JUMATATU WIKI YA 31 YA MWAKA-C
Somo:
Flp 2:1-4
Zab/Kit: 131:1, 2, 3
Injili: Lk 14:12-14
Nukuu:
“Basi ikiwako faraja yo
yote katika Kristo, yakiwako matulizo yo yote ya mapenzi, ukiwako ushirika wo
wote wa Roho, ikiwako huruma yo yote na rehema, ijalizeni furaha yangu, ili mwe
na nia moja, wenye mapenzi mamoja, wenye roho moja, mkinia mamoja,” Flp 2:1-2
“Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni,
usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye
mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo,” Lk 14:12
“Bali
ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa
kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki,”
Lk 14:13-14
TAFAKARI:
“Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu.”
Wapendwa wana wa Mungu,
leo tunaishi katika ulimwengu wa ushindani mkubwa sana, na mbaya zaidi ushindani unaojali nafsi na
ubinafsi. Hakuna anayetaka kwenda kwa hasara ingawa ndilo lengo la ye yote yule
aliye katika ushindani hasa ushindani wa kibiashara. Ni hulka ya binadamu
kutafuta mafaa katika faida. Hivyo kwa mazingira ya leo na mtazamo wake,
ukihimidi hali hii basi utaupata ulimwengu wote.
Hata hivyo, Yesu
anatupa angalizo hasa kwa wale wenye kusombwa na hulka hii kiasi kwamba kusahau
sehemu ile ya pili ambayo ni muhimu sana, yaani, NAFSI na ROHO. Binadamu ni
mwili, nafsi na roho, na vyote na vyote vitatu ndivyo vimfanyavyo binadamu
aliye hai. Mwili ni nyumba ya Nafsi na Roho, ingawa nafsi ipo kati ya mwili na
roho. Nafsi ikiegemea mwili utaishia katika matendo ya mwili ambayo kwayo
hakuna uzima wa milele, Gal 5:19-21. Na nafsi ikiegemea Roho matokeo yake ni
tunda la roho, ambalo kwalo kuna uzima wa milele, Gal 5:22-23.
Ni katika mazingira
haya Yesu anazihoji dhamiri zetu na kwa kutoa angalizo, na kusema, “kwa kuwa
itamfaidia mtu nin kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Ama
mtu atoe nini badala ya nafsi yake?” Mk
8:36-37. Basi nikiwa nafanya ushindani wowote ule ni ufanye nikilenga faida ya
wote. Hivyo “Basi ikiwako faraja yo yote katika Kristo, yakiwako matulizo yo
yote ya mapenzi, ukiwako ushirika wo wote wa Roho, ikiwako huruma yo yote na
rehema, ijalizeni furaha yangu, ili mwe na nia moja, wenye mapenzi mamoja,
wenye roho moja, mkinia mamoja,” Flp 2:1.2. Huu ni upendo na mwono wa kujali
kama wafuasi wake Kristo tukijifunza unyenyekevu wake na utii kwa Mungu Baba.
Mwito kwetu leo sote
kama wana wa Mungu na warithi wa ufalme wake, yatupasa kueneka katika hofu ya
Mungu. Na hofu hii ya Mungu utusuma kutenda bila majivuno bali kwa unyenyekevu
na kuwajali wengine. Na hili ndilo analosisitiza Mtume Paulo kwetu, kwamba,
tusitende, “neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa
unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake,” Flp
2:3. Na kama ni faida basi iwe kwa ajili ya wengi. Hivyo, “Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe,
bali kila mtu aangalie mambo ya wengine,” Flp 2:4. Mtindo huu katika kufikiri,
kuamua na kutenda, unasema zaidi kuhusu tabia ya Yesu Kristo na kuthibitisha
pendo lake kwetu. Naye Yesu katika kweli hii anasema, “hakuna aliye na upendo
mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh
15:13.
Na tabia ya Yesu
inasema zaidi kuhusu mtindo wake wa maisha ulivyokuwa. Yesu licha ya kwamba
hakuwa hata na mahali pa kulaza kichwa chake, Lk 9:58, marafiki zake wakubwa
walikuwa masikini, vilema, viwete, vipofu,
wadhambi, wakoma, wazinzi, watoto, akina mama, waliotengwa na wale wote
walikata tamaa. Ukaribu na urafiki wa Yesu katika makundi haya ya watu
haukulenga kudumisha mtindo wa maisha yao, bali kuwatoa katika hali zao za
unyonge, na kufurahia nuru na neema ya Mungu. Mimi na wewe tunahitaji nuru na
neema hiyo ya Mungu.
Tabia hii ya Yesu
inajidhihirisha katika Injili yetu ya leo hasa katika matendo yale ya upendo na
huruma. Namna yetu ya kufikiri, kuamua, na kutenda kuwe na mwelekeo wau pendo
na huruma hasa pale tunapoigusa jamii inayotuzunguka. Na katika kweli hii Yesu
anasema, “Ufanyapo chakula cha mchana au cha
jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako
wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo,” Lk 14:12. Kufanya
hivyo ni kuukubali upendo faida-nipe nikupe. Huu ni upendo linganishi na
shindanishi. Ni upendo usio tayari kupoteza kwa faida na mafaa ya wengi. Huu ni
upendo tasa na wenye kubaki katika hali ile ile ya mwenendo sawa bila
mabadiliko ya kupoteza.
Bali
kinyume chake Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, “Bali ufanyapo karamu waite
maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha
kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki,” Lk 14:13-14. Huu ni
upendo ule ulio tayari kutoa bila tegemeo la kupokea. Ni upendo wa kujitoa bila
faida. Ni upendo unaotazama mafaa ya kitu kama kilivyo kwani cha stahili. Ni
upendo wenye kuwajibisha kwa sababu huwezi kupenda ukaacha kutoa. Ni upendo
uliokomaa na ulio tayari kuzaa. Na kimo cha upendo huu ndicho hiki asemacho
Kristo Yesu, kwa namna nyingine, kwamba, “Chembe ya ngano isipoanguka katika
nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi,” Yoh
12:24.
Ndugu
yangu tuliyesafiri sote katika tafakari hii, hakuna haja ya kwenda mitaani, na
mijini kuwatafuta hawa marafiki na wapendwa wa Kristo Yesu. Marafiki hawa wa
Yesu na wapendwa wake unao hapo ulipo. Embu anza kutazama vizuri hapo nyumbani
kwako (Mke, watoto, ndugu, na wafanyakazi wote). Je, hawapo? Embu tazama vizuri
pia katika Jumuiya yako ndogo ya Kikristo (familia zake, wanajumuiya wote, na
mahitaji yao na Kanisa Mahalia). Je, hawapo? Bila shaka baada ya zoezi hili
utakutana na marafiki na wapendwa hawa wa Kristo Yesu. Fanya kitu kwa ajili
yao. Amina!
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Bali ufanyapo
karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana
cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki,” Lk 14:13-14
Tusali:-Ee Yesu Mwema,
nipe macho ya kuona marafiki na wapendwa wako, na nijalie moyo wa kuwapenda
kama ulivyo wapenda na kuwajali. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario