JUMATANO WIKI YA 27 YA MWAKA-C
Somo:
Gal 2:1-2, 7-14
Zab/Kit: 117:1, 2
Injili: Lk 11:1-4
Nukuu:
“Kisha, baada ya miaka
kumi na minne, nalipanda tena kwenda Yerusalemu pamoja na Barnaba, nikamchukua
na Tito pamoja name,” Gal 2:1
“Nami nalikwenda kwa
kuwa nalifunuliwa, nikawaeleza injili ile niihubiriyo katika Mataifa, lakini
kwa faragha kwa hao walio wenye sifa, isiwe labda napiga mbio bure, au nalipiga
mbio bure,” Gal 2:2
“Bwana, tufundishe sisi kusali, kama vile
Yohana alivyowafundisha wanafunzi wake,” Lk 11:1b
“Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi
tunamsamehe kila tumwiaye. Na usitutie majaribuni [lakini tuokoe na yule
mwovu]” Lk 11:4
TAFAKARI:
“Kuishi na kusimama katika kweli na haki. Michanganyo Bwana Yesu amekataa.”
Wapendwa wana wa Mungu,
kuongoka kwa Mtume Paulo kulimaanisha mwisho wa maisha yake ya zamani, na
kuzaliwa upya ndani na katika Kristo Yesu. Kuongaka huku kuliko maanisha
kuzaliwa upya ndani na katika Kristo Yesu, kunampa wajibu mpya Paulo mbele ya
Kristo Yesu, yaani, kuihubiri Habari Njema ya Wokovu. Mtume Paulo anaanza
mwelekeo mpya wa maisha yake ya kiimani ndani na katika Kristo Yesu.
Jukumu hili zito
hakulifanya mwenyewe, bali kwa kushirikiana na jumuiya ile ya kwanza ya
Kikristo, na chini ya mamlaka iliyokuwepo- Petro aliyejulikana kama Kefa. Naye
Paulo anasema, “Kisha, baada ya miaka kumi na minne, nalipanda tena kwenda
Yerusalemu pamoja na Barnaba, nikamchukua na Tito pamoja name,” Gal 2:1. Umoja
huu katika uinjilishaji, yaani, Paulo, Barnaba na Tito unatoka nje ya mipaka
ile ya Yerusalemu na kwenda kwa watu wa Mataifa, yaani, wale wasiokuwa
Wayahudi.
Tendo hili la kipekee
si tokeo la kukurupuka, bali limefunuliwa kwake Paulo kama asemavyo kwamba,
“Nami nalikwenda kwa kuwa nalifunuliwa, nikawaeleza injili ile niihubiriyo
katika Mataifa, lakini kwa faragha kwa hao walio wenye sifa, isiwe labda napiga
mbio bure, au nalipiga mbio bure,” Gal 2:2. Hali na mazingira ya nyakati zile
hayakuwa rafiki sana kwa kazi hii ya uinjilishaji. Licha ya miundo mbinu kuwa
mibovu, Paulo alipata upinzani mkubwa sana kutoka kwa Wayahudi wenzake.
Hata pamoja na upinzani
huo mkubwa, Paulo alisimama imara katika imani, kweli na haki na wala
hakuyumbishwa kwa kile alichokiamini. Hii yote ni neema ile ya Mungu iliyokuwa
ikifanya kazi ndani yake kama asemavyo, “kwa ajili ya kitu hicho nalimsihi Bwana mara tatu kwamba kinitoke. Naye
akaniambia, Neema yangu yakutosha; maana uweza wangu hutimilika katika udhaifu.
Basi nitajisifia udhaifu wangu kwa furaha nyingi, ili uweza wa Kristo ukae juu
yangu,” 2Kor 12:8-9. Kwa neema hii ndani yake, Paulo hakuwa na shaka lolote kwa
kile alichokuwa anaishi na kukihubiri.
Kwa msisitizo Paulo
anasema, na “tena walipokwisha kuijua ile neema niliyopewa; Yakobo, na Kefa, na
Yohana, wenye sifa kuwa ni nguzo, walinipa mimi na Barnaba mkono wa kuume wa
shirika; ili sisi tuende kwa Mataifa, na wao waende kwa watu wa tohara,” Gal
2:9. Watu wa tohara hapa ilimaanisha wale wafuatao mila na desturi za kiyahudi
na hasa swala zima la kutahiriwa. Na kwa kiasi kikubwa swala hili la kutahiriwa
lilitumika kama kigezo cha kuwa Mkristo. Mtaguso wa Yerusalema, Mdo 15,
ulizungumzima jambo hili pamoja na mambo mengine yaliyohusu kuhubiri Habari
Njema ya Wokovu.
Hivyo jukumu analopewa
Mtume Paulo kama lilivyo funuliwa kwake, na
kadiri ya jumuiya ile ya Wakristo wa Yerusalime ni kuihubiri Habari
Njema kwa Mataifa. Na katika kuhubiri huko Mtume Paulo anasema, “neno moja tu
walitutakia, tuwakumbuke maskini; nami neno lilo hilo nalikuwa na bidii
kulifanya,” Gal 2:10. Maagizo haya Mtume Paulo aliyafanya kwa nguvu zake zote
na bila kupindisha kweli ile.
Kinyume chake, Petro ambaye
alijukana kama Kefa, alipofika Antiokia alikuja na mtindo wake wa ‘mchanganyo,’
ambao ulimsikitisha sana Paulo. Naye Paulo anasema, “Lakini Kefa alipokuja
Antiokia, nalishindana naye uso kwa uso, kwa sababu alistahili hukumu,” Gal
2:11. Michanganyo hii ambayo Bwana wetu Yesu Kristo haitaki iliwa hivi; “kabla
hawajaja watu kadha wa kadha waliotoka kwa Yakobo, (Kefa) alikuwa akila pamoja
na watu wa Mataifa; lakini walipokuja wao (Wayahudi), akarudi nyuma akajitenga,
huku akiwaogopa waliotahiriwa,” Gal 2:12. Huu ni unafiki mkubwa aliokuwa
akiufanya Kefa-Petro. Hii ndiyo michanganyo tunayoiona katika imani hata leo.
Hali hiyo haikuwa tu
kwa Kefa, bali hata kwa wale waliokuwa kwenye njia, yaani, Imani, ndani na
katika Kristo Yesu. Hivyo, “Na hao Wayahudi wengine wakajigeuza pamoja naye,
hata na Barnaba pia akachukuliwa na unafiki wao,” Gal 2:13. Barnaba ambaye
alikuwa kundi moja na Paulo naye anaingia katika unafiki huu. Tendo hili
linamkwaza sana Paulo. Kwa kusimama katika kweli na mafundisho ya kweli, Paulo
anasema, “Walakini, nilipoona ya kuwa njia yao haiendi sawasawa na ile kweli ya
Injili, nalimwambia Kefa mbele ya wote, Ikiwa wewe uliye Myahudi wafuata
desturi za Mataifa, wala si za Wayahudi, kwa nini unawashurutisha Mataifa
kufuata desturi za Wayahudi?” Gal 2:14. Huu ndio uliokuwa unafiki wa Kefa na
michanganyo katika imani.
Hata
hivyo, pamoja na hatia alizokuwa nazo mtu, Mungu hubaki kuwa HURUMA, MSAMAHA,
UPENDO NA AMANI yetu. Huruma hii na upendo huu wa Mungu, tunaiona katika sala
ya Baba yetu ambayo leo mmoja wa wanafunzi wa Yesu anamwomba Yesu awafundishe
namna ya kusali. Katika sala hii inatufundisha na kuweka wazi ni nani
aliyekimbilio letu la pekee, na mapaswa yetu tungali hapa duniani. “Akawaambia, Msalipo, semeni, Baba [yetu uliye mbinguni], Jina
lako litakaswe, Ufalme wako uje, [Mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama
huko mbinguni.]” Lk 11:2.
Jambo lingine la
msingi ni huruma ya Mungu kwa
msamaha wa makosa yetu inayotokana na kiwango kile kile cha sisi kuwasamehe
wale waliotukosea. “Utusamehe dhambi zetu, kwa kuwa sisi nasi tunamsamehe kila
tumwiaye. Na usitutie majaribuni [lakini tuokoe na yule mwovu],” Lk 11:4.
Wapendwa wana wa Mungu, kama kipimo cha kupenda ni kupenda bila kipimo kama
asemavyo Mt. Agustino, basi ni hivyo hivyo masharti ya kusamehe ni kusamehe
bila masharti.
Ndugu
yangu, sintofahamu kati ya Paulo na Kefa haikuwa sababu ya kukwamisha wajibu
ule wa kuihubiri Habari Njema. Mara zote tujifunze kutoka makosa yetu, na mara
tuanze upya na kwa nguvu mpya.
Tumsifu
Yesu Kristo!
“Bwana, tufundishe sisi kusali,
kama vile Yohana alivyowafundisha wanafunzi wake,” Lk 11:1b
Tusali:-Ee
Yesu Kristo, tujalie neema zako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario