jueves, 6 de octubre de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 27 YA MWAKA-C


JUMAMOSI WIKI YA 27 YA MWAKA-C

Somo: Gal 3:22-29

Zab/Kit: 105:2-3, 4-5, 6-7

Injili: Lk 11:27-28

Nukuu:

“Lakini andiko limeyafunga yote chini ya nguvu ya dhambi, makusudi hao waaminio wapewe ile ahadi kwa imani ya Yesu Kristo,” Gal 3:22

 “Lakini kabla ya kuja ile imani tulikuwa tumewekwa chini ya sheria, tumefungwa mpaka ije ile imani itakayofunuliwa,” Gal 3:23

 “Ikawa alipokuwa akisema maneno hayo, mwanamke mmoja katika mkutano alipaza sauti yake, akamwambia, Heri tumbo lililokuzaa, na matiti uliyonyonya,” Lk 11:27

“Lakini yeye alisema, Afadhali, heri walisikiao neno la Mungu na kulishika,” Lk 11:28

TAFAKARI: “Heri walisikiao neno la Mungu na kulishika.”

Wapendwa wana wa Mungu, kutokana na ishara nyingi alizokuwa anafanya Yesu mbele za watu, mama mmoja hakuweza kuizuia furaha yake. Hivyo alitamka kwa furaha na kusema, “Heri tumbo lililokuzaa, na matiti uliyonyonya,” Lk 11:27b. Nani kama Mama? Ni uthibitisho ulio wazi kwamba Yesu alipata malezi mazuri kama mwanadamu. Sifa na utukufu kwanza kwa Mungu na kwa Mama Bikira Maria.

Pamoja na furaha hii ya huyu Mama, Yesu anatutaka tuende ndani na mbali zaidi. Kila mmoja wetu yampasa kulisikia neno la Mungu na kulishika. Kulishika neno la Mungu ni kulitafakari na kulifanya sehemu ya maisha yako. Maandiko Matakatifu yanaonyesha dhana hii ya maisha ya mtu kufanywa mapya baada ya kulisikia neno la Mungu na kulishika. Mungu wetu huyu aliye na subiri kwa kila mmoja wetu, utupatia muda wa kutosha kabisa. Tatizo letu kubwa ni pale tunaposhindwa kutumia fursa hiyo.

Hii ndiyo furaha kubwa sana ya Mungu na wateule wake, yaani, Watakatifu wote huko Mbinguni. Naye Yesu alimjibu mama yule, “Afadhali, heri walisikiao neno la Mungu na kulishika,” Lk 11:28. Ndugu unaye safiri nami katika tafakari hii, neno la Mungu lina nafasi gani katika maisha yako ya kila siku? Je, ni kitu gani kinachokupa uzima wako kila siku? Na mwisho, siku yako kila siku huanza na kitu gani? Jibu maswali hayo vyema. Majibu yako ndiyo ukaribu au umbali wako na Mungu anayekupa uhai kwa hayo unayofikiri ndiyo uhai wako.

Wapendwa wana wa Mungu, imani yetu bila Kristo Yesu ni sawa na kupanga safari katika kiza kinene na kwenda tusipopajua. Kristo Yesu ambaye ndiye Neno aliyefanyika mwili na kukaa kwetu Yoh 1:14, ndiye kielelezo cha kila kitu kwetu, ikiwa ni pamoja na uzima ule wa milele tunaoutafuta kila siku. Ukweli ni kwamba, “Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria, kusudi awakomboe hao waliokuwa chini ya sheria, ili sisi tupate kupokea hali ya kuwa wana,” Gal 4:4-5. Maisha yetu kama wafusi wa Kristo bila Kristo ni sawa na samaki kuishi jangwani. Na  “andiko limeyafunga yote chini ya nguvu ya dhambi, makusudi hao waaminio wapewe ile ahadi kwa imani ya Yesu Kristo,” Gal 3:22. Je, wamwamini Yesu Kristo?

Alipo Kristo Yesu kuna Imani, na katika Imani hiyo watu upokea neema na baraka. Torati-sheria ilikuwa maandalizi ya kuipokea Imani hiyo ya kweli, yaani, Neno huyo wa Mungu aliyefanyika mwili na kukaa kwetu. Ni kwa mantiki hiyo kwamba, “kabla ya kuja ile imani tulikuwa tumewekwa chini ya sheria, tumefungwa mpaka ije ile imani itakayofunuliwa,” Gal 3:23. Kristo Yesu kwa kuja kwake kayafunua yote yamuhusuyo Mungu Baba, na hakuna ufunuo mwingine zaidi ya huu. “Hivyo torati imekuwa kiongozi kutuleta kwa Kristo, ili tuhesabiwe haki kwa imani,” Gal 3:24. Ni katika kweli hii tunajiunga na Mtume Petro na kusema, “Wewe (Kristo Yesu) unayo maneno ya uzima wa milele. Nasi tumesadiki, tena tumejua, ya kuwa wewe ndiwe Mtakatifu wa Mungu,” Yoh 6:68b-69

Ikiwa Kristo ndiye kila kitu katika maisha yetu, hatuna sababu yoyote ya kuwa na hofu. Hivyo “iwapo imani imekuja, hatupo tena chini ya kiongozi,” Gal 3:25. Kiongozi hapa imetumika kama ‘mamlaka za kibinadamu.’ Kwa maana hiyo kama tumempokea Kristo na kuwa ndiye kielelezo cha maisha yetu, hakuna binadamu yeyote kwenye mamlaka ya kupora imani hiyo ndani yetu kwa sababu kwake huyo mwanadamu hakuna uzima huo wa milele bila Kristo mwenyewe. Ni kwa sababu hiyo,  “sisi sote tumekuwa wana wa Mungu kwa njia ya imani katika Kristo Yesu,” Gal 3:26. Na tumefanywa wana na warithi wa ufalme wa Mungu kwa njia ya Sakramenti ya ubatizo.  “Maana ninyi nyote mliobatizwa katika Kristo mmemvaa Kristo,” Gal 3:27. Hivyo ni jukumu la kila mbatizwa kuishi ahadi zake za ubatizo kwa uaminifu.

Kwa Sakramenti hii ya Ubatizo ambayo kwayo tumefanywa wana na warithi wa Ufalme wa Mungu, tu sawa wote mbele za Mungu. Tofauti zetu zilizozama katika ubinadamu wetu hazina tena nafas imbele ya Mungu ndani na katika Kristo Yesu. Hivyo, “Hapana Myahudi wala Myunani. Hapana mtumwa wala huru. Hapana mtu mume wala mtu mke. Maana ninyi nyote mmekuwa mmoja katika Kristo Yesu,” Gal 3:28. Huu ni upendeleo mkubwa sana kwetu. Huu ni upendo usio na kipimo kwetu ambao Yesu kampa kila kwenye hofu naye. “Na kama ninyi ni wa Kristo, basi, mmekuwa uzao wa Ibrahimu, na warithi sawasawa na ahadi,” Gal 3:29. Na ahadi alizopewa Ibrahimu ni hizi: Ibrahimu atakuwa taifa kuu, hodari na katika  yeyé mataifa yote ya dunia watabarikiwa, Mwa 18:18.

Tumsifu Yesu Kristo!

Heri tumbo lililokuzaa, na matiti uliyonyonya,” Lk 11:27b

Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema na baraka zako sawasawa na ahadi zako. Amina

No hay comentarios:

Publicar un comentario