sábado, 29 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMAPILI YA 3 YA PASAKA-A


JUMAPILI YA 3 YA PASAKA-A

Somo I: Mdo 2:14, 22-33

Zab: 16:1-2, 5, 7-8, 9-10, 11

Somo II: 1Pet 1:17-21

Injili: Lk 24:13-35

Nukuu:

“Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake,” Mdo 2:32

“Kisha Yesu akawaambia, Msiogope; enendeni, mkawaambie ndugu zangu waende Galilaya, ndiko watakakoniona,” Mt 28:10

“Na ikiwa mnamwita Baba, yeye ahukumuye kila mtu pasipo upendeleo, kwa kadiri ya kazi yake, enendeni kwa hofu katika wakati wenu wa kukaa hapa kama wageni,” 1Pet 1:17

Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19

Ikawa katika kuzungumza na kuulizana kwao, Yesu mwenyewe alikaribia, akaandamana nao,” Lk 24:15.

“Macho yao yakafumbwa wasimtambue,” Lk 24:16.

“Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli,” Lk 24:19-21.

“Akawaambia, Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake?” Lk 24:25-26.

Wakamshawishi wakisema, Kaa pamoja nasi, kwa kuwa kumekuchwa, na mchana unakwisha,” Lk 24:29.

TAFAKARI: “Kaa pamoja nasi Bwana.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya tatu ya Pasaka ya Mwaka “A” wa Kanisa. Masomo yetu ya leo yanatutafakarisha namna ya kukaa na Bwana wetu Yesu Kristo. Huu ni mkao wa Kipasaka. Ni mkao wa ufufuko. Ni mkao wa kuyatafuta yale ya juu Kristo aliko, Kol 3:1.

Wapendwa wana wa Mungu, moja ya kweli kwamba Kristo amefufuka na yu hai, ni ujasiri wa jumuiya ya kwanza ya Wakristo kuishi kwa matendo na kumuhubiri Kristo mfufuka bila shaka na wasiwasi wowote. Jumuiya hii ya kwanza wapo tayari kwa lolote limuhusuyo Kristo Mfufuka. “Yesu huyo Mungu alimfufua, na sisi sote tu mashahidi wake,” Mdo 2:32. Ushupavu huu ni kutokana na kuguswa na kuishi uhasilia wa Ufufuko wa Kristo. Hapana shaka kwamba Kristo amefufuka na yu hai katika maisha yetu na hali zetu kila siku.

Injili yetu ya leo inatupa umuhimu wa kukaa muda wote na Kristo Mfufuka. Maisha yetu yanapita kwa kasi sana kama moshi, na wakati mwingine tunaishi tukiwa wakavu sana kiroho. Yesu Kristo kwa walio wengi ni Yesu wa Historia. Kwa walio wengi Yesu huyu hana nguvu tena. Tatizo kubwa tunalokutana nalo katika maisha ni kuyaweka matamanio yetu mbele zaidi ya mafundisho na kweli anayotufundisha Kristo. Sintofahamu hii inawakuta wanafunzi wale ambao wanaona Kifo cha Kristo kama tukio la kudanganywa hivi, na hakuna maana kabisa kwa yule ambaye walimtegemea sana na leo anawaangusha. Kifo hiki cha aibu cha msalaba kwa wanafunzi hawa kimewatoa matumaini yote.

Yesu Kristo hata katika sintofahamu hizi, bado yupo tayari kutusikiliza na kuzidi kutufundisha, licha ya kwamba hatumuoni kwa kuificha taswira yake, ili mradi tu tumpe nafasi. “Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha. Nasi tulikuwa tukitumaini ya kuwa yeye ndiye atakayewakomboa Israeli,” Lk 24:19-21.

Yesu hachoki kutukumbusha yaliyompasa kufanya na yaliyotabiriwa juu yake. Haya yote yapo katika Maandiko Matakatifu. Mt. Jerome anasema hivi kuhusu Yesu Kristo, “tunapokuwa wajinga wa maandiko matakatifu, ni kwa namna hiyo hiyo tu wajinga kuhusu Yesu Kristo.” Kuhusu jambo hili Yesu anatupa sababu ya yale yote yaliyojiri kuhusu Kifo na Ufufuko wake. “Enyi msiofahamu, wenye mioyo mizito ya kuamini yote waliyoyasema manabii! Je! Haikumpasa Kristo kupata mateso haya na kuingia katika utukufu wake?” Lk 24:25-26. Ndugu yangu hapa tunakumbushwa pia, kwamba hakuna Utukufu pasipo Msalaba. Penye Msalaba pana Utukufu, na sasa ni rahisi kuupata Utukufu kwa sababa Kristo kesha ushinda Msalaba.

Wapendwa, Kristo anajifunua kwetu leo katika kuumega mkate. “Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao,” Lk 24:30-31. Kuumega mkate kunatanguliwa na kulishwa neno lake na kulielewa. Tukio la wanafunzi wa Yesu kukutana naye njiani kuelekea Kijiji cha Emau, ni mtiririko mzima wa adhimisho la Misa Takatifu. Adhimisho hili lina sehemu kuu mbili; Liturjia ya neno na liturjia ya Ekaristi Takatifu. Kwa mantiki hii, uwezekano wa Kristo kujifunua kwetu wakati wa Ekaristi Takatifu, unabebwa kwanza na ufahamu wetu wa kulisikiliza neno lake, kulipokea, kulitafakari, kulishirikisha, na kuliishi. Wanafunzi hawa wa Yesu wanakuwa na hamu ya kukaa naye zaidi baada ya kulishwa neno na Kristo ingawa hawakumfahamu.

Ndugu zangu, wale ambao wamezoea kuchelewa na mara nyingine kushiriki tu liturjia ya Ekaristi Takatifu, ni wavamizi wa Mlo Mtakatifu wasioujua vizuri. Ni sawa na kukishambulia chakula kitamu na kizuri wakati ukiwa na mikono michafu. Ni vizuri kuhudhuria sehemu zote mbili za kiliturjia na ndivyo inavyotakiwa kwa Mkristo na hasa kwetu, ambao Ekaristi Takatifu kicho kiini cha yote. Wapo kati yetu ambao huingia Kanisani na moja kwa moja kujongea Meza ya Bwana. Huu ni uhuni wa hali ya juu kufanywa na Mkristo. Mwisho na muhimu tusichoke kuudhuria mara kwa mara maadhimisho ya Maabudu ya Yesu wa Ekaristi-Sakramenti Kuu. Hapa anakaa kwetu na kujifunua kwetu.

Kukaa na Kristu kunatuwajibisha kubadili mitazamo yetu ikiwa ni pamoja na kuyaacha mazoea yetu yasiyokuwa na mwelekeo. Kukaa na Kristo ni kuishi maisha yanayoongozwa na malengo. Jambo hili si rahisi sana kwa sababu linakufanya uishi maisha ya kisadaka. Na sadaka nzuri na yenye kumpendeza Mungu ni ili inayouma. Ni sadaka ili inayasema zaidi kile ulicho, na ukitoe chote bila kujibakiza. Hili ndilo fumbo zima la Msalaba.

Pamoja na ugumu huo, Yesu anatutaka tutofautishe namna yetu ya kutenda na kuishi ili tulenge fumbo lile la kifo chake cha Msalaba ambapo ndipo ulipotundikwa wokovu wetu na kumpatia Kristo Utukufu wake, nasi kuhesabiwa haki ya kuwa wana wa Mungu bila ya mastahili yetu binafsi. Nanyi mfahamu kwamba mlikombolewa si kwa vitu viharibikavyo, kwa fedha au dhahabu; mpate kutoka katika mwenendo wenu usiofaa mlioupokea kwa baba zenu; bali kwa damu ya thamani, kama ya mwana-kondoo asiye na ila, asiye na waa, yaani, ya Kristo,” 1Pet 1:18-19.

Damu hii yenye thamani kubwa iwe chachu na kielelezo cha imani yetu na kumwamini Mungu. Ni kwa Damu hii ya Mwana-kondoo huyu aliye na hila, Yesu Kristo, “ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hata imani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu,” 1Pet 1:21. Hivyo tenda na ishi yetu isukumwe kwa kuthamini kukombolewa kwetu huku kuliko kwa thamani kubwa ajabu.

Kristo Yesu hali akijua hulka yetu wanadamu anatukumbusha kuepuka kutawala wengine kwa mabavu kama asemavyo, “Mwajua ya kuwa wale wanaohesabiwa kuwa wakuu wa Mataifa huwatawala kwa nguvu, na wakubwa wao huwatumikisha,” Mk 10:42. Kristo hataki hilo litokee kwa Mitume na wafuasi wake. Kinyume chake tutangulize mbele ‘kutumika vyema’ na siyo ‘kutumikiwa wala kuogopwa.’ “Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika, na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi,” Mk 10:45. Maana yake nini?

Wapendwa wana wa Mungu, Kristo anatutaka tuelewa kuwa utumishi ni kujitoa kwa watu kwa upendo na kuwapenda. Huwezi kuwatumikia watu vizuri kama huwapendi. Na ukifanya hivyo (kuwatumikia ukiwa huwapendi) basi nyuma yake kuna ubinafsi mkubwa na kujitazama wewe tu, familia yako, ndugu zako, marafiki zako, na mwisho kupoteza dhima nzima ya kutumika na umma. Hapa tunahitaji nidhamu ya hali ya juu na yenye kusukumwa na utii wa kweli. Hivyo, “Mkiisha kujitakasa roho zenu kwa kuitii kweli, hata kuufikilia upendano wa ndugu usio na unafiki, basi jitahidini kupendana kwa moyo,” 1Pet 1:22. Kupendana kwa moyo ni kumwona Kristo Yesu kwa wote unaotumika kwao. Hapa ndipo kule kutoa nafsi yako iwe fidia ya wengi, Mk 10:45b.

Pili, kuwa tayari kutumika kunatutaka kusahu uzamani wetu na mazoea yetu. Ni kuzaliwa mara ya pili kwa kuliishi neno la Mungu lenye uzima. Kuliishi neno la Mungu lenye uzima kwanza kabisa ni kuwa tayari kuhusu neno hilo. Pili, ni kuwa na uwezo wa kusikia neno, kulipokea neno, kulitafakari neno, kulishirikisha neno, na kuwa shahidi wa neno hilo likiakisi maisha yako. Kwa kuwa mmezaliwa mara ya pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu lenye uzima, lidumulo hata milele,” 1Pet 1:23. Ndugu yangu, neno hili tunahubiriwa kila siku. Lifanye kuwa sehemu ya maisha yako kwa sababu, Neno la Bwana hudumu hata milele. Na neno hilo ni neno lile jema lililohubiriwa kwenu,” 1Pet 1:25.

Tatu, kuwa tayari kutumika ni kuukubali utumishi kwanza ambao mwisho wa siku ndio utakao sadifu ukubwa ule kama kweli ndio unaoutamani. Hivyo, “bali mtu anayetaka kuwa mkubwa kwenu, atakuwa mtumishi wenu,” Mk 10:43b. Pili, kuikubali hali ya utumwa kwa ajili ya wote. Hali hii ya utumwa ndiyo itakayotuweka kuwa wa kwanza au wa mwisho. Hivyo, “na mtu anayetaka kuwa wa kwanza wenu, atakuwa mtumwa wa wote,” Mk 10:44.

Ndugu yangu, huu ndio utumishi na kutumika kwa yeyote yule mwenye hofu ya Mungu. Na kama upo tayari kutumika na unamatamanio haya, omba hivyo  ukifahamu wajibu wa kile ukiombacho. La sivyo hutotumika vyema na mwisho wa siku ni kupoteza vyote: Utakatifu wako, na uzima ule wa milele.

Mama Vituka aliye na Kilabu cha pombe ya kienyeji kwa jina la ‘Kilimani’ ni marufu sana kijijini Mtakuja. Jumapili iliyopita kwa jambo la kushangaza hakupata na wateja wa pombe yake ya kienje hadi ilipofika saa kumi na mbili jioni alipoinga mlevi mmoja maarufu kijijini hapa ajulikanaye kwa jina la Matumaini.

Matumaini alipofika kwenye Kilabu kile, Mama vituka alimpatia bohora la pombe la ulanzi. Matumaini alilifyonza kwa hisia kali huku akiimba wimbo wa mwanamzika Bob Marley, “Afrika Unity” akiwa akidesadesa.

Basi wapita njia walipomwoma Bwana Matumaini akikwa na bohora la ulazi huku akiimba kwa hisia wimbo ule, nao walijongea kwani ilipata kiashirio kwamba sehemu ile pombe ipo.

Baada ya nusu saa Kilabu kile kilijaa watu na pombe iliuzika haswa. Kwa kelele za Bwana Matumaini, Mama Vituka aliamua kumtimua nje ili wateja wake wapate utulivu. Kwa kitendo kile watu wote walisimama na kusema kwa ukali, “asingekuwa Bwana huyu, tusingelijua hapa kama kuna kinywaji hiki. Tunaomba usimbughuzi. Mpe pombe sisi tutamlipia.”

Ndugu zangu, wakati mwingine yawezekana mambo yakakuendea vizuri sana, ila usibweteke. Yawezekana kuna akina Bwana Matumaini wengi sana wamekufanya uwe kama ulivyo.

Hivyo, leo Kanisa letu lipo imara kwa sababu Yesu Kristo Mfufuka na aliye hai yupo nasi. Uwepo wa Ekaristi Takatifu waupa uhai Kanisa letu Takatikafu. Wengi miongoni mwetu na wasio jua fumbo hili wanaweza kubeza sana kwa sababu wanaona maumbo haya ya Mkate na Divai kama yalivyo kwa mwono wake wa nje, ila hawajui kile kibebacho fumbo hilo. Amina!

“Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao,” Lk 24:30-31.

Tusali:- Ee Yesu, kamwe usituache katika sintofahamu zetu. Kaa nasi daima. Amina.

No hay comentarios:

Publicar un comentario