JUMATATU WIKI YA 30 YA MWAKA-C
Somo:
Efe 4:32-5:8
Zab/Kit: 2:1-2, 3, 4, 6
Injili: Lk 13:10-17
Nukuu:
“tena iweni wafadhili ninyi
kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika Kristo
alivyowasamehe ninyi,” Efe 4:32
“Hivyo mfuateni Mungu,
kama watoto wanaopendwa; mkaenende katika upendo, kama Kristo naye
alivyowapenda ninyi tena akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu,
kuwa harufu ya manukato,” Efe 5:1-2
“Lakini uasherati
usitajwe kwenu kamwe, wala uchafu wo wote wa kutamani, kama iwastahilivyo
watakatifu; wala aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali
afadhali kushukuru,” Efe 5:3-4
“Yesu alipomwona
alimwita, akamwambia, Mama, umefunguliwa katika udhaifu wako,” Lk 13:12.
TAFAKARI:
“Sasa mmekuwa nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru.”
Wapendwa wana wa Mungu,
Injili ya leo inatupa maisha mapya ndani ya Kristo pale tunapomwamini. Maisha
ni mali na zawadi ya Mungu kwetu, kwani mbingu na vyote ni mali yake Mungu, Zab
24:1. Hakuna mbadala kuhusu uhai wa mtu. Yesu analithibitisha hili kwa kuvunja
taratibu za kisinagogi na kisabato kwa kumponya mwanamke aliyekuwa na pepo wa udhaifu muda
wa miaka kumi na minane, naye amepindana, hawezi kujinyosha kabisa.
Mateso na mahangaiko
yetu ufikia kikomo chake tukiwa na imani pasipo shaka juu ya Mwana wa Mungu.
Yesu hakuweza kukaa kimya anapoona udhaifu wa mama yule licha ya kwamba
taratibu za kisinagogi na kisabato hazikumruhusu kufanya aliyoyafanya. “Yesu alipomwona alimwita, akamwambia, Mama,
umefunguliwa katika udhaifu wako,” Lk 13:12. Tendo hili linaibua mjadala mkubwa
kuhusu uhalali wa Yesu kutoa huduma ile.
Jambo la ajabu Wayahudi
waliheshimu taratibu zao hizo, bila kuona upendo na huruma ya Mungu kwao na
watu wengine. Je, kwa nini basi mimi na wewe tunajisikia vibaya mmoja wetu
atendapo jambo jema na lenye kumpendeza Mungu? Ndugu uliyesafiri nami katika
tafakari hii kama unataka kuishi ndani na katika Kristo fuata lililo jema na
tenda mema siku zote.
Ikiwa kwa upendo na
furaha yake Mungu ilimpendeza kutuumba kwa sura na mfano wake, ni jukumu la
kila mmoja wetu kuona fahari hiyo ndani yake na kwa wale wote wanaomzunguka.
Tunadumu katika kweli hiyo ya kufanana naye Mungu pale tunapoendeleza upendo na
furaha hiyo kwa wengine. Naye Mtume Paulo katika kweli hii anatuwasa kwamba, “iweni
wafadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma, mkasameheane kama na Mungu katika
Kristo alivyowasamehe ninyi,” Efe 4:32. Kumbe yanipasa kuumia ndani yangu
naposhindwa kuona shida na mahangaiko ya jirani yangu, ambao ni wale wote wenye
uhitaji.
Ukristo wetu wapaswa
mara zote kufanana na tabia ya Yesu Kristo. Pamoja na mambo mengi aliyoyafanya
Mkombozi wetu Yesu Kristo, Kristo Yesu alikuwa karibu na rafiki ya wadhambi,
waliotengwa, wezi, wazinzi, wanawake na watoto. Aliyafanya haya siyo kuwafariji
na kuwapa moyo ili waendelee katika matendo yao ya giza au hali zao za kutokuwa
na matumaini, bali aliyafanya haya ili wamjeukie Mungu na wauone uso wa wake wa
upendo na huruma. Hivyo nasi kama wafuasi wake Kristo na ‘kama watoto
wanaopendwa; tuenende katika upendo, kama Kristo naye alivyotupenda sisi tena
akajitoa kwa ajili yetu, sadaka na dhabihu kwa Mungu, kuwa harufu ya manukato,’
Efe 5:1-2. Upendo ndiyo kila kitu ndani na katika Kristo Yesu.
Hata hivyo, kama wana
wa Mungu yatupasa kuishi katika matendo ya mwanga kila wakati. Hivyo tuyapige
vita matendo ya giza kama asemavyo Mtume Paulo; “uasherati usitajwe kwenu
kamwe, wala uchafu wo wote wa kutamani, kama iwastahilivyo watakatifu; wala
aibu wala maneno ya upuzi wala ubishi; hayo hayapendezi; bali afadhali
kushukuru,” Efe 5:3-4. Matendo haya ya giza hayana uzima ndani yake zaidi ya
kifo na kutokuuridhi ufalme wa Mungu, Gal 5:19-21. “Maana neno hili mnalijua
hakika, ya kwamba hakuna mwasherati wala mchafu wala mwenye tamaa, ndiye
mwabudu sanamu, aliye na urithi katika ufalme wa Kristo na Mungu,” Efe 5:5.
Kuepukana na kadhia hii ni kufuata alilotufundisha Kristo Yesu kwamba, ‘yatupasa
kuwa wakamilifu kama Baba yetu wa mbinguni alivyo mkamilifu,’ Mt 5:48. Ni hatua
muhimu sana ya kukua kiroho kila siku.
Leo katika mazingira
haya ya utandawazi, ipo mifumo mingi sana ya maisha yenye kubeba unafuu na uboreshaji.
Ila unapozama ndani zaidi ya hayo yabebayo mifumo hiyo utagundua kwa kiasi
kikubwa ni udanganyifu mtupu. Wito kwako na kwangu ni kwamba, “Mtu
asiwadanganye kwa maneno yasiyo na maana; kwa kuwa kwa sababu ya hayo hasira ya
Mungu huwajia wana wa uasi. Basi msishirikiane nao,” Efe 5:6-7. Ni vyema
tukajikatalia yale yote yasiyotupeleka katika uzima wa milele.
Ni wito kama
Kanisa-wabatizwa wote, kuisha maisha ya ufufuko pamoja na Kristo, yaani,
“tuyatafute yaliyo juu Kristo aliko, ameketi mkono wa kuume wa Mungu.
Yafikirini yaliyo juu, siyo yaliyo katika nchi,” Col 3:1-2. Tu ngali bado
katika giza kama hatuishi maisha ya ufufuko na pamoja na Kristo, na mwisho wa
siku ukombozi wetu ni bure. “Kwa maana zamani ninyi mlikuwa giza, bali sasa
mmekuwa nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru,” Efe 5:8. Ndugu yangu,
zama ndani ya wito wako na jikatalie yote yale ya giza.
Tumsifu Yesu Kristo!
"Zamani ninyi mlikuwa giza, bali
sasa mmekuwa nuru katika Bwana; enendeni kama watoto wa nuru," Efe 5:8
Tusali:-Ee
Yesu, tufanye vyombo vya upendo na huruma yako. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario