Somo
I: Kut 17:8-13
Zab/Kit: 121:1-2, 3-4, 5-6, 7-8
Somo II: 2Tim 3:14-4:2
Injili: Lk 18:1-8
Nukuu
“Ikawa, Musa alipouinua mkono wake, Israeli
walishinda; na alipoushusha mkono wake, Amaleki walishinda,” Kut 17:11
“Lakini mikono ya Musa ilikuwa mizito; basi wakatwaa
jiwe, wakaliweka chini yake akalikalia. Haruni na Huri wakaitegemeza mikono
yake, mmoja upande huu na mmoja upande huu; mikono yake ikathibitika hata jua
lilipokuchwa,” Kut 17:12
“Kila andiko,
lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na
kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili,
amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema,” 2Tim 3:16-17
“lihubiri neno,
uwe tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa
uvumilivu wote na mafundisho,” 2Tim 4:2
“Akawaambia mfano, ya kwamba imewapasa kumwomba Mungu
sikuzote, wala wasikate tamaa,” Lk 18:1
“Na Mungu, je!
Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni mvumilivu
kwao?” Lk 18:7
“Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini,
atakapokuja Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?” Lk 18:8
TAFAKARI: “Waweza kutoa bila kupenda, ila huwezi kupenda ukaacha kutoa.”
Wapendwa
wana wa Mungu, kuumbwa kwetu wanadamu halikuwa hitaji la Mungu, bali kwa upendo
wake alichakugua kutuumba kwa sura na mfano wake, Mwa 1:27. Kwa hiyo lengo la kwanza la
uumbaji wetu ni kuishi milele. Kwa tendo hili ni wazi kwamba lengo la pili la
uumbaji wetu ni kuwa na mahusiano na Mungu na sisi kwa sisi. Mahusiano haya
msingi wake ni upendo. “Tena
nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue
moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu,” 1Kor 13:3. Kadhi kama tulivyosoma na
kusikia Injili ya leo anampa mama mjane haki yake si kwa kupenda bali kwa
kulazimika kutokana na usumbufu. Naye anasema, “Ijapokuwa
simchi Mungu wala sijali watu, lakini,
kwa kuwa mjane huyu ananiudhi, nitampatia haki yake, asije akanichosha kwa
kunijia daima,” Lk 18:4b-5. Hivyo unaweza kutoa bila kupenda.
Tunapokuwa
na mahusiano mazuri na Mungu kamwe hawezi kutuacha katika mahangaiko yetu.
Bwana wetu Yesu Kristo anatupatia uhakikisho huyo. “Na
Mungu, je! Hatawapatia haki wateule wake wanaomlilia mchana na usiku, naye ni
mvumilivu kwao?” Lk 18:7. Uvumilivu wa Mungu
kwetu ni Imani ile tuliyo nayo juu yake. Kwa imani thabiti tunauhakika kwa
kuyapata yale tumwombayo Mungu wetu aliye huruma na upendo. Ukweli huu
unajidhihirisha pia katika historia ya ukombozi wetu, kama somo letu la kwanza linavyo simulia kisa kile
cha wana wa Israeli na Waamaleki.
Kwa imani na
matumaini makubwa waliyokuwa nayo Waisraeli chini ya uongozi wa Musa, Mungu
haachi kutoa huruma yake kwa sababu aliwapenda. Musa ni kielelezo cha uvumilivu
huo ambao Mungu anataka tuwe nao hasa katika mazingira yale ya sintofahamu.
Hivyo “Ikawa, Musa alipouinua mkono wake, Israeli
walishinda; na alipoushusha mkono wake, Amaleki walishinda,” Kut 17:11. Kwa
upande mwingine hili ni jaribu la Mungu kwetu hasa pale tunapozingirwa na hali
tatanishi. Lakini ukweli ni kwamba, pasipo njia Mungu huifanya njia. Hakuna
jaribu lolote tulipatalo katika maisha Mungu akashindwa kutuonyesha njia ikiwa
tutadumu katika uthabiti wa Imani. “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo
kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita
mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze
kustahimili,” 1Kor 10:13. Na jaribu alilolipata Musa ni mikono yake kuwa mizito
ilhali walitegemea ushindi kutoka kwa watesi wao-Waamaleki.
Tendo la kuishusha
mikono yake ilimaanisha kushindwa, na walizidiwa nguvu na Waamaleki. “Lakini
mikono ya Musa ilikuwa mizito; basi wakatwaa jiwe, wakaliweka chini yake
akalikalia. Haruni na Huri wakaitegemeza mikono yake, mmoja upande huu na mmoja
upande huu; mikono yake ikathibitika hata jua lilipokuchwa,” Kut 17:12. Na
walipodumu katika jaribu hili Mungu alifungua neema na baraka zake. Na ndipo “Yoshua akawaangamiza Amaleki na watu wake
kwa ukali wa upanga,” Kut 17:13. Imani ya kweli hujaribiwa. Na lengo la jaribu
ni kuimarisha imani hiyo ile kesho uwe shuhuda na shahidi kwa wengine walio na
imani haba.
Yesu anatupa pia
uhakika wa jambo hili, ila imani ni moja ya kielelezo kikuu kwa kile tuombacho.
Nawaambia, atawapatia haki upesi; walakini, atakapokuja
Mwana wa Adamu, je! Ataiona imani duniani?”
Lk 18:8. Je, unayoimani kwa hayo uyaombayo?
Kwa upande mwingine uwezi kupenda bila kutoa. Yesu
anasema, “Mimi ndimi mchungaji mwema. Mchungaji mwema huutoa
uhai wake kwa ajili ya kondoo,” Yoh 10:11. Yesu kwa kutupenda yupo tayari kutua
uhai wake kwaajili yetu. Upendo ndiyo amri yenyewe. Kristo ndiye kielelezo
chetu juu ya upendo na kupenda. Hili ndilo lile neno lililofanyika mwili nalo
likakaa kwetu.
Wapendwa wana wa Mungu, Ufalme wa Kristo ni tokeo la Yeye mwenyewe
kujitoa msalabani kwa hiari, awe sadaka safi iletayo amani, ili atimize mafumbo
ya ukombozi wa watu. Naye Yesu anasema hivi juu ya utayari wake katika kujitoa,
“Hakuna
mtu aniondoleaye, bali mimi nautoa mwenyewe. Nami ninao uweza wa kuutoa, ninao
na uweza wa kuutwaa tena. Agizo hilo nalilipokea kwa Baba yangu,” Yoh 10:18. Hakika “hakuna
aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki
zake,” Yoh 15:13. Ni Yesu tu na wale
wote aliowaridhia.
Ufalme wa Kristo na sifa zake, yaani, ‘ufalme wa kweli na uzima,
ufalme wa utakatifu na wa neema, ufalme wa haki, amani na mapendo’ ni kinyume
kabisa na ulimwengu wenye kufurahia ‘uovu,’ na mbaya kabisa pale mwanadamu kwa
kulijua hili ni ‘ovu’ anakufa ganzi, na kutokufanya chochote. Kufa ganzi huku
ni moja ya dalili ya kifo cha ile dhamiri hai ndani ya mtu. Na hapa ndipo leo
tunaposema kwamba watu siyo kwamba tu hawana imani, bali hawataki kusikia
kabisa habari za Mungu na habari njema.
Ni wazi kabisa kwa hali hii yeyote yule atakaye ishi ufalme wa Kristo,
katika maana ya maisha ya utauwa, awe tayari kuudhiwa. Ni vita kati ya mwanga
na giza. Ni katika mazingira haya Mtume Paulo anasema, “wote
wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa,” 2Tim 3:12. Leo
kuwa Mkristo kweli kweli, yakupasa kujipambanua vizuri. Jamii yetu ya leo kila
kona wafikiri na kuishi kwa ‘dilidili.’ Ni maisha ya ujanjaujanja yasiyo na
kweli ndani yake. Huu ni uthibitisho pia wa kufa ganzi kwa miimili ya dola.
Hali ya ‘udiliudili na ujanjaujanja’ inapoikumba miimili ya dola, sumu ile
ushuka hadi mtu wa chini kabisa, yaani akina siye ‘maisha heri ya jana,’ akina kabwela na kapuku. Je, tukubaliane na
hali hiyo na kuutupilia mbali ufalme wa Kristo, yaani, kuishi maisha ya utauwa?
La hasha!
Ndugu yangu unayesafiri nami katika
tafakari hii, elewa kwamba, kwenye dhiki nyingi, sintofahamu nyingi, na
miingiliano isiyo na utarajibu katika masiha, ndiyo mwisho na mwanzo wa tumaini
jipya na lenye heri. Kinachotakiwa ni kusimama katika kweli, haki, mapendo, na
amani bila kupoteza tumaini ile lililo mbele. Katika ukweli huu Mtume Paulo
anatushuhudia kwamba, “kila namna ya adha
niliyoistahimili, naye Bwana aliniokoa katika hayo yote,” 2Tim 3:11b. Mtume
Paulo anamtaka Timotheo na sisi leo kutokupoteza tumaini juu ya Yesu Kristo.
Yesu naye anatuambia, “Nanyi mtakuwa
mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kusaburi hata
mwisho, ndiye atakayeokoka,” Mk 13:13. Kuishi maisha ya utauwa ni kuliishi jina
la Yesu, ambalo kwalo ulimwengu utatuchukia ila tumaini halitaondolewa kwetu.
Ndugu yangu, “watu wabaya na wadanganyaji wataendelea, na
kuzidi kuwa waovu, wakidanganya na kudanganyika,” 2Tim 3:13. Kuendelea kwao sio
kwamba Mungu hana nguvu tena, Zab 77:7-9, bali tukumbuke kuwa Mungu ni Upendo,
Subira, Huruma, na Msamaha. Yupo tayari kuanza upya na yeyote yule ilimradi tu
aiache njia yake ovu, Isa 55:7. Je,
tabia hii ya Mungu inakukwaza? La hasha! Yanibidi kufanya iliyo sehemu yangu
kwa nguvu na ukamilifu wote. Katika hali hii, Mtume Paulo anamuasa Timotheo, na
sisi pia kwamba, “ukae katika mambo
yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao
ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu
utoto umeyajua Maandiko Matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate
wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu,” 2Tim 3:14-15. Na kama huyafahamu
Maandiko Matakatifu, huu ni wakati wa kuyatafakari.
Neno la Mungu ni uzima wetu. Ni kwa namna
hiyo, “Kila
andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa
yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili,
amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema,” 2Tim 3:16-17. Kristo hukaa ndani
yetu nasi ndani yake tulishikapo neno lake, Lk 11:28. Na hakuna mauti
tulishikapo neno la Bwana. “Amin, amin, nawaambia, Mtu akilishika neno langu,
hataona mauti milele,” Yoh 8:51. Je, waamini hilo?
Ni vyema mtu ajue vizuri kile akiaminicho, na siyo kukimeza tu bila
kukicheua. Usipo kijua vizuri kile ukiaminicho ni vigumu pia kukitetea au kuwa
sehemu ya maisha yako. Mtume Paulo anampa angalizo Timotheo, ambalo leo
tungelihusiha na utoaji wa Katekesi ya kina. Naye anasema, “lihubiri neno, uwe
tayari, wakati ukufaao na wakati usiokufaa, karipia, kemea, na kuonya kwa
uvumilivu wote na mafundisho,” 2Tim 4:2. Tusipo jali leo kuwapa waamini
katekesi ya kina juu ya imani ya kweli, muda si mrefu nasi tutakumbana na hiki
kinachoendelea katika Kanisa la Magharibi-kutokuamini uwepo wa Mungu. “Maana
utakuja wakati watakapoyakataa mafundisho yenye uzima; ila kwa kuzifuata nia
zao wenyewe watajipatia waalimu makundi makundi, kwa kuwa wana masikio ya
utafiti; nao watajiepusha
wasisikie yaliyo kweli, na kuzigeukia hadithi za uongo,” 2Tim 4:3-4. Sambamba
na kutoa katekesi ya kina, tuliopewa dhamana hiyo na Kanisa yatupasa kujifunza
kwa kina juu ya ‘teolojía ya mawasiliano.’ Pasipo mawasiliano katika
uinjilishaji vyote uvurugika. Ni sawa na kuujenga mnara wa babeli.
Waamini wanapaswa
kushirikishwa vizuri maswala ya uinjilishaji kadiri ya nafasi zao. Makleri
hawawezi kufanya mambo yote. Tujifunze historia ya Kanisa la mwanzo na
changamoto zake. “Wale Thenashara wakawaita jamii ya wanafunzi, wakasema,
Haipendezi sisi kuliacha neno la Mungu na kuhudumu mezani,” Mdo 6:2. Hii ni
faida ya kujifunza Teolojía ya mawasiliano. Kielelezo cha Teolojía hii ni uwepo
wa Utatu Mtakatifu, Mungu mmoja nafasi tatu. Na kweli hii ya mawasiliano
inajidhihirisha katika uumbaji wa mwanadamu. “Mungu akasema, Na tumfanye mtu
kwa mfano wetu, kwa sura yetu, wakatawale samaki wa baharini, na ndege wa
angani, na wanyama, na nchi yote pia, na kila chenye kutambaa kitambaacho juu
ya nchi,” Mwa 1:26. Mungu anayafanya haya na kuyatoa hayo yote kwa mwanadamu
kwa sababu anatupenda.
Paulo Serereka mwenye
ulemavu wa miguu ni mwana Parokia ya Huruma ya Mungu. Kila siku mapema asubuhi
huwahi Parokiani na ushinda hapo hadi jioni. Lengo na madhumuni yake kuwepo
hapo parokia ni kupata msaada kwa watu wanaofika hapo parokiani kwa sababu
mbalimbali.
Omba omba yake kwa watu
ilikuwa kero kwa uongozi wa parokia, na hata kwa Baba Paroko. “Kila mara upo
hapa tangu asubuhi hadi jioni na hakuna unachoweza kufanya hapa zaidi ya
kuomba,” Mhasibu wa Parokia alimkaripia Paulo Serereka. Kwa maneno hayo Paulo
alijikokota na gongo lake kuelekea geti kuu la Parokia.
Baada ya muda wa nusu
saa hivi, zilisikia sauti mwizi, mwizi, mwizi…, kutoka ofisi za Parokia na mtu
mmoja akiwa na mfuko fulani huku akikimbia kuelekea getini. Paulo Serereka
aliyekuwa getini alilitega gongo lake na mtu yule alidondoka. Ndipo wahudumu
wote wa parokia walikusanyika pale na kuanza kumpa kipigo mwizi yule. Mfuko ule
mdogo wa kaki ulikuwa na fedha. “Angalau leo nami mtaninenea lililo zuri
midomoni mwenu,” Paulo Serereka aliwaambia wale wahudumu wa Parokia.
Ndugu yangu, naye Paulo
Serereka ‘alitoa’ mchango wake kadiri ya hali na uwezo wake kwa sababu
‘aliipenda’ Parokia yake.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Walakini, atakapokuja Mwana wa
Adamu, je! Ataiona imani duniani?” Lk 18:8b
Tusali:-Ee
Yesu Mwema, tujalie nguvu ndani yetu ili tudumu katika imani thabiti
No hay comentarios:
Publicar un comentario