domingo, 9 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMANNE YA WIKI KUU


JUMANNE YA WIKI KUU

Somo: Isa 49:1-6

Zab: 71:1-2, 3-4a, 5ab-6ab, 15, 17

Injili: Yoh 13:21-33, 36-38

Nukuu:

“Wewe u mtumishi wangu, Israeli, ambaye katika wewe nitatukuzwa,” Isa 49:3

“Ni neno dogo sana wewe kuwa mtumishi wangu ili kuiinua kabila za Yakobo, na kuwarejeza watu wa Israeli waliohifadhiwa. Zaidi ya hayo nitakutoa uwe nuru ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya dunia,” Isa 49:6

“Amini, amin, nawaambieni: Mmoja wenu atanisaliti,” Yoh 13:21

“Ndiye mtu yule nitakayemtowelea tonge na kumpa.” Akatowelea tonge, akalitwaa akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote. Na baada ya hilo tonge Shetani alimwingia. Basi Yesu akamwambia, “Uyatendayo yatende upesi,” Yoh 13:26-27

“Amin, amin, nakuambia: Jimbi hatawika hata wewe utakapokuwa umenikana mara tatu.” Yoh 13:38

TAFAKARI: “Saa ya  kutukuzwa Bwana wetu Yesu Kristo inakaribia; hofu na mfadhaiko wa kusalitiwa vikirindima.”

Wapendwa wana wa Mungu, ni wazi tunakaribia saa ile muhumu sana katika safari ya wokovu wetu. Kuelewa siri ya muda na hali aliyokuwa nayo Yesu Kristo, yatupasa kuzama ndani ya tafakari hii kuhusu, “saa ya kutukuzwa Bwana wetu Yesu Kristo inakaribia; hofu na mfadhaiko wa kusalitiwa vikirindima.” Yesu Kristo akiwa na asili ya Kimungu na Kibinadamu, kama mwanadamu yupo katika wakati mgumu sana na mfadhaiko wa moyo ambao hakuna aliyeweza kushiriki naye katika mahangaiko haya. Hali hii ya mahangaiko na upweke ni kubwa na mateso makubwa kuliko tendo hile la kusulubiwa pale msalamani. Hapa Yesu anaumia na kujeruhiwa mwili na roho. Hakika ni mateso makubwa sana.

Ni ukweli usiotia shaka kwamba, hata wanafunzi wake, hawakuwa na wazo kama yatakayotokea baadaye pale msalabani yanaweza kuwa hivyo kwa mtu waliyemjua hasa kwa nje, juu ya uwezo wake, miujiza na nguvu ya ajabu. Kutokuamini huku kunajionyesha baada ya ufufuko wa Yesu Kristo kwa wale wanafunzi waliokuwa wakienda katika kijiji cha Emau, Lk 24:13-34. Kutokana na sintofahamu waliyokuwa nayo, Kristo Mfufuka anataka kujua kulikoni. Mmoja wao Kleopa, anamjibu Yesu bila kujua kama ndiye Bwana, na kusema,  “Je! Wewe peke yako u mgeni katika Yerusalemu, hata huyajui yaliyotukia humo siku hizi? Akawauliza, Mambo gani? Wakamwambia, Mambo ya Yesu wa Nazareti, aliyekuwa mtu nabii, mwenye uwezo katika kutenda na kunena mbele za Mungu na watu wote; tena jinsi wakuu wa makuhani na wakubwa wetu walivyomtia katika hukumu ya kufa, wakamsulibisha,” Lk 24:18-20. Ndugu yangu, ni kwa mtazamo huu waliokuwa nao wanafunzi kwamba kifo hakiwezi kumpata Kristo. Hivyo mahangaiko aliyonayo Yesu sasa na wakati huu, hakuna aliweza kuyashiriki, na mbaya zaidi hata wale aliokuwa nao karibu.

Ni simanzi kubwa na zito kuona mateso ndani yako, lakini wanaokuzunguka wazo hilo halipo kwao. Kwa mfadhaiko Yesu anasema, “Amini, amin, nawaambieni: Mmoja wenu atanisaliti,” Yoh 13:21. Ndugu yangu, hata katika hali hii, Yuda anapewa nafasi ya kujirudi na kuacha mpango wake. Yesu Kristo katika hali hii, hakutaka jambo hili liwe siri. Baada ya kuulizwa nani huyo ambaye anataka kumsaliti, Yesu analiweka wazi jambo hili na kusema, “Ndiye mtu yule nitakayemtowelea tonge na kumpa.” Akatowelea tonge, akalitwaa akampa Yuda, mwana wa Simoni Iskariote. Na baada ya hilo tonge Shetani alimwingia. Basi Yesu akamwambia, “Uyatendayo yatende upesi,” Yoh 13:26-27. Ndugu yangu, ni mara ngapi tunasutwa na dhamiri zetu katika kufanya jambo ovu na bado tunaendelea na mpango wetu huo mwovu?

Pamoja na hali hii, Yesu lazima atimize yale yote yaliyosemwa juu yake na Manabii. Yesu Kristo Mtumishi wa Mungu, anatukuzwa katika saa hii kupitia mateso na kifo cha msalaba, na kwa namna hiyo naye Mungu anatukuzwa. Nabii Isaya analitabiri hili kwa kusema, “Wewe u mtumishi wangu, Israeli, ambaye katika wewe nitatukuzwa,” Isa 49:3. Yesu Kristo anatimiza ahadi ya Mungu na kwa kupitia kifo chake wote tunapata wokovu naye anakuwa  nuru ya Mataifa yote. “Ni neno dogo sana wewe kuwa mtumishi wangu ili kuiinua kabila za Yakobo, na kuwarejeza watu wa Israeli waliohifadhiwa. Zaidi ya hayo nitakutoa uwe nuru ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya dunia,” Isa 49:6.

Yesu Kristo anapokaribia kutukuzwa na kumtukuza Mungu, hakosi kukumbana na usaliti ambao tumeuona kwa Yuda Iskariote, na sasa kwa upande wa Petro. Petro naye hayupo nyuma kutoa ahadi hewa kwa Yesu. Petro anamdanganya Kristo kwa kusema yupo tayari kuyatoa maisha yake kwa ajili ya kuzuia kifo cha Yesu. Yesu kwa mara nyingine anatoa angalizo kwa Petro kujirudi kabla ya saa ile. Yesu anamwambia Petro, “Amin, amin, nakuambia: Jimbi hatawika hata wewe utakapokuwa umenikana mara tatu.” Yoh 13:38. Ndugu yangu, katika safari hii ya kuelekea kilele cha wokovu wetu, Yesu hachoki kufundisha na kututaka kujirudi katika ahadi zetu zisizotekelezeka na hali yetu ya dhambi kwa ujumla. Petro kama mimi na wewe, tunapewa nafasi ya kufanya tafakari ya kina juu ya ahadi zetu katika maisha na wito wetu, na kutathimini yale tuyasemayo kama kweli yanaendana na matendo yetu. TAFAKARI NA CHUKUA HATUA!

Tumsifu Yesu Kristo!

“Amini, amin, nawaambieni: Mmoja wenu atanisaliti,” Yoh 13:21

Tusali:-Ee Yesu, nishirikishe mahangaiko yako katika SAA hii ninapoutazama Msalaba wako Mtakatifu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario