ALHAMISI WIKI YA 27 YA MWAKA-C
Somo:
Gal 3:1-5
Zab/Kit: Lk 1:69-70, 71-72, 73-75
Injili: Lk 11:5-13
Nukuu:
“Enyi Wagalatia msio na
akili, ni nani aliyewaloga, ninyi ambao Yesu Kristo aliwekwa wazi mbele ya
macho yenu ya kuwa amesulibiwa?” Gal 3:1
“Nataka kujifunza neno
hili moja kwenu. Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia
kunakotokana na imani?” Gal 3:2
“Basi, yeye awapaye Roho na kufanya miujiza
kati yenu, je! Afanya hayo kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana
na imani?” Gal 3:5
“Nami nawaambia,
Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa,” Lk
11:9
“Kwa kuwa kila aombaye
hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye atafunguliwa,” Lk 11:10
“Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa
watoto wenu vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho
Mtakatifu hao wamwombao?” Lk 11:13
TAFAKARI:
Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani?”
Gal 3:2
Wapendwa
wana wa Mungu, maneno haya ya Yesu kwetu leo ni uzima kwani yeye ndiye njia,
kweli na uzima wetu. Naye anasema, “kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye
abishaye atafunguliwa,” Lk 11.10. Tokeo la tendo hili utegemea sana kina cha
imani yako. Hata hivyo mara nyingi
hatuyapati yale tuyaombayo si kwa sababu Mungu hasikii maombi yetu, bali Yeye
mwenyewe anajua ni wakati gani ufao kutupatie kile tuombacho.
Kwa hiyo yatupasa kudumu katika maombi tukiwa na imani
thabiti bila kukata tamaa. Kwa upande mwingine yawezekana hatuyapati yale
tuyaombayo kwa sababu hatujui kuomba vizuri. Mtume Yakobo anatuambia hivi; “Hata mwaomba, wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili
mvitumie kwa tamaa zenu,” Yak 4:3. Kumbe kwa maana nyingine kuomba kwetu
kusilenge tu katika ubinafsi wetu. Sala uombayo ilenge pia makundi mengine
yenye mahitaji kama yako na hata yasio na mwelekeo na ya kwako.
Pamoja na
imani dhabiti, jambo linguine katika sala ni kuwa na msimamo endelevu na
komavu. Kutokuwa na msimamo katika sala ni tatizo kubwa sana katika kufunguliwa
kwetu kwa yale tuyaombayo. Uvumilivu katika sala ni muhimu sana, na huonyesha
ukomavu katika maisha ya kiroho. Tunapokosa utulivu wa ndani ni rahisi kubebwa
na kila wimbi au upepe. Mtu yeyote anayeruhusu hali hii maombi yake huwa ya
majaribio na kumfanya kuhama kutoka Kanisa moja kwenda lingine. Hali hii
inapoota mizizi humfanya muhusika kutoka imani moja na kwenda nyingine. Mtu
huyu anachotafuta ni kile kiitwacho ‘upako’ kwa kubahatisha bahatisha. Mungu
wetu sio wa kubahatisha na wala si wa majaribu.
Mwisho wa
siku mtu mwenye mwelekeo huu wa Imani huishia kutokuamini kabisa. Hukosa imani
kabisa na Mungu aliyekuwa anamwamini hapo mwanzo na kuishia kuwa asiyeamini
chochote. Somo letu la Injili linafafanua vizuri
dhana nzima ya wanyofu wa moyo na kuhesabiwa haki mbele za Mungu. Hawa ndio
waliomfanya Mungu kuwa kimbilio lao. Hawa ndio wale wasiokuwa na mbadala wa
maisha yao zaidi ya Mungu katika shida zao. Hawa ndio Yesu anaowaambia, “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona;
bisheni, nanyi mtafunguliwa,” Lk 11:9. Huu ndio uhusiano wa Mungu na
aliyemnyofu wa moyo.
Mungu kamwe hatosita kutokumhesabia haki katika kweli aliye
mnyofu wa moyo. “Kwa kuwa kila aombaye hupokea; naye atafutaye huona; naye abishaye
atafunguliwa,” Lk 11:10. Ni kweli hata aliyekatili aweza kutoa bila upendo kwa
yule anayemsumbua, lakini mwenye kupenda hawezi kuacha kutoa. Mungu wetu ni
upendo na anajua mahitaji yetu yote. Naye Yesu anaufunua upendo huu wa Mungu
kwetu kwa kusema, “Basi, ikiwa ninyi mlio waovu mnajua kuwapa watoto wenu
vipawa vyema, je! Baba aliye mbinguni hatazidi sana kuwapa Roho Mtakatifu hao
wamwombao?” Lk 11:13. Ndugu yangu
tunayesafiri pamoja katika tafakari hii,
jisalimishe kwake aliye Mungu wa kweli, upendo, haki na amani.
Hata
hivyo, Mtume Paulo katika somo letu la kwanza anaendelea
kuweka wazi kwamba kazi yoyote ya sheria yoyote ile haina uwezo wa
kumhesabia mtu haki kwa ajili ya dhambi
zake za zamani. Mungu anataka wewe na mimi na tulio wakristo kushika sheria
zake na amri katika dhamira iliyo hai, kamili, na ya kiroho. Kwa maana
hiyo, hakuna sheria yenye uwezo wa
kusamehe dhambi, au kumhalalisha kiroho mtu na Mungu, kutoa Roho Mtakatifu, au
kumpatia mtu uzima wa milele.
Kazi ya sheria za Mungu
na amri zake ni kufafanua dhambi: Gal 3:1-5, ‘Enyi Wagalatia, nani aliyewaloga
msitii kweli, ambao mbele ya macho ya Yesu Kristo, aliyesulibiwa, ilikuwa
imeelezwa katika maandishi na tangazo la wazi? Hii tu nataka kujifunza kutoka
kwenu: Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na
imani?” Gal 3:2. Je, mu wajinga kiasi
hicho? Baada ya kuanza katika Roho,
mnataka kukamilishwa sasa katika mwili?” Gal 3:3, [kwa kutii sheria za kimwili za kiyahudi]...
Kwa hiyo, fikiria hili: “Basi, yeye awapaye Roho na kufanya miujiza kati yenu,
je! Afanya hayo kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani?”
Gal 3:5
Wapendwa wana wa Mungu,
matendo ya sheria ni ‘kweli ile ya Mungu iliyopotoshwa ili kukidhi matakwa ya
kibinadamu.’ Na nyakati zile za Yesu na hata kipindi kile cha jumuiya ya kwanza
ya Wakristo, Wayahudi walifuata tafsiri ya Torati na masimulizi yake-Talmud
ambayo ilikuwa imejaa mbwembwe nyingi za kibinadamu bila utakatifu wa Mungu ndani
yake. Hivyo kwa kuyafuata matendo hayo ya sheria ni kupotea muda ikiwa ni
pamoja na chukizo kwa Mungu na maigizo kwa mwanadamu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Basi, yeye awapaye Roho na kufanya
miujiza kati yenu, je! Afanya hayo kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia
kunakotokana na imani?” Gal 3:5
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tujalie heri na baraka katika maisha yetu ya kila siku kadiri ya
wema na huruma yako kwa sababu watujua vyema. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario