martes, 25 de octubre de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 30 YA MWAKA-C


ALHAMISI WIKI YA 30 YA MWAKA-C

Somo: Efe 6:10-20

Zab/Kit: 144:1, 2, 9-10

Injili: Lk 13:31-35

Nukuu:

“Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani,” Efe 6:11

“Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho,” Efe 6:12

 “Saa ile ile Mafarisayo kadha wa kadha walimwendea, wakamwambia, Toka hapa, uende mahali pengine, kwa sababu Herode anataka kukuua,” Lk 13:31

“Akawaambia, Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika,” Lk 13:32

“Pamoja na hayo imenipasa kushika njia yangu leo na kesho na kesho kutwa; kwa kuwa haimkini nabii aangamie nje ya Yerusalemu,” Lk 13:33

TAFAKARI: Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani.”

Wapendwa wana wa Mungu, Mwana falsafa Spinoza aliwahi kusema “kifo hakiwezi kuepukika. Ni lazima tutakukufa. Kinachotusumbua ni hofu kuhusu kifo. Hivyo yatupasa kuishinda hofu. Na hivyo ni vizuri kufikiri kuhusu uhai.” Mpendwa, je wamwamini Kristo Yesu? Kama unamwamini Kristo Yesu hakuna sababu ya kuwa na hofu kuhusu kifo. Kristo Yesu kwa maisha yake, mateso, kifo, na ufufuko wake ni jibu kuhusu aina zote za uovu na kifo. Kristo Yesu ndiye kielelezo chetu kama wafuasi wake. Kristo Yesu ametupatia mfano na jibu kwamba hakuna uovu wowote unaoweza kudumu katika umilele wake. Yesu haogopi vitisho wala kifo.

Yesu anapoambiwa aondoke kwa kuwa Herode anataka kumuua aliwajibu, “Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika,” Lk 13:32. Mnyama huyu Mbweha alitafsiriwa kama mtu asiye na msimamo, kigeugeu na mwongo. Kristo hawezi kutishiwa na mtu wa hali hii na kuacha kutoa huduma kwa watu ikiwa ndiyo sababu na mpango kazi wake kwa watu wote. Ni kwa kupitia Kristo vipofu wanapata kuona, viwete wanakwenda, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema,” Mt 11:5. Kristo pia anaufunua Utukufu wake mara baada ya kuushinda uovu anaposema, ‘siku ya tatu nakamilika.’

Mateso tunayoyapata leo au tuliyokwisha yapata kupia wazazi wetu, siyo kwamba historia hiyo ya uovu Mungu haioni. Wakati utimiapo vyote vitafanywa upya. Yesu anapoutazama mji wa Yerusalemu anayakumbuka na kuyaona mateso na uovu wa manabii wake waliyofanyiwa na kusema, Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii na kuwapiga kwa mawe waliotumwa kwako, mara ngapi nimetaka kuwakusanya watoto wako kama vile kuku avikusanyavyo vifaranga vyake chini ya mbawa zake, wala hamkutaka,” Lk 13:34. Huu kwetu ni wito wa kuongoka na kuacha njia zetu mbaya na kujisalimisha kwa Kristo. Tusisubiri hadi siku ya Mwisho kwani hatutakuwa na muda tena wa kujisalimisha kwake. Utakuwa muda wa kupokea ukumu yetu kila mmoja kadiri ya matendo yake na livyotenda. Yesu anasema, Angalieni, mmeachiwa nyumba yenu! Nami nawaambia, Hamtaniona tena kamwe, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana,” Lk 13:35. Je, kuna sababu ya kusubiri hadi siku ya mwisho? Ndugu yangu natuanze kuishi maisha ya ufufuko kabla ya kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.

Maisha baada ya ufufuko ni maisha yaliyokamili. Tunayaishi maisha haya ya ufufuko kwa kuhesabiwa haki na kwa kuzaliwa mara ya pili kwa Roho Mtakatifu. Hivyo si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu; ambaye alitumwagia kwa wingi, kwa njia ya Yesu Kristo Mwokozi wetu; ili tukihesabiwa haki kwa neema yake, tupate kufanywa warithi wa uzima wa milele, kama lilivyo tumaini letu,” Tit 3:5-7. Je, una sababu yoyote ya kuwa na hofu juu ya maisha yako ukiwa na Kristo?

Ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, ni vyema ukafahamu kweli hii kwamba kwa wewe kuwa mfuasi wa Kristo ni uchaguzi uliyofanya dhidi ya giza, yaani, vita dhidi ya uovu. Ushuhuda ya maisha ya imani yako leo na sasa na hadi siku yako ya mwisho hapa duniani ni kuifia kweli na haki dhidi ya uovu na dhuluma. Hivyo katika vita hii mimi na wewe tulio Wakristo hai kwa kuishi kwa uaminifu ahadi zetu za ubatizo, yatupasa kuvaa “silaha zote za Mungu, tupate kuweza kuzipinga hila za Shetani,” Efe 6:11. Vita hii si lelemama. Yatupasa kusimama imara daima. Na tushindapo vita hii siyo kwamba shetani kaghairi, bali utuacha kwa muda tu, Lk 4:13

Ukweli ni kwamba, vita hii  “si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho,” Efe 6:12. Ni vita ya kiroho, nayo yatupasa kujiandaa kupambana kiroho. Kuishinda vita hii yakupasa kuwa na haya yafuatayo; Amani ya ndani na yenye kuneemeshwa na Injili, Imani thabiti, na Nguvu ya Roho Mtakatifu. “Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani; zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu,” Efe 6:14-16.

Vita hii inahitaji ujari, tena wa kujitoa bila kujibakiza. Na wokovu ikiwa ndiyo kushinda kwake ni kuvumilia hadi mwisho. Yawezekana twapambana kila siku na kwa bidii zote lakini matokeo yake ni kwamba afadhali ya jana kuliko leo na huko tuendapo. Katika hali na mazingira haya Yesu anatuambia hivi;  “Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka,” Mt 10:22. Ndugu yangu, penye mateso makali ndipo penye ukaribu wa furaha ile tuitumainiyo, yaani, utukufu.

Nguvu na faraja yetu na Roho yule wa Bwana, yaani, Roho Mtakatifu. Huyu ndiye atutiaye nguvu na kutufariji hasa pale tunapokumbana na sintofahamu zilizozidi ufahamu wetu. Naye Yesu katika hali na mazingira haya ya sintofahamu zilizozidi ufahamu wetu anatukumusha jambo hili la msingi juu ya Roho Mtakatifu kwamba, “Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema,” Mt 10:19. Tusipoteze muda mwingi kujitetea kwa yale yasiyo na kweli ndani yake na kuacha kusimama katika kweli na haki.

Kama jumuiya ya wenye hofu ya Mungu, yaani, familia, jumuiya ndogo ndogo ya Kikristo, au Kanisa mahalia, Mtume Paulo anatuambia, tupokee “chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu; kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote,” Efe 6:17-18. Kudumu katika sala ndiko tuchotapo nguvu ya kupambamba na vita hivi vya kiroho, yaani, aina zote za uovu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika,” Lk 13:32

Tusali:-Ee Yesu, uliyeshinda vita dhidi ya uovu, tujali nguvu na imani thabiti kupigana bila kuchoka dhidi ya uovu katika jamii yetu. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario