viernes, 31 de marzo de 2017

TAFAKARI: JUMAPILI YA 5 YA KWARESMA-A


JUMAPILI YA 5 YA KWARESMA-A

Somo I: Eze 37:12-14

Zab: 130:1-2, 3-4, 5-6, 7-8

Somo II: Rom 8:8-11

Injili: Yoh 11:1-45

Nukuu:

Basi tabiri, uwaambie, Bwana MUNGU asema hivi; Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu, nami nitawaingizeni katika nchi ya Israeli,” Eze 37:12

“Naye Yesu aliposikia, alisema, Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo,” Yoh 11:4

“Lakini Yesu alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa,” Yoh 11:13-14

“Yesu akamwambia, Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?” Yoh 11:25-26

“Akamwambia, Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni,” Yoh 11:27

“Basi Mariamu alipofika pale alipokuwapo Yesu, na kumwona, alianguka miguuni pake, akamwambia, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa,” Yoh 11:32

“Yesu akalia machozi,” Yoh 11:35

“Wale waufuatao mwili hawawezi kumpendeza Mungu,” Rum 8:8

“Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake,” Rum 8:9

“Na Kristo akiwa ndani yenu, mwili wenu umekufa kwa sababu ya dhambi; bali roho yenu i hai, kwa sababu ya haki,” Rum 8:10

“Lakini, ikiwa Roho yake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu,” Rum 8:11

TAFAKARI: “Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu. Nami nitatia roho yangu ndani yenu, nanyi mtaishi.”

Wapendwa wana wa Mungu, pamoja na maendeleo aliyoyafikia mwanadamu leo, ikiwa ni pamoja na kuishi kwa kujiwekea vilinda uhai wake, “life securities,” hata hivyo uhakika huo bila Mungu ni sawa na kutwanga maji katika kinu. “Kwa sababu hakuna mtu miongoni mwetu aishiye kwa nafsi yake, wala hakuna afaye kwa nafsi yake. Kwa maana kama tukiishi, twaishi kwa Bwana, au kama tukifa, twafa kwa Bwana. Basi kama tukiishi au kama tukifa, tu mali ya Bwana,” Rum 14:7-8. Ndugu yangu, pamoja na mipango yako ya muda mfupi na mrefu uliyojiwekea, kati yetu hakuna ajuaye ni kitu gani kitakachomtokea sekunde chachetu tu zijazo. Je, tusifanye chochote kwa kuwa huu ndio ukweli? Hapana! Tuyafanye na kuyapanga yote katika usahihi wake, na tufanye hivyo kwa kumshirikisha Mungu kwa kila jambo.

Mara nyingi penye mafanikio-‘kibinadamu,’ wengi wetu hitaji na uwepo wa Mungu huwa hitaji la nyongeza. Tunaamini yote huenda sawa bila Yeye (Mungu) kuwepo. Hiki ndicho kiburi kikubwa sana cha mwanadamu asiye na hofu ya Mungu ndani yake. Hali na mazingira haya yanawakuta wana wa Israeli nyakati zile za Nabii Ezekieli. Mungu anawafananisha waasi hawa wa imani kama mifupa isiyokuwa na nyama. Na hivi ndivyo wana hawa wa Israeli walivyofananishwa na Mungu (mifupa isiyo na nyama wala uhai) katika swala zima la imani. “Mifupa hii ni nyumba yote ya Israeli; tazama, wao husema, Mifupa yetu imekauka, matumaini yetu yametupotea; tumekatiliwa mbali kabisa,” Eze 37:11. Bila mkono wa Mungu tuyafanyayo hata kama yatavuma sana hayatakuwa na mwisho mzuri. Na hivi ndivyo Nabii Ezekieli alivyozamishwa na Mungu katika tafakari nzito na chukuliwa nje katika roho ya Bwana.

Hata katika hali hii ya uasi na kukosa dira katika imani, Mungu hapendi hata mmoja wetu apotee. Mungu ndiye uhai na uzima kwa kila kipumuacho, na Yeye huweza kubadili tabia na mienendo ya vyote alivyoviumba. “Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu,” 1Sam 2:6-7. Mungu akiwa ndiye yote na katika yote, kwa upendo na huruma wake, “humwinua mnyonge kutoka mavumbini, Humpandisha mhitaji kutoka jaani, Ili awaketishe pamoja na wakuu, Wakakirithi kiti cha enzi cha utukufu; Kwa maana nguzo za dunia zina Bwana, Naye ameuweka ulimwengu juu yake,” 1Sam 2:8. Tunapomrudia Mungu katika toba na majuto ya kweli, Mungu huyabadili maisha yetu na kutufanya wapya mbele za macho yake. Na hivi ndivyo alivyoitoa ahadi yake kwa wana wa Israeli na kusema, “Tazama, nitafunua makaburi yenu, na kuwapandisha kutoka katika makaburi yenu, enyi watu wangu, nami nitawaingizeni katika nchi ya Israeli,” Eze 37:12. Naye Mungu asema hivi juu ya mifupa ile ikiwa ni pamoja na hali nzima ya udhaifu wako na wangu kwamba, “Tazama, nitatia pumzi ndani yenu, nanyi mtaishi,” Eze 37:5. Hakuna jambo la kumshinda Mungu kwa sababu namna tulivyo, na vyote tulivyonavyo vyaonyesha Furaha ya Mungu, na kuufunua Utukufu wake.

Wapendwa katika Kristo, ukweli huu kwamba hakuna jambo la kumshinda Mungu, na kweli kwamba namna tulivyo na vyote ulivyonavyo vyaufunua utukufu na furaha ya Mungu, vinajidhihirisha katika Injili ya leo kwa Lazaro kurudishiwa uhai wake. “Naye Yesu aliposikia, alisema, Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo,” Yoh 11:4. Pamoja na kweli kwamba Wayahudi walimwinda Yesu ili wa mwangamize, Yesu hakuwa na hofu ya kurudi kwao na kuyafanya mapenzi ya Baba yake. Naye “…akawaambia wanafunzi wake, Twendeni Uyahudi tena,” Yoh 11:7. Wanafunzi wa Yesu kwa hofu iliyomwisha jengeka kwa kukoswa koswa Yesu kuuawa, wanapokea habari hii kwa mashaka. “Wale wanafunzi wakamwambia, Rabi, juzijuzi tu Wayahudi walikuwa wakitafuta kukupiga kwa mawe, nawe unakwenda huko tena?” Yoh 11:8.

Ndugu yangu, mpango ‘ovu wa mwanadamu’ kamwe hauwezi kufanikiwa kwa lile jema alilokwisha likusudia Mungu kulifanya, ingawa Mungu aweza ruhusu ovu ili kulipata jema katika ukamilifu wake. Yesu akiwa analijua hilo aliwaondolea hofu wanafunzi wake na kuwajibu, “Je! Saa za mchana si kumi na mbili? Mtu akienda mchana hajikwai; kwa sababu aiona nuru ya ulimwengu huu,” Yoh 11:9. Kwa maneno mengine Yesu anataka kukuambia wewe na mimi hivi: -‘palipo dhamiri njema na safi katika kulifanya jambo jema na lenye kumpendeza Mungu hapana sababu ya kuwa na hofu licha ya kweli kwamba mazingira ya kulifanya jambo hilo yameghubikwa na utata.’ Leo mambo mengi yanakwenda ndivyo sivyo kwa sababu tu kati yetu na tulio wengi tumejawa hofu pasipo hofu, kuifunga midomo yetu tunapotakiwa kusema, na mwisho wa siku kwa kujua twashirika moja kwa moja katika ‘ovu hilo’ licha ya kwamba twajiweka mbali na kweli hiyo. Na hapa ndipo penye anguko kubwa kwa sababu mmoja kati yetu “…“akienda usiku hujikwaa; kwa sababu nuru haimo ndani yake,” Yoh 11:10.

Ndugu yangu, kile alichokisema Yesu, yaani, “…mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru,” Yoh 8:32, ndicho anachotaka kukithibitisha mbele ya wanafunzi wake. Na zaidi ya hayo Yesu anakutaka wewe na mimi leo kuamini pasipo shaka yoyote kwamba Yeye ndiye njia, na kweli, na uzima; na mtu haji kwa Baba, ila kwa njia yake, Yoh 14:6. Ni katika mantiki hii Yesu anawaambia wanafunzi wake kwamba, “…Rafiki yetu, Lazaro, amelala; lakini ninakwenda nipate kumwamsha,” Yoh 11:11. Hata hivyo wanafunzi wake hawakufahamu alichomaanisha Yesu kwa maneno hayo. Tafsiri ya alichokisema Yesu ni hiki: “…alikuwa amenena habari ya mauti yake; nao walidhania ya kuwa ananena habari ya kulala usingizi. Basi hapo Yesu akawaambia waziwazi, Lazaro amekufa,” Yoh 11:13-14.

Ukweli ni kwamba hata baada ya Yesu kuiweka habari ile ya Rafiki yake wazi, yaani, Lazaro kuwa amekufa, Tomaso aitwaye Pacha-mwanafunzi wake Yesu, anabeba habari ile kwa wepesi mkubwa bila kufikiri na kuzama ndani kwa kile alichokisema Yesu. Na hivi ndivyo ilivyokuwa: “Basi Tomaso, aitwaye Pacha, akawaambia wanafunzi wenziwe, Twendeni na sisi, ili tufe pamoja naye,” Yoh 11:16. Hapa Tomaso anaonekana mtu asiye na hofu wala shaka, ila wakati utathibitisha kile alicho Tomaso. Ni Tomaso huyu huyu baada ya ufufuko wa Yesu aliyekuwa mtu mwenye mashaka mengi juu ya ufufuko wa Kristo.

Swali la kujiuliza ni hili:-ikiwa Yesu alijua fika habari ya kuumwa kwake Lazaro hadi kupatwa na mauti, kwa nini basi alijichelewesha kufika na kumponya ugonjwa wake kabla ya kufikwa na mauti hiyo? Ndugu yangu mpendwa, sehemu ya kwanza la swali hili Yesu mwenyewe kesha ijibu. Na jibu ni hili: -“Ugonjwa huu si wa mauti, bali ni kwa ajili ya utukufu wa Mungu, ili Mwana wa Mungu atukuzwe kwa huo,” Yoh 11:4. Na sehemu ya pili ya jibu la swali hili inathibitisha kile alicho Kristo Yesu, yaani, ndani na katika Yeye ipo njia, kweli na uzima, Yoh 14:6. Na ndiyo maana kwa makusudi kabisa Yesu anafika siku ya nne baada ya kifo cha rafiki yake Lazaro. Siku ya nne ikiwa mwili waanza kuoza hakuna tena uwezekano wa kurudi katika ‘hali hai’ kadiri ya mila na desturi za kiyahudi. Hivyo “…Yesu alipofika, alimkuta amekwisha kuwamo kaburini yapata siku nne,” Yoh 11:17

Kuchelewa kwa Yesu kunaongeza uzuni na majonzi kwa dada zake Lazaro- Martha na Mariamu. “Basi Martha akamwambia Yesu, Bwana, kama ungalikuwapo hapa, ndugu yangu hangalikufa. Lakini hata sasa najua ya kuwa yo yote utakayomwomba Mungu, Mungu atakupa,” Yoh 11:21-22, 32. Lakini ukweli ni kwamba alipo Kristo halijaharibika jambo kwa sababu, “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika,” Yoh 1:3. Yesu anawandolea hofu, mashaka, na uzuni Martha na Mariamu kwa kuthibitisha kile alicho, kwamba, “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi; naye kila aishiye na kuniamini hatakufa kabisa hata milele. Je! Unayasadiki hayo?” Yoh 11:25-26. Naye Martha pasipo shaka anamjibu Yesu, “Naam, Bwana, mimi nimesadiki ya kwamba wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu, yule ajaye ulimwenguni,” Yoh 11:27. Huzuni na majonzi haya ya Martha na Mariamu, pamoja na majirani zao, ikiwa ni pamoja na imani ile waliyokuwa nayo juu ya Kristo Yesu, inaunyong’onyeza moyo wa Yesu sana. “Yesu akalia machozi,” Yoh 11:35. Tendo hili linathibitisha pasipo shaka asili wa pili wa Yesu, yaani, ‘ubinadamu wake.’ Hakika Yesu anakupenda wewe na mimi upeo, Yoh 13:1.

Kwenye jambo hili la ‘ubinadamu wake Yesu,’ linakuwa kejeri kwa Wayahudi. “Basi Wayahudi wakasema, Angalieni jinsi alivyompenda. Bali wengine wao wakasema, Je! Huyu aliyemfumbua macho yule kipofu, hakuweza kumfanya na huyu asife?” Yoh 11:36-37. Ndugu yangu, alipo Kristo halijaharibika jambo! “Basi Yesu, hali akiugua tena nafsini mwake, akafika kwenye kaburi. Nalo lilikuwa ni pango, na jiwe limewekwa juu yake,” Yoh 11:38. Kwa nini basi Kristo ashindwe ikiwa “Vyote vilifanyika kwa huyo; wala pasipo yeye hakikufanyika cho chote kilichofanyika?” Yoh 1:3. Ni swala la wakati tu! Hapa tunakumbushwa kuwa na subira kwa kila jambo hasa pale tunapogubikwa na sintofahamu. Wewe na mimi katika hali hii ya sintofahamu twapaswa kumwachia Kristo Yesu usukani wa maisha yetu. Majigambo na kujikweza hakutatupeleka kokote. Kama wakati fulani ulifanikiwa na ukajiona mafanikio hayo ni kutokana na uwezo wa kiakili zako, utajiri wako, na misimamo yako kijamii na kisiasa, basi jua kwamba safari bado. Dhababu ili iwe thahabu kweli lazima iwe imepita katika moto mkali. Na utajua dhahabu hiyo imefika kiwango cha kuitwa dhahabu pale tu utakapoona sura yako kwenye dhahabu hiyo. Je, waujua udhaifu wako?

Wapendwa wana wa Mungu, ni Kristo peke yake awezaye kutuondolea uzuni na majonzi yetu. Mara  “Yesu akasema, Liondoeni jiwe. Martha, dada yake yule aliyefariki, akamwambia, Bwana, ananuka sasa; maana amekuwa maiti siku nne,” Yoh 11:39. Haijalishi ni kwa kiasi gani tumedhoofishwa na magonjwa yetu, mateso yetu, na sintofahamu zetu. Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba pamoja na hayo yote, ‘ukiamini utaona utukufu wa Mungu, Yoh 11:40. Na ndivyo ilivyo kuwa kwa familia ya Martha na Mariamu. “Basi wakaliondoa lile jiwe. Yesu akainua macho yake juu, akasema, Baba, nakushukuru kwa kuwa umenisikia. Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia siku zote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki kwamba ndiwe uliyenituma,” Yoh 11:41-42. Yesu ndiye kimbilio na mteteze wetu mwaminifu. Ni wewe na mimi kujiaminisha na kujisalimisha kwake.

Wapendwa wana wa Mungu, kwa imani Yesu hututoa katika vifungo vya udhaifu wetu. Kristo kesha ikata minyororo ya kuzimu naye anazo fungu za mauti na za kuzimu, Ufu 1:17-18. Kwa Kristo Yesu uzima upo. Hivyo “Naye akiisha kusema hayo, akalia kwa sauti kuu, Lazaro, njoo huku nje,” Yoh 11:43. Lazaro anarudishiwa uhai wake, na kwa tendo hilo Mungu anaufunua utukufu, uzuri, na furaha yake kwa wale wote wenye kumwamini. “Basi wengi katika Wayahudi waliokuja kwa Mariamu, na kuyaona yale aliyoyafanya, wakamwamini,” Yoh 11:45. Amina!

Hivyo wapendwa wana wa Mungu, ni vema ukafahamu jambo hili la msingi kuhusiana na uumbaji wa Mungu na sababu ya kuishi kwetu. Napenda kuyachukua maneno haya ya Mtume Paulo kwamba, “kwa kuwa vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea kwake. Utukufu una yeye milele. Amina,” Rum 11:36. Jambo la msingi hapa ni kweli kwamba Mungu hakuhitaji kukuumba wewe, bali alichagua kukuumba kama ulivyo kwa furaha na utukufu wake. Kwa maana hiyo, maisha yetu hapa duniani yapaswa kuufunua, kuuonyesha Utukufu wa Mungu, na furaha yake.

Ndugu zangu katika Kristo, mwanadamu angali akiwa hapa duniani utoa Utukufu wa Mungu na furaha yake kwa kufanya mambo yafuatayo: Mosi, kwa kumwabudu Mungu, yaani maisha yako yote, kwa kuwapenda watu wengine bila kumbagua ye yote. Pili, kwa kuishi na kuwa kama Kristo. Tatu, kwa kutumia vipaji vyako vyote kwa ajili ya wengine, yaani kufaidiana. Na nne, kwa kueneza habari njema za Mungu kila pande za dunia. Hata hivyo licha ya ukweli huu, mwanadamu huyu anaweza kuufunua utukufu wa Mungu na furaha yake kwa kutenda matendo ya roho, Gal 5:22-23, na siyo yale ya mwili yasiyo na uzima ndani yake, Gal 5:19-21. “Kwa kuwa nia ya mwili ni mauti; bali nia ya roho ni uzima na amani,” Rum 8:6. Mtu hawezi kumpenda Mungu kama anafuata matendo ya mwili wake tu.

Ni kweli kwamba kiini cha dhambi ni pale mtu anapojipenda yeye zaidi kuliko Mungu. “Wale waufuatao mwili hawawezi kumpendeza Mungu,” Rum 8:8. Hivyo basi kama tunataka kuishi na kuwa kama Kristo lazima tufuata sheria ya roho, yaani, matendo ya roho, ambayo ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria, Gal 5:22-23. Uzima huu tuupatao kwa matendo ya roho upo ndani ya Kristo pale tunapotaka kuishi na kufanana naye. “Kwa sababu sheria ya Roho wa uzima ule ulio katika Kristo Yesu imeniacha huru, mbali na sheria ya dhambi na mauti,” Rum 8:2. Hivyo kwa kuishi na kufanana kama Kristo tunaufunua Utukufu wa Mungu na furaha yake ya kutuumba.

Wapendwa wana wa Taifa la Mungu, kwa upande mwingine, sheria ya dhambi ni matendo yale yasiyo na uzima ndani yake, na kwayo kamwe hatuwezi kuurithi ufalme wa Mungu. Matendo haya ni haya; uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo. Mtume Paulo anasisitiza kwamba, “katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21. Je, hutaki kuurithi ufalme wa Mungu na maisha ya umilele?

Kuishi na kutenda kwetu ili kuwe kwa sifa na utukufu wake Mungu kwa tulazimu kufikiria mambo ya roho.Kwa maana wale waufuatao mwili huyafikiri mambo ya mwili; bali wale waifuatao roho huyafikiri mambo ya roho,” Rum 8:5. Ndugu yangu, utawezaje basi kuishi na kufanana na Kristo kama muda wote wa ufuata mwili na kufikiri mambo ya mwili? Hii ni changamoto kwa kila mmoja wetu. Ni kweli kwamba hatuwezi kuyawaza ya roho kama hatuna mwili. Jambo la msingi na la kufahamu hapa ni kwamba ‘vitu vyote vyatoka kwake, viko kwa uweza wake, tena vinarejea kwake. Utukufu una yeye milele,’ Rum 11:36. Hivyo hakuna kilicho chako katika maana ya umiliki halali zaidi ya dhambi zako. Sasa nifanye nini katika hali hii?

Wapendwa katika Kristo, tunahitaji roho wa Kristo ndani yetu ili tuyafuate matendo ya roho na mwisho tuwe mali ya Kristo. Roho huyu ni zawadi kwetu kutoka kwa Mungu, na hufanya kazi ndani yetu kadiri apendavyo yeye kututumia kadiri ya mpango mzima wa Mungu. Hivyo, “ikiwa Roho yake yeye aliyemfufua Yesu katika wafu anakaa ndani yenu, yeye aliyemfufua Kristo Yesu katika wafu ataihuisha na miili yenu iliyo katika hali ya kufa, kwa Roho wake anayekaa ndani yenu,” Rum 8:11. Hapa ndipo tunapoona Upendo na Huruma ya Mungu kwetu. Mungu hapendi hata mmoja wetu apotee kwa sababu ya dhambi zake. Mimi na wewe tunapewa kila siku fursa ya kutubu na kumrudia Mungu. Katika mantiki hii yanipasa kuzitazama dhambi zangu, kuzitubu, na mwisho kuwa huru kutoka utumwa huu wa dhambi. Ni kwa namna hiyo hiyo sina haki wala sababu ya msingi kuwanyooshea vidole wengine ilhali mimi mwenyewe nahitaji upendo na huruma ya Mungu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Wale waufuatao mwili hawawezi kumpendeza Mungu,” Rum 8:8

Tusali:-Ee Yesu na Mkombozi wangu, bila Wewe mimi si lolote wala chochote. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario