jueves, 13 de octubre de 2016

TAFAKARI: IJUMAA WIKI YA 28 YA MWAKA-C


IJUMAA WIKI YA 28 YA MWAKA-C

Somo: Efe 1:11-14

Zab/Kit: 33:1-2, 4-5, 12, 13

Injili: Lk 12:1-7

Nukuu:

“na ndani yake sisi nasi tulifanywa urithi, huku tukichaguliwa tangu awali sawasawa na kusudi lake yeye, ambaye hufanya mambo yote kwa shauri la mapenzi yake,” Efe 1:11

 “Ndiye aliye arabuni ya urithi wetu, ili kuleta ukombozi wa milki yake, kuwa sifa ya utukufu wake,” Efe 1:14

“Wakati huo, makutano walipokutanika elfu elfu, hata wakakanyagana, alianza kuwaambia wanafunzi wake kwanza, Jilindeni na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki,” Lk 12:1

 “Lakini nitawaonya mtakayemwogopa; mwogopeni yule ambaye akiisha kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni huyo,” Lk 12:5

TAFAKARI: “Jilindeni na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki.”

Wapendwa wana wa Mungu, hatuwezi kujihesabia haki kwa matendo yetu wenyewe na kujiinua pasipo kweli na haki. Hii ndiyo tahadhari anayotuambia Yesu katika Injili ya leo. Kujiinua kwa ubinafsi wako kwa lengo la  kupata mastahili mbele za watu na Mungu ni chachu mbaya sana. Yesu anakuambia wewe na  mimi kwamba, “jilindeni na chachu ya Mafarisayo, ambayo ni unafiki,” Lk 12:1b. Unafiki ni kuishi kwa uhakika kile ambacho sicho ulicho. Ni kuishi kwa kuwapendezesha watu kuwa wewe ni kitu fulani ilhali sivyo ndivyo.

Ndugu yangu tunayesafiri sote pamoja katika tafakari hii, ni ushauri wangu kwako hata kama hauna maana kwako ni kwamba, ‘ishi kile ulicho katika kweli na haki yake.’ Ni katika kweli hiyo na haki Mungu utunyanyua na kutupeleka pale alipo. Huku ndiko kuhesabiwa haki na  Mungu. Na kuishi katika kweli na haki ni kutambua kwanza kabisa mimi ni mwanadamu niliyeumbwa kwa sura na mfano wake Mungu, na amependa niwe kama nilivyo na kuishi katika kweli hii.

Hakuna haja ya kuogopa kuishi ukweli huu hata ikibidi kufa kwa ajili ya ukweli huu. Yesu ananiambia mimi na wewe kwamba, nami nawaambia ninyi rafiki zangu, msiwaogope hao wauuao mwili, kisha baada ya hayo hawana wawezalo kutenda zaidi,” Lk 12:4. Ndugu yangu, kuuishi ubinadamu wako kwa mapaswa ya Mungu aliyetuumba si kazi rahisi. Wengi wetu hatupendi kujipokea kama tulivyo ikiwa ndiyo sharti la kwanza kuuishi ubinadamu wako. Je, nina hoja nzito na ya kweli ya kutokujipokea? Ni nani basi ninayemwogopa? Je, ni nani yanipasa kumwagopa katika ubinadamu wangu na ulimwengu huu?

Wapendwa wana wa Mungu, leo Yesu ananipatia jibu mimi na wewe ni nani tupasaye kumwogopa. Naye anasema, mwogopeni yule ambaye akiisha kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni huyo,” Lk 12:5b. Ni Mungu mwenye uwezo wa kuua na kumtupa mtu Jehanum. “Bwana huua, naye hufanya kuwa hai; Hushusha hata kuzimu, tena huleta juu. Bwana hufukarisha mtu, naye hutajirisha; Hushusha chini, tena huinua juu,” 1Sam 2:6-7. Hivyo wa kumwogopa ni MUNGU peke yake. Huyu ndiye tunayepaswa kuwa na hofu naye na si vinginevyo. Huyu ndiye anayejua kwenda na kutoka kwetu. 

Wapendwa, ni Mungu wetu huyu kwamba “hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi,” Lk 12:7. Mungu wetu ndiye yote katika yote. Saratani mbaya na inayolimaliza Taifa letu leo ni unafiki. Na unafiki huo upo hapa; ‘hatupendi kuona uhalisia wa kitu kama ulivyo, na badala yake tunaona uhalisia wa kitu kama tulivyo.’ Ndiyo maana siyo jambo la kushangaza leo kusikia mipishano ya taarifa kwa kitu kile kile.

Hii ni ishara ya anguko, tena kubwa sana. Katika kweli hii Yesu anasema, “kila ufalme uliofitinika wenyewe kwa wenyewe hufanyika ukiwa; na nyumba juu ya nyumba huanguka,” Lk 11:17. Mipishano ya kauli kama tokeo la unafiki, ni ashirio kubwa la anguko! Je salama yetu ipo wapi?

Salama yetu kama familia na Taifa ipo katika kweli. Ni katika kweli tunawekwa huru, Yoh 8:32. Jamii yetu leo na hasa kwa maswala ya umma, ipo tayari kutumia gharama na nguvu kubwa sana kuubatiza uongo kuwa ukweli, kuliko kukiri kweli. Udhaifu wa mtu au taasisi inayoongozwa na watu, ni uthibitisho wa ubinadamu wa watu ambao kwayo kama wanadamu siyo wakamilifu. Jambo la kufanya katika ubinadamu wako ni kulenga mara zote katika ukamilifu hata kama udhaifu upo. Unapokiri udhaifu katika kweli na haki, tendo hilo ukupa nguvu, na mwanzo mpya wa tumaini jipya.

Ni katika udhaifu tunakuwa na nguvu kama asemavyo Mtume Paulo, kwamba, “napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo. Maana niwapo dhaifu ndipo nilipo na nguvu,” 2Kor 12:10. Ni kweli pasipo shaka kwamba, mwalimu mzuri ni ‘mang’amuzi yale tuliyoyapata na tuyapatayo katika mapito ya maisha katika kweli na haki, na zaidi pale tunaposhikamana na Kristo Yesu.’

Na ndani yake (Kristo Yesu) “sisi nasi tulifanywa urithi, huku tukichaguliwa tangu awali sawasawa na kusudi lake yeye, ambaye hufanya mambo yote kwa shauri la mapenzi yake,” Efe 1:11. Tupo katika ulimwengu huu kama warithi na wana wa Mungu kuyafanya mapenzi yake Mungu na siyo ya kwetu hata kama hali na mazingira  tuliyo nayo yanaruhusu.

Hivyo kufikiri kwangu, kuamua kwangu, na kutenda kwangu kusukumwe mara zote na hofu ya Mungu ndani yangu. Kristo Yesu awe kielelezo cha kila kitu katika maisha yangu. Huyu “ndiye aliye arabuni ya urithi wetu, ili kuleta ukombozi wa milki yake, kuwa sifa ya utukufu wake,” Efe 1:14. Maisha bila Kristo Yesu msingi  wake ni dhaifu sana!

Tumsifu Yesu Kristo!

“Mwogopeni yule ambaye akiisha kumwua mtu ana uweza wa kumtupa katika Jehanum; naam, nawaambia, Mwogopeni huyo,” Lk 12:5b

Tusali:-Ee Yesu na Mwokozi wangu, niweke huru katika kweli na haki yako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario