JUMATANO WIKI YA 28 YA MWAKA-C
Somo:
Gal 5:18-25
Zab/Kit:
2:1-2, 3, 4, 6
Injili:
Lk 11:42-46
Nukuu:
“Basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya,
uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu,
hasira, fitina, faraka, uzushi, husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na
hayo, katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba
watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu,” Gal 5:19-21
“Lakini tunda la Roho
ni upendo, furaha, amani, uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi;
juu ya mambo kama hayo hakuna sheria,” Gal 5:22-23
“Ole wenu, kwa kuwa mmefanana na makaburi
yasiyoonekana, ambayo watu wapitao juu yake hawana habari nayo,” Lk 11:44
TAFAKARI:
“Tukiishi kwa Roho, na tuenende kwa Roho.”
Wapendwa wana wa Mungu,
mtu kamili anakuwa katika sehemu kuu tatu:- Nafsi, Roho, na Mwili. “Mungu wa
amani mwenyewe awatakase kabisa; nanyi Nafsi zenu na Roho zenu na Miili yenu
mhifadhiwe mwe kamili, bila lawama, wakati wa kuja kwake Bwana wetu Yesu
Kristo.” I The 5:23. Katika hili Roho na Nafsi huwa pamoja na ndizo wewe
mwenyewe. Mwili ni nyumba ya roho na nafsi. Katika uumbaji Mungu aliumba mwili
kwa udongo halafu akapulizia pumzi puani ambayo ni roho yake ndipo mtu huyo
akawa nafsi iliyo hai. “Bwana Mungu akamfanya mtu kwa mavumbi ya ardhi,
akampulizia puani pumzi ya uhai; mtu akawa nafsi hai.” Mwa. 2:7. Miili
tuliyonayo ni nyumba ya Nafsi na Roho.
Kwa hali hii sisi binadamu ni wawili. Kuna mtu
wa ndani na mtu wa nje. Mtu wa ndani ni Nafsi na Roho, na mtu wa nje ni Mwili
lakini watu hawa wapo pamoja hatuwezi kuwatenganisha wala kumwona kwa macho ya
nyama huyu mtu wa ndani, ila yupo. Huyu mtu wa nje hukua, kuzeeka na kufa Mtu wa
ndani hakui, hazeeki, wala hafi Mtu wa ndani hubadilika kwa kuchakaa
kunakotokana na kujeruhiwa na kuumizwa kunakosababishwa na dhambi na matukio
mbalimbali yanayomsibu binadamu.
Mtu wa ndani alianza
tangu pale kutungwa mimba siku ya kwanza wakati yai na mbegu na pumzi ya Mungu
alipoweka roho yake Mtu huyu wa ndani hakui wala haongezeki ila hufanywa upya.
“Kwa hiyo hatulegei, bali ijapokuwa utu wetu wa nje unachakaa, lakini utu wetu
wa ndani unafanywa upya siku kwa siku,” 2Kor 4:16.
Nafsi ikiegemea rohoni
huleta matunda mzuri. “Lakini tunda la Roho ni upendo, furaha, amani,
uvumilivu, utu wema, fadhili, uaminifu, upole, kiasi; juu ya mambo kama hayo
hakuna sheria.” Gal. 5:22-23.
Ila nafsi inapoingia
katika Mwili mambo huwa mabaya kwani ufanya matendo ya mwili kama tusomavyo
katika maandiko matakatifu, “basi matendo ya mwili ni dhahiri, ndiyo haya:
uasherati, uchafu, ufisadi, ibada ya sanamu, uchawi, uadui, ugomvi, wivu,
hasira, fitina, faraka, uzushi husuda, ulevi, ulafi, na mambo yanayofanana na
hayo; katika hayo nawaambia mapema, kama nilivyokwisha kuwaambia, ya kwamba
watu watendao mambo ya jinsi hiyo hawataurithi ufalme wa Mungu.” Gal.5:19-21.
Ni vizuri kujua nafsi yako imeegemea wapi. Ikiegemea rohoni utaenda Mbinguni,
ikiegemea mwilini utaenda motoni.
Wapendwa wana wa Mungu,
Injili ya leo Yesu anawakemea Mafarisayo na wana sheria kwa kutokuishi katika
kweli na haki. Yesu anawafananisha Mafarisayo na wataka sifa bila kuwa na siha,
wajikwezao bila thaminisho la kweli, na mwisho wajipambao kwa uzuri na wema
ingali wameoza kabisa ndani yao. Haya ndiyo makaburi yanayovutia machoni mwa
watu ili hali ndani yake ni majanga na fedheha. “Ole
wenu, kwa kuwa mmefanana na makaburi yasiyoonekana, ambayo watu wapitao juu
yake hawana habari nayo,” Lk 11:44. Ndugu yangu, katika maisha yako jaribu mara
zote kuwa kile ulicho.
Hatua
ya kwanza ni kuwa binadamu na kuikubali hali hiyo ya kibinadamu. Mungu hawezi
kukupandisha ngazi nyingine kama haupo tayari kukubali ubinadamu wako aliyo
kuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Yesu alipowapa Mafarisayo ukweli juu
ya maisha yao, wanasheria walimjia juu na kutaka kujua kama wao nao wapo
salama. Yesu akawajibu, “akasema, Nanyi wana-sheria, ole wenu, kwa sababu
mwawatwika watu mizigo isiyochukulika, wala ninyi wenyewe hamwigusi mizigo hiyo
hata kwa kimoja cha vidole vyenu,” Lk 11:46. Wana-sheria yawapasa kusimama
katika kweli na haki siku zote.
Leo
katika jamii yetu, watu hawa (wana sheria) wanadhamana kubwa sana katika
mizania ya kweli na haki. Rushwa na ufisadi vimekuwa mitengo hatarishi sana
katika sekta zote za utumishi serikalini. Haki ya mtu haiwezi nunuliwa kwa
gharama yoyote ile. Uwepo wa mtu na haki yake ambayo inayochezewa, hali hiyo
imewekwa na Mungu mwenyewe kwa chapa ya uumbaji wake wa peke wa mtu huyo. Hivyo
ni Mungu mwenyewe anayestahili kulipwa haki hiyo.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Lakini mkiongozwa na Roho, hampo
chini ya sheria,” Gal 5:18
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tuongoze katika kweli yako daima. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario