JUMATATU WIKI YA 29 YA MWAKA-C
Somo:
Efe 2:1-10
Zab/Kit: 100:2, 3, 4, 5
Injili: Lk 12:13-21
Nukuu:
“Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na dhambi
zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na kwa
kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana wa
kuasi,” Efe 2:1-2
“Maana
tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea
awali Mungu aliyatengeneza ili tuenende nayo,” Efe 2:10
“Mtu mmoja katika
mkutano akamwambia, Mwalimu, mwambie ndugu yangu anigawie urithi wetu,” Lk
12:13
“Akawaambia, Angalieni, jilindeni na choyo,
maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo,” Lk 12:15
“Ndivyo alivyo mtu
ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu,” Lk 12:21
TAFAKARI:
“Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo katika wingi wa vitu
vyake alivyo navyo.”
Wapendwa wana wa Mungu,
masomo yetu ya leo na hasa Injili,
yanatualika tutafakari kwa undani maisha yetu na uhusiano wake na mali. Ndugu
moja anamwendea Yesu mbele ya mkutano na kumwamuru amwambie ndugu yake amgawie
urith wao, Lk 12:13. Badala yake, Yesu anamuuliza swali la msingi na la
kushangaza. “Akamwambia, Mtu wewe,
ni nani aliyeniweka mimi kuwa mwamuzi au mgawanyi juu yenu?” Lk 12:14. Swali hili linatutaka kuweka bayana
nini maana ya maisha yetu na mahusiano yake na mali. Ndugu yangu unayesafiri
nami katika tafakari hii, elewa leo kwamba maisha yako ni dhamana hapa duniani,
na mali tulizo nazo tumeazimwa tu kwa muda. Mali ni za Mungu.
Wapendwa wana wa Mungu,
muda wetu hapa duniani na nguvu zetu, akili, nafsi, mahusiano, na mali zetu
zote ni zawadi toka kwa Mungu ambazo ametukabidhi tuvitunze na kuvitumia
vizuri. Sisi ni mawakili wa yale Mungu atupayo. Wazo hili la uwakili huanza na
utambuzi wa kuwa Mungu ndiye mmiliki wa kila kitu na kila mtu duniani.
"Nchi na vyote viijazavyo ni mali ya Bwana, dunia na wote wakaao ndani
yake." Zab 24:1. Hivyo Yesu anamtahadharisha kijana yule na sisi pia kwa
kutuambia kwamba, “Angalieni, jilindeni na choyo, maana uzima wa mtu haumo
katika wingi wa vitu vyake alivyo navyo,” Lk 12:15. Uzima wako na furaha yako
ya kweli haitokani na wingi wa mbali ulizokuwa nazo. Kwa maana nyingine, vitu
hivyo kwa kuwa navyo kwa wingi havituhesabii haki mbele za Mungu.
Ndugu yangu, kama
humwamini yule aliyefufuliwa kutoka wafu yaani, Kristo Yesu, wingi wa utajiri
wako ni bure kabisa kwa sababu mali zote ni za Bwana ukiwa na wewe mwenyewe.
Mtume Paulo anasema, “sisi tunaomwamini
yeye aliyemfufua Yesu Bwana wetu katika wafu; ambaye
alitolewa kwa ajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili mpate kuhesabiwa haki,”
Rum 4:24b-25. Hivyo wingi wa mali zako bila Imani juu ya Kristo mfufuka ni
bure.
Hakika
"hatumiliki" chochote kwa wakati wetu mfupi wa kuishi duniani. Mungu
"hutukopesha" dunia tunapoishi hapa. Ilikuwa mali ya Mungu kabla
hujaja, na Mungu anamkopesha mtu mwingine ukifa. Je unabisha? Ndugu, ukweli ni
kwamba unaifurahia dunia hii kwa muda mfupi tu. Injili ya leo inatuambia kwamba
asiyefahamu ukweli huu ni MPUMBAVU kama mkulima yule tajiri aliyetaka
kufurahisha nafsi yake kwa kusema, ‘pumzika basi, ule, unywe, ufurahi,” bila
kujua ni nani aliye sababu ya uzima wake. “Lakini
Mungu akamwambia, Mpumbavu wewe, usiku huu wa leo wanataka roho yako! Na vitu
ulivyojiwekea tayari vitakuwa vya nani? Ndivyo
alivyo mtu ajiwekeaye nafsi yake akiba, asijitajirishe kwa Mungu,” Lk 12:20-21. Ndugu yangu bado furaha yako ipo kwenye mali?
Mungu alipowaumba Adamu na Hawa,
aliwakabidhi uangalizi wa uumbaji wake na akawaweka kuwa wadhamini wa uumbaji
wa mali yake. "Zaeni, mkaongezeke, mkaijaze nchi, na kuitiisha; mkatawale
samaki wa baharini, na ndege wa angani, na kila kiumbe chenye uhai kiendacho
juu ya nchi," Mwa 1:28
Ndugu unayesafiri nami katika tafakari
hii, kazi ya kwanza ambayo Mungu aliwapa wanadamu ni kuangalia na kutunza
"vitu" vya Mungu duniani. Wajibu huu haujaondolewa kamwe. Ni sehemu
ya malengo yetu leo. Kila kitu tunachokifurahia yapasa tukione kama dhamana
ambayo Mungu ameiweka mikononi mwetu. "Hapo tena inayohitajiwa katika
mawakili, ndiyo mtu aonekane kuwa mwaminifu." 1Kor 4:2
Yesu mara kwa mara anaonyesha kuwa
maisha ni dhamana na anatoa mfano wa talanta, mfanya biashara alikabidhi
watumishi utajiri wake alipo safiri. Aliporudi alitathmini kazi ya kila
mtumishi na kumpa ujira sawasawa na kazi yake. Yule tajiri anasema, "vema, mtumwa mwema na mwaminifu;
ulikuwa mwaminifu kwa machache, nitakuweka juu ya mengi; ingia katika furaha ya
Bwana wako," Mt 25:21.
Ndugu yangu, mwisho wa maisha yako
duniani utatathminiwa kulingana na ulivyotumia yale Mungu aliyokukabidhi. Hii
inamaana kwamba mambo yote unayofanya, hata yale mambo madogo madogo ya kila
siku, yana matokeo ya umilele.
Kama utaona mambo yote kuwa dhamana,
Mungu anaahidi zawadi tatu katika maisha ya milele. Kwanza, utapewa
"uthibitisho". Atasema, "kazi nzuri! umefanya vyema." Kisha
"utapandishwa" daraja na utapewa jukumu kubwa katika umilele:
"nitakuweka uwe mwangalizi wa vitu vingi." Na mwisho utakaribishwa
katika "karamu." "Njoo ushiriki katika furaha ya Bwana wako.
Watu wengi wanashindwa kufahamu kuwa
pesa ni jaribu na dhamana toka kwa Mungu. Mungu anatumia pesa kutufundisha
kumtegemea; na kwa watu wengi fedha ni jaribu kuu kupita yote. “Maana
shina moja la mabaya ya kila namna ni kupenda fedha; ambayo wengine hali
wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani, na kujichoma kwa maumivu mengi,” 1Tim
6:10. Mungu anaangalia jinsi tunavyotumia pesa ili kupima jinsi gani
tunaaminika. "Basi, kama ninyi hamkuwa waaminifu katika mali ya udhalimu,
ni nani atakayewapa amana mali ya kweli?" Lk 16:11. Ndugu yangu,
unapoelekea kwenye chaguzi mbalimbali, na hata zile chaguzi kuu, unampimaje
yule anayekuja kwako nakuomba ridhaa ya uongozi na kusimamia mali ya umma kwa uaminifu? Je,
historia yake huko nyuma inathibitisha ukweli wa hicho anachokiomba kwenu?
Tusiwakabidhi fisi zizi la kondoo. Hakika kondoo hawatakuwa salama.
Huu ni ukweli wa muhimu sana. Mungu
anasema kuna uhusiano wa moja kwa moja baina ya ninavyotumia pesa zangu au
utajiri wangu na hali yangu ya kiroho. Jinsi ninavyotawala pesa zangu
"utajiri wa dunia" ni kigezo cha kiasi gani Mungu anaweza kunikabidhi
baraka za kiroho, "utajiri wa kweli".
Hebu jiulize ndugu yangu, Je, namna
ninavyotumia fedha zangu yaweza kumzuia Mungu kufanya mambo zaidi maishani
mwangu? Je, ninaweza kuaminiwa katika utajiri wa kiroho? Wapo watu wachache
katika mazingira na maisha yetu, walioweza kuthibitisha uhusiano wa moja kwa
moja baina ya walivyotumia pesa zao na hali ya kiroho ya maisha yao. Pesa au
utajiri wao havikuwa kipao mbele katika maisha yao.
Watu na maisha yao ya dhiki ilikuwa kero
zake na mara zote alijitahidi kutafuta suluhu ya kero hizo za watu. Mtu wa
namna hii ndiye tunayeweza kuumpa dhamana ya kusimamia mali ya umma.
Alilolisema ndilo alilolifanya. Dhima hii ndiyo iliyompa nguvu ya Kimaadili.
Mfano wa mtu huyu ni Baba yetu wa Taifa; Julius Kambarage Nyerere,
aliyetutangulia katika haki. Mungu amlaze mahali pema peponi. Sina shaka katika
maisha yake. Ipo siku atapewa uangalizi mkubwa zaidi na Mama Kanisa na kuwa
Mwombezi wetu-Mtakatifu.
Yesu Kristo anasema, "na yule
asiyejua, naye amefanya yastahiliyo mapigo, atapigwa kidogo. Na kila aliyepewa
vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake
huyo watataka na zaidi." Lk 16:48. Maisha ni dhamana. Na kadiri Mungu
anavyokupa zaidi, ndivyo anakutaka uwajibike zaidi.
Hakuna uzima ndani yake kama hatuta
bandukana na haya ya leo na kesho katika ulimwengu huu. Je, hayana nafasi
katika maisha yetu? La hasha! Kwayo kama yalivyo yatumike vizuri katika maana
ya kutuwezesha kuyafikia maisha yale ya umilele ambalo ndilo kusudi la kuumbwa
kwetu. Ni kukosa pale unapoyapa haya ya dunia nafasi ya pekee na ya mwisho
katika maisha yetu.
Ndani na katika Kristo Mkombozi wetu
hatupaswi kuenenda kwa mtindo huo. “Nanyi mlikuwa wafu kwa sababu ya makosa na
dhambi zenu; ambazo mliziendea zamani kwa kuifuata kawaida ya ulimwengu huu, na
kwa kumfuata mfalme wa uwezo wa anga, roho yule atendaye kazi sasa katika wana
wa kuasi,” Efe 2:1-2. Tukienenda katika stahi hii mbele ya safari kuna anguko
kubwa.
Mtume Paulo anaiona kweli hiyo-anguko
hilo, naye mwenyewe anajichukulia kama mfano wa watu hao “ambao zamani, sisi sote nasi tulienenda kati
yao, katika tamaa za miili yetu, tulipoyatimiza mapenzi ya mwili na ya nia,
tukawa kwa tabia yetu watoto wa hasira kama na hao wengine,” Efe 2:3. Maisha ya
tumaini kwa Mkristo ni kuishi maisha ya UFUFUKO.
Na maisha haya ya ufufuko ni kuuvua utu
ule wa zamani, na kuuvaa utu mpya, Efe 4:22-28. “Kwa maana kama mlivyounganika
naye katika mfano wa mauti yake, kadhalika mtaunganika kwa mfano wa kufufuka
kwake; mkijua neno hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulibishwa pamoja naye,
ili mwili wa dhambi ubatilike, tusitumikie dhambi tena; kwa kuwa yeye aliyekufa
amehesabiwa haki mbali na dhambi,” Rum 6:5-7. Uhakika huu ujidhihirisha tu katika
maisha ya Ufufuko tunapoishi ndani na katika Kristo Yesu.
Na yote haya yanafanyika kwetu si kwa
mastahili yetu, yaani, kadiri ya wasifu wetu, bali ni kwa upendo wake Mungu
kwetu, na ndiye amuhesabiaye mtu haki kadiri aonavyo Yeye na inavyompendeza.
Hapa ndipo tunapoona NEEMA ya Mungu kama asemavyo Mtume Paulo kwamba, “Lakini
Mungu, kwa kuwa ni mwingi wa rehema, kwa mapenzi yake makuu aliyotupenda; hata
wakati ule tulipokuwa wafu kwa sababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na
Kristo; yaani, tumeokolewa kwa neema,” Efe 2:4-5. Na tunapoongelea ‘neema’ ya
Mungu hakuna swala la juhudi binafsi. “Kwa maana mmeokolewa kwa neema, kwa njia
ya imani; ambayo hiyo haikutokana na nafsi zenu, ni kipawa cha Mungu; wala si
kwa matendo, mtu awaye yote asije akajisifu,” Efe 2:8-9. Hakika hatuna chochote
cha kujisifu kwa kile tulicho na yale tuyafanyayo.
Fundisho hili la Mtume Paulo kuhusu
NEEMA linalandana kabisa na kile alichokisema Yesu Kristo juu ya mzabibu na
matawi, akifananisha uhusiano wake na sisi katika safari nzima ya ukombozi.
Naye Yesu anasema, “Mimi ni mzabibu; ninyi ni matawi, akaaye ndani yangu nami
ndani yake, huyo huzaa sana; maana pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lo
lote. Mtu asipokaa ndani yangu, hutupwa nje kama tawi na kunyauka; watu
huyakusanya na kuyatupa motoni yakateketea. Ninyi mkikaa ndani yangu, na maneno
yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa,” Yoh 15:5-7. Hakika bila Kristo Yesu hatuwezi lolote lile, liwe
dogo au kubwa! Na sababu ni hii kwamba; “tu kazi yake, tuliumbwa katika Kristo
Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu aliyatengeneza ili
tuenende nayo,” Efe 2:10. Je, kweli hii katika tafakari ya
leo inasema chochote kuhusu maisha yako?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Maana tu kazi yake, tuliumbwa
katika Kristo Yesu, tutende matendo mema, ambayo tokea awali Mungu
aliyatengeneza ili tuenende nayo,” Efe 2:10
Tusali:-
Ee Yesu Mwema, tujalie tudumu siku zote ndani na katika Wewe uliye kila kitu
katika maisha yetu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario