lunes, 31 de octubre de 2016

TAFAKARI: WAAMINI WOTE MAREHEMU


WAAMINI WOTE MAREHEMU

Somo I: Hek 3:1-9

Zab: 23:1-3a, 3b-4, 5, 6

Somo II: Rum 5:5-11

Injili: Yoh 6:37-42

Nukuu:

“Bali roho zao wenye haki wamo mkononi mwa Mungu, wala maumivu hayatawagusa,” Hek 3:1

“Na kufariki kwao kulidhaniwa kuwa ni hasara yao, na kusafiri kwao kutoka kwetu kuwa ni uharibifu wao; bali wao wenyewe wamo katika amani,” Hek 3:2b-3

 Kwa maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu,” Rum 5:6 

Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi,” Rum 5:8

 Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe,” Yoh 6:37 

Na mapenzi yake aliyenipeleka ni haya, ya kwamba katika wote alionipa nisimpoteze hata mmoja, bali nimfufue siku ya mwisho,” Yoh 5:39 

Kwa kuwa mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba kila amtazamaye Mwana na kumwamini yeye, awe na uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:40

TAFAKARI: “Roho zao wenye haki wamo mkononi mwa Mungu, wala maumivu hayatawagusa.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa pote duani anaadhimisha Misa Takatifu kwa heshima ya Waamini Marehemu Wote waliotutangulia katika haki. Kanisa la wana wa Mungu limegawanyika katika makundi makuu matatu. Katika mgawanyiko huo lipo Kanisa la hija, yaani, Kanisa linalosafiri hapa duniani ikiwa ndiyo mahali pa kujindaa kwa ajili ya uzima wa milele. Lipo Kanisa la toharani, ambalo tunaamini ni Kanisa linaloteseka, na kwa kiasi kikubwa linategemea maombezi ya Kanisa la hija na la Watakatifu Wote Mbinguni. Mgawanyiko wa mwisho ni Kanisa la Watakatifu wa Mungu, ambalo ndilo mwombezi wa Kanisa la hija na linaloteseka, yaani, Toharani. Kanisa hili ndilo lililodhihirika la wateule wa Mungu, na wote waishio humo wanafana na Kristo na kufurahia Utukufu wake na kumwona Mungu kama alivyo.  Lakini wapenzi, sasa tu wana wa Mungu, wala haijadhihirika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihirishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo,” 1Yoh 3:2.

Wapendwa wana wa Mungu, tungali hapa duniani yatupasa kuishi katika matumaini hayo niliyoyasema pasipo shaka yoyote tukijua wazi kwamba maisha ya umelele yakilinganishwa na haya ya duniani, tu hapa kwa muda mfupi sana. Hivyo, “kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu,” 1Yoh 3:3. Kanisa hili la hija linatoa sadaka hii ya Misa Takatifu kwa matumaini makubwa likijua kabisa kwa sadaka ile ya Bwana wetu Yesu Kristo pale msalaba ni kielelezo cha utakaso wa Kanisa hili linaloteseka huko toharani lipate Utakakatifu. “Wenye kumtumaini watafahamu yaliyo kweli, na waaminifu watakaa naye katika upendo; mradi neema na rehema zina wateule wake,” Hek 3:9. Kanisa la hija linawajibu huu kama Sakaramenti ya wokovu kwa watu wote. Mungu pekee ambaye ni Huruma, Upendo, na Msamaha na Haki ndiye mwenye kuwahesabia haki wote waliotutangulia na hasa Kanisa hili la toharani.

Haki hiyo ya Mungu tutahesabiwa kutokana na  sadaka ya damu ya Mwanaye Mpenzi Yesu Kristo pale Msalabani. Hivyo, “Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye,” Rum 5:9. Yapo maswali mawili ya msingi kwako na kwangu tutakayo ulizwa siku ya Mwisho. La kwanza; Je, umefanya nini na upendo wa wangu [Mungu] kupitia mwanangu Yesu Kristo kwa sadaka yake pale msalabani?  La pili; Je, umefanya nini na vipaji nilivyokupa? Ili uweze kujibu vizuri siku ya mwisho yakupasa kujiandaa vyema kuyajibu maswali haya sasa kupitia ushuhuda wa maisha yako leo. Hatuwezi kuwa na kesho yenye matumaini ya kweli kama hatuishi leo yenye matumaini ya kweli.

 Wapendwa katika Kristo, maisha ya ushuhuda wa kweli yanagharama zake. Kama yalivyo majira ya mwaka, yaani, kipindi cha baridi, joto, vuli, na kipupwe, ndivyo yalivyo maisha ya binadamu. Yatupasa kuwa wastahimilivu katika vipindi vyote vya shida, taabu, mateso na furaha, na hata kufa kwa ajili ya haki na kweli. Pamoja na maumivu tutakayoyapata katika safari hii ya kuelekea uzima wa milele, roho zetu zenye haki zitakuwa mikononi mwa Mungu. “Bali roho zao wenye haki wamo mkononi mwa Mungu, wala maumivu hayatawagusa,” Hek 3:1. Imani na matumaini ndiyo dira ya kushinda na kufikia hatua hii muhimu.

Maisha ya ulimwengu wa leo ni maisha yenye kusukumwa na falsafa ya umimi na ujimbilikiziaji wa mali. Katika hali hii ni vigumu sana jamii inayokuzunguka kusadifu majitoleo yako kwa wahitaji. Tupo kwenye ulimwengu wa kila mtu na yake na wakati wake. Hata katika hali na changamoto hizi tusimuonee aibu Kristo Yesu hasa tunapojali na kuithaminisha damu yake iliyomwagika pale msalabani. Kufa katika hali hii hakuna hasara yoyote. “Na kufariki kwao kulidhaniwa kuwa ni hasara yao, na kusafiri kwao kutoka kwetu kuwa ni uharibifu wao; bali wao wenyewe wamo katika amani,” Hek 3:2b-3. Tunayo amani na matumaini kwa sababu Kristo alikufa kwa ajili ya waovu, na hasa pale tulipokuwa hatuna nguvu za kuushinda uovu. Kwa maana hapo tulipokuwa hatuna nguvu, wakati ulipotimia, Kristo alikufa kwa ajili ya waovu,” Rum 5:6.

Licha ya udhaifu wetu kama binadamu, upendo wa Mungu unajidhihirisha kwetu kwa kumtoa mwanaye afe kwa ajili yetu tungali tuna dhambi. Huu ni upendo Mkubwa sana kwetu. Bali Mungu aonyesha pendo lake yeye mwenyewe kwetu sisi, kwa kuwa Kristo alikufa kwa ajili yetu, tulipokuwa tungali wenye dhambi,” Rum 5:8. Sadaka hii ya Yesu pale Msalabani ni upatanisho wetu na Mungu, na kurudishiwa hadhi ya kuwa wana wake Mungu, waridhi wa ufalme wake, na maisha ya uzima wa milele. Hivyo, Kwa maana ikiwa tulipokuwa adui tulipatanishwa na Mungu kwa mauti ya Mwana wake; zaidi sana baada ya kupatanishwa tutaokolewa katika uzima wake,” Rum 5:10. Je, tufanye nini sasa?

Wapendwa wana wa Mungu, wenzetu wesha tutangulia katika haki ni jukumu langu mimi na wewe tuishi kama tunayo siku hii ya leo na muda huu wa sasa. Hakuna kati yetu anayejua litakalotokea kwake sekunde moja ijayo. Kristo Yesu yupo daima kutusubiri na anayemwendea hawezi akampoteza. Wote anipao Baba watakuja kwangu; wala ye yote ajaye kwangu sitamtupa nje kamwe,” Yoh 6:37. Kumwendea Kristo ni kuwa karibu naye kila wakati. Ni kuishi maisha yasiyo na hatia. Ni kuupigania ukamilifu ingawa udhaifu upo. Ni kuishi maisha ya kisakramenti na kuchota huko neema na baraka za Mungu kila wakati na kwa kila nafasi tuipatayo kushiriki masakramenti hayo. Ni kuwa waaminifu katika sheria na amri za Bwana kwa kuzishika na kuziishi. Ni kuwa tayari kupokea neema na huruma ya Mungu, na kuwa vyombo vya amani na upendo katika kusambaza neema na huruma hiyo ya Mungu kwa watu wengine.

Kwa kuyashika na kuyaishi haya kamwe Kristo Yesu awezi kutuacha leo, siku ya kufa kwetu, na mwisho siku ya ufufuo wetu. Kwa kufanya hivyo tutakuwa kwenye mpango wa wokovu wa Bwana wetu Yesu Kristo, naye atayatimiza mapenzi ya Mungu kwetu. Na mapenzi yake aliyenipeleka ni haya, ya kwamba katika wote alionipa nisimpoteze hata mmoja, bali nimfufue siku ya mwisho,” Yoh 5:39.  Kumtazama Mwana na kumwamini kuna maanisha kujazwa uzima wa milele.

Ndugu yangu unaye safiri nami katika tafakari hii, tunamtazama Mwana na kumwamini tunapowajali wahitaji hasa wagonjwa, wafungwa, wenye njaa, wenye kiu hasa ya haki, wageni, na walio uchi, Mt 25:36-40. Kwa kuwa mapenzi yake Baba yangu ni haya, ya kwamba kila amtazamaye Mwana na kumwamini yeye, awe na uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho,” Yoh 6:40. Je, hujakutana na Kristo Yesu bado kwa kumtazama na kumwamini? Usiende mbali bali anza hapo hapo ulipo utakutana naye.

Tumsifu Yesu Kristo!

Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida,” Flp 1:21

Tusali:-Ee Yesu, nijalie kifo chema. Amina

domingo, 30 de octubre de 2016

TAFAKARI: SIKUKUU YA WATAKATIFU WOTE


Sikukuu ya Watakatifu Wote

Somo I: Ufu 7:2-4, 9-14

Zab: 24:1bc-2, 3-4ab, 5-6

Somo II: 1Yoh 3:1-3

Injili: Mt 5:1-12a

Nukuu:

Na malaika wote walikuwa wakisimama pande zote za kile kiti cha enzi, na za hao wazee, na za wale wenye uhai wanne, nao wakaanguka kifulifuli mbele ya kile kiti cha enzi, wakamsujudu Mungu,” Ufu 7:11

“Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Ufu 7:14b

Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye,” 1Yoh 3:1

Na kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu,” 1Yoh 3:3 

Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni,” Mt 5:11-12

TAFAKARI: “Utakatifu ndiyo Cheo chako.”

Wapendwa katika Kristo, leo Mama Kanisa kwa furaha kubwa anaadhimisha sikukuu ya Watakatifu wote. Kwa namna ya pekee kabisa mimi na wewe leo tunakumbushwa kwamba ‘Utakatifu ndiyo Cheo chetu.’ Malengo ya Mbatizwa yeyote ni kuwa mkamilifu kama Baba yetu wa mbinguni alivyo mkamilifu. Basi ninyi mtakuwa wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu,” Mt 5:48. Huu ndio wito wa kila mbatizwa ili kuifikia taji ile la Utakatifu ambayo ndilo cheo chako. Ni kuwa na matumaini na Mungu na kila siku kujitakasa na kuepuka kuishi katika hatia. Nakila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa, kama yeye alivyo mtakatifu,” 1Yoh 3:3 

Ndugu yangu, tungali hapa dunia wengi wetu hupenda kujipambambanua na ubora wa familia zetu, koo zetu, makabila yetu, itikadi zetu za kisiasa na kidini, na hata utaifa wetu. Tukiishi katika ngazi hii tu bado hatujajua hatma ya uwepo wetu hapa duniani. Huko Mbinguni hatutajulikana kwa hayo niliyoyataja, bali tutajulikana kwa  usafi wetu uliotokana na UTAKATIFU wetu tuliouishi hapa duniani ikiwa ni mahali tu pa maandalizi na kupita, na kwa muda mfupi tu.

Kila mmoja wetu aweza kuwa Mtakatifu. Utakatifu wako ni matokeo ya kuwa mwaminifu kwa mambo madogo madogo ya kila siku, na kuyafanya hayo kwa ukamilifu wake. Ni kuwa tayari kumpa Kristo nafasi ya ndani ya moyo wako ili atende kazi nawe kwa yale yanayompendeza Mungu na jirani yako. Utakatifu wako ni tokeo pia la kufungua milango kwa wote wenye uhitaji bila kujali historia zao na mapungufu yao. Ni kujaribu kufanana na Yesu katika kuwaza, kutathmini, na kutenda. Tunapokuwa karibu na Kristo ndivyo tunavyofunuliwa siri za Baba yetu wa mbinguni na Ufalme wake.

Ukaribu huu niliousema, utufanya kuwa watoto wapendwa wa Mungu katika utii usio shuruti. Tunatii kwa sababu Mungu anatupenda na anatutakia mema katika ukamilifu wake. Ndugu yangu, Tazameni, ni pendo la namna gani alilotupa Baba, kwamba tuitwe wana wa Mungu; na ndivyo tulivyo. Kwa sababu hii ulimwengu haututambui, kwa kuwa haukumtambua yeye,” 1Yoh 3:1. Maisha haya ya utakatifu yatatudai na yanatudai kila siku kusimama katika kweli na haki, na wakati mwingine tutapimwa katika kweli hiyo, yaani,  Imani yetu.

Kupimwa huku kwa Imani kwa weza pia kutuondolea uhai wetu ambao ndio kitu cha thamani kupita vyote tungali hapa duniani. Basi, hili litakapotokea yatupasa kuyasema maneno haya pasipo shaka yoyote, “kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida,” Flp 1:21. Ni kuyaona yote yaliyofaida kwako ni hasara kwa ajili ya Kristo, Flp 3:7. Tunapoyaachia maisha yetu katika kiwango hiki, Kristo kamwe hawezi kutuacha katika taabu hizo. Kristo hubaki kuwa faraja kubwa kwetu katika dhiki na taabu hizo. Naye anatuambia nyakati kama hizo tuwe watu wa kufurahi kwa sababu tunamruhusu Mungu kutenda mambo katika hali yetu ya uduni na Mateso. Heri ninyi watakapowashutumu na kuwaudhi na kuwanenea kila neno baya kwa uongo, kwa ajili yangu. Furahini, na kushangilia; kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni,” Mt 5:11-12. Je, wayafurahia mateso yako?

Mtawa mmoja wa kiume katika Monasteri fulani alijijengea ukaribu sana na Yesu wa Ekaristi Takatifu. Mtawa huyu alikuwa mpishi wa muda mrefu katika Monasteri hiyo. Aliipenda sana kazi yake na kwake ilikuwa moja ya kumtukuza Mungu kupitia huduma hii kwa wanajumuiya wenzake. Kamwe hakuwahi kunung’unika hata pale ambapo kazi zilikuwa nyingi kupita uwezo wake.

Kila asubuhi Mtawa huyu mara baada ya masifu ya asubuhi, na Misa Takatifu, huenda bustanini kuchuma mboga, na vitu vingine kama maandalizi ya chakula cha Mchana na jioni. Bustani ile ilikuwa baada ya kulipita Kanisa. Hivyo alijiwekea ahadi ya kuongea na Yesu wa Ekaristi Takatifu kila siku kabla ya kufika bustanini.

Siku moja akiwa na kikapu chake na kisu aliingia Kanisani na kuanza kusali na kutafakari mbele ya ‘Terbenakulo,’ Sehemu zinapohifadhiwa Hostia Takatifu. Mara alishtushwa na sauti ya kengele ya Malaika wa Bwana, iliyoashiria pia ni muda wa chakula cha mchana. Mtawa huyu aliingiwa na hofu kubwa sana kwani alikuwa bado hata bustanini hakuwa amefika.

Mtawa huyu aliondoka kwa haraka ili awahi kuomba msamaha kwa watawa wenzake kwa kutokuandaa chakula kile cha mchana. Maajabu ni kwamba alipofika tu eneo la jikoni alikaribishwa na harufu nzuri sana ya chakula na kusikia watawa wenzake wakimsifu kwa chakula kitamu alichoandaa. Kila mmoja alitaka kuongea naye na kumpa asante kwa kazi nzuri aliyofanya.

Akiwa ameshika kikapu chake na kisu ndani yake, alionekana akitokwa na machozi ya furaha huku akisema “asante Yesu kwa kuniona na kuniondolea aibu hii.” Watawa wote walibaki midomo wazi! Ndugu huyu alisimulia yote yaliyotokea. Jumuiya yote ilijawa na furaha na kumtukuza Mungu.

Wapendwa wana wa Mungu, tunapokuwa karibu na Mungu, kamwe hawezi kutuacha. Mungu atatupigania hadi mwisho. Hivyo tuwe waaminifu na kufanya yote kwa ukamilifu tukimtanguliza Mungu kwa kila kitu. Mtume Yakobo anatuambia siri hii kwa kusema, Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi. Itakaseni mikono yenu, enyi wenye dhambi, na kuisafisha mioyo yenu, enyi wenye nia mbili,” Yak 4:8. Haya ndiyo maandalizi ya cheo chako, yaani, Utakatifu wako.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Ufu 7:14b

Tusali:-Ee Yesu, na Bwana wangu, kwako yote yawezekana. Amina

TAFAKARI: JUMATATU WIKI YA 31 YA MWAKA-C


JUMATATU WIKI YA 31 YA MWAKA-C

Somo: Flp 2:1-4

Zab/Kit: 131:1, 2, 3

Injili: Lk 14:12-14

Nukuu:

“Basi ikiwako faraja yo yote katika Kristo, yakiwako matulizo yo yote ya mapenzi, ukiwako ushirika wo wote wa Roho, ikiwako huruma yo yote na rehema, ijalizeni furaha yangu, ili mwe na nia moja, wenye mapenzi mamoja, wenye roho moja, mkinia mamoja,” Flp 2:1-2

 “Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo,” Lk 14:12

“Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki,” Lk 14:13-14

TAFAKARI: “Msitende neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo tunaishi katika ulimwengu wa ushindani mkubwa sana,  na mbaya zaidi ushindani unaojali nafsi na ubinafsi. Hakuna anayetaka kwenda kwa hasara ingawa ndilo lengo la ye yote yule aliye katika ushindani hasa ushindani wa kibiashara. Ni hulka ya binadamu kutafuta mafaa katika faida. Hivyo kwa mazingira ya leo na mtazamo wake, ukihimidi hali hii basi utaupata ulimwengu wote.

Hata hivyo, Yesu anatupa angalizo hasa kwa wale wenye kusombwa na hulka hii kiasi kwamba kusahau sehemu ile ya pili ambayo ni muhimu sana, yaani, NAFSI na ROHO. Binadamu ni mwili, nafsi na roho, na vyote na vyote vitatu ndivyo vimfanyavyo binadamu aliye hai. Mwili ni nyumba ya Nafsi na Roho, ingawa nafsi ipo kati ya mwili na roho. Nafsi ikiegemea mwili utaishia katika matendo ya mwili ambayo kwayo hakuna uzima wa milele, Gal 5:19-21. Na nafsi ikiegemea Roho matokeo yake ni tunda la roho, ambalo kwalo kuna uzima wa milele, Gal 5:22-23.

Ni katika mazingira haya Yesu anazihoji dhamiri zetu na kwa kutoa angalizo, na kusema, “kwa kuwa itamfaidia mtu nin kuupata ulimwengu wote, akipata hasara ya nafsi yake? Ama mtu atoe nini badala  ya nafsi yake?” Mk 8:36-37. Basi nikiwa nafanya ushindani wowote ule ni ufanye nikilenga faida ya wote. Hivyo “Basi ikiwako faraja yo yote katika Kristo, yakiwako matulizo yo yote ya mapenzi, ukiwako ushirika wo wote wa Roho, ikiwako huruma yo yote na rehema, ijalizeni furaha yangu, ili mwe na nia moja, wenye mapenzi mamoja, wenye roho moja, mkinia mamoja,” Flp 2:1.2. Huu ni upendo na mwono wa kujali kama wafuasi wake Kristo tukijifunza unyenyekevu wake na utii kwa Mungu Baba.

Mwito kwetu leo sote kama wana wa Mungu na warithi wa ufalme wake, yatupasa kueneka katika hofu ya Mungu. Na hofu hii ya Mungu utusuma kutenda bila majivuno bali kwa unyenyekevu na kuwajali wengine. Na hili ndilo analosisitiza Mtume Paulo kwetu, kwamba, tusitende, “neno lo lote kwa kushindana wala kwa majivuno; bali kwa unyenyekevu, kila mtu na amhesabu mwenziwe kuwa bora kuliko nafsi yake,” Flp 2:3. Na kama ni faida basi iwe kwa ajili ya wengi. Hivyo,  “Kila mtu asiangalie mambo yake mwenyewe, bali kila mtu aangalie mambo ya wengine,” Flp 2:4. Mtindo huu katika kufikiri, kuamua na kutenda, unasema zaidi kuhusu tabia ya Yesu Kristo na kuthibitisha pendo lake kwetu. Naye Yesu katika kweli hii anasema, “hakuna aliye na upendo mwingi kuliko huu, wa mtu kuutoa uhai wake kwa ajili ya rafiki zake,” Yoh 15:13.

Na tabia ya Yesu inasema zaidi kuhusu mtindo wake wa maisha ulivyokuwa. Yesu licha ya kwamba hakuwa hata na mahali pa kulaza kichwa chake, Lk 9:58, marafiki zake wakubwa walikuwa masikini, vilema, viwete, vipofu, wadhambi, wakoma, wazinzi, watoto, akina mama, waliotengwa na wale wote walikata tamaa. Ukaribu na urafiki wa Yesu katika makundi haya ya watu haukulenga kudumisha mtindo wa maisha yao, bali kuwatoa katika hali zao za unyonge, na kufurahia nuru na neema ya Mungu. Mimi na wewe tunahitaji nuru na neema hiyo ya Mungu.

Tabia hii ya Yesu inajidhihirisha katika Injili yetu ya leo hasa katika matendo yale ya upendo na huruma. Namna yetu ya kufikiri, kuamua, na kutenda kuwe na mwelekeo wau pendo na huruma hasa pale tunapoigusa jamii inayotuzunguka. Na katika kweli hii Yesu anasema, “Ufanyapo chakula cha mchana au cha jioni, usiwaite rafiki zako, wala ndugu zako, wala jamaa zako, wala jirani zako wenye mali; wao wasije wakakualika wewe ukapata malipo,” Lk 14:12. Kufanya hivyo ni kuukubali upendo faida-nipe nikupe. Huu ni upendo linganishi na shindanishi. Ni upendo usio tayari kupoteza kwa faida na mafaa ya wengi. Huu ni upendo tasa na wenye kubaki katika hali ile ile ya mwenendo sawa bila mabadiliko ya kupoteza.

Bali kinyume chake Yesu anakuambia wewe na mimi kwamba, “Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki,” Lk 14:13-14. Huu ni upendo ule ulio tayari kutoa bila tegemeo la kupokea. Ni upendo wa kujitoa bila faida. Ni upendo unaotazama mafaa ya kitu kama kilivyo kwani cha stahili. Ni upendo wenye kuwajibisha kwa sababu huwezi kupenda ukaacha kutoa. Ni upendo uliokomaa na ulio tayari kuzaa. Na kimo cha upendo huu ndicho hiki asemacho Kristo Yesu, kwa namna nyingine, kwamba, “Chembe ya ngano isipoanguka katika nchi, ikafa, hukaa hali iyo hiyo peke yake; bali ikifa, hutoa mazao mengi,” Yoh 12:24.

Ndugu yangu tuliyesafiri sote katika tafakari hii, hakuna haja ya kwenda mitaani, na mijini kuwatafuta hawa marafiki na wapendwa wa Kristo Yesu. Marafiki hawa wa Yesu na wapendwa wake unao hapo ulipo. Embu anza kutazama vizuri hapo nyumbani kwako (Mke, watoto, ndugu, na wafanyakazi wote). Je, hawapo? Embu tazama vizuri pia katika Jumuiya yako ndogo ya Kikristo (familia zake, wanajumuiya wote, na mahitaji yao na Kanisa Mahalia). Je, hawapo? Bila shaka baada ya zoezi hili utakutana na marafiki na wapendwa hawa wa Kristo Yesu. Fanya kitu kwa ajili yao. Amina!

Tumsifu Yesu Kristo!

“Bali ufanyapo karamu waite maskini, vilema, viwete, vipofu, nawe utakuwa heri, kwa kuwa hao hawana cha kukulipa; kwa maana utalipwa katika ufufuo wa wenye haki,” Lk 14:13-14

Tusali:-Ee Yesu Mwema, nipe macho ya kuona marafiki na wapendwa wako, na nijalie moyo wa kuwapenda kama ulivyo wapenda na kuwajali. Amina

sábado, 29 de octubre de 2016

TAFAKARI: JUMAPILI YA 31 YA MWAKA-C



Somo I: Hek 11 :22-12:2

Zab/Kit: 145:1-2-3, 8-9, 10-11, 13cd-14

Somo II: 2The 1:11-2:2

Injili: Lk 19:1-10

Nukuu:

 “ulimwengu wote mbele zako ni kama chembe moja katika mizani, na mfano wa tone moja katika mizani, na mfano wa tone moj ala umande lishukalo asububi juu ya ardí,” Hek 11:22

“Lakini Wewe unaviachilia vyote, kwa kuwa ni vyako,  Ee Mfalme Mkuu mpenda roho za watu; maana roho yako isiyoharibika imo katika vyote,” Hek 11:26

“jina la Bwana wetu Yesu litukuzwe ndani yenu, nanyi ndani yake, kwa neema ya Mungu wetu na ya Bwana Yesu Kristo,” 2The 1:12

“kwamba msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno, wala kwa waraka unaodhaniwa kuwa ni wetu, kana kwamba siku ya Bwana imekwisha kuwapo,” 2The 2:2

Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako,” Lk 19:5

 Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu,” Lk 19:9 

TAFAKARI:Hata wewe na mimi wadhambi, leo wokovu umefika nyumbani mwetu, tuikimbile nuru ambaye ndiye Kristo Yesu, na tuachane na giza la umauti.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Dominika ya 31 ya Mwaka “C” wa Kanisa. Ujumbe wa leo kwetu na kwa kila mmoja wetu ni kwamba, “hata wewe na mimi wadhambi leo wokovu umefika nyumbani mwetu, tuikimbile nuru ambaye ndiye Kristo Yesu, na tuachane na giza la umauti.” Hivyo masomo ya leo yanaonyesha ukaribu huo wa Mungu kwetu, na ukuu wake usio na kipimo kwetu kwa sababu anatupenda upeo.

Ukuu wa Mungu wetu ni waajabu sana. Hatuwezi kuupima wala kuukisia. Naye ndiye Mungu kwa maana, “ulimwengu wote mbele zako ni kama chembe moja katika mizani, na mfano wa tone moja katika mizani, na mfano wa tone moja la umande lishukalo asububi juu ya ardí,” Hek 11:22. Ukuu huu wa Mungu na katika upendo wake usio na kipimo, ndiyo ukubwa wa huruma na msamaha wake kwetu. Na kwa namna hiyo katika kweli na haki, Mungu huwahurumia, ‘watu wote, kwa sababu anao uwezo wa kutenda mambo yote, naye huwaachilia wanadamu dhambi zao, ili wapate kutubu,’ Hek 11:23

Ndugu yangu, hakuna aishiye leo katika ulimwengu huu kwa hali yoyote ile, iwe ya dhiki au ya heri kwa bahati mbaya. Mimi na wewe ni kusudi la Mungu, kwa maana Mungu ameviumba “vitu vyote vilivyopo, wala hukichikii kitu chochote ulichokiumba,” Hek 11:24. Mimi na wewe na vyote tulivyonavyo iwe mali na utajiri wa dunia hii, au vipawa mbalimbali, vyote ni mali yake Mungu kama asemavyo Mzaburi 24:1. Kile ulicho na unachomiliki katika kweli na haki, uifunua sura, utukufu, na furaha ya Mungu kwako na kwa ulimwengu mzima. Na kwa sababu hiyo, Mungu huviachilia ‘vyote, kwa kuwa ni vyake, ndiye Mfalme Mkuu mpenda roho za watu; maana roho yake isiyoharibika imo katika vyote,’ Hek 11:26

Na katika upendo huu wa ajabu wa Mungu, tunaona katika Injili ya leo makutano kati ya Yesu na Zakayo. Zakayo hamwoneyi Yesu aibu pamoja na watu kuyajua madhaifu yake na ufupi aliokuwa nao. Bado anaona salama yake ipo kwa Kristo tu na siyo mitazama ya wale walikuwa wanamzunguka. Ili amwone Yesu, Zakayo alipanda juu ya mkuyu. Na Yesu, alipofika mahali pale, alitazama juu, akamwambia, Zakayo, shuka upesi, kwa kuwa leo imenipasa kushinda nyumbani mwako,” Lk 19:5.

Ni wazi kwamba huwezi kuwa mrefu zaidi ya wewe mwenyewe. Na kwa kuwa huu ni ukweli wa lazima, kumbe kuvijua na kuviona vile vilivyo nje ya uwezo na kimo chako yakupasa kufanya juhudi ili kuujua ukweli ule ulio nje vya vimo yako. Hivyo Zakayo anatufundisha kwamba hata kama ulimwengu ushatuhukumu, na hali na mazingira yetu yanatukwamisha, bado tunaweza kukutana na upendo na huruma ya Mungu tufanyapo bidii. Mtakatifu Agustino wa Hippo katika kweli hii anasema, “aliyekuumba wewe pasipo wewe, hataweza kukusaidia wewe pasipo wewe.” Hizo Zakayo kwa juhudi zake, na mpango mahususi wa Mungu, anafanikisha ndoto yake, na Yesu anakuwa mgeni wake.

Tendo hili la Yesu linawashangaza wengi na wengine wananung’unika. Hata watu walipoona, walinung'unika wote, wakisema, Ameingia kukaa kwa mtu mwenye dhambi,” Lk 19:7. Hapa tunakumbushwa pia moja ya kazi ya Yesu Kristo katika safari na historia hii ya wokovu kama asemavyo yeye mwenyewe kwamba, “sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu,” Lk 5:32.

Kwa utayari wa Yesu kwenda nyumbani kwa Zakayo, kwa furaha aliyokuwa nayo Zakayo hakuweza kuificha. Hivyo Zakayo anayaweka yote wazi mbele ya Yesu.  Zakayo akasimama, akamwambia Bwana, Tazama, Bwana, nusu ya mali yangu nawapa maskini, na ikiwa nimenyang'anya mtu kitu kwa hila namrudishia mara nne,” Lk 19:8. Hii ni toba ya kweli na maungamo ya wazi mbele ya Yesu aliye sasa njia, kweli na uzima.

Maungamo haya ya kweli toka moyoni mwa Zakayo yanaifunua furaha na upendo wa Mungu kupitia mwanaye Yesu Kristo na kuonyesha kile hasa Yesu alichokijia ulimwenguni. Yesu akamwambia, Leo wokovu umefika nyumbani humu, kwa sababu huyu naye ni mwana wa Ibrahimu,” Lk 19:9. Wokovu ni kwa kila mmoja na hasa pale tunapouridhia wokovu huo kwa utashi wetu wenyewe na kwa dhamiri iliyo hai na safi. 

Mungu anatazama utayari wako katika upya wa kuyaanza yote nawe na siyo historia ya maisha yako mabaya yaliyopita. Tu wapya mbele ya Mungu siku na muda wowote. Ni wewe na mimi tu kujisalimisha mbele ya uso wake wau pendo, huruma, na Mtakatifu. Kwa kuwa Mwana wa Adamu alikuja kutafuta na kuokoa kile kilichopotea,” Lk 19:10. Ndugu yangu, afadhali kufa kwa heshima kuliko kuishi kwa unajisi.

Nafasi ndiyo sasa kusimama katika kweli na haki, na kuchukia uovu wa aina yoyote ile kwenye maisha yako na jamii inayotuzunguka. Hivyo kwako na kwangu ni mwito tunaopatiwa leo kila mmoja kadiri ya nafasi na wito wake pale alipo. Kwa yeyote aliyepewa dhamana na umma kwake vitahitajika vingi pia. Naye Yesu anasema, “Na kila aliyepewa vingi, kwake huyo vitatakwa vingi; naye waliyemwekea amana vitu vingi, kwake huyo watataka na zaidi,” Lk 12:48b

Kwa namna hiyo, kiongozi licha ya kuwa tumaini kwa watu, kiongozi ni mwonyesha tumaini hasa pale tumaini hilo linapotoweka. Na katika hali na mazingira haya ambayo tumaini hilo hutoweka, Mtume Paulo anatuwasa na maneno haya ya uzima, msifadhaishwe upesi hata kuiacha nia yenu, wala msisitushwe, kwa roho, wala kwa neno,” 2The 2:2a. Ndugu yangu, hapa na pale tunapoona kusalitiwa kwa wale tulio waamini tusiiache kweli na haki, bali ni wakati wa kusimama imara katika kweli na haki hiyo.

Hivyo, “Mtu awaye yote asiwadanganye kwa njia yo yote; aliyowaitia ninyi kwa injili yetu, ili kuupata utukufu wa Bwana wetu Yesu Kristo,” 2The 2:3a, 4. Matumaini yetu tuyaweke kwa yule atutiaye nguvu, Flp 4:13. Kila mtu kadiri ya imani yake ayashike maadili yaliyo mema na kuupinga uovu kwa nguvu zake zote.

Masumbuko Mponda Kokoto kila siku mapenda alfajiri huondoka na nyundo yake na kurudi jioni. Huondoka akiwa nadhifu na kurudi akiwa nadhifu. Ni mke wake tu katika familia ile wa watoto wanne aliyekuwa anajua kazi ya mumewe.  Kwa kazi hii nzito na ngumu, watoto wake wake walisoma, kula vizuri, kuvaa vizuri na kuwa na makazi mazuri.

Siku mmoja Jumamosi, kama kawaida yake, Masumbuko alijidamka na kuchukua nyundo yake na kuondoka. Mtoto wake wa kwanza wa kiume-Immanuel,  kwa muda mrefu alikuwa anapenda kujua alichokuwa anafanya  Baba yake na nyundo ile. Basi kwa siri alimfuata nyuma polepole hadi eneo lile la kazi.

Mara baada ya kufika Masumbuko alibadili nguo zake na kuvaa nguo za kazi zilizokuwa chafu na kuukuu. Na mara alianza kuyaponda mawe moja baada ya lingine hadi kupata umbo dogo sana, yaani, kokoto. “Dah! Kumbe kula, kuvaa, na kusoma kwetu kwa raha kunatokana na kazi hii ngumu ya Baba? Hakika tunamkosea haki sana pale tunapompigia kelele akiwa amepumzika,” Immanuel alisema kwa masikitiko makubwa.

Hivyo kijana wake-Immanuel baada ya kuyaona yale, alisogea karibu, na Baba yake alipoinua kichwa alikutana na uso wa mtoto wake. “Mbona hupo mahali hapa? Ilikupasa uwe nyumbani unafanya kazi leo jumamosi,” Masumbuko alimuuliza mtoto wake kwa mshangao. “Imenilazimu kujua kila siku huko uendapo na nyundo yako. Na leo nimeona ukweli wote. Baba pole sana kwa kazi ngumu hii,” kijana wake alimjibu Baba yake huku machozi yakimtoka.

“Mwanangu, maisha ni wito, kuchagua, na kuyapenda. Niliona na kujisikia wito huu wa familila, nikachagua kuwa na familia, na hiki ninachokifanya ni ishara ya kupenda kile nilichokichagua. Hivyo katika hali zote nawapenda na nitawapenda daima. Nafurahi kwa sababu mnafuraha kila mara nirudipo nyumbani,” Baba yake alimjibu mwanaye huku akiyapangusa machozi yake.

Ndugu yangu, huu ni upendo wa kweli kwa Wazazi wetu kwa familia zao. Baba yetu wa Mbinguni anatuwazia mazuri zaidi kwa sababu uwepo wetu  uifunua Furaha na Utukufu wake. “Maana  najua mawazo ninayowawazia ninyi, asema Bwana, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho,” Yer 29:11

Tumsifu Yesu Kristo!

“Lakini Wewe unaviachilia vyote, kwa kuwa ni vyako,  Ee Mfalme Mkuu mpenda roho za watu; maana roho yako isiyoharibika imo katika vyote,” Hek 11:26

Tusali:-Ee Yesu, asante kwa kutuona hata sisi wadhambi kwa sababu kwako tu upo usalama. Amina

jueves, 27 de octubre de 2016

TAFAKARI: JUMAMOSI WIKI YA 30 YA MWAKA-C


JUMAMOSI WIKI YA 30 YA MWAKA-C

Somo: Flp 1:18b-26

Zab/Kit: 42:2, 3, 5abc

Injili: Lk 14:1, 7-11

Nukuu:

“Lakini kwa njia zote, ikiwa ni kwa hila, au ikiwa ni kwa kweli, Kristo anahubiriwa; na kwa hiyo nafurahi, naam, nami nitafurahi,” Flp 1:18b

 “Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida,” Flp 1:21

 “Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma,” Lk 14:8-9

 “Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11

TAFAKARI: “Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo katika somo la Injili Yesu anatupa angalizo hasa tunapoalikwa kwenye tafrija mbalimbali. Tukizama ndani zaidi tunaona kwamba uhai tulionao na maisha tunayoyaishi ni sawa na kualikwa kwenye furaha ya Mungu na Utukufu wake. Basi ni vyema mimi na wewe kutambua duniani hapa tunapita tu, na tupo kwa maandalizi ya maisha ya umilele. Yesu anatuwasa hivi kuhusu ukweli huu; Ukialikwa na mtu arusini, usiketi katika kiti cha mbele; isiwe kwamba amealikwa mtu mwenye kustahiwa kuliko wewe, akaja yule aliyewaalika wewe na yeye, na kukuambia, Mpishe huyu! Ndipo utakapoanza kwa haya kushika mahali pa nyuma,” Lk 14:8-9.

Kama sote tumealikwa harusini ni wazi tumepewa mastahili yaliyo sawa na yule aliyetualika. Basi yatupasa kujua kuwa sote ni waalikwa na siyo ‘mgeni rasmi.’ Kwa utaratibu wa kawaida mbele palipoandaliwa si mastahili yangu. Kumbe ni vyema na busara kutafuta nafasi nyingine. Ili kuwa sehemu salama zaidi, Yesu anatuasa hivi; Bali ukialikwa, nenda ukaketi mahali pa nyuma, ili ajapo yule aliyekualika akuambie, Rafiki yangu, njoo huku mbele zaidi; ndipo utakapokuwa na utukufu mbele ya wote walioketi pamoja nawe,” Lk 14:10. Huku ndiko kwa maneno mengine kupungua ili Mungu awe na nafasi juu ya maisha yako.

Ndugu yangu unaye safiri nami katika tafakari hii utakubaliana nami kwamba kati yetu kwa nafasi tulizokuwa nazo na madaraka tuliyonayo yaliyopitiliza hututia upofu na kutufanya kuwa ndiyo fimbo ya kuchapia wengine. Jeuri hii ndugu yangu tunaipata wapi wakati Maandiko Matakatifu yanatuambia, Siku za miaka yetu ni miaka sabini, Na ikiwa tuna nguvu miaka themanini; Na kiburi chake ni taabu na ubatili, Maana chapita upesi tukatokomea mara,” Zab 90:10. Jinyenyekeshe basi na kuwa kile Mungu alichokusudia katika maisha yako.

Mfano mzuri wa unyenyekevu huu tunaupata kutoka somo letu la kwanza, na hasa juu ya maisha ya Mtume Paulo. Paulo mara tu baada ya kuongoka kwake, dira ya maisha yake yote ni kupungua ili Kristo aliye Njia, Kweli, na Uzima awe na nafasi juu ya maisha yake. Na hii ndiyo njia sahihi ya kufuata kama waja na wana wa Mungu. Na kauli mbiu ya Mtume Paulo ni hii; “Kwa maana kwangu mimi kuishi ni Kristo, na kufa ni faida,” Flp 1:21. Kwa mtazamo huu, Paulo hana cha kujisifia wala kujikweza zaidi ya neema ile ya Mungu ifanyayo kazi ndani ya maisha yake.

Mpendwa katika Kristo, mimi na wewe yatupasa kupungua ili Kristo aongezeke kwa wanyonge, mayatima, wajane, masikini, wafungwa, wagonjwa, waliokata tamaa, wanaoonewa kwa ajili ya haki, wafiwa, wadhabi, wanaodhulumiwa, na wale wate walitengwa kwa kusimama katika kweli na haki. Watu hawa ndio waliokuwa karibu na zaidi, marafiki wa Yesu Kristo kama asemavyo mwenyewe kwamba, “sikuja kuwaita wenye haki, bali wenye dhambi, wapate kutubu,” Lk 5:32. Leo mimi ninayepumua na kufurahia afya njema nione wajibu huo mkubwa wa Kristo mbele yangu.

Na kwa kutambua wajibu huo mkubwa na mwendelezo wa kazi ile ya wokovu wetu, ndani na katika Kristo Yesu, nijue kwamba,  “kwa njia zote, ikiwa ni kwa hila, au ikiwa ni kwa kweli, Kristo anahubiriwa; na kwa hiyo nafurahi, naam, nami nitafurahi,” Flp 1:18b. Kama ilivyo kwamba hakuna aliyekuwa masikini kwa kutoa kile alichonacho, vivyo hivyo hakuna atakayepoteza muda wake kwa kulihubiri neno la Mungu kila siku, na zaidi kwa maisha yake ya kumcha Mungu.

Tendo la kupeleka habari njema kwa wengine, ni tendo la neema na baraka. Kuna furaha kubwa sana kwa Mungu na Watakatifu wake siku moja ukiwa mbele ya Mungu, na mmoja kati ya wale waliohesabiwa haki na Mungu kutoa ushuhuda juu yako kwamba, ‘utakatifu wake ulitokana na kuijua siri hiyo ya mbinguni na kwa kumjua Mungu kupitia wewe.’

Na hii ndiyo maana ya maneno haya ya Paulo ambaye sasa kwa ajili ya Injili hakuna alichopoteza, anachopoteza, na atakachopoteza. Naye anasema, “Maana najua ya kuwa haya yatanigeukia kuwa wokovu wangu, kwa sababu ya kuomba kwenu, na kuruzukiwa Roho wa Yesu Kristo; kama vile nilivyotazamia sana, na kutumaini, kwamba sitaaibika kamwe, bali kwa uthabiti wote, kama sikuzote na sasa vivyo hivyo Kristo ataadhimishwa katika mwili wangu; ikiwa kwa maisha yangu, au ikiwa kwa mauti yangu,” Flp 1:19-20. Hakika Mtume Paulo katika hatua hii hana alichokibakiza kwa ajili yake mwenyewe, yote kesha yakabidhi kwa Kristo Yesu na yeye Kristo ni yote katika yote.

Hata hivyo, Mtume Paulo anatupa leo angalizo, tena zito sana. Kamwe mimi na wewe tusijilinganishe na yale tuyafanyayo, na kamwe kwayo kama yalivyo yasiwe ndiyo chanzo na mwisho wa furaha yetu. Hilo likiwa ndilo lengo la maisha yako, basi ujue bado hujajitambua na kutambua kusudi lako la kuumbwa na uwepo wako hapa duniani. Hapa na pale unaweza kupewa pongezi na hata kupigiwa makofi. Lakini mara uonavyo hivyo, usibaki na pongezi hizo na makofi hayo, bali mara mrudishie Mungu sifa na shukrani hiyo, na kuwabariki wale wote waliotambua kweli hiyo ndani yako, nawe uwe wa mwisho katika kundi hilo la stahili ya baraka hiyo. Ni kwa maana hii Mtume Paulo anasema juu ya kuishi maisha yanayoongozwa na malengo, kwamba, “ikiwa kuishi katika mwili, kwangu mimi ni matunda ya kazi; basi nitakalolichagua silitambui,” Flp 1:22.

Ndugu yangu, maisha yako katika hali salama lazima yasukumwe na mambo mawili; kukaa na Kristo, na kudumu katika huduma kwa ajili ya watu. Naye Mtume Paulo anasema hivi katika kweli hii, “Ninasongwa katikati ya mambo mawili; ninatamani kwenda zangu nikae na Kristo maana ni vizuri zaidi sana; bali kudumu katika mwili kwahitajiwa zaidi kwa ajili yenu,” Flp 1:23-24. Kumpenda Kristo na kuishi ndani na katika Kristo Yesu kutakulazimu kutumika kwa ajili ya wengine, tena bila faida binafsi.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Kwa maana kila ajikwezaye atadhiliwa, naye ajidhiliye atakwezwa,” Lk 14:11

Tusali:-Ee Yesu, tujalie neema ya kudumu ndani na katika wewe tu kwa sababu kwako kuna furaha ya kweli. Amina

 

TAFAKARI: SIKUKUU YA WATAKATIFU SIMONI NA YUDA, MITUME


Sikukuu ya watakatifu Simoni na Yuda, Mitume

Somo: Efe 2:19-22

Zab: 19:2-3, 4-5

Injili: Lk 6:12-16

Nukuu:

Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni,” Efe 2:20 

Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana,” Efe 2:21

Katika yeye ninyi nanyi mnajengwa pamoja kuwa maskani ya Mungu katika Roho,” Efe 2:22

akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume; Simoni, aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na Filipo na Bartolomayo, na Mathayo na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote,  na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa msaliti,” Lk 6:13b-16 

TAFAKARI: “Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, Kristo ni jiwe la pembeni.”

Wapendwa wana wa Mungu, leo Mama Kanisa anaadhimisha Sikukuu ya Mitume Simoni (Mkananayo-Zelote) na Yuda (Tadei-wa Yakobo).

Simoni Mkananayo alikuwa mmojawapo kati ya Mitume wa Yesu. Ili kumtofautisha na mtume mwenzake Simoni Petro anaitwa Mkananayo, yaani Mwenye juhudi kwa ukombozi wa Israeli kutoka ukoloni wa Roma. Jina lake linapatikana katika orodha zao zote, lakini hatuna habari zake zaidi, isipokuwa masimulizi mbalimbali yasiyo na hakika. Inasadikika kuwa kaburi lake liko Komani (Georgia).

Yuda Tadei ni jina la mmojawapo kati ya Mitume wa Yesu, ambalo Injili zinajitahidi kumtofautisha na Yuda Iskarioti, msaliti wa Yesu. Habari zake za hakika zinategemea Agano Jipya ambamo anatajwa katika orodha ya Thenashara ambao waliteuliwa na Yesu Kristo kama msingi wa taifa jipya la Mungu wakatumwa naye kuhubiri na kuponya.

Injili ya Yohane tu inaripoti neno lake moja, katika simulizi la karamu ya mwisho, alipomuuliza Yesu imekuwaje atajifunua kwao lakini si kwa ulimwengu (14:22). Yesu alimjibu kwamba yeyote anayempenda atashika neno lake, na Baba atampenda na kufanya maskani yake kwake pamoja na Mwana. Anafikiriwa na wengi kuwa mwandishi wa Waraka wa Yuda, lakini hakuna hakika kwa sababu jina hilo la babu wa Wayahudi wote lilikuwa la kawaida mno.

Mitume kwa ujumla wao, yaani, wale kumi na mbili, kwa maisha yao na ushuhuda wao wa Imani ndiyo msingi Imara wa Kanisa letu kama tunavyoliona hii leo. Akachagua kumi na wawili miongoni mwao, ambao aliwaita Mitume; Simoni, aliyemwita jina la pili Petro, na Andrea nduguye, na Yakobo na Yohana, na Filipo na Bartolomayo, na Mathayo na Tomaso, na Yakobo wa Alfayo, na Simoni aitwaye Zelote,  na Yuda wa Yakobo, na Yuda Iskariote, ndiye aliyekuwa msaliti,” Lk 6:13b-16. Sadaka yao kwa maisha yao ya Imani juu ya Kristo Yesu, Kanisa linaendelea kutimiza wajibu wake kama Sakramenti ya wokovu wetu. Kristo Yesu mwenyewe ndiye jiwe kuu la pembeni.

Ukristo wetu na Imani yetu imejengwa juu ya msingi wa Mitume na Manabii, na Kristo Yesu akiwa jiwe kuu la pembeni. Mmejengwa juu ya msingi wa mitume na manabii, naye Kristo Yesu mwenyewe ni jiwe kuu la pembeni,” Efe 2:20. Ni fahari ya kila aliyebatizwa kuishi ahadi zake za ubatizo na kuendeleza msingi huu imara wa Imani. Hivyo kila mmoja wetu kwa njia ya Kristo na kwa sadaka ya maisha yake na wito wake, ameunganishwa na hekalu la Mungu. Katika yeye jengo lote linaungamanishwa vema na kukua hata liwe hekalu takatifu katika Bwana,” Efe 2:21.

Mitume tunaowasheherekea leo ni mfano wa kuingwa kwetu. Mitume hawa walikuwa mashahidi na manabii katika kipindi chao. Maisha hayakuwa rahisi tunapolitazama Kanisa la Mwanzo. Wengi wao walikufa kwa kuuwawa kikatili, ila hakuna aliyemsaliti Kristo zaidi ya Yuda Eskariote. Leo miongoni mwetu akina Yuda wapo wengi sana. Ni ni changamoto ya Kanisa na maisha yetu ya kijamii.

Wapendwa wana wa Mungu, leo Kanisa linachangamoto nyingi sana. Ili kuzikabili changamoto hizi, yampasa kila mbatizwa kuishi ahadi zake za ubatizo. Pili, kila mmoja wetu kadiri ya wito wake ajitahidi kila siku kufanana na Kristo ambaye ndiye jiwe kuu la pembeni ambapo maisha yetu na sadaka yake upewa maana. Huu ni ushuhuda tosha wa ukimya hata pale ambapo Kristo hakubaliki kutokana na mitazamo tofauti ya Kiimani.

Matendo yetu mema humwakilisha vizuri Kristo popote kuliko kile tukiaminicho kwa nadharia tu. Mtume Yakobo anatupatia changamoto hii kwa kusema, Lakini mtu atasema, Wewe unayo imani, nami ninayo matendo. Nionyeshe imani yako pasipo matendo, nami nitakuonyesha imani yangu kwa njia ya matendo yangu,” Yak 2:18.

Wapendwa wana wa Mungu, tuwe waaminifu kwa wito wetu kila mmoja kadiri ya namna yake,  na upendo uliobeba matendo yetu mema kwa watu wote.

Mitume wa Yesu: Wa kwanza, Simoni Petro, Andrea, Yakobo Mkubwa, Yohane, Filipo, Bartholomayo, Tomaso, Mathayo, Yakobo Mdogo, Simoni Mkananayo, Yuda Tadei, Yuda Iskarioti; ambaye  baada ya kifo chake, nafasi yake ilishikwa na Mathiya

Tumsifu Yesu Kristo!

Tusali:-Ee Yesu Mwema, tujalie moyo ya Kitume na Kimisionari kuanzia pale tulipo. Amina

Watakatifu Simoni, na Yuda Mitume, Mtuombee. Amina

martes, 25 de octubre de 2016

TAFAKARI: ALHAMISI WIKI YA 30 YA MWAKA-C


ALHAMISI WIKI YA 30 YA MWAKA-C

Somo: Efe 6:10-20

Zab/Kit: 144:1, 2, 9-10

Injili: Lk 13:31-35

Nukuu:

“Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani,” Efe 6:11

“Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho,” Efe 6:12

 “Saa ile ile Mafarisayo kadha wa kadha walimwendea, wakamwambia, Toka hapa, uende mahali pengine, kwa sababu Herode anataka kukuua,” Lk 13:31

“Akawaambia, Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika,” Lk 13:32

“Pamoja na hayo imenipasa kushika njia yangu leo na kesho na kesho kutwa; kwa kuwa haimkini nabii aangamie nje ya Yerusalemu,” Lk 13:33

TAFAKARI: Vaeni silaha zote za Mungu, mpate kuweza kuzipinga hila za Shetani.”

Wapendwa wana wa Mungu, Mwana falsafa Spinoza aliwahi kusema “kifo hakiwezi kuepukika. Ni lazima tutakukufa. Kinachotusumbua ni hofu kuhusu kifo. Hivyo yatupasa kuishinda hofu. Na hivyo ni vizuri kufikiri kuhusu uhai.” Mpendwa, je wamwamini Kristo Yesu? Kama unamwamini Kristo Yesu hakuna sababu ya kuwa na hofu kuhusu kifo. Kristo Yesu kwa maisha yake, mateso, kifo, na ufufuko wake ni jibu kuhusu aina zote za uovu na kifo. Kristo Yesu ndiye kielelezo chetu kama wafuasi wake. Kristo Yesu ametupatia mfano na jibu kwamba hakuna uovu wowote unaoweza kudumu katika umilele wake. Yesu haogopi vitisho wala kifo.

Yesu anapoambiwa aondoke kwa kuwa Herode anataka kumuua aliwajibu, “Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika,” Lk 13:32. Mnyama huyu Mbweha alitafsiriwa kama mtu asiye na msimamo, kigeugeu na mwongo. Kristo hawezi kutishiwa na mtu wa hali hii na kuacha kutoa huduma kwa watu ikiwa ndiyo sababu na mpango kazi wake kwa watu wote. Ni kwa kupitia Kristo vipofu wanapata kuona, viwete wanakwenda, wenye ukoma wanatakaswa, viziwi wanasikia, wafu wanafufuliwa, na maskini wanahubiriwa habari njema,” Mt 11:5. Kristo pia anaufunua Utukufu wake mara baada ya kuushinda uovu anaposema, ‘siku ya tatu nakamilika.’

Mateso tunayoyapata leo au tuliyokwisha yapata kupia wazazi wetu, siyo kwamba historia hiyo ya uovu Mungu haioni. Wakati utimiapo vyote vitafanywa upya. Yesu anapoutazama mji wa Yerusalemu anayakumbuka na kuyaona mateso na uovu wa manabii wake waliyofanyiwa na kusema, Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii na kuwapiga kwa mawe waliotumwa kwako, mara ngapi nimetaka kuwakusanya watoto wako kama vile kuku avikusanyavyo vifaranga vyake chini ya mbawa zake, wala hamkutaka,” Lk 13:34. Huu kwetu ni wito wa kuongoka na kuacha njia zetu mbaya na kujisalimisha kwa Kristo. Tusisubiri hadi siku ya Mwisho kwani hatutakuwa na muda tena wa kujisalimisha kwake. Utakuwa muda wa kupokea ukumu yetu kila mmoja kadiri ya matendo yake na livyotenda. Yesu anasema, Angalieni, mmeachiwa nyumba yenu! Nami nawaambia, Hamtaniona tena kamwe, hata mtakaposema, Amebarikiwa ajaye kwa jina la Bwana,” Lk 13:35. Je, kuna sababu ya kusubiri hadi siku ya mwisho? Ndugu yangu natuanze kuishi maisha ya ufufuko kabla ya kuja kwake Bwana wetu Yesu Kristo.

Maisha baada ya ufufuko ni maisha yaliyokamili. Tunayaishi maisha haya ya ufufuko kwa kuhesabiwa haki na kwa kuzaliwa mara ya pili kwa Roho Mtakatifu. Hivyo si kwa sababu ya matendo ya haki tuliyoyatenda sisi; bali kwa rehema yake, kwa kuoshwa kwa kuzaliwa kwa pili na kufanywa upya na Roho Mtakatifu; ambaye alitumwagia kwa wingi, kwa njia ya Yesu Kristo Mwokozi wetu; ili tukihesabiwa haki kwa neema yake, tupate kufanywa warithi wa uzima wa milele, kama lilivyo tumaini letu,” Tit 3:5-7. Je, una sababu yoyote ya kuwa na hofu juu ya maisha yako ukiwa na Kristo?

Ndugu yangu tunaye safiri sote katika tafakari hii, ni vyema ukafahamu kweli hii kwamba kwa wewe kuwa mfuasi wa Kristo ni uchaguzi uliyofanya dhidi ya giza, yaani, vita dhidi ya uovu. Ushuhuda ya maisha ya imani yako leo na sasa na hadi siku yako ya mwisho hapa duniani ni kuifia kweli na haki dhidi ya uovu na dhuluma. Hivyo katika vita hii mimi na wewe tulio Wakristo hai kwa kuishi kwa uaminifu ahadi zetu za ubatizo, yatupasa kuvaa “silaha zote za Mungu, tupate kuweza kuzipinga hila za Shetani,” Efe 6:11. Vita hii si lelemama. Yatupasa kusimama imara daima. Na tushindapo vita hii siyo kwamba shetani kaghairi, bali utuacha kwa muda tu, Lk 4:13

Ukweli ni kwamba, vita hii  “si juu ya damu na nyama; bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya majeshi ya pepo wabaya katika ulimwengu wa roho,” Efe 6:12. Ni vita ya kiroho, nayo yatupasa kujiandaa kupambana kiroho. Kuishinda vita hii yakupasa kuwa na haya yafuatayo; Amani ya ndani na yenye kuneemeshwa na Injili, Imani thabiti, na Nguvu ya Roho Mtakatifu. “Basi simameni, hali mmejifunga kweli viunoni, na kuvaa dirii ya haki kifuani, na kufungiwa miguu utayari tupatao kwa Injili ya amani; zaidi ya yote mkiitwaa ngao ya imani, ambayo kwa hiyo mtaweza kuizima mishale yote yenye moto ya yule mwovu,” Efe 6:14-16.

Vita hii inahitaji ujari, tena wa kujitoa bila kujibakiza. Na wokovu ikiwa ndiyo kushinda kwake ni kuvumilia hadi mwisho. Yawezekana twapambana kila siku na kwa bidii zote lakini matokeo yake ni kwamba afadhali ya jana kuliko leo na huko tuendapo. Katika hali na mazingira haya Yesu anatuambia hivi;  “Nanyi mtakuwa mkichukiwa na watu wote kwa ajili ya jina langu; lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka,” Mt 10:22. Ndugu yangu, penye mateso makali ndipo penye ukaribu wa furaha ile tuitumainiyo, yaani, utukufu.

Nguvu na faraja yetu na Roho yule wa Bwana, yaani, Roho Mtakatifu. Huyu ndiye atutiaye nguvu na kutufariji hasa pale tunapokumbana na sintofahamu zilizozidi ufahamu wetu. Naye Yesu katika hali na mazingira haya ya sintofahamu zilizozidi ufahamu wetu anatukumusha jambo hili la msingi juu ya Roho Mtakatifu kwamba, “Lakini hapo watakapowapeleka, msifikiri-fikiri jinsi mtakavyosema; maana mtapewa saa ile mtakayosema,” Mt 10:19. Tusipoteze muda mwingi kujitetea kwa yale yasiyo na kweli ndani yake na kuacha kusimama katika kweli na haki.

Kama jumuiya ya wenye hofu ya Mungu, yaani, familia, jumuiya ndogo ndogo ya Kikristo, au Kanisa mahalia, Mtume Paulo anatuambia, tupokee “chapeo ya wokovu, na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu; kwa sala zote na maombi mkisali kila wakati katika Roho, mkikesha kwa jambo hilo na kudumu katika kuwaombea watakatifu wote,” Efe 6:17-18. Kudumu katika sala ndiko tuchotapo nguvu ya kupambamba na vita hivi vya kiroho, yaani, aina zote za uovu.

Tumsifu Yesu Kristo!

“Nendeni, mkamwambie yule mbweha, Tazama, leo na kesho natoa pepo na kuponya wagonjwa, siku ya tatu nakamilika,” Lk 13:32

Tusali:-Ee Yesu, uliyeshinda vita dhidi ya uovu, tujali nguvu na imani thabiti kupigana bila kuchoka dhidi ya uovu katika jamii yetu. Amina