JUMANNE WIKI YA 30 YA MWAKA-C
Somo:
Efe 5:21-33
Zab/Kit:
128:1-2, 3
Injili: Lk 13:18-21
Nukuu:
“Lakini kama vile
Kanisa limtiivyo Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila
jambo,” Efe 5:24
“Enyi waume, wapendeni
wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa ajili yake; ili
makusudi alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno apate kujiletea Kanisa
tukufu, lisilo na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu
lisilo na mawaa,” Efe 5:25-27
“Maana hakuna mtu anayeuchukia mwili wake po
pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea Kanisa,” Efe
5:29
“Lakini kila mtu ampende mke wake kama nafsi
yake mwenyewe; wala mke asikose kumstahi mumewe,” Efe 5:33
“Kisha
alisema, Ufalme wa Mungu umefanana na nini? Nami niufananishe na nini?” Lk
13:18
“Umefanana
na punje ya haradali aliyotwaa mtu akaitupa katika shamba lake; ikamea, ikawa
mti; ndege wa angani wakakaa katika matawi yake,” Lk 13:19
“Umefanana
na chachu aliyotwaa mwanamke akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata
ukachacha wote pia,” Lk 13:21
TAFAKARI:
“Upendo wa Kristo na Kanisa lake.”
Wapendwa wana wa Mungu,
upendo wa Kristo na Kanisa lake ndicho kiini cha pendo zote. Upendo huu wa
Mungu kwa watu wake yatupasa kuuona katika mambo yote yenye kutupeleka katika
umoja wake, upendo wake, ushirikiano wake na hata katika maagano yetu katika
maisha. Ni kwa kupitia umoja huo, upendo huo, na ushirikiano huo wa Mungu na
mwanaye mpenzi Yesu Kristo, Mungu hujidhihirisha kwetu kila siku ya maisha yetu
hapa duniani.
Upendo wa Mungu na
mshikamano na mwanaye tunauona katika Masakramenti yake, na hasa leo
tunavyotafakari kwa ukaribu Sakramenti hii ya ndoa. Naye Mtume Paulo anasema, “Enyi wake, watiini waume zenu kama kumtii Bwana
wetu. Kwa maana mume ni kichwa
cha mkewe, kama Kristo naye ni kichwa cha Kanisa; naye ni mwokozi wa mwili,”
Efe 5:22-23. Hapa upendo wa Mungu kupitia Kristo mwenyewe unaonekana kwa utii
huu wanaoishi wana ndoa, na hasa kwa mke kumtiii mumewe. Je, ndoa zetu leo ni
salama? Akina mama mnaishi ukweli huu katika agano lenu la ndoa? Leo baadhi ya
wanawake wamefikia kuwaita waume zao vyuma chakavu. Je, hayo ndiyo makusudio ya
Mungu na muungano wenu huo?
Kwa upande wa wanaume
yawapasa kuwapenda wake zao katika kweli na haki. Upendo huu unafananishwa na
upendo wa Kristo na Kanisa lake. “Enyi
waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda Kanisa, akajitoa kwa
ajili yake; ili makusudi
alitakase na kulisafisha kwa maji katika neno; apate kujiletea Kanisa tukufu, lisilo
na ila wala kunyanzi wala lo lote kama hayo; bali liwe takatifu lisilo na
mawaa,” Efe 5:25-27. Wanaume zieshimuni ndoa zetu kwani ndipo penye utakatifu
wenu mnapoziishi katika kweli na haki. Wake zenu hawahitaji mambo ya pekee sana
zaidi ya nyie kuyasadifu yale wayatendayo wake zenu kila siku katika familia.
Tabia ya kuwaita wake zetu magoli kipa ni chukizo mbele ya Mungu. Muunganiko
wenu ni makusudio ya Mungu, na ndivyo alivyoona inafaa.
Utii wa kweli si utumwa
kwenu, bali ni ukamilifu wa makusudio ya Mungu katika maisha ya umilele. Wito
wenu wa ndoa ni kuufikia umelele wa maisha yenu mlioandaliwa kupitia Sakramenti
hiyo. Hivyo, “kama vile Kanisa limtiivyo
Kristo vivyo hivyo wake nao wawatii waume zao katika kila jambo,” Efe 5:24. Ni
kuwa na utii katika Kristo kwa sababu yeye anayo maneno la uzima wa milele. Ni
kwa kupitia NENO huyu vyote vilifanyika, na kwa kupitia NENO huyu vyote huwa na
uzima wa milele, Yoh 1:3. “Kwa sababu hiyo
mtu atamwacha baba yake na mama yake, ataambatana na mkewe na hao wawili
watakuwa mwili mmoja,” Efe 5:31.
Tendo hili la ajabu
katika Sakramenti hii ya ndoa halimwesabii haki mmoja wa wanandoa kuwa na mambo
yake ya pekee na binafsi tena. Hakuna msamiati huu tena wa kusema hiki changu
na hiki chako. Kwa kufanya hivyo ni kuujeruhi mwili huu mmoja. Je, jambo hili
lina ukweli katika ndoa yako? Je, ni mambo mangapi ya siri unayoyafanya bila
kumuhusisha mwenzi wako wa ndoa? Je, hujui kwa kufanya hayo unaijeruhi ndoa
yako? Ndugu yangu kama unaishi ukweli huu na kinyume cha Sakramenti hiyo ya ndoa,
elewa kwamba ndoa hiyo ishakufa katika uhalisia wa mambo na ukweli wa Kimungu.
Kilicho baki ni maigizo tu, na wote mmekuwa wasanii katika Sakramenti hii
Takatifu.
Hata hivyo, hayo yote
tuishiyo kila mmoja kadiri ya wito yake ulenga katika imani ya kweli itupelekayo
katika uzima wa milele. Swali ni hili; Je,
imani hiyo itupelekeayo kwenye Ufalme wa Mungu ina mfanano gani?
Jibu la swali hili limetolewa katika
Injili ya leo. Yesu anauliza aufananishe na nini na ufalme wa mbingu? Kwanza
Yesu anasema ufalme huu, “Umefanana
na punje ya haradali aliyotwaa mtu akaitupa katika shamba lake; ikamea, ikawa
mti; ndege wa angani wakakaa katika matawi yake,” Lk 13:19. Maana yake nini?
Ndugu yangu unayesafiri nami katika tafakari hii, imani ni kuamini na kusadiki
pasipo shaka yale mambo madogo madogo yanayoonekana na yasiyooneka na yenye
kuufunua utukufu wa Mungu.
Punje ya haradali ni
ndogo sana. Lakini katika udogo huu mwisho wake huwa mti mkubwa na ndege wa
angani wakakaa katika matawi yake. Imani si jambo la siku moja, bali imani ukua
hatua kwa hatua kadiri tunavyoishi na kuona vitu na mazingira yake kwa mwono wa
Kimungu, (Kila kitu kuwa na sababu yake).
Pili, Yesu anasema
ufalme wa Mungu “umefanana na chachu aliyotwaa mwanamke
akaisitiri ndani ya pishi tatu za unga, hata ukachacha wote pia,” Lk 13:21.
Imani ya kweli na thabiti ni nguvu ya ndani ya ajabu kwa mtu ambayo hubadili
kabisa mwonekano wa vitu kwa mtu, utendaji, na hata namna ya kuyachukulia
mambo. Chachu katika uchache wake hubadili kabisa mwono na umbo wa kile
kilichochachushwa. Imani hii ndiyo inayotupa nguvu na dira mpya ya kuyaona
maisha kwa namna ya pekee licha ya ufupi wake na sababu ya kuishi kwetu hapa
duniani, katika maana ya makazi ya muda mfupi. Makazi haya ni sehemu ya
maandalizi ya maisha ya umilele ambayo ndiyo Ufalme wenyewe wa Mungu.
Hivyo ndugu yangu,
tunapoishi hapa duniani mambo haya yafuatayo yatupasa kuyazingatia. Moja, msingi wa maisha yetu lazima ujengwe katika
haki. Kwani, “yaliyo haki kabisa ndiyo utakayoyafuata, ili upate
kuishi na kuirithi nchi upewayo na Bwana, Mungu wako,” Kumb 16:20. Pili,
tusienende katika tamaa za wanadamu. “Tangu sasa msiendelee kuishi katika tamaa za
wanadamu, bali katika mapenzi ya Mungu, wakati wenu uliobaki wa kukaa hapa
duniani,” 1Pet 4:2. Na tatu na mwisho, kuishi kwetu kuwe ndani na katika
Kristo. “Kwa maana kwangu
mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida!” Flp 1:21. Kristo ndiye mtetezi wetu
na mwokozi wetu. Amina
Tumsifu Yesu Kristo!
“Maana hakuna mtu anayeuchukia
mwili wake po pote; bali huulisha na kuutunza, kama Kristo naye anavyolitendea
Kanisa,” Efe 5:29
Tusali:-Ee
Yesu, nijalie furaha ya kweli katika wito wangu. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario