sábado, 15 de abril de 2017

TAFAKARI: JUMAMOSI YA OKTAVA YA PASAKA


JUMAMOSI YA OCTAVA YA PASAKA

Somo: Mdo 4:13-21

Zab: 118:1, 14-15ab, 16-18, 19-21

Injili: Mk 16:9-15

Nukuu:

Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu,” Mdo 4:13.

“Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia,” Mdo 4:19-20.

“Nao walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa sababu ya watu; kwa kuwa watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa hayo yaliyotendeka,” Mdo 4:21.

Walakini hao waliposikia kama yu hai, naye amemwona, hawakusadiki,” Mk 16:13.

“Baadaye akaonekana na wale kumi na mmoja walipokuwa wakila, akawakemea kwa kutokuamini kwao na ugumu wa mioyo yao, kwa kuwa hawakuwasadiki wale waliomwona alipofufuka katika wafu,” Mk 16:14.

Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe,” Mk 16:15.

TAFAKARI: “Mungu hutenda mambo makuu kwa wanyenyekevu wa moyo; msingi wa yote ni kuamini na kujisalimisha kwake.”

Wapendwa wana wa Mungu, jumuiya ya kwanza ya Wakristo haikujengwa na mijitu yenye upeo mkubwa sana wa akili na maarifa. Jumuiya hii ilijengwa na MAJITU YA SIFA, nikimaanisha; wanyenyekevu wa moyo na wenye imani ya kweli kwa yale waliyokuwa wanaamini juu ya Yesu Kristo. Jambo hili lilikuwa mshangao mkubwa kwa watesi wao, yaani, Wayahudi walikuwa na msimamo mkali, hasa lile baraza lao la Kiyahudi.

Watesi wao wanatoa ushuhuda wa jumuiya hii ya Wakristo. Basi walipoona ujasiri wa Petro na Yohana, na kuwajua ya kuwa ni watu wasio na elimu, wasio na maarifa, wakastaajabu, wakawatambua ya kwamba walikuwa pamoja na Yesu,” Mdo 4:13. Ingawa hawakuwa na Yesu katika hali ya kushikika/kimwili, Kristo mwenyewe ndiye aliyekuwa Kiongozi wa jumuiya hii. Jina lake lilikuwa tishio kubwa sana. Ni kupitia jina lake hili wengi waliponywa na wanazidi kuponywa hadi sasa.

Ili kuondokana na karaha hii, na kushindwa kwao kuwazuiya, Baraza la Kiyahudi linatoa amri ya wao kutokusema tena juu ya Jina hili Tukufu la Bwana wetu Yesu Kristo. Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, “Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia,” Mdo 4:19-20. Ujasiri huu wa Petro na Yohana unathibitisha uthabiti wa Imani ya kweli juu ya kile walichoona na kuamini.

Wapendwa wana wa Mungu, kunamsemo unaosema kwamba ‘mara zote historia hujirudia.’ Leo tunaona Wakristo kusongwa sana na kuuwawa kwa sababu tu ya Jina hili Kuu kupita majina yote. Mitume walichapwa viboko hadharani na wengine kuuwawa kama Bwana wao Yesu Kristo, ila hawakusita kutoa ushuhuda wa kweli. Damu zao ndiyo msingi wa Kanisa letu leo. Leo Wakristo wenzetu wanapatwa na msukosuko na mateso hayo kwa njia tofauti tofauti. Wapo wanochinjwa kama kuku, kuchomwa kwa moto, kupigwa risasi, na vifo vya ukatili ambavyo havijawahi tokea. Mfano kule Irak wapo walioingiziwa misalaba kinywani hadi kufa. Leo twapaswa kusimama Imara katika Imani yetu.

Nyakati zile, Mitume walitishwa kwa kufungwa magerezani, kuchapwa na kulazimishwa kutolitaja tena Jina hili. “Nao walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa sababu ya watu; kwa kuwa watu wote walikuwa wakimtukuza Mungu kwa hayo yaliyotendeka,” Mdo 4:21. Tunaposimama katika jina hili, yote yanawezekana kwa sababu mwenye kuliongoza Kanisa hili ni Kristo mwenyewe.

Imani ni msingi wa yote yale tunayoyasema na kuyasimamia. Tusipokuwa na Imani ya kweli na thabiti, ni vigumu kuitetea na wala kuwa Mashahidi wa Imani hiyo. Leo tunalazimishwa kulikana hili Jina badala yake kusilimishwa. Watu wengi kati yetu kutokana na ugumu wa maisha wameshajisilimisha ingawa wamebaki na majina yao Kikristo kama makapi. Tukio la ufufuko wa Bwana yetu Yesu Kristo kadiri ya Injili ya leo halikuwa jambo la kuaminika kwa urahisi hata kwa mitume wenyewe. “Walakini hao waliposikia kama yu hai, naye amemwona, hawakusadiki,” Mk 16:13. Mariamu Magdalena anapopeleka habari za ufufuko wa Yesu kwa Mitume, hawakuamini. Ni kweli isiyo shaka kwamba namna na kifo cha Bwana wetu Yesu Kristo kilivyokuwa kiliwatia hofu kubwa sana wafuasi wake na hasa Mitume hata kufikiri wenyewe kupoteza maisha yao kwa kuuwawa kikatili kama Mwalimu wao.

Katika hofu hii, Yesu Kristo Mfufuka anawatokea. Baadaye akaonekana na wale kumi na mmoja walipokuwa wakila, akawakemea kwa kutokuamini kwao na ugumu wa mioyo yao, kwa kuwa hawakuwasadiki wale waliomwona alipofufuka katika wafu,” Mk 16:14. Baada ya Yesu kuwakeamea anawapa majukumu ya kufanya. “Akawaambia, Enendeni ulimwenguni mwote, mkaihubiri Injili kwa kila kiumbe,” Mk 16:15. Majukumu haya ya kuihubiri Injili ulimwenguni mwote na kwa kila kiumbe ndicho kitambulisha cha Kristo Mfufuka na aliye hai. Jukumu hili ni kwa kila mbatizwa na yule mwenye kuamini kwa kushika ahadi zake za ubatizo.

Leo ndugu zangu tunachangamoto nyingi sana katika jumuiya yetu na Kanisa letu. Ikiwa tunaona aibu kufanya ishara ya msalaba hadharani, na hasa sehemu za kula kama mahotelini, itakuwaje sasa kusimama wazi na kusema mimi ni Mkristo, na ninamwamini Kristo, na nipo tayari kufa kwa anjili ya Jina hili? Vile vile natoa angalizo kwa wale wanaopenda kuwa na uraia pacha wa Imani. Watu hawa ni wale mara wanapokuwa kwenye alaiki ya watu na kwenye masherehe upoteza uhalisia wao kwa kutoa salamu za kuwapendezesha kila kundi la watu.

Utamsikia Mkristu anaanza utambulisho wake kwa mbwembwe; Wasalam Maleku, Bwana asifiwa, Kristo mshinda, Bwana ni jibu, Tumsifu Yesu Kristo, nk. Hatuna upacha katika IMANI. Ni vigumu sana kumsikia Muislamu akijitambulisha mbele ya alaiki ya watu kama sisi. Ni aheri kukaa kimya kuliko kuonyesha ujinga wako katika swala hili la Imani. Hivyo ni heri kuwa baridi au joto kiimani, kuliko kuwa vuguvugu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia,” Mdo 4:19-20

Tusali:-Ee Yesu, lisimamie Kanisa lako, na utupe ujasiri wa kutosha kuisimamia Imani yetu na kuiishi pasipo woga. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario