JUMAMOSI WIKI YA 29 YA MWAKA-C
Somo:
Efe 4:7-16
Zab/Kit:
122:1-2, 3-4a, 4b-5
Injili: Lk 13:1-9
Nukuu:
“Lakini kila mmoja wetu alipewa neema kwa kadiri ya
kipimo cha kipawa chake Kristo,” Efe 4:7
“Naye alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa
manabii; na wengine kuwa wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu,”
Efe 4:11
“Akawajibu
akawaambia, Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa wenye dhambi kuliko
Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo?” Lk 13:2
“Nawaambia, Sivyo; lakini msipotubu, ninyi nyote
mtaangamia vivyo hivyo,” Lk 13:3
TAFAKARI: “Msipotubu, ninyi nyote mtaangamia vivyo hivyo.”
Wapendwa wana wa Mungu,
Injili ya leo inatuasa kutumia vyema fursa hii ya upendo na huruma ya Mungu kwa
kuishi matendo ya roho na kuachana na matendo ya mwili. Tusipoteze Muda mwingi
kuzitazama dhambi za watu wengine na hata maafa ya watu wengine tukafikiri
kwamba wao ni waovu kupita sisi.
Yesu analiona hilo kwa
wayahudi wanapomsimulia tukio lile la Pilato kuchanganya damu za Wagalilaya na
dhabibu zao. Yesu akawaambia, “Je! Mwadhani ya kwamba Wagalilaya hao walikuwa
wenye dhambi kuliko Wagalilaya wote, hata wakapatwa na mambo hayo?” Lk 13:2.
Je, nasi tunatofauti na hao Wayahudi kwa fikra na matendo yetu? Ndugu yangu,
mimi na wewe tunaambiwa hivyo hivyo na Yesu.
Miongoni mwetu wapo baadhi yetu ambao ni hodari sana wa
kuyasema maovu ya watu wengine na wakati mwingine wayasemayo na kuyashuhudia
hayana ukweli wowote juu ya kile wakisemacho au kukishuhudia. Uzushi katika
jamii yetu leo umekuwa ndiyo wimbo tuupendao na uujazao vinywa vyetu. Je,
tumepata nafasi ya kuyachunguza maisha yetu kwa undani? Kama hatufanyi jambo
hili hatuwezi kuepuka kuwa wanafiki.
Yesu anatukaripia kwa
nguvu zote kuhusu unafiki wa mtindo huu na kusema, “Mnafiki wewe, itoe kwanza ile boriti katika jicho lako mwenyewe; ndipo
utakapoona vema kukitoa kile kibanzi katika jicho la ndugu yako,” Mt 7:5.
Hakuna njia ya kuepukana na unafiki huu kama hatutafanya tafiti moyo na kufanya
toba ya kweli. “Nawaambia, lakini msipotubu, ninyi nyote mtaangamia
vivyo hivyo,” Lk 13:3. Kilichowapata
wengine kwa mtindo ule ule kitatupata nasi tusipotubu na kumrudia Mungu.
Mungu wetu ambaye ni Upendo na Huruma
humjalia kila mmoja wetu nafasi na muda wa kutosha kujirekebisha. Mungu huyu
asingekuwa hivyo, tusingeendelea kuishi hata kwa sekunde moja tungali na dhambi
zetu. Ukimya wa Mungu juu ya dhambi zako siyo kwamba haoni kinachoendelea ndani
yako, bali anakupa muda wa kutosha
kufanya tafiti moyo na toba ya kweli.
Mungu wetu ni huruma kama mtunza bustani
alivyomjibu mmiliki wa mtini kwa kutokuzaa matunda yake kwa miaka mitatu
mfululizo. “Bwana, uuache mwaka huu nao, hata
niupalilie, niutilie samadi; nao
ukizaa matunda baadaye, vema! La, usipozaa, ndipo uukate,” Lk 13:8-9. Mungu
wetu ni Mvumilivu sana kwa sababu anatupenda sana. Ni kwa sababu ya Upendo wake
Mungu alichagua kutuumba kama tulivyo kwa sifa na utukufu wake.
Ndugu yangu tunaye
safiri sote katika tafakari hii yatupasa kutumia vyema nafsi na muda tulionao
kuyatenda matendo ya roho. Huu siyo wakati wa kupoteza muda kwa kuyatazama
makandokando ya wengine. Ni vyema ukatambua uzito na vilema vyako ili upata
kumtukuza Mungu kwa yale aliyokujalia ya pekee. Ukweli ni kwamba, “kila mmoja
wetu alipewa neema kwa kadiri ya kipimo cha kipawa chake Kristo,” Efe 4:7. Basi
ni vyema kutumia muda katika kuvitambua vipawa hivi na kuvitumia kwa sifa na
utukufu wake Mungu.
Mungu wetu aliye
Upendo, amemkirimia kila mmoja wetu vipawa na karama kadiri ya hitaji lake yeyé
aliyemwuumba, yaani, Mungu. Hakuna sababu yoyote ya kuwa kivuli kwa kutamani
vipawa vya wengine. Ni katika maana hii kwamba, Mungu kadiri alivyoona inafaa
“alitoa wengine kuwa mitume, na wengine kuwa manabii; na wengine kuwa
wainjilisti na wengine kuwa wachungaji na waalimu,” Efe 4:11. Mpangilio huu una
kusudi lake.
Utofauti huu siyo ile
hali ya kuzidiana na kujiona nani zaidi, bali katika utofauti huu tuweze
kufaidiana. Na kufaidiana huku ndiko tunapokamilishana katika kuujenga mwili wa
Kristo, yaani, Kanisa lake-wote waliobatizwa. Na hili ndilo lengo la Mungu,
yaani, “kwa kusudi la kuwakamilisha watakatifu, hata kazi ya huduma itendeke,
hata mwili wa Kristo ujengwe,” Efe 4:12. Na hatma ya ukamilisho huu ni
“kuufikia umoja wa imani na kumfahamu sana Mwana wa Mungu, hata kuwa mtu
mkamilifu, hata kufika kwenye cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo,” Efe 4:13.
Na cheo cha kimo cha utimilifu wa Kristo ni Utakatifu ule ambao mimi na wewe
yatupasa kuuchuchumilia usiku na mchana. Bila UTAKATIFU huwezi kuuona uso wa
Mungu.
Ukomavu wa Kiroho ni
hatua ya kuufikia ukamilisho, yaani, utakatifu wako. Lengo la makuzi haya ya
kuufikia ukomavu huo “ili tusiwe tena watoto wachanga, tukitupwa huku na huku,
na kuchukuliwa na kila upepo wa elimu, kwa hila ya watu, kwa ujanja,
tukizifuata njia za udanganyifu,” Efe 4:14. Na dalili ya kutokuwa na ukomavu wa
kiroho ni pale unapoona Mkristo akiyumbishwa hapa na pale kwa kukosa imani
thabiti. Leo utamsikia kaokoka, na kesho kutwa kasilimu. Ukomavu wa kiroho ni
kuishika kweli ndani na katika Kristo Yesu. Hivyo, “tuishike kweli katika
upendo na kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeyé aliye kichwa, Kristo,” Efe
4:15. Kristo ndiye Njia, kweli, na Uzima, Yoh 14:6. Amina!
Tumsifu Yesu Kristo!
“Tuishike kweli katika upendo na
kukua hata tumfikie yeye katika yote, yeye aliye kichwa, Kristo,” Efe 4:15
Tusali:-Ee
Yesu, tujalie neema ili tuzame ndani zaidi mioyoni mwetu ili tuvijue vipawa
ulivyotujali, na tuvitumie kwa sifa na utukufu wako.
No hay comentarios:
Publicar un comentario