IJUMAA WIKI YA 27 YA MWAKA-C
Somo:
Gal 3:7-14
Zab/Kit: 111:1-2, 3-4, 5-6
Injili: Lk 11:15-26
Nukuu:
“Na andiko, kwa
vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa kwa imani,
lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe Mataifa yote
watabarikiwa,” Gal 3:8
“Basi hao walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu
aliyekuwa mwenye imani,” Gal 3:9
“Naye akajua mawazo yao, akawaambia, Kila ufalme
uliofitinika wenyewe kwa wenyewe hufanyika ukiwa; na nyumba juu ya nyumba
huanguka,” Lk 11:17
“Basi, ikiwa Shetani naye amefitinika juu ya nafsi
yake, ufalme wakemutasimamaje? Kwa kuwa ninyi mnasema kwamba mimi natoa pepo
kwa Beelzebuli,” Lk 11:18
“Mtu ambaye si
pamoja nami yu kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutawanya,” Lk
11:23
TAFAKARI: “Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa
kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana.”
Wapendwa wana wa Mungu, katika
somo letu la Injili ikiwa ni mwendelezo ule ule wa kumkomboa mwanadamu, Yesu
anapata shutuma za kutoa pepo kwa kutumia nguvu za Pepo Mkuu- Beelzebuli. Je, mawazo hayo ya kishirikina yanatoka
wapi kwa wana hawa wa Israeli? Kama kweli walikuwa wanamwabudu Mungu mmoja,
iweje wawe na mawazo kama hayo? Wapendwa wana wa Mungu, tusipoachana na yaliyo
yetu na ubinadamu wetu hatutaweza kuondokana na hisia za kishirikina. Ni wazi
kwamba licha ya kuwa walimwamini Mungu moja, watu hawa hawakuachana na yaliyo
yao na ubinadamu wao. Hisia hizo mbaya juu ya uwezo wa Yesu wa kutoa pepo kwa
nguvu wasiyoijua, zinakuja kwa sababu miongoni mwao walikuwa na mazoea ya
kufanya hivyo. Mara nyingi mtu humwekea hisia mbaya mtu mwingine kwa kile
ambacho yeye huwa anakifikiri na kukitenda.
Kutokana na tuhuma hizo za Wayahudi
juu ya uwezo wake Yesu wa kutoa pepo, ilhali Yesu akiyajua mawazo yao,
anawafikirisha kidogo na kusema, “Kila
ufalme uliofitinika wenyewe kwa wenyewe hufanyika ukiwa; na nyumba juu ya
nyumba huanguka,” Lk 11:17. Hoja hapa ni kwamba, kama Yeye, yaani, Kristo,
anayafanya hayo yote na watu wanapona kwa kuutoa utawala wa pepo, kuna sababu
gani ya kufanya hivyo kwa maana ya kwenda kinyume cha yule aliyempa nguvu hizo
yaani Beelzebuli? Kwa kufanya hivyo kama hoja yao inamshiko ni kujichanganya
kwa utawala huo wenyewe. Ila Yesu anawaambia kwama hayo yote anayafanya kwa
uwezo wa Mungu mwenyewe. Na kwa mantiki hiyo Ufalme wa Mungu huu kati yao
tayari. Hawana sababu ya kuwa na hofu. “Lakini,
ikiwa mimi natoa pepo kwa kidole cha Mungu, basi ufalme wa Mungu umekwisha
kuwajilia,” Lk 11:20. Ni mara ngapi tunapata nguvu na uponyaji kwa njia ya sala
na maombi na mara tupatapo tena shida kama hiyo tunakosa imani na kwenda kwa
waganga wa kienyeji? Kwa nini basi
unatapatapa katika Imani?
Wapendwa
wana wa Mungu, kujitenga kwetu na Mungu kwa kufuata mambo yetu na ubinadamu
wetu ndiko kunakotunyima neema na baraka zake. Tunajifungia milango wenyewe na
tunapokosa neema na baraka hizo tuna mtafuta mchawi aliyeturoga. Ni sawa na
mlevi aliyepoteza ufunguo kwenye Kilabu cha pombe akawa usiku kucha anatafuta
ufungua barazani mwa jirani yake eti kwa sababu tu pale kuna mwanga. Je,
ataupata ufunguo huo? Ndiyo maana Yesu leo anatuambia maneno haya mazito, “Mtu ambaye si pamoja nami yu kinyume changu; na
mtu asiyekusanya pamoja nami hutawanya,” Lk 11:23. Ndugu yangu, hakuna namna
nyingine tuwezayo kupata neema na baraka kama hatutajisalimisha moja kwa moja
kwa Kristo.
Imani
yetu ndani na katika Kristo Yesu Mwokozi wetu ndiyo ponya yetu kwa sababu, “Yeye ndiye jiwe lile lililodharauliwa na ninyi
waashi, nalo limewekwa kuwa jiwe kuu la pembeni. Wala hakuna wokovu katika mwingine
awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu
litupasalo sisi kuokolewa kwalo,” Mdo 4:11-12. Na kwa kutokuamini kwao
Wayahudi, Mtume Paulo anawarudisha nyumba kwa Ibrahimu ambaye Mungu alimhesabia
haki na kuwa mfano wa mtu aliyekuwa na Imani thabiti. “Na
andiko, kwa vile lilivyoona tangu zamani kwamba Mungu atawahesabia haki Mataifa
kwa imani, lilimhubiri Ibrahimu habari njema zamani, kusema, Katika wewe
Mataifa yote watabarikiwa,” Gal 3:8. Na kwa kuhesabiwa haki huku kwa Ibrahamu
kama Baba wa Imani haikuwa kwa sababu ya matendo ya sheria.
Akiwa ndio mfano na
muhimili wa Imani katika agano lile la kale, waliokuwa na Imani kabla ya ujio
wa Bwana wetu Yesu Kristo walibarikiwa pamoja
Ibrahimu. Kwa mantiki hiyo, “hao
walio wa imani hubarikiwa pamoja na Ibrahimu aliyekuwa mwenye imani,” Gal 3:9.
Matendo ya sheria ambayo yalikuwa ni ukweli wa Mungu ulipotoshwa kwa kukidhi
matakwa ya kibinadamu hayakuwa na Umungu ndani yake, na hivyo kuhesabika kama
laana. Na Yeremia Nabii anasema, “Bwana
asema hivi, Amelaaniwa mtu yule amtegemeaye mwanadamu, Amfanyaye mwanadamu kuwa
kinga yake Na moyoni mwake amemwacha Bwana. Na,
amebarikiwa mtu yule anayemtegemea Bwana, Ambaye Bwana ni tumaini lake,” Yer
17:5,7. Yaliyo ya kibinadamu na yenye lengo la kunyanyua binadamu katika
ubinafsi wake hayana thawabu mbele ya Mungu.
Ni vyema kuelewa kuwa
Mtume Paulo haipingi torati kama ilivyoachwa na Musa, bali anapinga tafasiri ile
ya torati-Talmud, ambayo ilipewa kipaumbele zaidi ya torati yenyewe. Hata Yesu
mwenyewe haipingi torati zaidi ya kuikamilisha kama asemavyo, “Msidhani ya kuwa nalikuja kuitangua torati au
manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza. Kwa maana, amin, nawaambia, Mpaka
mbingu na nchi zitakapoondoka, yodi moja wala nukta moja ya torati
haitaoondoka, hata yote yatimie,” Mt 5:17-18. Hivyo ni makosa kufikiri kwamba
Mtume Paulo anaipinga torati kama ilivyo.
Ni
katika mazingira haya ya tafasiri ya torati, Mtume Paulo anayasema haya kwamba,
“wale
wote walio wa matendo ya sheria, wako chini ya laana; maana imeandikwa,
Amelaaniwa kila mtu asiyedumu katika yote yaliyoandikwa katika kitabu cha
torati, ayafanye,” Gal 3:10. “Yaliyoandikwa katika kitabu cha torati ayafanye,”
ni yale yaliyofafsiriwa na walimu wa sheria kutoka torati yenyewe, na
yaliyobeba ubinadamu zaidi kuliko Umungu. Kwa kuyafuata hayo kuna laana ndani
yake. Yamebeba utukufu wa mwanadamu ambao kwayo hauwezi kumkomboa. Ni mbwembwe
tu.
Ni kwa mantiki hiyo
kwamba, “ni dhahiri ya kwamba hakuna mtu ahesabiwaye haki mbele za Mungu katika
sheria; kwa sababu Mwenye haki ataishi kwa imani,” Gal 3:11. Kwenye haki
ataishi milele kwa sababu tunda la haki ni amani, na penye amani upendo
ujidhihirisha. Na penye haki, amani, na upendo Mungu hujidhihirisha, na imani
ukolezwa zaidi na zaidi. Kwa mtazamo huu, “torati haikuja kwa imani, bali,
Ayatendaye hayo ataishi katika hayo,” Gal 3:12. Torati ambayo ni sheria ya
Mungu katika upana wake, utusaidia kuibainisha dhambi, na kuishi kadiri ya
mapenzi yake Mungu. Ni Kristo Yesu pekee aliye muhimuli kati ya hiyo
torati-sheria, na upendo huo wa Mungu Baba usio na kipimo.
Kristo Yesu ndiye
anayeweza kututoa katika anguko hili la laana. “Kristo alitukomboa katika laana
ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwa ajili yetu; maana imeandikwa,
Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti; ili kwamba baraka ya Ibrahimu
iwafikilie Mataifa katika Yesu Kristo, tupate kupokea ahadi ya Roho kwa njia ya
imani,” Gal 3:13-14. Kwa kifo chake cha Msalaba na kwa ufufuko wake, Mungu
“akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; juu sana kuliko ufalme
wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si
ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; akavitia vitu vyote chini ya
miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya kanisa; ambalo
ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote,” Efe
1:20-23. Huyu ndiye twapaswa kushikamana naye kwa sababu ndani na katika yeye
ipo njia, kweli, na uzima, Yoh 14:6.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Mtu ambaye si pamoja nami yu
kinyume changu; na mtu asiyekusanya pamoja nami hutawanya,” Lk 11:23
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tujalie neema tudumu katika imani ndani na katika Wewe. Amina.
No hay comentarios:
Publicar un comentario