domingo, 16 de octubre de 2016

TAFAKARI: SIKUKUU YA MTAKATIFU LUKA, MWINJILI


SIKUKUU YA MTAKTIFU LUKA, MWINJILI

Somo: 2Tim 4:10-17b

Zab/Kit: 145:10-11, 12-13, 17-18

Injili: Lk 10:1-9

Nukuu:

 “Katika jawabu langu la kwanza hakuna mtu aliyesimama upande wangu, bali wote waliniacha; naomba wasihesabiwe hatia kwa jambo hilo, ili kwa kazi yangu ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu, hata wasikie Mataifa yote; nami nikaokolewa katika kinywa cha simba,” 2Tim 4:16-17b

Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake,” Lk 10:2

Basi, kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake. Msihame-hame kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii,” Lk 10:7

Na mji wo wote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu; waponyeni wagonjwa waliomo, waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia,” Lk 10:8-9

TAFAKARI: “Kuishi na kuuhubiri Ufalme wa Mungu.”

Wapendwa katika Kristo, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Mtakatifu Luka Mwinjili. Kama jumuiya ya wenye hofu ya Mungu, Yesu anatualika kuliomba hili kadiri ya maitaji ya kanisa lake, na kusema, “Mavuno ni mengi, lakini watenda kazi ni wachache; basi mwombeni Bwana wa mavuno apeleke watenda kazi katika mavuno yake,” Lk 10:2. Hili ni jukumu la kila mbatizwa.

Kufikia lengo la kuutangaza ufalme wa Mbinguni kwa wengine kama alivyofanya Mwinjili Luka, sisi tuliopata habari hii ya wokovu yatupasa kulisimamia jambo hilo kwa weledi mkubwa, kwa kuwa waaminifu kwalo, na kuushikila ukweli huu bila kutetereka. Yesu anatutaka kuwa makini sana huko tuendako kuupeleka ujumbe wa wokovu. Naye anasema, Basi, kaeni katika nyumba iyo hiyo, mkila na kunywa vya kwao; maana, mtenda kazi amestahili kupewa ujira wake. Msihame-hame kutoka nyumba hii kwenda nyumba hii,” Lk 10:7. Na lifanyike jambo moja kwa wakati.

Hii ni pamoja na kuwa makini kwa jambo lile lile tu. Tusibebe ajenda nyingi katika safari hii ya uinjilishaji. Mambo hayo {mfuko, mkoba, viatu na wala kuwaamkie mtu njiani} tukiambatana nayo yatatuchanganya na kutufanya tupoteze mwelekeo. Tuambatane na kubeba yale tu tunayohitaji kwa utume huo. Tusipokuwa na uchache wa vitu furaha na amani ya kweli hutoweka. Tusiuzunike pale ambapo tunaona mambo hayakwenda kama tulivyotarajia. Kufanya hivyo ni kupoteza muda bure kwani muda hautungoji hata kidogo.

Katika jambo hili Yesu anasema, “Na mji wo wote mtakaouingia, nao hawawakaribishi, tokeni humo, nanyi mkipita katika njia zake semeni, Hata mavumbi ya mji wenu yaliyogandamana na miguu yetu tunayakung'uta juu yenu. Lakini jueni hili, ya kuwa Ufalme wa Mungu umekaribia,” Lk 10:10-11. Jambo la msingi la kuzingatia ni kufanya yale tu tuliyotarajia kuyafanya na kuwa na mahusiano mazuri na wale tuliokusudia kuwainjilisha neno la Mungu. Na mji wo wote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu; waponyeni wagonjwa waliomo, waambieni, Ufalme wa Mungu umewakaribia,” Lk 10:8-9. Tuyafanyapo haya kwa unyenyekevu bila kujibakiza huwa msingi wa furaha na Amani yetu.

Mtakatifu Luka Mwinjili sifa yake ya pekee ni utayari wake wa kutoka nje ya mazingira yake na kupeleka habari njema kwa mataifa. Ni Mwinjili pia ambaye kwa kiasi fulani haionyeshi ubaguzi au upendeleo kwa dhima nzima ya historia ya wokovu wa mwanadamu. Kwa upendo wake Mungu, na kwa vile tumeumbwa kwa sura na mfano wake, wote tumeitwa kuurithi ufalme wa mbinguni. Na jambo hili linajidhihirisha katika kweli hii, kwamba, “Katika jawabu langu la kwanza hakuna mtu aliyesimama upande wangu, bali wote waliniacha; naomba wasihesabiwe hatia kwa jambo hilo, ili kwa kazi yangu ule ujumbe utangazwe kwa utimilifu, hata wasikie Mataifa yote; nami nikaokolewa katika kinywa cha simba,” 2Tim 4:16-17b. Safari ya uinjilishaji siyo lelemama. Ni kujitoa muhanga haswa na bila kujibakiza.

Leo kwa kufuata nyayo za Mtakatifu Luka Mwinjili, kila mbatizwa na mwimarishwa ni jukumu lake la msingi pale alipo kufanya uinjilishaji mpya. Na yote tuyafanyayo yajengwa juu ya msingi imara wa Kristo mwenyewe. Mimi na wewe tuliyebatizwa na kuimarishwa tuwe chumvi na mwanga katika dhima hii mpya, yaani, uinjilishaji mpya pale nilipo.

Tumsifu Yesu Kristo

“Na mji wo wote mtakaouingia, wakiwakaribisha, vileni vyakula viwekwavyo mbele yenu; waponyeni wagonjwa waliomo, waambieni, Ufalme wa Munguumewakaribia,” Lk 10:8-9

Tusali:-Ee Yesu, tufanye vyombo vyako katika uinjilishaji mpya pale tulipo. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario