jueves, 13 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMAPILI YA PASAKA


JUMAPILI YA PASAKA

MISA YA MCHANA

Somo I: Mdo 10:34; 37-43

Zab: 118:1-2, 16-17, 22-23

Somo II: Kol 3:1-4

SEKWENSIA

Injili: Yoh 20:1-9

Nukuu:

Petro akafumbua kinywa chake, akasema, Hakika natambua ya kuwa Mungu hana upendeleo,” Mdo 10:34

“Nasi tu mashahidi wa mambo yote aliyoyatenda katika nchi ya Wayahudi na katika Yerusalemu; ambaye walimwua wakamtundika mtini,” Mdo 10:39

“Akatuagiza tuwahubiri watu na kushuhudia ya kuwa huyu ndiye aliyeamriwa na Mungu awe Mhukumu wa walio hai na wafu. Huyo manabii wote humshuhudia, ya kwamba kwa jina lake kila amwaminiye atapata ondoleo la dhambi,” Mdo 10:42-43

“Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1

“Basi Petro akatoka, na yule mwanafunzi mwingine, wakashika njia kwenda kaburini,” Yoh 20:3

“Akainama na kuchungulia, akaona vitambaa vya sanda vimelala; lakini hakuingia,” Yoh 20:5

“Basi akaja na Simoni Petro, akaingia ndani ya kaburi,” Yoh 20:6

“Basi ndipo alipoingia naye yule mwanafunzi mwingine aliyekuwa wa kwanza wa kufika kaburini, akaona na kuamini,” Yoh 20:8

TAFAKARI: “Tuyatafute yaliyo juu Kristo aliko; Yote yatafunuliwa katika Maisha yetu kuelekea alikoketi mkono wa kuume wa Mungu,”

Wapendwa wana wa Mungu, jumapili hii ya Pasaka yaani tukio hili la kufufuka kwake Bwana wetu Yesu Kristo, ndiyo uliokuwa mwanzo wa Wakristo, yaani wafuasi wake Yesu Kristo, kuanza kuadhimisha Matendo Makuu ya Mungu, ambayo kwa leo hii inajulikana kama Misa Takatifu. Kanisa kama lilivyo leo kupitia historia nzima ya wokovu wetu, na hasa jumuiya ya kwanza ya Wakristo, iliweka msisitizo wa kufanya mkukanyiko wao siku ya kwanza ya Juma, yaani Jumapili ya tokeo ya Ufufuko wa Kristo, tofauti na siku ya Jumamosi-kupumzika kwake Mungu katika swala la uumbaji kadiri ya masimulizi ya kikasisi “Priestly Traditional.” Masimulizi haya ndiyo yalikuwa kielelezo cha Wayahudi cha kufanya siku ya Jumamosi kuwa pekee na kutojishughulisha na maswala ya kazi, bali kumsifu Mungu na kumwabudu. Ufufuko wa Kristo unaanzisha mpango mpya na wenye kuitimiliza torati (sheria) kwa kumwabudu Mungu na kumsifu. Hili ndilo tendo Kubwa la kipasaka. Na haya ndiyo makusudi na fundisho la Yesu Kristo juu ya sheria yaani torati. “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza,” Mt 5:17

Kwa maana hiyo, leo basi kwa namna ya pekee, tuyatafakari maneno haya, “Tuyatafute yaliyo juu Kristo aliko; Yote yatafunuliwa katika Maisha yetu kuelekea alikoketi mkono wa kuume wa Mungu.” Tendo la Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo linatusukuma toka ndani ya mioyo yetu na imani yetu kuyatafuta yaliyo juu kule Kristo aliko. Kwa Mkristo yeyote hapa duniani asipolifanya jambo hili kuwa kielelezo cha maisha yake, basi ajue kwake Ufufuko hauna maana ye yote. Mtume Paulo anasema hivi kuhusu ufufuko, “tena kama Kristo hakufufuka, basi, kuhubiri kwetu ni bure na imani yenu ni bure,” 1Kor 15:14. Ufufuko wa Kristo ndiyo kiini cha Imani yetu.

Ndugu yangu, tunapotambua jambo hili ni rahisi kuona upendo na mapendeleo ya Mungu kwetu katika maisha ya kila siku. Mtume Petro analiona hilo kwa wale anaowahudumia ambao hapo mwanzoni hawakuwa katika Taifa lile Teule, yaani Israeli. Mpango mpya wa Mungu kwa watu wote wenye kumcha ulianza pale siku ya ijumaa kuu lilipopasuka Pazia. “Naye Yesu akiisha kupaza sauti tena kwa nguvu, akaitoa roho yake. Na tazama, pazia la hekalu likapasuka vipande viwili toka juu hata chini; nchi ikatetemeka; miamba ikapasuka; makaburi yakafunuka; ikainuka miili mingi ya watakatifu waliolala; nao wakiisha kutoka makaburini mwao, baada ya kufufuka kwake, wakauingia mji mtakatifu, wakawatokea wengi,” Mt 27:50-53. Kupasuka huku kwa pazia la hekalu ni mwanzo mpya wa kumwabudu Mungu kuliko kuzuri na ukamilifu zaidi. Kuabudu huku kumetoa matabaka yote, na kushirikisha kila mwenye hofu ya Mungu kuupata utakatifu ambao sasa ndiyo cheo chetu. Haya Yesu aliyasema hata kabla ya kupasuka kwa hekalu. “Lakini saa inakuja, nayo sasa ipo, ambayo waabuduo halisi watamwabudu Baba katika roho na kweli. Kwa maana Baba awatafuta watu kama hao wamwabudu. Mungu ni roho, nao wamwabuduo yeye imewapasa kumwabudu katika roho na kweli.” Yoh 4:23-24.

Ndugu yangu, saa yenyewe ndiyo sasa baada ya kutukuzwa Mwana wa Adamu, nikimaanisha baada ya kuyashinda mateso, na umauti. Kristo sasa yupo kwenye Utukufu wake. Hili ndilo lengo kuu la kuyatafuta yale yaliyo juu kule ambako Kristo yupo yaani kwenye Utukufu na Utakatifu. Ni katika msingi huu, Petro haoni haya kusema mambo haya, “Nasi tu mashahidi wa mambo yote aliyoyatenda katika nchi ya Wayahudi na katika Yerusalemu; ambaye walimwua wakamtundika mtini,” Mdo 10:39. Ndugu yangu, Petro alikuwa na elimu ya kawaida sana. Alikuwa mvuvi wa kawaida, ila mzoefu kutokana na Umri wake. Ila alikuwa shujaa na mwenye elimu kubwa kutokana na ufunuo wa Imani yake iliyotokana na upya wa maisha ya ufufuko. Katika jambo hili anaona wazi maagizo ya Kristo ndani ya imani hii ya kweli na kusema, “Akatuagiza tuwahubiri watu na kushuhudia ya kuwa huyu ndiye aliyeamriwa na Mungu awe Mhukumu wa walio hai na wafu. Huyo manabii wote humshuhudia, ya kwamba kwa jina lake kila amwaminiye atapata ondoleo la dhambi,” Mdo 10:42-43.

Ndugu yangu, hii ndiyo imani ya kweli kwa Mkristo ye yote baada ya ufufuko. “Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1. Mara nyingi tumependa kuchukulia mambo kwa mazoea. Bila shaka kwa umri uliokuwanao umekwisha sheherekea Pasaka nyingi. Kwa mantiki hii, yawezekana pia nyakati zote hizo hukuwahi kufufuka na Kristo. Ndugu yangu tafakari kwa makini ufufuko wa Kristo ndani ya maisha yako. Lifanye jambo hili kuwa la pekee katika maisha yako sasa, na achana na mambo ya kale umvae Kristo. Mtakatifu Augustino alikuwa ndani ya Kristo na Katika Kristo, baada ya kufahamu jambo hili pale alipofungua Biblia Takatifu baada ya kusikia sauti ikisema, ‘chukua usome,’ “Kama ilivyohusika na mchana na tuenende kwa adabu; si kwa ulafi na ulevi, si kwa ufisadi na uasherati, si kwa ugomvi na wivu. Bali mvaeni Bwana Yesu Kristo, wala msiuangalie mwili, hata kuwasha tamaa zake,” Rum 13:13-14. Hii ndiyo “METANOIA” yaani kugeuka na kuanza upya ndani na katika Kristo.

Ndugu yangu, pamoja na Injili kuelezea tukio la ufufuko wa Bwana Yetu Yesu Kristu, imekazia mambo makuu mawili. Kwanza, nafasi ya Kanisa, na pili, nafasi ya Mtume Petro. Kwa namna ya pekee naomba tuyatafakari mambo haya. Tuelewe kwamba Yesu Kristo alikwisha weka mfumo fulani wa uongozi kabla ya mateso, kifo na ufufuko wake. Ni katika mfumo huyo wafuasi wake wapaswa kuufuata. “Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba wako huu nitalijenga Kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda,” Mt 16:18. Jambo hili na nafasi hii ya Petro inajitokeza na kujionyesha wazi wakati wa Ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo. “Basi akaja na Simoni Petro, akaingia ndani ya kaburi,” Yoh 20:6. Licha ya kwamba Mtume Yohani ambaye Yesu alimpenda sana kuliko Mitume wote, ikiwa ni moja ya sifa yake na uhusiano wake na Yesu Kristo, pia alikuwa ni kijani kuliko wote; hakuwa wa kwanza kuingia katika kaburi licha ya kwamba alikimbia kuliko Mtume Petro na kufika wa kwanza Kaburini baada ya kupata taarifa ya Kristo Mfufuka. Yohane Mtume anatambua nafasi ya Petro kama kiongozi halali aliyepewa mamlaka na Kristo mwenyewe. Hapa ndipo tunapoona nafasi ya Baba Mtakatifu kama HALIFA wa Kristo. Huyu ndiye Petro, yaani mwamba ambapo Kanisa lake limeoteshwa na kukua.

Kwa sababu hiyo, Mtume Petro anakuwa wa kwanza kuingia Kaburini. Na baada ya Petro, Mtume Yohane anaingia na kuona na kuamini. “Basi ndipo alipoingia naye yule mwanafunzi mwingine aliyekuwa wa kwanza wa kufika kaburini, akaona na kuamini,” Yoh 20:8. Kuona na kuamini kwa Mtume Yohane, kunachukuliwa kwa namna mbili. Moja, Mtume Yohane mwenyewe kwa upendo aliokuwa nao Kristo juu yake, na upendo wa Mtume Yohane juu ya Kristo. Pili, Yohane Mtume katika jambo hili la kuona na kuamini, anasimama badala ya Mama Kanisa kama mshuhudia na mshuhuda wa kweli wa ufufuko wake Yesu Kristo. Kanisa tuishilo leo na sasa linaishi katika ushuhuda huu wa Ufufuko. Kanisa halipo kama hakuna Imani hii ya Ufufuko. Je, jambo hili linasema nini kuhusu vipaumbele vyako katika Imani?

Ndugu yangu, yale ambayo yanachukua muda wako mwingi katika maisha yako, ndiyo hayo yanayoakisi maisha yako baada ya kifo. Yawezekana hadi sasa huna mpangilio wa maisha yako. Mambo ya muhimu kufanya katika maisha yako mapya ya ufufuko ni haya:

Moja, Mshukuru Mungu kwa kukutumia vyema, endapo unaishi vyema utume wako kadiri ya wito wako. Katika jambo hili utafunuliwa siri ya umilele.

Pili, kila mmoja wetu yampasa kufanya mkataba na Kristo kama ishara ya kuanza maisha mapya ya ufufuko. Mkataba wako ulenge kufanya jambo jema kwa ajili ya Kristo kila siku. Hapa haitegemei ukubwa wa jambo au udogo wake.

Tatu, lifanye jambo hilo kuwa kiu yako kila siku na usichoke kulifanya. Nakuhakikishia utaanza kuona mabadiliko makubwa katika maisha yako yakiambatana na Neema na Baraka za ajabu.

Nne, Sala kuu yako iwe kushukuru hata kwa yale ambayo bado kuyapata. Hapa ni kumwachia Kristo usukani wa maisha yako. Yesu Kristo ndiye dereva maarufu kuliko wote waliokwisha kutokea. Yeye ndiye “Njia, na Ukweli, na Uzima,” Yoh 14:6

Na mwisho, omba kifo Chema kila siku na hasa mara uamkapo. Sala hii iambatane na Neema ya kutoa msamaha bila kujibakiza.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Basi mkiwa mmefufuliwa pamoja na Kristo, yatafuteni yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu,” Kol 3:1

Tusali:-Ee Yesu, nijalie neema ya kutafuta yale yakuelekeayo katika maisha yangu kila siku. Amina.

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario