IJUMAA WIKI YA 29 YA MWAKA-C
Somo:
Efe 4:1-6
Zab/Kit:
24:1-2, 3-4ab, 5-6
Injili: Lk 12:54-59
Nukuu:
“Kwa hiyo nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana,
mwenende kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa,” Efe 4:1
“kwa unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu,
mkichukuliana katika upendo,” Efe 4:2
“Enyi wanafiki, mwajua kuutambua
uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya?” Lk
12:56
“Maana,
unapofuatana na mshitaki wako kwenda kwa mwamuzi, hapo njiani fanya bidii kupatanishwa
naye, asije akakuburuta mpaka mbele ya kadhi; yule kadhi akakutia mikononi
mwake mwenye kulipiza, na yule mwenye kulipiza akakutupa gerezani,” Lk 12:58
TAFAKARI: “Mwenende kama inavyoustahili wito wenu mlioitiwa.”
Wapendwa wana wa Mungu, hakuna yeyote kati yetu kwa
kile alicho leo kwake ni bahati mbaya. Iwe leo mimi ni mlei, mtawa, mtawa na
mkleri, au mkleri, yote ni kwa mpango na kusudi la Mungu kuishi kusudi lile la
kuumbwa kwangu; yaani, nimjue muumba wangu, nimpende, nimtumikie, na mwisho
nirudi kwake mbinguni. Na hatma ya maisha yako na yangu ni umilele. Hivyo
wajibu msingi kwa kila mmoja hapa duniani ni kuenenda kama ilivyostahili wito
wake alioitiwa. Na huu ndio ujumbe wa Mtume Paulo kwangu na kwako, kwamba,
“nawasihi, mimi niliye mfungwa katika Bwana, mwenende kama inavyoustahili wito
wenu mlioitiwa,” Efe 4:1.
Paulo ni mfungwa wa Kristo katika maana ya
kuyasalimisha maisha yake yote ndani na katika Kristo Yesu. Kama
ni tunu ya thamani katika maisha yake Paulo Mtume ni ‘Kristo katika yote.’ Hivyo
kujisalimisha kwangu kwa Kristo kusiwe kwa asimila kadhaa tu. Asilimia 95
hazitoshi! Leo katika maisha ya ufufuko, mimi na wewe lisiwe lengo la kuisha
kwa kukubaliana kwa kutokubaliana. Ni kuishi yote katika yote, yaani, “kwa
unyenyekevu wote na upole, kwa uvumilivu, mkichukuliana katika upendo,” Efe
4:2. Tunapochukiliana katika hali na mazingira haya, Roho Mtakatifu huyaongoza
na kuyaratibisha yote hata pale tunapokosa majibu katika hali ya sintofahamu.
Na hili ndilo
alilomaanisha Yesu kwamba, “lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri
jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema. Kwa kuwa si ninyi
msemao, bali ni Roho wa Baba yenu asemaye ndani yenu,” Mt 10:19-20. Hivyo ni
jukumu langu na lako “kujitahidi kuuhifadhi umoja wa Roho katika kifungo cha
amani,” Efe 4:3. Na kuishi katika kweli hii kunamaanisha kuishi katika “Mwili mmoja, na Roho mmoja, kama na
mlivyoitwa katika tumaini moja la wito wenu. Bwana mmoja, imani moja, ubatizo
mmoja,” Efe 4:4-5. Na Mungu huyu tunayemwamini, mwabudu, na kumpa shukrani zetu
“ni Baba wa wote, aliye juu ya yote na katika yote na ndani ya yote,” Efe 4:6.
Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, elewa kwamba, ndani na katika
Kristo Yesu upo salama. Unachoitajika kukifanya ni kimoja tu, yaani, jisalimishe
kwake bila kujibakiza. Na hii ndiyo kweli na siri ya maisha yale ya umilele.
Lakini siri hii ya
maisha ya umilele ujifunua hatua kwa hatua tunapoishi na kuenenda kwa uaminifu
kila mmoja kama ilivyostahili wito wake alioitiwa. Je, niende wapi kumtafuta
Kristo? Ndugu yangu, tukio lile la ufufuko wa Bwana wetu Yesu Kristo limeweka
wazi ni wapi yanipasa kumtafuta na kukutana na Kristo Yesu. Katika hali ya
kufadhaika kwa wale waliokwenda kaburini
na kulikuta lipo wazi, watu wawili waliosimama karibu nao, wamevaa nguo za
kumeta-meta, waliwaamba, “kwa nini mnamtafuta aliye hai katika wafu?” Lk 24:5.
Watu wale waliwaambia wakumbuke aliyoyasema Yesu alipokuwapo nao Galilaya.
Kuanzia siku ile Kristo Yesu hakuwa anapatikana makaburini, yaani, kusiko kuwa
na tumaini, bali kwenye tumaini jipya yaani, Galilaya. “Lakini enendeni zenu,
mkawaambie wanafunzi wake, na Petro, ya kwamba awatangulia kwenda Galilaya;
huko mtamwona, kama alivyowaambia,” Mk 16:7. Ndugu yangu, Galilaya yako leo ni
kile ulichoitiwa kadiri ya wito wako. Hapo utakutana na Kristo Yesu endapo
utaishi kwa uaminifu na hofu yake Mungu. Na hapo ndipo penye utakatifu wako.
Hata hivyo ukweli ni
kwamba, sheria ya Mungu katika utu wa ndani, ni UHURU aliyopewa mwanadamu
umsaidia katika mambo mazuri kumwelekea Yeye na ufalme wake. Kufurahia uhuru
huu katika ubaya ndilo anguko la mwanadamu. Sheria ya utu huu wa ndani, yaani
uhuru ulionao unapoifanya nafsi yako kuegemea mwili, ndipo mtu anapodondoka
kwenye dhambi iliyo katika viungo vyake. Hii ni sawa na nafsi kupigwa mwereka
na uhuru huu ambao ndiyo sheria ya ndani ya utu wako. “Kwa
maana naifurahia sheria ya Mungu kwa utu wa ndani, lakini katika viungo vyangu naona
sheria iliyo mbali, inapiga vita na ile sheria ya akili zangu, na kunifanya
mateka ya ile sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu,” Rum 7:22-23.
Kujinasua katika mtego huu ni kutambua na kuyafanya matendo ya Roho ambayo
ndani kwayo yamejaa uhai na uzima, Gal 5:22-23.
Unapotambua hali hiyo
na usifanye chochote ndicho anachosema leo Yesu katika Injili. “Enyi wanafiki, mwajua kuutambua uso wa nchi na
mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya?” Lk 12:56. Ni kuujua ukweli kama ulivyo nawe ukabaki katika ubishi na ung’ang’anizi
usio na uzima ndani yake. Watesi wa Yesu nyakati zake, hasa Waandishi,
Mafarisayo na Wanasheria, waliujua ukweli lakini waliupindisha kwa makusudi
kukidhi haja zao na maslahi yao.
Yesu anawashauri na kutushauri sisi leo
kwamba, kama tunaufahamu ukweli basi tuufuate na kuufanya tungali hai kwani
hakimu wetu Mungu yupo anasafiri nasi kuelekea kwenye kiti cha hukumu. “Maana, unapofuatana na
mshitaki wako kwenda kwa mwamuzi, hapo njiani fanya bidii kupatanishwa naye,
asije akakuburuta mpaka mbele ya kadhi; yule kadhi akakutia mikononi mwake
mwenye kulipiza, na yule mwenye kulipiza akakutupa gerezani,” Lk 12:58. Kumbe
kabla ya kutupwa gerezani, yaani kwenye mateso yasiyo na mwisho, Mama Kanisa
anatushirikisha huruma ya Mungu kwa kupitia Sakramenti ya upatanisho. Sote
tunahitaji toba na kupatanishwa na Mungu kila tunapodondoka katika dhambi.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Enyi wanafiki, mwajua kuutambua
uso wa nchi na mbingu; imekuwaje, basi, kuwa hamjui kutambua majira haya?” Lk
12:56
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, nifunulie hatua kwa hatua siri ile ya uzima wa milele kadiri ya
zawadi ya wito ulionijalia. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario