domingo, 23 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 2 YA PASAKA


JUMATATU WIKI YA 2 YA PASAKA

Somo: Mdo 4:23-31

Zab: 2:1-3, 4-6, 7-9

Injili: Yoh 3:1-8

Nukuu:

Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake,” Mdo 4:26

Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote,” Mdo 4:29

ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu,” Mdo 4:30

Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri,” Mdo 4:31

Yesu akajibu, akamwambia, Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu,” Yoh 3:3

“Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu,” Yoh 3:5

Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho,” Yoh 3:6

TAFAKARI: “Kuishi na kuongozwa na Roho Mtakatifu ni kuzaliwa mara ya pili na huku ni kuuona ufalme wa Mungu.”

Wapendwa wana wa Mungu, tukiwa bado tunaitafakari jumuiya ya kwanza ya Wakristo, pamoja na umoja na upendo wao wa kindugu, jumuiya hii iliongozwa kwa Nguvu za Roho Mtakatatifu. Umoja wao na upendo wao, ni tunda la Roho Mtakatifu. Kwa kupitia Roho Mtakatifu, waliweza kufanya mambo makubwa sana dhidi ya ukweli waliousimamia na kuushuhudia. Kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, mateso yao na manyanyaso yao walijeuka kuwa tunu na msingi wa Imani. Roho Mtakatifu aliwaongoza vyema na kuwawezesha kuyapokea mateso kama sehemu ya kujipatia utakatifu.

Kilio cha Jumuiya ya kwanza ya Wakristo kwa kadiri ya mateso yao, walikielekeza kwa Mungu aliye yote katika yote. Na hapa tunapata umoja wao huo katika kuishi, kunena, na kutenda kwao. Wanajua sababu ya chanzo cha mateso yao na mahangaiko yao kimetokana na nini. Sababu ya mateso na manyanyaso yao kimetokana na kuishi kweli katika Kristo. “Wafalme wa dunia wamejipanga, Na wakuu wamefanya shauri pamoja Juu ya Bwana na juu ya Kristo wake,” Mdo 4:26. Ndugu yangu, hatutaweza kushinda vita vya kiroho kama hatujui tunapigana na nini, na kimbilio letu ni nina. Leo kuna mashambulio mengi ya kiroho. Yapo mashambulio yanayotoka nje na ndani ya nafsi yetu. Mashambulio yatokayo nje ya nafsi yetu ni moja ya mikataba tunayoweka kwa kujua au kwa kutokujua. Mikatamba hii ambayo mwisho wake ni mateso bila Kristo, ni pamoja na ibada na mitambiko ya mizimu.

Wapo Wakristo wengi na tena wale wa jumapili ambao kwayo ibada hizi ndizo vielelezo vya maisha na Imani yao. Ukristo kwao ni kama chuma kilichopakwa dhahabu kwa nje tu. Ukikikwangua kidogo chuma hiki unakutana na uhalisia wa chuma chenyewe. Kwa maana nyingine ni kwamba ukristo wao ni wa juu juu tu ya ngozi. Kabla ya kuikuta damu, unakutana na upagani uliokithiri. Wakristo wa mtindo huu waliobatizwa na kumpoteza Roho Mtakatifu, kamwe hawataweza kuyasema maneno haya waliyoyasema jumuiya ya kwanza ya wakristo mbele ya watesi wao. “Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote,” Mdo 4:29.

Mkristo wa mtindo wa Ibada za kuzimu na mvaa mahirizi, hataweza kunena, kushinda uovu kwa nguvu ya Roho Mtakatifu, wala kuwa na uwezo wa kufanya ishara na maajabu kwa mkono wa Yesu. Mambo haya yawezekana tu kwa wale waliozaliwa mara ya pili, yaani wa Roho Mtakakatifu. Hawa ndiyo wenye mamlaka ya kunyoosha “mikono yao kuponya; ishara na maajabu na hufanyika kwa jina la Mtumishi wao Mtakatifu Yesu,” Mdo 4:30.

Waliozaliwa mara ya pili ni watu wale ambao mara baada ya sala na maombi hunena kwa ujasiri bila woga, na mahali hapo hutikiswa kwa nguvu ya Roho Mtakatifu. Roho anapofanya kazi yake, mahali hapo hutakaswa. Huku ndiko maana halisi kwa kutikiswa. Jambo hili linatokea kwa jumuiya ya kwanza ya Wakristo. “Hata walipokwisha kumwomba Mungu, mahali pale walipokusanyika pakatikiswa, wote wakajaa Roho Mtakatifu, wakanena neno la Mungu kwa ujasiri,” Mdo 4:31. Roho huyu katika kufanya kazi yake mara baada ya kumpokea huleta umoja na upendo katika jamii husika.

Jambo la kusikitisha leo kumetokea mifumuko ya nyumba za sala zenye mwelekeo wa ubinafsishaji wa Roho Mtakatifu. Roho Mtakatifu hatuwezi kumzuia kwa ukuta. Roho Mtakatifu hufanya kazi yake kadiri apendavyo na kwa yeyote ampendaye. Ninayaita “makanisa” haya nyumba za sala kwa sababu utambulika kwa majina binafsi ya wachungaji wao, mfano; Kanisa la Edgar, Kanisa la nabii Ngowi, Kanisa la Mzee wa Mpako Kagesa, nk. Kanisa ni la Kristo, na Roho huyu ufanya kazi katika Kristo na ndani ya Kristo.

Somo letu la Injili, Bwana Yesu Kristo anakazia sana kuzaliwa kwa mara ya pili. Naye anamjibu Nikodemo, na anasema, “Amin, amin, nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu,” Yoh 3:3. Ndugu yangu, kumbe kuuona ufalme wa Mungu ni kuzaliwa mara ya pili. Nikodemo ambaye alikuwa Mfarisayo aliyebobea, alikuwa mfuasi wa Kristo wa usiku, yaani wa siri. Kristo anapomshauri azaliwe mara ya pili anamtaka kuvunja mikataba yake ya siri, na hasa mashambulio ya ndani ya nafsi. Kuzaliwa huku mara ya pili ni kujiachia kabisa bila kujibakiza nafsi yako kwa chochote nje ya Mungu Baba, Kristo na Roho Mtakatifu. Ni kumruhusu Roho Mtakatifu awe mtawala wa hekalu lako yaani mwili wako.

Ndugu yangu kukubali mikataba hii ya ndani na nje ya nafsi, ni kubaki tu ndani ya mwili na kwa ajili ya mwili, ambao hushambuliwa sana kwa sababu uhasilia wake, yaani, mwili ni kuchoka na kuzeeka. Naye Yesu anasema, Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho,” Yoh 3:6. Umilele wetu upo kwenye Roho ya kweli ya Mungu kwa sababu yeye ni Roho halisi. Roho huyu ndiye atupaye uwezo wa kulitamka jina la Yesu lenye mamlaka. Mtume Paulo anasema, “kwa hiyo nawaarifu, ya kwamba hakuna mtu anenaye katika Roho wa Mungu, kusema, Yesu amelaaniwa; wala hawezi mtu kusema, Yesu ni Bwana, isipokuwa katika Roho Mtakatifu,” 1Kor 12:3.

Wapendwa ni vizuri ukafahamu ukweli wa jambo hili. Mtu kamili anakuwa katika sehemu kuu tatu:-NAFSI, ROHO, na MWILI. “Mungu wa amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi Nafsi zenu na Roho zenu na Miili yenu mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.” I The 5:23. Katika mwono huo, Roho na Nafsi huwa pamoja na ndizo wewe mwenyewe. Mwili ni nyumba ya Roho na Nafsi. Katika uumbaji Mungu aliumba mwili kwa udongo halafu akapulizia pumzi puani ambayo ni roho yake ndipo mtu huyo akawa nafsi iliyo hai. “Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi, akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Mwa. 2:7. Miili tuliyonayo ni nyumba ya NAFSI na ROHO. Kwa hali hii sisi binadamu ni wawili. Kuna mtu wa ndani na mtu wa nje. Mtu wa ndani ni Nafsi na Roho, na mtu wa nje ni Mwili lakini watu hawa wapo pamoja hatuwezi kuwatenganisha wala kumwona kwa macho ya nyama huyu mtu wa ndani, ila yupo.

Kwa maana hiyo, kwenye Nafsi ndipo penye magonjwa yenyewe kwani ni katikati ya Roho na Mwili. Je, maumivu ya ndani hutoka wapi? Tuone haya yafuatayo:-Kudumu katika madhara ya dhambi na kuendelea kuhifadhi moyoni, Matukio mabaya yanayokusononesha, Kutosamehe kwa muda mrefu. Vile vile hupata maumivu kutoka ROHONI:- Dhambi na Laana. Maumivu kutoka MWILINI:-Mazingira, Tabia za watu wanaokuzunguka, Mateso na matukio ya kuhuzunisha. Tuelewe kwamba NAFSI hutawaliwa na Hisia, mfano:-Hofu, Chuki, Hasira, Kujihukumu, Kujikataa, Kukosa furaha, Kukosa upendo, Kukosa amani, n.k

Wapendwa katika hali hii tufanye nini? Ni muhimu sana mtu atawale hisia zake. Nafsi ambayo ipo katikati ya Mwili na Roho, ikiegemea rohoni huleta matunda mzuri. “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo hakuna sheria.” Gal. 5:22-23. Ila nafsi inapoingia katika Mwili mambo huwa mabaya kwani ufanya matendo ya mwili kama tusomavyo katika maandiko matakatifu, “basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya: uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu, hasira, fitina, faraka, uzushi husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na hayo; katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” Gal.5:19-21. Ni vizuri kujua nafsi yako imeegemea wapi. Ikiegemea rohoni utaenda Mbinguni, ikiegemea mwilini hutaiona mbingu. Ni kwa ukweli huu ambao Yesu leo anaoungelea kwa Nikodemo na kusema, “Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu,” Yoh 3:5

Roho huyu Mtakatifu ndiye atupaye muhuri wa ukombozi. “Wala msimhunishe yule Roho Mtakatifu wa Mungu; ambaye kwa yeye mlitiwa muhuri hata siku ya ukombozi,” Efe 4:30. Roho Mtakatifu ndiye hutupa mastahili mbele ya Mungu na si kwa matendo ya haki, au,  ujanja na werevu wetu hapa duniani. “Si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu,” Tit 3:5. Je, ndugu yangu umefanya mkataba na nani katika maisha yako? Je, nafsi yako imeegemea wapi?

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu,” Yoh 3:5

Tusali:-Ee Yesu Kristo, tuwezeshe sisi kama viungo na Kanisa lako Takatifu kuzaliwa mara ya pili kila siku ya maisha yetu tunapo mruhusu Roho wako afanye kazi ndani yetu. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario