyewe anapomjibu Kristo baada ya Kristo kumtaka kuvitia vidole vyake kwenye makovu na majeraha yake, akisema, “Bwana wangu na Mungu wangu!” Yoh 20:28. Mwisho wa kukutana huku, kila mmoja anapata majeraha ya UTUKUFU, na kuwa tayari kuponya wengine wenye maumivu.

Wapo maelfu ya watu wameumizwa na kujeruhiwa miongoni mwetu. Wengine wanabeba chuki kwa usiri mkubwa ndani ya mioyo yao kwa kusalitiwa kulikotokana na kutokuwa na uaminifu kwa mwenzi wake wa ndoa. Wengine wanabeba chuki dhidi ya wanaofisi wenzao kwa kuwaenezea umbea na uongo mitaani. Wengine pia wanabeba ndani ya mioyo yao chuki na manung’unika kwa milongo ya miaka iliyopita kwa kukosa sehemu ya kuponyeshwa na kusikilizwa. Wengine maumivu haya wanayabeba tangu kuzaliwa kwao hadi sasa kutokana na namna ya kutungwa mimba kwao kuliko kataliwa na kwa bahati mbaya au nzuri akazaliwa. Wengine wamesalitiwa na wapenzi wao na kuyabeba hayo hadi sasa hata kama wanaishi maisha yao ya ndoa. Wapo wengi sana waliojeruhiwa na kuumizwa vibaya kwa namna tofauti tofauti. Jambo hili linaweza kutokea kwa yeyote yule, iwe mlei, mtawa na hata mtawa na mkleri.

Ndugu yangu, hata kama tutayaficha majereha na maumivu yetu, kwa binadamu itafika wakati lazima atayaonyesha tu wazi kwa kutafuta uponyaji. Ni njia mojawapo ya kurudisha mizania ya ndani katika uumbaji wetu. Ukweli ni kwamba walioumizwa kweli na kupata majeraha ya ndani hawawezi kuficha na kuvaa kinyago hicho kwa muda mrefu. Wanaweza kuwadanganya wanaowazunguka kwa wakati tu, ila hawawezi kujidanganya wenyewe na kuficha ukweli huu. Maumivu ya ndani ni vigumu sana kuyavumilia.

Watu hawa wanahitaji uponyaji. Wangepewa nafasi na uchaguzi, wote wangependa kugusa majeraha ya Kristo. Wanapenda kujua kwa uhakika kama kuna mtu anayewapenda vya kutosha kwa kujeruhiwa kwao na mtu huyo yupo tayari kufa kwa kuwapenda. Tatizo kubwa ni kwamba hawawezi kumwona tena Kristo. Wanaweza tu kuwaona watu wanaojiita Wakristo. Wakristo ambao wanajulikana kwa kujinadi kulibeba jina la Kristo na siyo kumuishi Kristo. Swali ni hili: Je wakristo hawa wapo kweli kama Kristo? Je, wakristo leo wameumizwa vya kutosha kwa UPENDO kiasi kwamba wanaweza kuwaponya walioumizwa? Je, ni kweli wakristo leo wamefufuka kutoka kifo cha kujijali wenyewe, na ubinafsi, kwamba wanaweza kuwa matumaini na kielelezo cha kuwarudisha waliopotea kwenye kundi kwa kuumizwa kwao?

Ndugu yangu, kuurithi ufalme wa Mungu, ni kuishi vyema wito wako na vipaji alivyo kupa Mungu. Vipaji hivyo siyo mali yako bali viwafaidie wengine, na hasa katika kuyaponyesha majeraha na maumivu waliyokuwa nayo. Hiki ndicho kielelezo cha maisha yetu kama Wakristo na wafuasi wa Kristo Mfufuka. Jambo hili si katika kuangamizana, bali katika ufaidiana na kuongozana katika umilele ambao ndiyo makusudi ya Ufalme wa Mungu.

Wapendwa katika Kristo, ulimwengu wa leo unamwitaji sana Kristo. Kama ulimwengu usipomwona Kristo kwa Wakristo wa leo, waliojerehiwa watajitoa kwa Mungu, na kubeba mioyo yao inayovuja damu na vidondo visivyoponyeka kwingine kusipo Mungu. Na wanavyojitoa huku ufikia mahali na kuinamisha vichwa vyao na kufikiri katika akili zao: “Mungu amekufa!”

Wapendwa wana wa Mungu, ikiwa wewe ni Mkristo uliye hai ni vyema ukafahamu thamani ya Ukristo wako, yaani umekombolewa kwa Damu ya thamani kubwa sana, yaani Mwana-kondoo, Yesu Kristo. “Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19. Hivyo maisha yako na yangu hapa duniani tunapaswa kuyasalimisha yote na kwa asilimia zote kwa Yesu Kristo Mwana wa Mungu aliye hai. Tendo hili la kujisalimisha ndiko kuabudu kwenyewe kuliko hai na kwenye kumpendeza Mungu.

Kujiita Wakristo bili Kristo ni kupotea muda kabisa kwa sababu kwa kufanya hivyo maisha hayo hayana njia, kweli, uzima (tungali hapa duniani) na ufufuo (maisha ya uzima wa milele), Yoh 14:6. Hivyo ndugu yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, tungali hapa duniani wakuhimidiwa ni Mungu, na kwa njia ya pekee na ufunuo uliokamilika kwa Yeye aliyemwilishwa (Neno), Bwana wetu Yesu Kristo. Kwa Kristo Yesu kuna Njia, Kweli, Uzima, na Ufufuo wa wafu. Kwake Yesu na kupitia kwake tunahesabiwa haki na Mungu kwa wana na warithi wa ufalme wake Mungu. Na kwa namna hiyo, “Ahimidiwe Mungu, Baba wa Bwana wetu Yesu Kristo, ambaye kwa rehema zake nyingi alituzaa mara ya pili ili tupate tumaini lenye uzima kwa kufufuka kwake Yesu Kristo katika wafu; tupate na urithi usioharibika, usio na uchafu, usionyauka, uliotunzwa mbinguni kwa ajili yenu,” 1 Pet 1:3:4. Ndugu yangu, tumaini yenye uzima lipo kwa Kristo Yesu, na siyo kwa kile tulicho au yale tunayoyamiliki hapa duniani. Tungali hapa duniani tu waangalizi wa muda mfupi kwa yale tunayoyamiliki. Kwayo (tunayoyamiliki) kama yalivyo hayana umilele ingawa tuliyakuta na tutayaacha.

Hivyo wapendwa katika Kristo, yatupasa mimi na wewe kuyashinda majaribu tukiwa na ufahamu kwamba ‘maisha ni jaribu,’ na kulishinda jaribu ndipo kunakotupatia Imani yenye thamani kupita yote tuwezayo kuwa nayo. Vita vyetu vya kiimani kama anavyotufundisha Mtume Petro ni kulishinda jaribu ili kwamba kujaribiwa kwa imani yenu, ambayo ina thamani kuu kuliko dhahabu ipoteayo, ijapokuwa hiyo hujaribiwa kwa moto, kuonekane kuwa kwenye sifa na utukufu na heshima, katika kufunuliwa kwake Yesu Kristo,” 1Pet 1:7. Tokeo la kubebwa na ulimwengu wa vitu ni anguko kubwa la ‘uzuni.’ Furaha ya kweli ipo pale tunapoyasalimisha yote kwa Kristo Yesu. Kristo awe tegemeo na msukumu wa yote tuyafanyayo, na tumuone kwa wengine yale yote tuyafanyayo katika jamii tunayoishi. Lengo hapa siyo tu kuzishika au kuzifahamu amri za Mungu kama ndege yule ‘kasuku,’ bali amri hizo za Mungu zimulike uhai uliopo ndani yetu binafsi na wale wote tuliowekwa dhamana kwao ikiwa ni pamoja na  wale wenye uhitaji wa pekee.

Bwana na Bibi Bakari Salum wenye asili ya Uarabuni walijijenga kwa muda mrefu kwenye biashara yao ya kuuza juice ya embe. Iliwachukua miaka 12 hivi kwa shida na taabu, na leo wana kiwanda kikubwa cha juice.

Miaka miwili iliyopita baada ya biashara kupanuka walimwajira kijana mmoja kutoka China kama Meneja masoko. Hata hivyo kwa muda wote huo wa kuishi pamoja familia hii haikubahatika kupata mtoto ingawa ilikuwa hamu yao kubwa.

Mwaka mmoja uliopita ikiwa ni pamoja na kupanuka kwa biashara yao ya juice, walibahatika kumpata mtoto wao wa kwanza wa kiume. Mtoto huyu tangu siku za uchanga wake alionekana akiwa na macho madogo sana. Hali hii haikumfurahisha Bwana Bakari Salum. Hivyo aliona ni vyema kuonana na Daktari bingwa wa macho kujua kulikoni.

“Daktari, mtoto wangu huyu tangu kuzaliwa kwake naona ana tatizo la macho, na kama ikiwezekana afanyiwe upasuaji ili aone vizuri,” Bakari alimweleza Daktari. Hata hivyo baada ya vipimo Daktari hakuona tatizo lolote kuhusu macho ya mtoto yule.

“Ndugu Bakari, mtoto wako ana macho ya kawaida kabisa na hana tatizo lolote. Tofauti ni kwamba macho yake ni madogo kuliko yenu wazazi. Nafikiri mtu wa kufanyiwa upasuaji ni wewe ili uone vizuri,” Daktari alimweleza Babari huku akitabasamu.

“Daktari wataka niambia nini kwa jibu hili?” Bakari alimuuliza Daktari kwa taharuki. “Nenda nyumbani kwako na kazini mwako mtafute mwenye mfanano wa macho ya mtoto wako. Ila kuwa na kifua kama mwanamme,” Daktari alisisitiza.

Mara Bakari ilimjia picha ya Meneja wake wa masoko, na hasa ukaribu wake na mke wake. Ujumbe wa Daktari ulifika mahali pake!

“Bwana wangu na Mungu wangu!” Yoh 20:28.

Tusali:-Ee Yesu Mwema kwa majeraha yako ya Utukufu, yaponye maumivu yetu ya ndani. Amina.

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario