lunes, 3 de abril de 2017

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 5 YA KWARESMA


IJUMAA WIKI YA 5 YA KWARESMA

Somo: Yer 20:10-13

Zab: 18:1-2a, 2bc-3, 4-5, 6

Injili: Yoh 10:31-42

Nukuu:

“Lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha, kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili, wataona aibu ya milele, ambayo haitasahauliwa kamwe. Lakini, Ee Bwana wa majeshi, wewe wawajaribu wenye haki, waona viuno na mioyo, nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu,” Yer 20:11

“Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba,” Yoh 10:37-38

TAFAKARI: “Uovu wa mtu hufunika mema yote, Mungu mtetezi wa mwenye haki.”

Wapendwa wana wa Mungu, “uovu wa mtu hufunika mema yote ya mtu mwenye haki, ila Mungu hubaki kuwa mtetezi wa mwenye haki.” Chuki iliyojaa wivu kwa mtu humfanya kuwa kipofu na hivyo kutokuona mazuri kwa wenzeke. Hali hii inajitokeza kwa Yeremia na Yesu Kristo. Mtu mwenye haki anafanyiwa hila za kila namna ilimradi hasiweze kufanikisha jambo alifanyalo.

Yeremia anafanyiwa njama na kukatishwa tamaa kutokana na msimamo wake juu ya imani yake na Mungu. Mtu kwenye haki anaposimama katika lililojema, Mungu huwa muhimili wake. Kupingwa vita kwa kutenda mema ni vita ya kiroho. Hapa yakupasa kusimama imara katika kweli na kamwe usitie shaka kwa hicho unachokisimamia. Mungu hatokuacha. Mungu atakupigania daima.

Nabii Yeremia anajikuta katika wakati mgumu, hasa pale anapoona hakuna hata mmoja anayemuunga mkono licha ya ujumbe wa Mungu anaoutoa. Yeremia anafahamu kuwa anachofanya si chake bali ni ujumbe wa Mungu. Yeremia hatii shaka juu ya Mungu. Na hivi anasema, “Lakini Bwana yu pamoja nami, mfano wa shujaa mwenye kutisha, kwa hiyo hao wanaonionea watajikwaa, wala hawatashinda; watatahayarika sana. Kwa sababu hawakutenda kwa akili, wataona aibu ya milele, ambayo haitasahauliwa kamwe. Lakini, Ee Bwana wa majeshi, wewe wawajaribu wenye haki, waona viuno na mioyo, nijalie kuona kisasi chako juu yao; kwa maana nimekufunulia wewe neno langu,” Yer 20:11

Mara zote tunapomtegemea Mungu, hatuachi katika sintofahamu zetu. Hali aliyokuwa nayo Yeremia kwa watesi wake, ndiyo hiyo hiyo Yesu anayopambana nayo na Wayahudi. Wayahudi hawaoni mema ayafanyayo Yesu, na hivyo njia pekee iliyobaki ni kuutoa uhai wake. Makuhani na Mafarisayo wanapatwa na hofu kwa vile Yesu anakubalika kwa mafundisho yake na hasa ukweli anaoufundisha kuhusu ufalme wa Mungu.

Hofu za kisiasa, kimaslahi na kimadaraka zinawafanya Makuhani na Mafarisayo kumwangamiza Yesu Kristo mapema. Yesu Kristo anapewa shutuma ya kukufuru kwa kujiita yeye ni mwana wa Mungu. Lakini jambo la ajabu ni Wayahudi kuwa na mioyo migumu na kutotambua ukweli, nguvu na uwezo aliokuwa nao Yesu. Kutambua kwamba anachofanya si kwa mapenzi yake ila ya Mungu, Yesu anawasihi kwa kusema, “Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba,” Yoh 10:37-38

Ndugu yangu, kutambua mema kutoka kwa wenzetu ni kutambua uzuri na Utukufu wa Mungu ambao ujifunua na kujionyesha kwa viumbe vyake alivyoviumba kwa namna hiyo ya ajabu. Hii ni njia mojawapo muhimu ya kukua na kukomaa kiroho. Kutotambua ukweli huu, hutupofusha na kupelekea kufanya dhambi ya mauti. Ndugu yangu, unapokosa uimara katika kuona mema kutoka kwa mwenzako itakuwia vigumu kuwa na mizania sawa katika kutoa hukumu ya kweli. Badala yake utaruhusu na kusukumwa sana na hisia na vionjo vyako. Hata kama hatumpendi mtu kwa kile alicho, basi tuona uzuri wake kwa yale ayafanyao.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kama sizitendi kazi za Baba yangu, msiniamini; lakini nikizitenda, ijapokuwa hamniamini mimi, ziaminini zile kazi; mpate kujua na kufahamu ya kuwa Baba yu ndani yangu, nami ni ndani ya Baba,” Yoh 10:37-38

Tusali:-Ee Mungu, nijalie mara zote kuona na kutambua wema na uzuri ulio kwa mwenzangu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario