JUMANNE WIKI YA 28 YA MWAKA-C
Somo:
Gal 4:31b-5:6
Zab/Kit: 119:41, 44, 45, 47, 48
Injili: Lk 11:37-41
Nukuu:
“Tazama, mimi Paulo
nawaambia ninyi ya kwamba, mkitahiriwa, Kristo hatawafaidia neno,” Gal 5:2
“Maana katika Kristo Yesu kutahiriwa hakufai
neno, wala kutokutahiriwa, bali imani itendayo kazi kwa upendo,” Gal 5:6
“Bwana akamwambia, Ninyi Mafarisayo mwasafisha
kikombe na sahani kwa nje, lakini ndani yenu mmejaa unyang'anyi na uovu,” Lk
11:39
“Lakini, toeni sadaka vile vya ndani, na
tazama, vyote huwa safi kwenu,” Lk 11:41
TAFAKARI:
“Toeni sadaka vile vya ndani, na tazama, vyote huwa safi kwenu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
maneno haya ya Yesu, “toeni sadaka vile vya ndani, na tazama, vyote huwa safi
kwenu,” yanatutaka tujue ni kipi hasa kimtiacho mtu unajisi. Mara nyingi
tunapoteza muda wetu mwingi kwa kutazama mambo ya nje na kusahau yale ya ndani
ambayo kwayo hubeba kile ulicho. Katika kweli hii, Yesu anakuambia wewe na
mimi, “Hivi hata ninyi hamna akili? Hamfahamu ya kwamba kila kitu kilicho nje
ya mtu, kikimwingia, hakiwezi kumtia unajisi,” Mk 7:18. Ukweli ni kwamba mambo
ya nje hayamtii mtu unajisi kwayo kama yalivyo. Na mantiki ya hicho asemacho
Yesu kipo hapa, kwamba, vyote alivyoviumba Mungu aliona vinafaa, na vyote vina
malengo yake, Mdo 11:9. “Kwa sababu hakimwingii moyoni, ila tumboni tu; kisha
chatoka kwenda chooni? Kwa kusema hivi alivitakasa vyakula vyote,” Mk 7:19.
Kwa maana nyingine,
“Kimtokacho mtu ndicho kimtiacho unajisi,” Mk 7:20. Ndani ya mtu ndipo lilipo
sanduku la hazina yake. Na ndani ya moyo wa mtu ndipo penye kiwanda cha
kuzalisha mema au maovu. “Kwa maana ndani ya mioyo ya watu hutoka mawazo
mabaya, uasherati, wivi, uuaji, uzinzi, tamaa mbaya, ukorofi, hila, ufisadi,
kijicho, matukano, kiburi, upumbavu,” Mk 7:21-22. Haya ndiyo yanayomtia mtu
unajisi, na yaliyo maovu yatoka ndani ya mtu, Mk 7:23. Ni katika mazingira haya
Yesu anapenda tujue ni wapi kwa kuweka mkazo kama tunataka kukua kiroho.
Yesu alipokaribishwa
nyumbani kwa mfarisayo mmoja alionekana akila bila ya kunawa mikono. Na
“Farisayo huyo alipomwona, alistaajabu kwa sababu hakunawa kabla ya chakula,”
Lk 11:38. Mafarisayo waliyapa mambo haya ya nje nafasi ya pekee sana. Lakini
pamoja na kufanya hayo yote ndani ya mioyo yao walikuwa wakavu sana. Naye Yesu
anawaambia, “Ninyi Mafarisayo mwasafisha kikombe na sahani kwa nje, lakini
ndani yenu mmejaa unyang'anyi na uovu,” Lk 11:39. Ni kama asemavyo Mzaburi
kwamba, “kwa kinywa chao hubariki; kwa moyo wao hulaani,” Zab 62:4b. Hakika
hili ndilo chukizo kwa Mungu, na maigizo kwa mwanadamu.
Yesu haachi kutukaripia
katika maigizo haya tuyafanyao mbele za Baba yake wa Mbinguni. Naye anasema,
“Enyi wapumbavu; aliyevifanya vya nje, siye yeye aliyevifanya vya ndani pia?”
Lk 11:40. Huu ukinzani na mpasuko wa nafsi unatoka wapi? Na tunafanya hayo yote
kwa faida ya nani, au kumfaidia nani? Kumbe ni muhimu sana kuwa makini na yale
tuyatoayo ndani ya mioyo yetu. Mtakatifu Agustino anasema, “onja moyoni
utamkayo mdomoni.” Na Yesu katika hili anatuambia, “toeni sadaka vile vya ndani, na tazama,
vyote huwa safi kwenu,” Lk 11:41.
Haya mambo ya nje ndiyo
anayoyakemea Mtume Paulo kwa jumuiya ile ya Galatia. Tendo la kutahiriwa
lilibeba tafsiri kubwa sana kwa Wayahudi, Rej, Mwa 34:17, Yos 5:5, 8. Lakini
Mtume Paulo anasema, “kutahiriwa si kitu, na kutokutahiriwa si kitu bali
kuzihifadhi amri za Mungu,” 1Kor 7:19. Kumbe kuzishika kwa uaminifu amri za
Mungu kwa sema zaidi kuliko mambo haya ya nje. “Basi ikiwa yeyé asiyetahiriwa
huyashika maagizo ya torati, je! Kutokutahiriwa kwake hakutahesabiwa kuwa
kutahiriwa?” Rum 2:26. Wakati mwingine tunapoteza muda sana kwa haya ya nje na
ya kibinadamu zaidi na yasiyo na utakatifu ndani yake.
Je, kutahiriwa kwa sema
nini ndani na katika Kristo Yesu? Mtume Paulo anasema, “mkitahiriwa, Kristo hatawafaidia neno,” Gal
5:2b. Kwa maana nyingine Mtume Paulo anatuambia kwa kufanya hivyo tu
(kutahiriwa) hakuna thawabu yoyote zaidi ya mambo ya kimwili na kiafya. Hakuna
uhusiano wowote ule na swala zima la kiroho. Na katika hili (kutahiriwa), Mtume
Paulo hapingi kama watu watafanya hivyo, ila kwa kufanya hivyo hakuna uhusiano
wowote ule na swala la kiroho. Naye anasema, “Tena namshuhudia kila mtu
atahiriwaye, kwamba ni wajibu wake kuitimiza torati yote,” Gal 5:3. Ila
angalizo lipo hapa: “Mmetengwa na Kristo, ninyi mtakao kuhesabiwa haki kwa
sheria; mmeanguka na kutoka katika hali ya neema,” Gal 5:4. Matendo haya ya
sheria, mfano, wa hili la kutahiriwa, ni ‘kweli ya Mungu iliyopotoshwa,’
linapohusishwa na swala la kiroho. Matendo hayo ya nje wakati mwingine ni
mateso pasipo neema ndani yake.
Ndugu yangu tuyesafiri
sote katika tafakari hii, mimi na wewe, “kwa Roho tunalitazamia tumaini la haki
kwa njia ya imani,” Gal 5:5. Na kwa mantiki hiyo, “katika Kristo Yesu
kutahiriwa hakufai neno, wala kutokutahiriwa, bali imani itendayo kazi kwa
upendo,” Gal 5:6. Haya ya nje yasipoteze muda wako, na kuukosa Utakatifu ule
ambao ndio cheo chako cha pekee.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Maana sisi kwa Roho tunalitazamia
tumaini la haki kwa njia ya imani,” Gal 5:5
Tusali:-Ee
Yesu na Mwalimu wetu, tujalie mwanga wa Roho wako tuyajue yale ya uzima wa
milele. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario