JUMATANO WIKI YA 30 YA MWAKA-C
Somo:
Efe 6:1-6
Zab/Kit:
145:10-11, 12-13ab, 13cd-14
Injili: Lk 13:22-30
Nukuu:
“Enyi watoto, watiini
wazazi wenu katika Bwana, maana hii ndiyo haki,” Efe 6:1
“Waheshimu baba yako na
mama yako; amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, Upate heri, ukae siku
nyingi katika dunia,” Efe 6:2-3
“Mtu mmoja
akamwuliza, Je! Bwana, watu wanaookolewa ni wachache? Akawaambia,” Lk 13:23
“Jitahidini
kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi
watataka kuingia, wasiweze,” Lk 13:24
“Naye
atasema, Nawaambia, Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji
wa udhalimu,” Lk 13:27
“Na
tazama, wako walio wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na wa kwanza watakaokuwa wa
mwisho,” Lk 13:30
TAFAKARI: “Jitahidini
kuingia katika mlango ulio mwembamba.”
Wapendwa
wana wa Taifa la Mungu, masomo ya leo yanatualika tutafakari kwa kina mwenendo
wa maisha yetu na wito wa kujitahidi kila mara kuingia katika mlango ulio
mwembamba. Bila shaka wembamba wa mlango huu ni mwaliko wa kuishi kadiri ya
yale yanayompendeza Mungu kila mmoja kadiri ya wito wake. Ni kuishi upendo wa
Mungu Baba kweli na kuwa na hofu ya Mungu kwa kushika na kuziishi vyema amri za
Mungu na Kanisa lake kama familia yake.
Utii
katika amri za Mungu ni kumpenda Mungu pasipo shaka. “Mkinipenda,
mtazishika amri zangu,” Yoh 14:15. Kuzishika na kuishi katika amri zake ni
pamoja na kutambua ukweli huu kwamba kwa kupitia Mwanaye Mpendwa Yesu Kristo
tutaiona njia ya kuelekea kwake, tunapata uzima wa kweli, na ndani na katika
Kristo mwanaye ndipo penye ukweli wa Mungu Baba na maisha ya umilele. Yesu
anathibitisha ukweli huu kwa kusema, “Mimi
ndimi njia, na kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh
14:6.
Upendo
wa Yesu, ikiwa ni pamoja na mahusiano yake na Mungu Baba, na Roho Mtakatifu
(Famili ya Utatu Mtakatifu, na Umoja usiogawanyika), kwa kiasi fulani katika
mawasiliano yake, unafanana na umoja na mawasiliano katika familia. Famili
katika ukamilifu wake ujidhihirisha na uwepo wa Baba, Mama, na Watoto, ingawa
katika ndoa watoto ni tunda la ndoa, na bila watoto ndoa ubaki kuwa ndoa katika
ukamilifu wake. Ili kufikia hazma yake, yaani, ule utakatifu katika familia,
kila mmoja katika familia lazima atimize wajibu wake. Na moja ya nyajibu hizo
ni heshima katika familia (KUHESHIMIANA)
Familia
isiyo na utaratibu, ikiwa ni pamoja na kutokuheshimiana, upoteza; tunu, lengo,
na utakatifu ule iliyoitiwa. Hivyo ni wajibu wa watoto kuwatii wazazi wao kama
Mtume Paulo anavyotufundisha, “Enyi watoto, watiini wazazi wenu
katika Bwana, maana hii ndiyo haki,” Efe 6:1. Kuwatii wazazi wetu si jambo la
shuruti, bali ni haki yao. Wazazi wetu ni Viumbe shirikishwa vya Mungu katika
uumbaji pamoja na Mungu. Nafasi na hadhi hii yaliyopewa Wazazi wetu hata
malaika hawakupewa ingawa muda wote Malaika humzunguka Mungu wakiwa wanamwabudu
na kumsifu. Hivyo, kuwaheshima Baba na Mama yako, “amri hii ndiyo amri ya
kwanza yenye ahadi, Upate heri, ukae siku nyingi katika dunia,” Efe 6:2-3.
Furaha waipatayo wazazi wako kwa wewe kutimiza wajibu wako katika kweli na haki,
ndiyo baraka na neema kwako.
Hata hivyo, wazazi wetu
yawapaswa kutimiza wajibu wao, ikiwa ni pamoja na kuwapatia malezi mema watoto
wao na yenye kumpendeza Mungu, yaani, watoto na hata walelewa wao kuwa na hofu
ya Mungu. Hivyo, “Nanyi, akina baba, msiwachokoze watoto wenu; bali waleeni
katika adabu na maonyo ya Bwana,” Efe 6:4. Leo kuna mporomoko wa kasi ya ajabu
katika malezi na familia kwa sababu tu wazazi wa leo hawapendi kufanya na
kutimiza majukumu na nyajibu zao. Hii sayansi na hili ‘teke linalotujia kila
siku kwa kasi ya ajabu, bila kujiandaa, na bila kufahamu’ limetupumbaza, badala
ya kutufanya kuwa werevu katika majukumu yetu ya kila siku na familia kama
sababu ya jana yetu, leo yetu, na kesho yetu. Leo hakuna tena ule muda na
uwanja wa wazazi kuwafunda watoto wao kila mmoja kadiri ya jinsia yake. Simu ya
mkononi imechukua asilimia 75 ya malezi katika familia. Je, kizazi kijacho na
Kanisa kwa ujumla wake litakuaje?
Nasi sote kwa ujumla
wake, ikiwa kila mmoja na wito wake, ndani na katika wito huo yupo yule tunaye mtumikia.
Na kwa namna hii na mwono huu, sisi sote tu watumwa wa yule tunayemtumikia
katika kweli na haki. Na ujumbe ni uleule kwamba, “Enyi watumwa, watiini wao
walio bwana zenu kwa jinsi ya mwili, kwa hofu na kutetemeka, kwa unyofu wa
moyo, kana kwamba ni kumtii Kristo; wala si kwa utumwa wa macho tu kama
wajipendekazao kwa wanadamu bali kama watumwa wa Kristo, mkitenda yampendezayo
Mungu kwa moyo,” Efe 6:5-6. Na tunapotambua kweli katika utumwa huu, basi tuyafanye
hayo yote kwa hofu ya Mungu.
Ndugu
yangu tunayesafiri sote katika tafakari hii, ukweli wa Kristo na Mungu
tunaupata katika Maandiko Matakatifu, uzima wake tunaupata katika Masakramenti,
na njia ya wokovu wetu ni Utukufu tuupatao kupitia njia ile aliyoichagua Kristo Yesu, yaani, Msalaba.
Hivyo tunampenda Mungu tunapolishika vyema neno lake. Yesu
anatuambia kweli hii kwa kusema, “Mtu
asiyenipenda, yeye hayashiki maneno yangu; nalo neno mnalolisikia silo langu,
ila ni lake Baba aliyenipeleka,” Yoh 14:24.
Kuishi
upendo wa kweli, kuzitii na kuzishika amri za Mungu na Kanisa, na kuwa na hofu
ya Mungu katika yale yote tunayofikiri, tenda, na kuishi ndiko kuchaguliwa
kwetu toka asili. “Na
wale aliowachagua tangu asili, hao akawaita; na wale aliowaita, hao
akawahesabia haki; na wale aliowahesabia haki, hao akawatukuza,” Rum 8:30. Hii
ndiyo sababu ya Mungu kama ilivyo mpendeza na kuchagua kutuumba kwa sura na
mfano wake.
Mungu
anapenda tuwe wakamilifu kama Yeye alivyo Mkamilifu. “Basi
ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48.
Hii ndiyo furaha ya Mungu kwetu. Mungu hupenda kufanya kazi na wale wampendao
pasipo shaka yoyote. Mtume Paulo anathibitisha jambo hili kwa kusema, “Nasi twajua ya kuwa katika mambo yote Mungu
hufanya kazi pamoja na wale wampendao katika kuwapatia mema, yaani, wale
walioitwa kwa kusudi lake,” Rum 8:28. Kila
mwenye hofu ya Mungu ndani yake ameitwa kwa kusudi lake. Ni vyema ukaanza sasa
kuelewa ukweli huu ndani yako na kuishi kadiri Mungu apendavyo.
Katika safari hii ya
kuelekea uzima wa milele tumepewa Roho wa Mungu kutuongoza katika kweli na haki
na kutusaidia katika udhaifu wetu kama wanadamu. “Kadhalika
Roho naye hutusaidia udhaifu wetu, kwa maana hatujui kuomba jinsi itupasavyo,
lakini Roho mwenyewe hutuombea kwa kuugua kusikoweza kutamkwa,” Rum 8:26.
Hatuombi jinsi ipasavyo kwa sababu tunaomba kwa ajili ya tamaa zetu na mara
tupatapo kile tulichokiomba tunatumia vibaya.
Ombi la mtindo huu
haliwezi jibiwa kwa sababu hatumruhusu Roho atuongoze. Mtume Yakobo anatupa
sababu ya kushindwa kwetu. “Hata mwaomba,
wala hampati kwa sababu mwaomba vibaya, ili mvitumie kwa tamaa zenu,” Yak 4:3.
Mungu anatupenda kweli na hutupatia yale tuombayo kadiri ya mahitaji yetu. Hivyo hatupaswi kuwa na
mashaka mara tumwendeapo na kuomba yale tunayohitaji. Mashaka katika maishi
hututia hofu na mwisho wa siku tunatawaliwa na mambo mengi na yasiyo ya msingi
na kukosa dira ya malengo ya maisha yetu hapa duniani.
Katika Injili ya leo
tunamwona mtu mmoja mwenye mashaka anamuuliza Yesu, “Je! Bwana, watu
wanaookolewa ni wachache?” Lk 13:23. Jibu la Yesu linaturudisha kwenye msingi
na malengo ya maisha yetu hapa duniani kama nilivyokwisha elezea hapo mwanzo.
Yesu anatujibu kwa pamoja hasa sisi tulio na mashaka, “Jitahidini
kuingia katika mlango ulio mwembamba, kwa maana nawaambia ya kwamba wengi
watataka kuingia, wasiweze,” Lk 13:24. Mlango huu mwembamba unatuwajibisha
kujua lengo la maisha yetu hapa duniani, namna ya kuishi ili kufikia lengo
hilo, na ni mambo gani ya msingi yatupasa kuyapa umuhimu katika maisha.
Tusipozingatia jambo
hilo kama nilivyokwisha elezea hapa mwanza, tusishangae siku ya mwisho kuambiwa
maneno haya, “Siwajui mtokako; ondokeni kwangu ninyi nyote mlio wafanyaji wa
udhalimu,” Lk 13:27. Udhalimu wa kwanza kwa
mtu utakuwa hali ile ya kutokutumia muda wake vizuri na neema anazopatiwa bure
na Mungu kupitia Mama Kanisa.
Tutashangaa na kupigwa butwaa
tutakapoona wale waliotumia vyema muda wao na neema walizojifunua kwao
wakiingia katika maisha ya umilele. Wengi wao ni wale leo tunaowaona wamwisho
kwa kila kitu kwa sababu tu hawaendani na mambo ya ulimwengu huu na tamaa zake.
“Na
tazama, wako walio wa mwisho watakaokuwa wa kwanza, na wa kwanza watakaokuwa wa
mwisho,” Lk 13:30. Ndugu yangu tuliyesafiri pamoja katika tafakari hii, ni
wakati sasa wa kuzama ndani yako na kuhoji nafsi yako kwa hili Yesu
alilotuambia leo, “Jitahidini kuingia katika
mlango ulio mwembamba.” Je, lina
ukweli wowote juu ya maisha yako?
Tumsifu Yesu Kristo!
“Waheshimu baba yako na mama yako;
amri hii ndiyo amri ya kwanza yenye ahadi, Upate heri, ukae siku nyingi katika
dunia,” Efe 6:2-3
Tusali:-Ee
Yesu, tuimarishe kila mmoja wetu kadiri ya wito ule uliomwitia. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario