Somo
I: Hek 11 :22-12:2
Zab/Kit: 145:1-2-3, 8-9, 10-11,
13cd-14
Somo II: 2The 1:11-2:2
Injili:
Lk 19:1-10
Nukuu:
“ulimwengu wote mbele zako ni kama chembe moja
katika mizani, na mfano wa tone moja katika mizani, na mfano wa tone moj ala
umande lishukalo asububi juu ya ardí,” Hek 11:22
“Lakini Wewe
unaviachilia vyote, kwa kuwa ni vyako,
Ee Mfalme Mkuu mpenda roho za watu; maana roho yako isiyoharibika imo
katika vyote,” Hek 11:26
“jina la Bwana wetu
Yesu litukuzwe ndani yenu, nanyi ndani yake, kwa neema ya Mungu wetu na ya
Bwana Yesu Kristo,” 2The 1:12
“kwamba msifadhaishwe
upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno, wala
kwa waraka unaodhaniwa kuwa ni wetu, kana kwamba siku ya Bwana imekwisha
kuwapo,” 2The 2:2
Na
Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi,
kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako,” Lk 19:5
“Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa
sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu,” Lk 19:9
TAFAKARI: “Hata wewe na mimi wadhambi, leo wokovu
umefika nyumbani mwetu, tuikimbile nuru ambaye ndiye Kristo Yesu, na tuachane
na giza la umauti.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 31 ya Mwaka “C” wa Kanisa. Ujumbe wa
leo kwetu na kwa kila mmoja wetu ni kwamba, “hata wewe na mimi wadhambi leo
wokovu umefika nyumbani mwetu, tuikimbile nuru ambaye ndiye Kristo Yesu, na
tuachane na giza la umauti.” Hivyo masomo ya leo yanaonyesha ukaribu huo wa
Mungu kwetu, na ukuu wake usio na kipimo kwetu kwa sababu anatupenda upeo.
Ukuu wa Mungu wetu ni
waajabu sana. Hatuwezi kuupima wala kuukisia. Naye ndiye Mungu kwa maana,
“ulimwengu wote mbele zako ni kama chembe moja katika mizani, na mfano wa tone
moja katika mizani, na mfano wa tone moja la umande lishukalo asububi juu ya
ardí,” Hek 11:22. Ukuu huu wa Mungu na katika upendo wake usio na kipimo, ndiyo
ukubwa wa huruma na msamaha wake kwetu. Na kwa namna hiyo katika kweli na haki,
Mungu huwahurumia, ‘watu wote, kwa sababu anao uwezo wa kutenda mambo yote,
naye huwaachilia wanadamu dhambi zao, ili wapate kutubu,’ Hek 11:23
Ndugu yangu, hakuna
aishiye leo katika ulimwengu huu kwa hali yoyote ile, iwe ya dhiki au ya heri
kwa bahati mbaya. Mimi na wewe ni kusudi la Mungu, kwa maana Mungu ameviumba
“vitu vyote vilivyopo, wala hukichikii kitu chochote ulichokiumba,” Hek 11:24.
Mimi na wewe na vyote tulivyonavyo iwe mali na utajiri wa dunia hii, au vipawa
mbalimbali, vyote ni mali yake Mungu kama asemavyo Mzaburi 24:1. Kile ulicho na
unachomiliki katika kweli na haki, uifunua sura, utukufu, na furaha ya Mungu
kwako na kwa ulimwengu mzima. Na kwa sababu hiyo, Mungu huviachilia ‘vyote, kwa
kuwa ni vyake, ndiye Mfalme Mkuu mpenda roho za watu; maana roho yake
isiyoharibika imo katika vyote,’ Hek 11:26
Na
katika upendo huu wa ajabu wa Mungu, tunaona katika Injili ya leo makutano kati
ya Yesu na Zakayo. Zakayo hamwoneyi Yesu aibu pamoja na watu kuyajua madhaifu
yake na ufupi aliokuwa nao. Bado anaona salama yake ipo kwa Kristo tu na siyo
mitazama ya wale walikuwa wanamzunguka. Ili amwone Yesu, Zakayo alipanda juu ya
mkuyu. “Na Yesu, alipofika mahali pale,
alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda
nyumbani mwako,” Lk 19:5.
Ni
wazi kwamba huwezi kuwa mrefu zaidi ya wewe mwenyewe. Na kwa kuwa huu ni ukweli
wa lazima, kumbe kuvijua na kuviona vile vilivyo nje ya uwezo na kimo chako
yakupasa kufanya juhudi ili kuujua ukweli ule ulio nje vya vimo yako. Hivyo
Zakayo anatufundisha kwamba hata kama ulimwengu ushatuhukumu, na hali na mazingira
yetu yanatukwamisha, bado tunaweza kukutana na upendo na huruma ya Mungu
tufanyapo bidii. Mtakatifu Agustino wa Hippo katika kweli hii anasema,
“aliyekuumba wewe pasipo wewe, hataweza kukusaidia wewe pasipo wewe.” Hizo
Zakayo kwa juhudi zake, na mpango mahususi wa Mungu, anafanikisha ndoto yake,
na Yesu anakuwa mgeni wake.
Tendo
hili la Yesu linawashangaza wengi na wengine wananung’unika. “Hata
watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye
dhambi,” Lk 19:7. Hapa tunakumbushwa pia moja ya kazi ya Yesu Kristo katika
safari na historia hii ya wokovu kama asemavyo yeye mwenyewe kwamba, “sikuja
kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu,” Lk 5:32.
Kwa
utayari wa Yesu kwenda nyumbani kwa Zakayo, kwa furaha aliyokuwa nayo Zakayo
hakuweza kuificha. Hivyo Zakayo anayaweka yote wazi mbele ya Yesu. “Zakayo
akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini,
na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne,” Lk 19:8. Hii
ni toba ya kweli na maungamo ya wazi mbele ya Yesu aliye sasa njia, kweli na
uzima.
Maungamo
haya ya kweli toka moyoni mwa Zakayo yanaifunua furaha na upendo wa Mungu
kupitia mwanaye Yesu Kristo na kuonyesha kile hasa Yesu alichokijia
ulimwenguni. “Yesu akamwambia, Leo wokovu
umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu,” Lk 19:9.
Wokovu ni kwa kila mmoja na hasa pale tunapouridhia wokovu huo kwa utashi wetu
wenyewe na kwa dhamiri iliyo hai na safi.
Mungu anatazama
utayari wako katika upya wa kuyaanza yote nawe na siyo historia ya maisha yako
mabaya yaliyopita. Tu wapya mbele ya Mungu siku na muda wowote. Ni wewe na mimi
tu kujisalimisha mbele ya uso wake wau pendo, huruma, na Mtakatifu. “Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile
kilichopotea,” Lk 19:10. Ndugu yangu, afadhali kufa kwa heshima kuliko kuishi
kwa unajisi.
Nafasi
ndiyo sasa kusimama katika kweli na haki, na kuchukia uovu wa aina yoyote ile
kwenye maisha yako na jamii inayotuzunguka. Hivyo kwako na kwangu ni mwito
tunaopatiwa leo kila mmoja kadiri ya nafasi na wito wake pale alipo. Kwa yeyote
aliyepewa dhamana na umma kwake vitahitajika vingi pia. Naye Yesu anasema, “Na
kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu
vingi, kwake huyo watataka na zaidi,” Lk 12:48b
Kwa namna hiyo,
kiongozi licha ya kuwa tumaini kwa watu, kiongozi ni mwonyesha tumaini hasa
pale tumaini hilo linapotoweka. Na katika hali na mazingira haya ambayo tumaini
hilo hutoweka, Mtume Paulo anatuwasa na maneno haya ya uzima, “msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala
msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno,” 2The 2:2a. Ndugu yangu, hapa na pale tunapoona kusalitiwa kwa
wale tulio waamini tusiiache kweli na haki, bali ni wakati wa kusimama imara
katika kweli na haki hiyo.
Hivyo, “Mtu
awaye yote asiwadanganye kwa njia yo yote; aliyowaitia ninyi kwa injili yetu,
ili kuupata utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo,” 2The 2:3a, 4. Matumaini yetu
tuyaweke kwa yule atutiaye nguvu, Flp 4:13. Kila mtu kadiri ya imani yake
ayashike maadili yaliyo mema na kuupinga uovu kwa nguvu zake zote.
Masumbuko Mponda Kokoto
kila siku mapenda alfajiri huondoka na nyundo yake na kurudi jioni. Huondoka
akiwa nadhifu na kurudi akiwa nadhifu. Ni mke wake tu katika familia ile wa
watoto wanne aliyekuwa anajua kazi ya mumewe.
Kwa kazi hii nzito na ngumu, watoto wake wake walisoma, kula vizuri,
kuvaa vizuri na kuwa na makazi mazuri.
Siku mmoja Jumamosi,
kama kawaida yake, Masumbuko alijidamka na kuchukua nyundo yake na kuondoka.
Mtoto wake wa kwanza wa kiume-Immanuel,
kwa muda mrefu alikuwa anapenda kujua alichokuwa anafanya Baba yake na nyundo ile. Basi kwa siri
alimfuata nyuma polepole hadi eneo lile la kazi.
Mara baada ya kufika
Masumbuko alibadili nguo zake na kuvaa nguo za kazi zilizokuwa chafu na kuukuu.
Na mara alianza kuyaponda mawe moja baada ya lingine hadi kupata umbo dogo
sana, yaani, kokoto. “Dah! Kumbe kula, kuvaa, na kusoma kwetu kwa raha
kunatokana na kazi hii ngumu ya Baba? Hakika tunamkosea haki sana pale
tunapompigia kelele akiwa amepumzika,” Immanuel alisema kwa masikitiko makubwa.
Hivyo kijana wake-Immanuel
baada ya kuyaona yale, alisogea karibu, na Baba yake alipoinua kichwa alikutana
na uso wa mtoto wake. “Mbona hupo mahali hapa? Ilikupasa uwe nyumbani unafanya
kazi leo jumamosi,” Masumbuko alimuuliza mtoto wake kwa mshangao. “Imenilazimu
kujua kila siku huko uendapo na nyundo yako. Na leo nimeona ukweli wote. Baba
pole sana kwa kazi ngumu hii,” kijana wake alimjibu Baba yake huku machozi
yakimtoka.
“Mwanangu, maisha ni
wito, kuchagua, na kuyapenda. Niliona na kujisikia wito huu wa familila,
nikachagua kuwa na familia, na hiki ninachokifanya ni ishara ya kupenda kile
nilichokichagua. Hivyo katika hali zote nawapenda na nitawapenda daima.
Nafurahi kwa sababu mnafuraha kila mara nirudipo nyumbani,” Baba yake alimjibu
mwanaye huku akiyapangusa machozi yake.
Ndugu yangu, huu ni
upendo wa kweli kwa Wazazi wetu kwa familia zao. Baba yetu wa Mbinguni
anatuwazia mazuri zaidi kwa sababu uwepo wetu
uifunua Furaha na Utukufu wake. “Maana
najua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala
si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11
Tumsifu Yesu Kristo!
“Lakini Wewe unaviachilia vyote,
kwa kuwa ni vyako, Ee Mfalme Mkuu mpenda
roho za watu; maana roho yako isiyoharibika imo katika vyote,” Hek 11:26
Tusali:-Ee
Yesu, asante kwa kutuona hata sisi wadhambi kwa sababu kwako tu upo usalama.
Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario