JUMAMOSI WIKI YA 28 YA MWAKA-C
Somo:
Efe 1:15-23
Zab/Kit:
8:2-3a, 4-5, 6-7
Injili:
Lk 12:8-12
Nukuu:
“Kwa sababu hiyo mimi
nami, tangu nilipopata habari za imani yenu katika Bwana Yesu, na pendo lenu
kwa watakatifu wote, siachi kutoa shukrani kwa ajili yenu; nikiwakumbuka katika
sala zangu,” Efe 1:15-16
“Mungu wa Bwana wetu
Yesu Kristo, Baba wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika
kumjua yeyé,” Efe 1:17
“Nami nawaambia, kila atakayenikiri mbele ya
watu, Mwana wa Adamu naye atamkiri yeye mbele ya malaika wa Mungu; na mwenye
kunikana mbele ya watu, huyo atakanwa mbele ya malaika wa Mungu,” Lk 12:8-9
“Na watakapowapeleka ninyi mbele ya masinagogi
na maliwali na wenye mamlaka, msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu jinsi
mtakavyojibu au kusema; kwa kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile
yawapasayo kuyasema,” Lk 12:11-12
TAFAKARI:
“Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile yawapasayo kuyasema.”
Wapendwa wana wa Mungu,
hatuna kitu chochote cha kumficha Mungu wetu. Mungu kesha tupatia namna ya
kumfikia kwa kupitia uwepo wa Mwanaye Yesu Kristo. Yesu ananiambia mimi na wewe
leo na sasa kwamba, “Mimi ndimi njia, na
kweli, na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi,” Yoh 14:6. Je, ndugu
yangu tunayesafiri pamoja katika tafakari hii wasadiki maneno hayo ya Yesu
Kristo? Kusadiki maneno haya ya Kristo
Yesu ni kukiri kwamba katika maisha ninayoishi leo na sasa Yesu Kristo yupo hai
ndani yangu, na kwa wale wote wanaonizunguka.
Nisipolifanya jambo hili nisijeshangaa siku ya mwisho napishana
na Kristo Yesu katika maana ya kutokunitambua mbele ya Baba yake wa Mbinguni. “Nami nawaambia, kila
atakayenikiri mbele ya watu, Mwana wa Adamu naye atamkiri yeye mbele ya malaika
wa Mungu,” Lk 12:8. Ukiri wangu katika maisha na ushuhuda mbele za watu, ndiyo
salama yangu mbele ya Mungu.
Kinyume chake ni
kwamba, “na mwenye kunikana mbele ya watu,
huyo atakanwa mbele ya malaika wa Mungu,” Lk 12:9. Inasikitisha kwamba wapo
miongoni mwetu ambao watakanwa milele kwa vile tu walishindwa kutambua uwepo wa
Mungu katika maisha yao na kuuishi ukweli huo kwa Imani iliyo hai. Wakati
mwingine matatizo yako yanaweza kuwa sababu ya kutokuona uwepo wa Mungu na hali
hiyo ikakufanya ukate tamaa kabisa. Je, kunasababu ya kukata tamaa tukifikiri
kuwa Mungu ametuacha?
Ukimya wa Mungu juu ya
matatizo yako siyo kwamba haoni wala hajali. Mungu anajua ni wakati gani
unaofaa kukupa kile anachoona kitakufaa katika maisha yako ya umilele. Hivyo
Mungu hawezi kukusahau kabisa kwasababu alikuumba kwa sura na mfano wake, na
anampango madhubuti na maisha yako. Yesu anatuamba, “lakini ninyi, hata nywele
za vichwa vyenu zimehesabiwa zote,”Mt 10:30. USIOGOPE hasa pale mambo
yanapoanza kwenda ndivyo sivyo. Huo nao ni mtihani wa imani yako. Mungu anajua
utashinda tu ukimtumainia.
Mungu utuwazia mema
kila wakati. “Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana,
ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za
mwisho,” Yer 29:11. Ndugu yangu huna sababu ya kukata tamaa. Kukata tamaa katika maisha ni kosa kubwa sana
kulifanya kama unaishi kwa malengo. Kosa hili au dhambi hii ni kumkufuru Roho
Mtakatifu.
Kwa
tendo hili, yaani, kukata tamaa hatuwezi kupata msamaha wake. “Na kila mtu atakayenena
neno juu ya Mwana wa Adamu atasamehewa, bali aliyemkufuru Roho Mtakatifu
hatasamehewa,” Lk 12:10. Je, ni mara ngapi nimemkufuru Roho Mtakatifu kwa
kukata tamaa? Roho Mtakatifu utuondolea
mifadhahiko yote hasa pale tunaposhindwa kujitetea kutokana na mazingira yetu,
hali zetu, na ubinadamu wetu.
Tunapokuwa
na Roho Mtakatifu, huyatakatifuza yote na kuyafanya mapya na yenye nguvu.
HivyoYesu anatuambia, “msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu
jinsi mtakavyojibu au kusema; kwa
kuwa Roho Mtakatifu atawafundisha saa ile ile yawapasayo kuyasema,” Lk
12:11b-12. Je, naitaji silaha gani zaidi ya kiroho kumshinda Roho Mtakatifu?
Kusimama imara katika
imani kunakupa furaha ya ndani ambayo hakuna mtu wa kukuondolea, Yoh 16:22.
Nasi kama wafuasi wake Kristo Yesu tunayofuraha kwa sababu Kristo ni mshindi na
ushindi huo umekwisha jidhihirisha katika tendo lile la ufufuko. Hivyo ufuasi
wetu kwake siyo wa kubabaisha au kujaribu jaribu. “Kwa sababu hiyo mimi nami,
tangu nilipopata habari za imani yenu katika Bwana Yesu, na pendo lenu kwa
watakatifu wote, siachi kutoa shukrani kwa ajili yenu; nikiwakumbuka katika
sala zangu,” Efe 1:15-16. Mtume Paulo haoni haya kuisema furaha ile iliyoko
ndani ya moyo wake ndani na katika Kristo Yesu.
Hatuna tena shaka
yoyote ile ya kumfikia Baba Yetu aliye mbinguni kwa sababu Kristo Yesu kesha
tuonyesha njia hiyo ambayo ndiyo Yeye Mwenyewe. Kesha tuonyesha kweli ikiwa
Yeye Mwenyewe ndiyo Kweli hiyo, yaani, “Hapo mwanzo kulikuwako Neno, naye Neno
alikuwako kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu,” Yoh 1:1. Naye ndiye uzima wetu
tunaposhiriki Sakramenti Takatifu katika stahili yake. Ekaristi Takatifu ndiyo
kelelezo cha uzima huo tunaposhiriki pasipo hatia. “Kwa maana mwili wangu ni
chakula cha kweli, na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na
kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Hiki ndicho
chakula kishukacho kutoka mbinguni; si kama mababa walivyokula, wakafa; bali
akilaye chakula hicho ataishi milele,” Yoh 6:55-56, 58.
Ndani na katika Kristo
Yesu tunapata roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua Mungu Baba aliyejifua
wazi kwa njia ya Neno wake kufanyika mwili na kukaa kwetu (Yoh 1:14, Ebr 11:1,
Gal 4:4-5), yaani, Yesu Kristo. Hivyo, “Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba
wa utukufu, awape ninyi roho ya hekima na ya ufunuo katika kumjua yeyé,” Efe
1:17. Na katika Kristo Yesu twatiwa nuru na tumaini la kweli. “Macho ya mioyo
yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake jinsi lilivyo; na utajiri wa
utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi ulivyo,” Efe 1:18. Kumbe ndani
ya ulinzi wa Bwana wetu Yesu Kristo hakuna tunachopoteza, zaidi ya
kuhakikishiwa uzima ule wa milele.
Kwa hiyo kama mfuasi
wake Kristo, yanipasa kuamini pasipo shaka ndani na katika Kristo Yesu. Ni kwa
maana hivyo kwamba, “ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi
ulivyo; kwa kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake,” Efe 1:19. Hivyo matendo
yangu yaakisi ukweli ule wa Yesu ndani yangu. Mateso, kifo, na ufufuko wake
Kristo ni uthibitisho dhahiri kuwa vita dhidi ya uovu haina nguvu tena.
Kwa ushindi wake
Kristo, Mungu Baba kesha “vitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe
kichwa juu ya vitu vyote kwa ajili ya Kanisa; ambalo ndilo mwili wake,
ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote,” Efe 1:22-23. Kanisa
Takatifu leo ndio chombo wazi na Sakramenti hai ya wokovu wetu.
Tumsifu Yesu Kristo!
“Na watakapowapeleka ninyi mbele ya
masinagogi na maliwali na wenye mamlaka, msifadhaike kwa kuwaza maneno yenu
jinsi mtakavyojibu au kusema,” Lk 12:12a
Tusali:-Ee
Yesu, tujalie uthabiti katika imani, na kusimama katika kweli na haki. Amina
No hay comentarios:
Publicar un comentario