Sikukuu ya Watakatifu Wote
Somo
I: Ufu 7:2-4, 9-14
Zab:
24:1bc-2, 3-4ab, 5-6
Somo
II: 1Yoh 3:1-3
Injili:
Mt 5:1-12a
Nukuu:
“Na malaika wote
walikuwa wakisimama pande zote za kile kiti cha enzi, na za hao wazee, na za
wale wenye uhai wanne, nao wakaanguka kifulifuli mbele ya kile kiti cha enzi,
wakamsujudu Mungu,” Ufu 7:11
“Hao ndio
wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe
katika damu ya Mwana-Kondoo,” Ufu 7:14b
“Tazameni, ni pendo la
namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa
sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye,” 1Yoh 3:1
“Na kila mwenye
matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu,” 1Yoh 3:3
“Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila
neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini,
na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni,” Mt 5:11-12
TAFAKARI: “Utakatifu ndiyo Cheo chako.”
Wapendwa katika Kristo, leo Mama Kanisa kwa furaha kubwa
anaadhimisha sikukuu ya Watakatifu wote. Kwa namna ya pekee kabisa mimi na wewe
leo tunakumbushwa kwamba ‘Utakatifu ndiyo Cheo chetu.’ Malengo
ya Mbatizwa yeyote ni kuwa mkamilifu kama Baba yetu wa mbinguni alivyo
mkamilifu. “Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama
Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Huu ndio wito wa kila
mbatizwa ili kuifikia taji ile la Utakatifu ambayo ndilo cheo chako. Ni kuwa na
matumaini na Mungu na kila siku kujitakasa na kuepuka kuishi katika hatia. Na “kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama
yeye alivyo mtakatifu,” 1Yoh 3:3
Ndugu yangu, tungali hapa dunia wengi wetu hupenda kujipambambanua
na ubora wa familia zetu, koo zetu, makabila yetu, itikadi zetu za kisiasa na
kidini, na hata utaifa wetu. Tukiishi katika ngazi hii tu bado hatujajua hatma
ya uwepo wetu hapa duniani. Huko Mbinguni hatutajulikana kwa hayo niliyoyataja,
bali tutajulikana kwa usafi wetu
uliotokana na UTAKATIFU wetu tuliouishi hapa duniani ikiwa ni mahali tu pa
maandalizi na kupita, na kwa muda mfupi tu.
Kila mmoja wetu aweza kuwa Mtakatifu. Utakatifu wako ni
matokeo ya kuwa mwaminifu kwa mambo madogo madogo ya kila siku, na kuyafanya
hayo kwa ukamilifu wake. Ni kuwa tayari kumpa Kristo nafasi ya ndani ya moyo
wako ili atende kazi nawe kwa yale yanayompendeza Mungu na jirani yako.
Utakatifu wako ni tokeo pia la kufungua milango kwa wote wenye uhitaji bila
kujali historia zao na mapungufu yao. Ni kujaribu kufanana na Yesu katika
kuwaza, kutathmini, na kutenda. Tunapokuwa karibu na Kristo ndivyo
tunavyofunuliwa siri za Baba yetu wa mbinguni na Ufalme wake.
Ukaribu huu niliousema, utufanya kuwa watoto wapendwa wa
Mungu katika utii usio shuruti. Tunatii kwa sababu Mungu anatupenda na
anatutakia mema katika ukamilifu wake. Ndugu yangu, “Tazameni, ni pendo la
namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa
sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye,” 1Yoh 3:1. Maisha
haya ya utakatifu yatatudai na yanatudai kila siku kusimama katika kweli na
haki, na wakati mwingine tutapimwa katika kweli hiyo, yaani, Imani yetu.
Kupimwa
huku kwa Imani kwa weza pia kutuondolea uhai wetu ambao ndio kitu cha thamani
kupita vyote tungali hapa duniani. Basi, hili litakapotokea yatupasa kuyasema
maneno haya pasipo shaka yoyote, “kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni
faida,” Flp 1:21. Ni kuyaona yote yaliyofaida kwako ni hasara kwa ajili ya Kristo,
Flp 3:7. Tunapoyaachia maisha yetu katika kiwango hiki, Kristo kamwe hawezi
kutuacha katika taabu hizo. Kristo hubaki kuwa faraja kubwa kwetu katika dhiki
na taabu hizo. Naye anatuambia nyakati kama hizo tuwe watu wa kufurahi kwa
sababu tunamruhusu Mungu kutenda mambo katika hali yetu ya uduni na Mateso. “Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na
kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa
thawabu yenu ni kubwa mbinguni,” Mt 5:11-12. Je, wayafurahia mateso yako?
Mtawa mmoja wa kiume katika Monasteri fulani alijijengea
ukaribu sana na Yesu wa Ekaristi Takatifu. Mtawa huyu alikuwa mpishi wa muda
mrefu katika Monasteri hiyo. Aliipenda sana kazi yake na kwake ilikuwa moja ya
kumtukuza Mungu kupitia huduma hii kwa wanajumuiya wenzake. Kamwe hakuwahi
kunung’unika hata pale ambapo kazi zilikuwa nyingi kupita uwezo wake.
Kila asubuhi Mtawa huyu mara baada ya masifu ya asubuhi, na
Misa Takatifu, huenda bustanini kuchuma mboga, na vitu vingine kama maandalizi
ya chakula cha Mchana na jioni. Bustani ile ilikuwa baada ya kulipita Kanisa.
Hivyo alijiwekea ahadi ya kuongea na Yesu wa Ekaristi Takatifu kila siku kabla
ya kufika bustanini.
Siku moja akiwa na kikapu chake na kisu aliingia Kanisani na
kuanza kusali na kutafakari mbele ya ‘Terbenakulo,’ Sehemu zinapohifadhiwa
Hostia Takatifu. Mara alishtushwa na sauti ya kengele ya Malaika wa Bwana,
iliyoashiria pia ni muda wa chakula cha mchana. Mtawa huyu aliingiwa na hofu
kubwa sana kwani alikuwa bado hata bustanini hakuwa amefika.
Mtawa huyu aliondoka kwa haraka ili awahi kuomba msamaha
kwa watawa wenzake kwa kutokuandaa chakula kile cha mchana. Maajabu ni kwamba
alipofika tu eneo la jikoni alikaribishwa na harufu nzuri sana ya chakula na
kusikia watawa wenzake wakimsifu kwa chakula kitamu alichoandaa. Kila mmoja
alitaka kuongea naye na kumpa asante kwa kazi nzuri aliyofanya.
Akiwa ameshika kikapu chake na kisu ndani yake, alionekana
akitokwa na machozi ya furaha huku akisema “asante Yesu kwa kuniona na
kuniondolea aibu hii.” Watawa wote walibaki midomo wazi! Ndugu huyu alisimulia
yote yaliyotokea. Jumuiya yote ilijawa na furaha na kumtukuza Mungu.
Wapendwa wana wa Mungu, tunapokuwa karibu na Mungu, kamwe
hawezi kutuacha. Mungu atatupigania hadi mwisho. Hivyo tuwe waaminifu na
kufanya yote kwa ukamilifu tukimtanguliza Mungu kwa kila kitu. Mtume Yakobo
anatuambia siri hii kwa kusema, “Mkaribieni Mungu,
naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na
kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili,” Yak 4:8. Haya ndiyo maandalizi ya
cheo chako, yaani, Utakatifu wako.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Hao ndio wanatoka
katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika
damu ya Mwana-Kondoo,” Ufu 7:14b
Tusali:-Ee Yesu, na Bwana
wangu, kwako yote yawezekana. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario