JUMANNE WIKI YA 3 YA PASAKA
Somo: Mdo 7:51-59
Zab: 31:3cd-4, 6, 7b,
8a, 17, 21ab
Injili: Yoh 6:30-35
Nukuu:
“Enyi
wenye shingo gumu, msiotahiriwa mioyo wala masikio, siku zote mnampinga Roho
Mtakatifu; kama baba zenu walivyofanya, na ninyi ni vivyo hivyo,” Mdo 7:51
“Lakini yeye akijaa
Roho Mtakatifu, akakaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa
Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu,” Mdo 7:55
“Akasema, Tazama!
Naona mbingu zimefunguka, na Mwana wa Adamu amesimama mkono wa kuume wa Mungu,”
Mdo 7:56
“Wakapiga kelele
kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja,” Mdo 7:57
“Wakamtoa nje ya
mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa kijana
mmoja aliyeitwa Sauli,” Mdo 7:58
“Wakampiga kwa mawe
Stefano, naye akiomba, akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu,” Mdo 7:59
“Wakamwambia,
Unafanya ishara gani basi, ili tuione tukakuamini? Unatenda kazi gani?” Yoh 6:30
“Yesu
akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha
mbinguni, bali Baba yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni,”
Yoh 6:32
“Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha
uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu
kamwe,” Yoh 6:35
TAFAKARI:
“Kifo Chema ni kuishi katika Kristo na ndani ya Kristo, yeye ndiye chakula cha
uzima.”
Wapendwa wana wa Mungu,
hakuna shaka kabisa wote tuliozaliwa ipo siku wote tutakufa kila mmoja kwa
wakati wake. Kifo kwa Mkristo ni daraja ya kuvuka kwenda upande mwingine wenye
mazingira tofauti na haya tuliyonayo: wenye uzima na uhai. Kifo kwa
anayemwamini Kristo ni mlango ambao watupitisha kwenye maisha mengine ya
umilele. Kifo kina maana ndani na katika Kristo kwa sababu kupitia mateso yake,
na kifo chake msalabani, laana ya kifo imefutwa. Kwa Mkristo kwenye imani, kifo
si kitu cha kuogopa bali ni tukio la kujiandaa.
Maandalizi ya kifo
Chema ni kuishi kweli ya Kristo kila siku. Ni kumshuhudia Kristo kwa yale
yaliyomema na anayotuwasa kuyafanya kama watoto wa Mungu. Ni kutokumwonea aibu
Kristo mbele za watu hata kama yatupasa kufa kwa ajili ya kweli. Ukweli huu
ndiyo anaouishi Shahidi Stefano na kuhushuhudia. Stefano Shahidi anawaaambia Wayahudi,
“Enyi wenye shingo gumu, msiotahiriwa mioyo
wala masikio, siku zote mnampinga Roho Mtakatifu; kama baba zenu walivyofanya,
na ninyi ni vivyo hivyo,” Mdo 7:51. Jambo la kuelewa hapa katika maisha yetu ya
Kiroho, hatuwezi kupingana na mpango wa Roho Mtakatifu. Sifa na kazi mojawapo
wa Roho Mtakatifu ni kuleta umoja wa kweli na wakimungu kwa wote walioumbwa kwa
sura na mfano wa Mungu, Mwa 1:26.
Palipo
na Roho Mtakatifu kuna umoja wa kweli na hapo Roho Mtakatifu utenda mambo yake
kwa wale aliwaridhia. Shihidi Stefano, “akijaa Roho Mtakatifu, akakaza macho
yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa
mkono wa kuume wa Mungu,” Mdo 7:55. Stefano Shahidi anapewa hakikisho la kile
anachokisimamia na kukishuhudia. Pamoja na ukweli huu, watesi wake “wakapiga
kelele kwa sauti kuu, wakaziba masikio yao, wakamrukia kwa nia moja,” Mdo 7:57.
Ndugu yangu, ni mara
ngapi katika mazingira yetu tunakutana na hali kama hii na wala hatufanyi
chochote? Yawezekana hali isiwe kama ya Shahidi Stefano ya kupondwa mawe. Ila
wote ni mashahidi na labda tumeshaona jinsi watoto wadogo wanavyotendwa kwenye
usafiri wetu wa daladala. Mzazi ambaye naye anamtoto kama huyo anayeteswa na
kunyanyapaliwa na kondakta, asemi wala akemei chochote. Je, tunatofauti gani na
waliomrarua Shahidi Stefano? “Wakamtoa
nje ya mji, wakampiga kwa mawe. Nao mashahidi wakaweka nguo zao miguuni pa
kijana mmoja aliyeitwa Sauli,” Mdo 7:58. Sauli, ambaye leo anajulikana sana
kama Mtume Paulo, anashiriki katika kosa hili. Mtume Paulo analifanya kosa hili
kwa kutetea mila na desturi za mababu zake, ambaye baada ya kuongoka kwake
anakuwa mtetezi mashuhuri wa Kristo na mkosoaji wa mila na desturi hizo. Huku
ndiko maana halisi ya kuongoka.
Katika
kipigo hiki cha kikatili, Stefano anaikabidhi roho yake kwa Mungu, kama Bwana
wetu Yesu Kristo alivyofanya. “Wakampiga kwa mawe Stefano, naye akiomba,
akisema, Bwana Yesu, pokea roho yangu,” Mdo 7:59. Hata katika hali hii ya
kutisha, Stefano Shahidi habadili msimamo wake, wala hakatishwi tamaa kwa
kujitoa kwake muhanga. Mungu anabakia kuwa tumaini lake hadi mwisho. Wengi wetu
katika hali kama hii na mara nyingine tunapo ugua kwa muda mrefu bila kujua
sawasawa sababu ya magonjwa yetu, hukata tamaa na kusaliti Imani yetu na Mungu
wetu. Ni mara ngapi tunawaona Wakristo waliokuwa mstari wa mbele wanakwenda
kupiga ramli na hata wengine wanakutwa na umauti kwa waganga wa kienyeji?
Mpendwa,
haijalishi wewe ni nani ila kuwa Mkristo bila kuwa na imani thabiti ni hatari
sana. Ni sawa na mkate usioiva vizuri kwani ni hatari kwa tumbo. Yesu Kristo
katika Injili ya leo anawashangaa wale wasio mwamini pamoja na yote anayoyaishi
na kuyatenda. Nao wanataka kuona ishara ili wamsadiki kwamba yeye ndiye kweli
wanayemtumainia. “Wakamwambia, Unafanya ishara gani basi,
ili tuione tukakuamini? Unatenda kazi gani?”
Yoh 6:30. Kwa Wayahudi, Musa alikuwa na nafasi ya pekee sana hata kuweza kuvuka
uelewa wa Mungu. Kwa mantiki hiyo, yeyote aliyekwenda kinyume na kile
alichosema au fanya Musa alionekana kama mhaini hivi. Yesu kabla ya yote
anawapa uelewa wa Mungu ni nani na Musa ni nani. “Yesu akawaambia, Amin,
amin, nawaambieni, Siye Musa aliyewapa chakula kile cha mbinguni, bali Baba
yangu anawapa ninyi chakula cha kweli kitokacho mbinguni,” Yoh 6:32. Musa
aliweza kuyafanya hayo yote kwa mkono wa Mungu, ila Kristo ni zaidi ya Musa
kwani kwake upo uzima. Kiu na mahangaiko yetu yote yanamajibu tunapoishi katika
yeye na ndani yake. “Yesu akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye
kwangu hataona njaa kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe,” Yoh 6:35. Je,
unamwamini Kristo? Hakuna sababu ya kutafuta ulizi kwa njia ya giza kama tunaye
Kristo. Hakuna sababu ya kuzindika majumba yetu na kutembea na mahirizi kama
tunaye Kristo.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Yesu
akawaambia, Mimi ndimi chakula cha uzima; yeye ajaye kwangu hataona njaa
kabisa, naye aniaminiye hataona kiu kamwe,” Yoh 6:35
Tusali:-Ee
Yesu wangu, nami nasadiki wewe ndiye chakula na uzima wangu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario