jueves, 27 de octubre de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 30 YA MWAKA-C


JUMAMOSI WIKI YA 30 YA MWAKA-C

Somo: Flp 1:18b-26

Zab/Kit: 42:2, 3, 5abc

Injili: Lk 14:1, 7-11

Nukuu:

“Lakini kwa njia zote, ikiwa ni kwa hila, au ikiwa ni kwa kweli, Kristo anahubiriwa; na kwa hiyo nafurahi, naam, nami nitafurahi,” Flp 1:18b

 “Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida,” Flp 1:21

 “Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma,” Lk 14:8-9

 “Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11

TAFAKARI: “Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo katika somo la Injili Yesu anatupa angalizo hasa tunapoalikwa kwenye tafrija mbalimbali. Tukizama ndani zaidi tunaona kwamba uhai tulionao na maisha tunayoyaishi ni sawa na kualikwa kwenye furaha ya Mungu na Utukufu wake. Basi ni vyema mimi na wewe kutambua duniani hapa tunapita tu, na tupo kwa maandalizi ya maisha ya umilele. Yesu anatuwasa hivi kuhusu ukweli huu; Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma,” Lk 14:8-9.

Kama sote tumealikwa harusini ni wazi tumepewa mastahili yaliyo sawa na yule aliyetualika. Basi yatupasa kujua kuwa sote ni waalikwa na siyo ‘mgeni rasmi.’ Kwa utaratibu wa kawaida mbele palipoandaliwa si mastahili yangu. Kumbe ni vyema na busara kutafuta nafasi nyingine. Ili kuwa sehemu salama zaidi, Yesu anatuasa hivi; Bali ukialikwa, nenda ukaketi mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe,” Lk 14:10. Huku ndiko kwa maneno mengine kupungua ili Mungu awe na nafasi juu ya maisha yako.

Ndugu yangu unaye safiri nami katika tafakari hii utakubaliana nami kwamba kati yetu kwa nafasi tulizokuwa nazo na madaraka tuliyonayo yaliyopitiliza hututia upofu na kutufanya kuwa ndiyo fimbo ya kuchapia wengine. Jeuri hii ndugu yangu tunaipata wapi wakati Maandiko Matakatifu yanatuambia, Siku za miaka yetu ni miaka sabini, Na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; Na kiburi chake ni taabu na ubatili, Maana chapita upesi tukatokomea mara,” Zab 90:10. Jinyenyekeshe basi na kuwa kile Mungu alichokusudia katika maisha yako.

Mfano mzuri wa unyenyekevu huu tunaupata kutoka somo letu la kwanza, na hasa juu ya maisha ya Mtume Paulo. Paulo mara tu baada ya kuongoka kwake, dira ya maisha yake yote ni kupungua ili Kristo aliye Njia, Kweli, na Uzima awe na nafasi juu ya maisha yake. Na hii ndiyo njia sahihi ya kufuata kama waja na wana wa Mungu. Na kauli mbiu ya Mtume Paulo ni hii; “Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida,” Flp 1:21. Kwa mtazamo huu, Paulo hana cha kujisifia wala kujikweza zaidi ya neema ile ya Mungu ifanyayo kazi ndani ya maisha yake.

Mpendwa katika Kristo, mimi na wewe yatupasa kupungua ili Kristo aongezeke kwa wanyonge, mayatima, wajane, masikini, wafungwa, wagonjwa, waliokata tamaa, wanaoonewa kwa ajili ya haki, wafiwa, wadhabi, wanaodhulumiwa, na wale wate walitengwa kwa kusimama katika kweli na haki. Watu hawa ndio waliokuwa karibu na zaidi, marafiki wa Yesu Kristo kama asemavyo mwenyewe kwamba, “sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu,” Lk 5:32. Leo mimi ninayepumua na kufurahia afya njema nione wajibu huo mkubwa wa Kristo mbele yangu.

Na kwa kutambua wajibu huo mkubwa na mwendelezo wa kazi ile ya wokovu wetu, ndani na katika Kristo Yesu, nijue kwamba,  “kwa njia zote, ikiwa ni kwa hila, au ikiwa ni kwa kweli, Kristo anahubiriwa; na kwa hiyo nafurahi, naam, nami nitafurahi,” Flp 1:18b. Kama ilivyo kwamba hakuna aliyekuwa masikini kwa kutoa kile alichonacho, vivyo hivyo hakuna atakayepoteza muda wake kwa kulihubiri neno la Mungu kila siku, na zaidi kwa maisha yake ya kumcha Mungu.

Tendo la kupeleka habari njema kwa wengine, ni tendo la neema na baraka. Kuna furaha kubwa sana kwa Mungu na Watakatifu wake siku moja ukiwa mbele ya Mungu, na mmoja kati ya wale waliohesabiwa haki na Mungu kutoa ushuhuda juu yako kwamba, ‘utakatifu wake ulitokana na kuijua siri hiyo ya mbinguni na kwa kumjua Mungu kupitia wewe.’

Na hii ndiyo maana ya maneno haya ya Paulo ambaye sasa kwa ajili ya Injili hakuna alichopoteza, anachopoteza, na atakachopoteza. Naye anasema, “Maana najua ya kuwa haya yatanigeukia kuwa wokovu wangu, kwa sababu ya kuomba kwenu, na kuruzukiwa Roho wa Yesu Kristo; kama vile nilivyotazamia sana, na kutumaini, kwamba sitaaibika kamwe, bali kwa uthabiti wote, kama sikuzote na sasa vivyo hivyo Kristo ataadhimishwa katika mwili wangu; ikiwa kwa maisha yangu, au ikiwa kwa mauti yangu,” Flp 1:19-20. Hakika Mtume Paulo katika hatua hii hana alichokibakiza kwa ajili yake mwenyewe, yote kesha yakabidhi kwa Kristo Yesu na yeye Kristo ni yote katika yote.

Hata hivyo, Mtume Paulo anatupa leo angalizo, tena zito sana. Kamwe mimi na wewe tusijilinganishe na yale tuyafanyayo, na kamwe kwayo kama yalivyo yasiwe ndiyo chanzo na mwisho wa furaha yetu. Hilo likiwa ndilo lengo la maisha yako, basi ujue bado hujajitambua na kutambua kusudi lako la kuumbwa na uwepo wako hapa duniani. Hapa na pale unaweza kupewa pongezi na hata kupigiwa makofi. Lakini mara uonavyo hivyo, usibaki na pongezi hizo na makofi hayo, bali mara mrudishie Mungu sifa na shukrani hiyo, na kuwabariki wale wote waliotambua kweli hiyo ndani yako, nawe uwe wa mwisho katika kundi hilo la stahili ya baraka hiyo. Ni kwa maana hii Mtume Paulo anasema juu ya kuishi maisha yanayoongozwa na malengo, kwamba, “ikiwa kuishi katika mwili, kwangu mimi ni matunda ya kazi; basi nitakalolichagua silitambui,” Flp 1:22.

Ndugu yangu, maisha yako katika hali salama lazima yasukumwe na mambo mawili; kukaa na Kristo, na kudumu katika huduma kwa ajili ya watu. Naye Mtume Paulo anasema hivi katika kweli hii, “Ninasongwa katikati ya mambo mawili; ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo maana ni vizuri zaidi sana; bali kudumu katika mwili kwahitajiwa zaidi kwa ajili yenu,” Flp 1:23-24. Kumpenda Kristo na kuishi ndani na katika Kristo Yesu kutakulazimu kutumika kwa ajili ya wengine, tena bila faida binafsi.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11

Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema ya kudumu ndani na katika wewe tu kwa sababu kwako kuna furaha ya kweli. Amina

 

No hay comentarios:

Publicar un comentario